Mambo 8 muhimu ya kukusaidia kufaulu katika usaili wa kazi

MUME MASKINI

Senior Member
Jun 11, 2019
196
253
cid%3ACE3F553F-A23D-433D-9481-546FD428DE67@mobilenotes.apple.com

Kupata kazi ya ndoto zako si jambo jepesi, na inawezekana ikawa ni vigumu zaidi kama hujui waajiri wanataka nini kutoka kwako.
Ulimwengu wa wa ajira - kwa kampuni kubwa na ndogo - unabadilika kwa kasi sana.
Lakini kuna eneo moja ambalo ni la muhimu kuzingatiwa kwa kila msaka ajira: usaili wa ana kwa ana.
"Usaili huo ni sehemu kubwa zaidi ya mchakato wa ajira," amesema Jane Tippin, ambaye ni gwiji wa masuala ya rasilimali watu ambaye hutumiwa na kampuni kubwa ya benki nchini Uingereza ya Lloyds.
Bi Tippin anaamini kuwa uwezo wako wa kujibu maswali mbele ya mtu ama jopo la watu linaweza kujenga ama kubomoa mustakabali wako wa kupata ajira.
Hivyo, unahitajika kujiandaa kikamilifu kabla ya kuingia kwenye chumba cha usaili wa ana kwa ana.
Zifuatazo ni dondoo muhimu zitakazokusaidia kufaualu usaili huo:
1. Fanya utafiti
Chunga usije kushtukizwa na mawswali ndani ya chuma cha usaili, unaweza kupata tabu kuyajibu.
Kama kampuni au taasisi imekupatia majina ya watu watakaokusaili, jaribu kufanya utafiti wa kujua wao ni akina nani na wanafanya nini.
Pia itafiti kampuni ama taasisi hiyo kwa undani: Ipi ni biashara ama shughuli yao kuu? Nani anaiongoza? Ina umuhimu ama nafasi gani katika fani husika? Na kampuni au taasisi zipi ni washindani wao wa kibiashara.
Yawezekana ukawa unajiuliza utazipata wapi taarifa husika, sehemu nzuri ya kuanzia ni kwenye tovuti ya kampuni ama taasisi.
Chukua dondoo na andaa maswali ya kuuliza mwishoni mwa usaili ili kuwaonesha umefanya utafiti kiasi gani kuwahusu.
Utafiti ndiyo kazi ya muhimu ambayo unaweza kuifanya kabla kuingia kwenye chumba cha usaili, na hakika utaona faida yake.
2. Fanya majaribio
Baada ya utafiti wa kina andaa maswali ambayo unahisi utaulizwa na fanya majaribio ya kuyajibu.
Na endapo utakuwa na shida yeyote ile, rudi mtandaoni. Kuna tovuti kadha wa kadha ambazo hutoa maswali muhimu ambayo huulizwa kwenye chumba cha usaili kwa fani mbalimbali.
Uandaapo majibu yako, fikiria katika muundo wa kujieleza ulio na mtiririko bora. Andaa mifano hai ya namna gani umefanikisha ama unaweza fanikisha yae yote ambayo yanatakiwa katika nafasi ya ajira uliyoomba.
Hadithi fupi fupi za namna gani ulifaulu awali kwenye ajira zako nyengine na uzoefu wako inabidi zioneshe ni kwa namna gani utafaidisha kampuni inayokusaili endapo watakupa ajira.
3. Vaa uvutie
Muonekano wa awali una nguvu kubwa sana. Baadhi ya waajiri hufanya maamuzi ndani ya sekunde 30 za mwanzo za kukutana na mtahiniwa wa usaili.
Unaweza ukawa na majibu mazuri ya maswali, lakini kama mavazi na haiba yako haikuwapendeza watahini wako, utakuwa unapigana katika pambano ambalo lazima ushindwe.
Virginia Eastman, ambaye ni mtaalamu mstaafu wa kutahini watu kwenye usaili anamuelezea bwana mmoja ambaye alimsaili kwa nafasi ya kuongoza kampuni ya habari.
"Harufu yake mbayailitangulia chumbani dakika tatu kabla yeye mwenyewe kuingia. Alikuwa amevaa hovyo: soksi zimechakaa, chakula kimenasia kwenye ukosi wa koti lake...yaani ilikuwa ni moja ya vitu vya ovyo kabisa ambavyo nimewahi kuvishuhudia."
Bila kuuliza, bwana huyo aliikosa ajira aliyoomba.
Japo kampuni inaweza kuwa na sera ya mavazi ya kawaida, hawatakutegemea uende kwenye usaili ukiwa umevalia suaruali ya jeans. Wataalammu wa rasilimali watu wanashauri uvae suti.
Iwapo usaili si wa kazi rasmi, basi inashauriwa uvae shati jeupe na suruari au sketi.
Hakikisha muonekano wako ni nadhifu. Piga pasi siku moja kabla, na hakikisha hauli chakula cha michuzi au rangi rangi kabla ya kuingia kwenye usaili.
4. Salimia kwa kujiamini
Hiki ni kitu ambacho wengi hukisahau lakini ni muhimu sana.
Mwajiri wako anaweza kukupunguzia alama kwa namna utakavyosalimia uingiapo chumba cha usaili.
Kama unasailiwa na mtu mmoja au unashauriwa uwape mkono huku ukiwaangalia machoni.
Salamu imara inaashiria kuwa unajiamini, unajua ukifanyacho na ni mweledi.
Lakini, chunga usijiamini kupitiliza, utaonekana kuwa ni mkorofi. Ila usipojiamini napo utaonekana kuwa ni muoga.
Pia hakikisha una kitambaa mfukoni, futa jasho kwenye viganja kabla ya kutoa salamu. Hakuna mtu anayependa kupewa mkono wenye jasho.
Na unapokuwa ndani ya chumba cha usaili hakikisha unawaangalia machoni , kuangalia chini ni dalili ya woga.
5. Tabasamu!
Hili ni jambo jepesi kulitaja kuliko kulitenda hususani pale moyo wako unapokuwa unaenda puta, tumbo lako limevurugika na unaweza hata kusahau jina lako.
Hata hivyo, tabasamu ni lugha ya kimataifa ya kusema: "Nina furaha kuwa hapa, mimi ni mtu mwema."
Hivyo basi tandaza tabasamu kubwa unapoingia kwenye chumba cha usaili. Usiliangushe tabasamu hilo wakati wote wa usaili. Ni njia bora ya kupata alama.
Hata hivyo, chunga mikao yako, usijilegeze kwenye kiti, kaa kikakamavu.
6. Usikubali woga ukakutawala
Ukiruhusu uoga ukutawale, kinachofuata kinaweza kuwa... balaa kubwa.
Uoga unaweza kufanya ukasahau kila kitu kwenye utafiti ulioufanya awali, unaweza ukafanya mikono yako ikawa inatetemeka na kutokwa na jasho.
Uoga pia unaweza ukakufanya kushindwa hata kutabasamu.
Kama unajua woga unaweza kukuathiri, basi jaribu kuvuta pumzi na kusema na moyo wako kuwa unaweza, na ndio maana umeitwa kwenye usaili.
Wataalamu wanasema kuwa, endapo utaweza kuushinda woga, basi yawezekana ukapata ujasir wa hali ya juu na kufaulu usaili wako.
7. Kuwa mchangamfu
Kabla ya kuketi kwenye kiti cha usaili, tafakari "kipi kinakufanya uwe wa tofauti?"
Ukishajiuliza hivyo, usisite kuwa mchangamfu na kuonesha haiba yako, waoneshe kuwa wewe unastahili. Kumbuka si peke yako uliyeomba kazi hiyo na kuitwa kwenye usaili.
Usisahau pia kusema mambo mazuri kuhusu kazi uliyoiomba - na unapofikia mwisho wa usaili kumbuka kuisifia kampuni na vipi itakuwa fahari kwako kupata kazi hiyo.
Kumbuka uchangamfu na haiba yako ndiyo vitu pekee ambavyo vinaweza kukutofautisha na wengine.
8. Usikate tamaa njiani
Hata kama mambo yamekuwa mazito kiasi gani katika chumba cha usaili, usikate tamaa.
Kuna kipindi maswali yanakuwa magumu kiasi kwamba unaweza kudhani kuwa basi na kazi yenyewe ushaikosa.
Usifanye kosa la uamini kitu hicho, jitahidi, pambana mpaka dakika ya mwisho, yawezekana wewe ndiyo umefanya vizuri kuliko mtu yeyote katika usaili huo.
Pia yawezekana swali linalofuatia ndilo ambalo unalimudu kuliko yote yaliyopita.
Ni muhimu kujituliza kifikra mambo yanapokuwa magumu. Una nguvu kubwa ndani yako.
Fanyia kazi dondoo hizi, utaona matokeo!
 
Shukrani Kwa ushauri mkuu, nimeona kuna umuhimu sana Wa kuifahamu vizuri company/taasisi unayoenda kufanyia interview, like what they offer,history kidogo kuhusu co,say anything good about them.

Imenisaidia hii kuna interview nilienda maswali magumu hayo ila niliponea ponea hapo kwenye kuifahamu co yao. Nikapitaa
 
1 Reactions
Reply
Back
Top Bottom