Malumbano ya Spika Sitta na Mzee Mrema

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,722
21,775
SPIKA wa Bunge, Samuel Sitta amemuelezea mwenyekiti wa Tanzania Labour Party (TLP), Augustine Mrema kuwa amekwisha kisiasa na kipesa na sasa anahangaika kujinasua kutoka katika hali hiyo.

Spika, ambaye anaonekana kuwa kwenye mapambano makali na wapinzani wake wa kisiasa ndani ya chama chake, alidiriki hata kumtuhumu waziri huyo wa zamani wa serikali ya awamu ya pili kuwa anapata fedha ili kuipigia debe CCM.

Sitta alitoa kauli hiyo baada ya Mwananchi kutaka maoni yake kuhusu madai ambayo Mrema aliyatoa katika mkutano wake na waandishi wa habari jana kuwa spika huyo wa Bunge la Jamhuri ya Muungano amekiuka maadili ya uongozi kwa kuendeleza mjadala wa kashfa ya Richmond pamoja na kushiriki katika ziara ya baadhi ya wabunge wanaojipambanua kuwa ni wapambanaji wa ufisadi.



Akizungumzia madai hayo ya Mrema, Spika Sitta alisema: “Mrema ni mhuni na amepitwa na wakati... pia amefilisika kisiasa na kipesa sasa anatafuta njia ya kujinasua kutoka katika hali hiyo.


"Kutokana na maneno yake hayo ninajipanga kumshtaki ili athibitishe hicho anachokisema"


Spika Sitta alisema kuwa madai na shutuma zote alizozitoa Mrema ni za uongo na zimejaa uzushi na alishangazwa na kauli za Mrema kuhoji sababu za kiongozi huyo wa TLP kuzungumzia masuala ya CCM sasa.

"Kinachoshangaza yeye ni mwenyekiti wa TLP lakini ndiye wa kwanza kuzungumzia matatizo yaliyomo ndani ya CCM, kama ameshindwa huko ni bora arejee CCM ili tupambane huku" alisema Sitta.


"Kuna uwezekano huyu bwana anapata pesa ili kuipigia debe CCM."

Sitta alisema anajiandaa kumfikisha mahakamani Mrema ili athibitishe matamshi yake ya kwamba alishirikiana na wabunge wanaojipambanua kama makamanda wa vita dhidi ya ufisadi pamoja na wafadhili wao kufanya ziara mikoani. na si muda mrefu mtasikia kahamia CCM,atuna kinyongo tunamkaribisha

Awali akizungumza na waandishi wa habari Mrema, ambaye ameshaeleza bayana kuwa atampigia debe Rais Jakaya Kikwete kwenye uchaguzi mkuu ujao, alisema Sitta anatumia makanisa kutangaza kuwa alitaka kufukuzwa uanachama kwa sababu ya msimamo wake katika suala la Richmond.


Katika mkutano huo Mrema, ambaye alivuliwa uwaziri baada ya kukiuka kanuni ya uwajibikaji wa pamoja mwaka 1995, alikwenda mbali na kumtaka Sitta ajiuzulu au aondolewe ili asiendelee kuwa spika katika Bunge lijalo.



"Kitendo cha Sitta kuamua kuendeleza mjadala wa sakata la Richmond wakati Bunge limeshafunga ni cha uchochezi na kinaweza kuvuruga amani ya nchi," alisema Mrema ambaye pia aliwahi kuwa mbunge wa Temeke kwa tiketi ya NCCR baada ya kupoteza ubunge wa jimbo la Vunjo kutokana na kuihama CCM baada ya sakata hilo la uwajibikaji wa pamoja.


"Pia Sitta alishirikiana na wabunge wanaojipambanua kama makamanda wa vita dhidi ya ufisadi pamoja na wafadhili wao kufanya ziara mikoani na kudhihirisha kuwa ana kundi ndani ya chama chake huku akiwa kama mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM kitu ambacho ni kinyume na taratibu za Bunge na kiongozi mkubwa kama yeye," alisema Mrema.


Mrema alisema kitendo cha Sitta kuendelea kujadili suala la Richmond ni kukiuka na kwenda kinyume na taratibu za Bunge na kuwalaghai wananchi wamuone kwamba yupo mstari wa mbele katika vita dhidi ya ufisadi.


"Ni yeye Sitta ndiye aliyetangaza kuufunga rasmi mjadala wa Richmond na kuonya kwamba atakayeufufua mjadala huo atachukuliwa hatua, lakini badala yake amekuwa mstari wa mbele kuongelea mjadala huo. Hii ni sawa na kuwalaghi na kufanya uchochezi kwa wananchi. Ni lazima ajiuzulu," alisisitiza Mrema.

Akitoa mfano wa kuendelea kwa mjadala huo, Mrema alisema Sitta amekuwa akipita makanisani na kusema kuwa walitaka kumfukuza uanachama kwa sababu ya msimamo wake juu ya mjadala wa Richmond.

Mrema alidai kiongozi huyo wa Bunge hadi leo ameendelea pamoja na kunusurika kufukuzwa CCM, haogopi na ataendelea na mapambano na kusisitiza kuwa huo ndio msimamo wake.

"Spika kama mwamuzi anayesimamia haki ndani ya Bunge hakupaswa kuonyesha ushabiki au kujionyesha kwamba anaunga mkono upande fulani na badala yake alipaswa asiwe na upande wowote," aliongeza mwenyekiti huyo.


Mrema alidai Sitta ameweka kitu moyoni hivyo ajiuzulu ili awe huru kukitoa na si kuendelea kuzungumzia kitu ambacho mjadala wake ulishafikia mwisho.
 
Anadai yeye ni usalama wa taifa - kwa hiyo anafanya haya yote na meingine wa maslahi ya taifa letu.

Hawezi kukaa kimya wakati watu wachache wanataka kulitia taifa kwenye vita na mifarakano isiyo ya lazima- bado ni mwana-usalama na ataendelea kupigania inji hii hadi aitwe na mwenyezi mungu.

duh - mimi nipo hoi kwa kauli ya huyu mwana usalama anayejitangaza hadharani.
kwake kunafuka moshi - badala yake anapuliza moto jikoni kwa jirani ili viive haraka walivyovipika.
ni huyu huyu mrema nayemjua mimi au mwingine?
 
Spika sitta nae kafulia tuache kumpamba najiuliza ni kwanini alifunga mjadala wa Richadmonduli kiyamela badala ya kushinikiza serekali itekeleze maazimio yote ya bunge yeye kakimbilia kuzima mjadala.
 
Hivi Mrema kagundua lini kuwa amani inatoweka wakati ule anaongoza maandamano alikuwa hasababishi amani kuvunjika au wakati ule damu ya binadamu ilikuwa haina thamani kama ya wakati huu aache ushamba wa kitoto na kujipendekeza kijinga amekuwa kama zezeta sasa hata mtu anayemsifia mwisho atamuona ni bogus
 
Spika sitta nae kafulia tuache kumpamba najiuliza ni kwanini alifunga mjadala wa Richadmonduli kiyamela badala ya kushinikiza serekali itekeleze maazimio yote ya bunge yeye kakimbilia kuzima mjadala.

Ungelikuwa wewe peke yako ungefanyaje
 
Spika sitta nae kafulia tuache kumpamba najiuliza ni kwanini alifunga mjadala wa Richadmonduli kiyamela badala ya kushinikiza serekali itekeleze maazimio yote ya bunge yeye kakimbilia kuzima mjadala.
Hilo ndo swali muhimu analotakiwa kuwajibu Watanzania kwa ufasaha na sio blah blah kwa Mrema..

Kanishangaza eti anataka kumfungulia Mrema mashitaka mahakamani? Aachee siasa za maji taka!
 
mnafki njia yake siku zote ni fupi, kwani amani inayovunjika tanzanioa ni ipi? mi na nadjhani Mrema angewasaidia wale wanaopambana ufisadi wa richmond ambayo pia iliongezea uvunjifu wa amani iliyokuwa imevunjika, hawezi kuniambia tanzania pana amani labda kwa maamuma!
 
Hilo ndo swali muhimu analotakiwa kuwajibu Watanzania kwa ufasaha na sio blah blah kwa Mrema..

Kanishangaza eti anataka kumfungulia Mrema mashitaka mahakamani? Aachee siasa za maji taka!
Nani amfungulie mashitaka Mrema keshajichokea yule nikujitafutia lawama bure
 
Hilo ndo swali muhimu analotakiwa kuwajibu Watanzania kwa ufasaha na sio blah blah kwa Mrema..

Kanishangaza eti anataka kumfungulia Mrema mashitaka mahakamani? Aachee siasa za maji taka!
watanzania tuache unafki, we ni nilini ulipoona bunge halifanyi yale unayoona hayafai likiwa chini ya Sitta, ukaandamana au kuingia mitaani kudai haki yako, kama wewe uko kimya hadi sasa, siasa zako wewe zisizo za maji taka ni zipi au na wewe unajidabadua tu bila kujua utakuwa sawa tu Mrema
 
Sitta ajibu hoja za Mrema na sio kumtukana binafsi...yeye mwenyewe alifunga mjadala wa Richmond na alisema atakae ufukua ataadhibiwa na kanuni za bunge..leo hii kwenye makanisa ansema alitaka kufukuzwa kwa ajili hiyo....huo ujasiri wa Siita angetuonyesha wakati bunge lina funga mjadala wa Richmond...unnaaa watanzania hatutaki...........
 
watanzania wepi wanaotakiwa kujibiwa kwa ufasaha, na kwa maswali gani ambayo hawana majibu yake, au ni kale katabia ka kimbumbu kujifanya hatuyaoni mpaka yatufike ndani ya nyumba tunazoishi tena vyumbani?
 
kuna kila dalili Mrema maeshapewa fungu kubwa sana la kumng'oa kimaro kule jimboni sasa anachofanya ni kurudisha fadhira kwa bwana mkubwa, anakoelekea ni kuwa msemaji wa CCM,
 
Katika umri nilionao sijaona SPIKA mahiri kuliko sita na angekuwepo enzi ya MSEKWA nadhani mambo mengi ya kipuuzi tunayoyaona leo yasingekuwepo.Kuifunga rich monduli c kwa amri yake ni NEC YA WEZI
 
Nadhani Mrema anahoja ya msingi kwa Sitta. Sitta kama kiongozi wa bunge amelizika swala la Richomnd mwenyewe halafu analifukulia kwenye madhabahu, kwanini asingekataa kulifunga mpaka serikali iseme kinagaubaga imeyatekeleza vipi maamuzi au mapendekezo ya bunge katika swala la Richmond?
Ni kweli kuwa Sitta anaendekeza makundi ndani na nje ya Bunge na haya yanajionyesha kwa kauli zake zinavyotafunana kila wakati. Nadhani hata ubunge wa Urambo Mashariki upo mashakani kwake, nadhani aende jimboni kujiimarisha zaidi unless otherwise anataka jimbo moja la Dar Es Salaam. Aende Jimbo la Ubungo atapita kiurahisi kabisaaa!!!!
 
Katika umri nilionao sijaona SPIKA mahiri kuliko sita na angekuwepo enzi ya MSEKWA nadhani mambo mengi ya kipuuzi tunayoyaona leo yasingekuwepo.Kuifunga rich monduli c kwa amri yake ni NEC YA WEZI
Lakini Bunge ni huru, naye ameshasema bunge ni huru, sasa inakuwaje afunge halafu aanze kutapatapa?
 
Ndugu wana JF naomba tujadili hoja na si watu..........nawasilisha hoja ya Mrema na waandishi wa habari jana dhidi ya Spika

SPIKA WA BUNGE LA TANZANIA MH.SAMWELI SITTA AMEKOSA SIFA YA KUWA MHIMILI WA DOLA

Ndugu Waandishi wa Habari, leo nimewaiteni ili kutoa dukuduku langu kuhusu baadhi ya viongozi wakuu wa nchi wanavyoleta uchochezi ambao unaweza kusababisha uvunjifu wa amani na utulivu hapa nchini.

Mimi nikiwa mkereketwa wa amani na utulivu hapa nchini, siwezi kukaa kimya wakati kuna viongozi ambao wanatoa kauli za uchochezi ambazo zinaweza kuhatarisha amani na utulivu.

Nimesikitishwa sana na kauli zinazotolewa na Spika wa Bunge Mh Samweli Sitta ambaye amekaririwa na vyombo vya habari akisema kwamba kulikuwepo na mipango ya kumfukuza uanachama wa CCM kwa sababu ya msimamo wake kuhusu suala la Richmond.

Mh Spika ameyasema hayo akijua wazi kwamba Bunge la Jamhuri lilishafunga mjadala huo na ni yeye aliyedai kuwa yeyote atakae aanzisha mjadala huo anapaswa kushughulikiwa kwa mujibu wa kanuni za Bunge. Kwa kauli hiyo Mh Spika amekiuka Azimio la Bunge, jambo ambalo ni kinyume cha maadili ya uongozi.

Aidha Mh Spika anataka kushawishi watu wamuone kwamba anaonewa katika suala zima la Richmond na kwamba huenda pengine serikali ilikuwa inataka kuficha kitu fulani kuhusu suala la Richmond, ndio maana CCM ilitaka kumfukuza uanachama wa CCM. Huo ni uchochezi, ni sawa na kuwapaka matope viongozi wenzake wa chama na serikali.

Akiwa kama Spika wa Bunge anapaswa kuwa mtu wa kwanza kulinda Azimio la Bunge na si vinginevyo.



SPIKA ALIKUWA MWAMUZI NA MCHEZAJI

Tangu mwanzoni mwa mgogoro wa Richmond Mh Spika alionyesha kuwa alikuwa mchezaji na mwamuzi.

Spika kama mwamuzi anayesimamia haki ndani ya Bunge hakupaswa kuonyesha ushabiki au kujionyesha kwamba anaunga mkono upande fulani, alitakiwa asiwe na upande wowote. Lakini yeye alionyesha kabisa kwamba yuko pamoja na wabunge wanaojiita ‘makamanda wa vita dhidi ya ufisadi’, hapo tayari ana kundi lake. Na hatimaye alifanya ziara mikoani akifuatana na wabunge hao pamoja na wafadhili wao.

Kwa maana hiyo Spika alikuwa mwamuzi na mchezaji kwa wakati mmoja jambo ambalo ni kinyume na utawala bora.

Spika hadi leo anaendelea kuonyesha ukereketwa wake kwa kusema kwamba alinusurika kufukuzwa CCM lakini bado haogopi, bali ataendelea na mapambano. Na anasisitiza kwa kusema kwamba ‘huo ndio ukweli kwani tatizo lipo wapi?’

Hiyo ina maana kwamba ameshaamua kuegemea upande mmoja dhidi ya upande mwingine, wakati yeye akiwa msimamizi wa haki. Je kwa staili hiyo haki itatendeka?

Je, kwa mfano Jaji Mkuu angesema kwamba yeye ni mkereketwa wa vita dhidi ya ufisadi. Je,. watuhumiwa wa ufisadi wangepewa haki yao ya kujitetea mahakamani?

Kwa kauli zake Spika anathibitisha kwamba yeye bado yuko pamoja na wabunge ambao wanajiita makamanda wa vita vya ufisadi. Ambao wanasema hawajaridhika kwa sababu baadhi ya Maazimio ya Kamati ya Bunge bado hayajatekelezwa.

Vile vile kauli za Spika zinawachochea na kuwapa nguvu wanaharakati ambao wanasema wataandamana nchi nzima kupinga jinsi serikali ilivyolishughulikia suala zima la Richmond
JINSI YA KUONDOA MAKUNDI NDANI YA BUNGE

Mgawanyiko ndani ya Bunge hauwezi kuisha kama Spika ataendelea kuwa na makundi. Kwa sababu yeye tayari ameonyesha kwamba ana kundi lake ndani ya Bunge. Na pia ameshindwa kusimamia haki ndani ya Bunge, kwa sababu amekuwa mwamuzi na wakati huo huo mchezaji.

Vile vile analeta migogoro na uchochezi baina ya Bunge na Serikali kutokana na kauli zake. Ili kuleta upendo na mshikamano ndani ya Bunge, na kuondoa migongano na migogoro kati ya Bunge na Serikali, nashauri Mh Spika Sitta ajiuzulu au aondolewe, na asiendelee kuwa Spika wa Bunge lijalo.

Pia namshauri Spika pamoja na hao wabunge wanaojiita makamanda wa vita dhidi ya ufisadi, kwamba endapo hawaridhiki na jinsi serikali ilivyolishughulikia suala la Richmond, wajiondoe CCM, badala ya kuleta uchochezi ambao unaweza kuhatarisha amani na utulivu.
 
Sitta ajibu hoja za Mrema na sio kumtukana binafsi...yeye mwenyewe alifunga mjadala wa Richmond na alisema atakae ufukua ataadhibiwa na kanuni za bunge..leo hii kwenye makanisa ansema alitaka kufukuzwa kwa ajili hiyo....huo ujasiri wa Siita angetuonyesha wakati bunge lina funga mjadala wa Richmond...unnaaa watanzania hatutaki...........
Ajibu hoja za watu waliofulia,sijui jot yuko wapi akamzomee
 
Hilo ndo swali muhimu analotakiwa kuwajibu Watanzania kwa ufasaha na sio blah blah kwa Mrema..

Kanishangaza eti anataka kumfungulia Mrema mashitaka mahakamani? Aachee siasa za maji taka!
Great thinker haki ya mtu kwenda mahakamani ni haki ambayo haihojiwi, wala huna mamlaka yakumzuia mtu yoyote kwenda huko, unless uruhusu mambo ya kibazazi , kuviziana, kupigana ngumi.
kama Sitta anahisi maneno ya Mrema yamemkeji na kumvunjia hadhi na HESHIMA Anahaki ya kwenda kushitaki na kudai damage.
 
Katika umri nilionao sijaona SPIKA mahiri kuliko sita na angekuwepo enzi ya MSEKWA nadhani mambo mengi ya kipuuzi tunayoyaona leo yasingekuwepo.Kuifunga rich monduli c kwa amri yake ni NEC YA WEZI
Hayo ndo maneno ya kweli, nami naamini Mh Sitta angekuwepo wakati wa Msekwa Misamaha mibovu mibovu na mikataba hewa isingekuwepo,Hongera sana SPIKA wetu tupo pamoja achana na watu wapo katika umri wa bata
 
Sitta ajibu hoja za Mrema na sio kumtukana binafsi...yeye mwenyewe alifunga mjadala wa Richmond na alisema atakae ufukua ataadhibiwa na kanuni za bunge..leo hii kwenye makanisa ansema alitaka kufukuzwa kwa ajili hiyo....huo ujasiri wa Siita angetuonyesha wakati bunge lina funga mjadala wa Richmond...unnaaa watanzania hatutaki...........
Hoja za Mrema zipi? Kwamba kupambana na mafisadi ni kuvunja amani? Nilikua namfagilia sana huyu mzee wa kiraracha lakini kwa kauli zake hizi nimegundua amepoteza mwelekeo. Au ni kwa vile anaumwa maskini tumsamehe bure? Lakini asishambulie watu kwa kujikomba sisi em. Ni kweli amefulia.
 
Back
Top Bottom