Makinda ashangaa mafisadi kusafishwa

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,792
287,994
Makinda ashangaa mafisadi kusafishwa

na Godfrey God, Iringa
Tanzania Daima~Sauti ya Watu

NAIBU Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Anna Makinda amewakoromea baadhi ya wabunge na watu wanaofanya kazi ya kuwasafisha mafisadi kuacha mara moja kwa madai kuwa hawawatendei haki Watanzania wenzao.

Makinda ambaye pia ni Mbunge wa Njombe Kusini, alitoa kauli hiyo nzito jana wakati akiwasalimia wapiga kura wake katika Kata ya Njombe Mjini kwenye mkesha wa Mwenge wa Uhuru.

Ametoa kauli hiyo kipindi ambacho Bunge limegawanyika makundi mawili, moja likiwatetea mafisadi, lingine likiwapinga huku likiishinikiza serikali kuchukua hatua.

Ingawa hakutaja majina ya watu wanaofanya kazi ya kuwasafisha mafisadi, Makinda alisema binafsi amekuwa akishangazwa na baadhi ya wabunge wa aina hiyo.

“Binafsi nimekuwa nikiwashangaa sana watu wa aina hiyo, waliokubali kufanya kazi ya kuwasafisha viongozi wanaotuhumiwa ufisadi, kwa kupewa fedha kidogo na kusahau utaifa,” alisema Makinda.

Alisema moto wa ufisadi unaoendelea kuwashwa ndani ya Bunge, ni jambo la kuungwa mkono na wananchi bila kujali itikadi, na kusisitiza kwamba wanaoamua kuwatetea mafisadi nao hawajui kama ni sehemu ya ufisadi unaolalamikiwa.

“Inashangaza kusikia na kuona kikundi cha Watanzania wachache wakifanya kazi ya kuwasafisha mafisadi wakati wanatambua kuwa ufisadi unaangamiza taifa zima. Mimi nawataka Watanzania waendelee kulivalia njuga suala hilo ikiwa ni pamoja na kuliombea taifa kwa Mungu ili aweze kuteketeza shetani ufisadi,” alisema Makinda.

Makinda ambaye ni mmoja wa wabunge wa muda mrefu nchini, alisema suala la ufisadi halivihusu vyama vya upinzani, wala Chama Cha Mapinduzi (CCM) pekee, bali linamhusu mtu mmoja mmoja, na kwamba ni rahisi mno kupambana na ufisadi iwapo kila Mtanzania kwa nafasi yake atauchukia.

Kutokana na hali hiyo, Makinda alisema kwa nafasi yake kama Naibu Spika wa Bunge, ataendelea kukemea kwa nguvu zote tabia iliyoibuka hivi karibuni ya baadhi ya wabunge waliosahau utaifa, na kuamua kuwasafisha mafisadi kwa sababu ya fedha wanazozawadiwa.

Hata hivyo, aliwatia moyo wananchi kwamba, licha ya kuwapo kwa wabunge wachache wanaofanya kazi ya kuwasafisha mafisadi, wapo wabunge ambao hawalali kwa ajili ya kukemea mafisadi, na hivyo kuwataka kushikamana nao ili kuwafichua mafisadi wadogo na wakubwa.

Alisema sehemu ya ujumbe wa mwenge mwaka huu, unaelezea mapambano dhidi ya vitendo vya ufisadi, ambavyo kwa Watanzania wanaofuatilia vikao vya Bunge, wamekuwa wakishuhudia jinsi wabunge wanavyopambana kwa nguvu zote dhidi ya ufisadi na rushwa.

“Kwanza ningependa kuwapongeza wananchi wangu wa Njombe pamoja na Watanzania wengine wote ambao mmekuwa mkifuatilia vikao vya Bunge...Bunge la sasa halijalala kwani wenyewe ni mashahidi na mmekuwa mkishuhudia wabunge wanavyofichua ufiasadi,” alisema na kuongeza kuwa wananchi wasiogope kuwatumia wabunge wao, madiwani na hata viongozi wengine wa vijiji, kata na hata wilaya katika kuwaripoti watu wanaojihusisha na ufisadi.

Alisema vitendo vya ufisadi, vimekuwa vikichangia kwa kiasi kikubwa taifa kuyumba kiuchumi na kuwa ni vyema sasa kila mwananchi kupambana na ufisadi kwa kuwafichua wahusika wa ufisadi na ufisadi.

Makinda ambaye alikuwa ameambatana na wabunge wawili wa CCM, akiwemo Yono Kevela (Njombe Magharibi) na Pindi Chana (Viti maalum), Mkoa wa Iringa, alisema wabunge hao ni sehemu ya wabunge wa Mkoa wa Iringa na Tanzania ambao wamekuwa mstari wa mbele kukemea rushwa.

Katika siku za hivi karibuni ndani ya wabunge, kumekuwa na makundi ya wazi yakiwatetea kwa uwazi baadhi ya watuhumiwa wa kashfa ya Richmond, kuwa walionewa.

Waliokumbwa na kashfa hiyo ni pamoja na aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Dk. Ibrahim Msabaha na Nazir Karamagi.

Pia wapo wabunge wanaomtetea Rais mstaafu, Benjamin Mkapa kutokana na kashfa zinazomwandama wakati akiwa madarakani.

Akizungumzia dhana ufisadi, kwa upande wake Chana, alisema ni vyema Watanzania wakaepuka kujihusisha na vitendo vya ufisadi na CCM kwani ni vitu viwili tofauti na kuwa mafisadi si wanaCCM, na hata CCM yenyewe haiwapendi kuwaona watu hao.

Alitahadharisha kuwa iwapo kuna wapo watu wanaojihusisha na vitendo vya ufisadi, wakiwa ndani ya chama, ni vyema wakajiondoa na kubaki na ufisadi wao badala ya kuendelea kuongoza kwa misingi ya kujificha na ufisadi wao.

Chana alisema kati ya wenyeviti wa CCM ambao wanachukizwa na ufisadi ni pamoja na Rais Jakaya Kikwete na kuwa mafisadi hao wameweza kufichuliwa kipindi hiki cha awamu ya nne.

Mapema akikabidhi taarifa ya utii kwa rais kwa kiongozi wa mbio za mwenge kitaifa, Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Darry Rwegasira alisema wilaya hiyo ina mpango wa muda wa kati ambao unaratibu na kutekelezwa kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Alisema moja ya jitihada hizo ni kutoa elimu kwa wananchi dhidi ya rushwa ikiwa ni pamoja na kutoa mafunzo kwa wadau mbalimbali kuhusu kupambana na rushwa katika maeneo yao.

Mkuu huyo wa wilaya alisema watumishi 291 wamepatiwa mafunzo hayo na mikutano ya hadhara minne imefanyika ukiwemo mdahalo mmoja ulioambatana na utoaji wa vipeperushi 100.

Alisema tayari kumekuwepo na mafanikio makubwa kuhusu elimu hiyo na kwamba mpaka sasa matukio 47 ya rushwa, yameripotiwa na sita yamefikishwa mahakamani.

Kuhusu shughuli za kimaendeleo, alisema wananchi wamekuwa mstari wa mbele kubuni, kuanzisha na kuendeleza miradi ya kimaendeleo na kuwa kwa mwaka huu pekee, mwenge umeweza kupitia miradi mitano yenye thamani ya sh 207,808,606, ambayo imekaguliwa wakati miradi mitatu yenye thamani ya sh 86,223,733, imefunguliwa na mingine mitatu yenye thamani ya sh 2,053,231,200 imewekewa mawe ya msingi.

Alisema miradi hiyo imetekelezwa kwa nguvu za wananchi, serikali kuu, halmashauri ya wilaya na wadau mbalimbali.
 
karinu jukwaanikwetu dada yetu makinda, hapa hasafishwi mtu wala haogeshwi kamwe, hapa mtu atajisafisha mwenyewe, na kuoga mwenyewe. kama Mungu yupo upande wetu, je ni nani atakuwa kinyume nasi?
 
Mnaposema halihusu Chama hilo si kweli ,maana inakuwaje kuwaje mtu anafika kusema suala la mafisadi halihusu Chama ? Wakati hadi leo wanaotuhumiwa ni wanaCCM magogo ,kama Chama hakihusiki Je ni hatua gani kimewachukulia ? Kama Chama hakihusiki ni msimamo gani kimetoa ? Kama Chama hakihusiki ni kwa nini waliofikia kuuzuliwa kinyemela nyemela kwa kutaka wajiuzulu wenyewe kabla hawajaumbuliwa bado wamebaki ndani ya Chama na nyadhifa zao ?
Kama Chama hakihusiki tunataka kuona kinawafuta uanachama mara moja na kufanya uwepo urahisi wa kuwapeleka watuhumiwa mahakamani bila ya kuoneana haya au kulindana ,naamini kabisa kubaki ndani ya Chama kwa watuhumiwa wa Ufisadi ni kulindwa na Chama husika.
Hivyo msiende huko vijijini na kuwahadaa wananchi kwa kauli za kujionesha kama mna ujasiri , wafukuzeni uanachama na muwe mstari wa mbele kuwafikisha mahakamani hapo kidogo wananchi wataweza kupima baada ya hukumu.
Kama kusafika au kuzidi uchafu wananchi na wahusika watajua baada ya watu mafisadi waliomo ndani ya CCM kuwekwa kizimbani na kujibu suali baada ya suali linalohusiana na tuhuma.

Tazama mafisadi wanavyolindwa ...Akizungumzia dhana ufisadi, kwa upande wake Chama, alisema ni vyema Watanzania wakaepuka kuvihusisha vitendo vya ufisadi na CCM kwani ni vitu viwili tofauti na kuwa mafisadi si wanaCCM, na hata CCM yenyewe haiwapendi kuwaona watu hao.

Sasa hiyo kauli hapo inabidi ijadiliwe (nimeifanyia matengenezo kidogo maana muandishi aliipotosha na kuandika songombingo)
Je mafisadi si wana CCM ? Tunataka ufafanuzi wa kauli hii .wana CCM mpo ? Maana watuhumiwa wote ni CCM mijoka ile ilikuwa haiogopi tena.
 
Ingekuwa hawa watu wanasimama huko huko bungeni na kusema haya mambo mengi yangekuwa yameshabadilika. kama mtu anamaanisha hayo anayoyasema awe tayari kuyasema hali popote pale na sio kwenda kuyasema vijijini tena kwenye mkesha wa Mwenge na wakati mwingine hakuna hata mtu anayekusikiliza.

Hebu you style up
 
'mafisadi si wana ccm' kakusudia nin?
kwa vile wanaoshutumiwa na ufisadi wote ni wanchama wa ccm, kakusudia usema kuwa hawa watu si mafisadi ndo maana wakawa bado ccm au?
 
Huyu mama ni mjumbe wa CC, NEC na Naibu Spika. Je, hayo aliyoyasema huko kwa wapiga kura wake aliyasema kwenye vikao vyao vya kinafiki (NEC na CC)? Iweje aende kusema hayo maneno huko kwa wapiga kura wake? Halafu akiwa kwenye vikao vya NEC na CC ambako ndiko maamuzi mazito yanakofanyika anakaa kimya?

Ukweli ni kwamba wameishagundua kwamba wananchi wameanza kuamka na kwa hiyo wanakwenda kujiosha kwao ili 2010 wasije wakapigwa chini. Ningekuwa ni mpiga kura wake lazima ningemuuliza: Kwanini aje jimboni kusema hayo wakati akiwa kwenye vikao vinavyofanya maamuzi mazito anakaa kimya?
 
Ni katika malengo ya kukumbushana na kuweka rekodi hadharani.. yawezekana alimaanisha maneno yake..
 
Sasa kama aliyaongea haya mbona anatupa dfn mpya ya mafisadi
Uku akijua fika mafisadi ni akina nani?
 
mhhh naogopa kutoa comments zangu maana MODS wakali sana this week..Kuna ndugu yangu kapigwa BAN kwa kumgusa huyu Supika wa Bunge retu ra jamuri
 
Ni katika malengo ya kukumbushana na kuweka rekodi hadharani.. yawezekana alimaanisha maneno yake..

Ngoja tuone
"Binafsi nimekuwa nikiwashangaa sana watu wa aina hiyo, waliokubali kufanya kazi ya kuwasafisha viongozi wanaotuhumiwa ufisadi, kwa kupewa fedha kidogo na kusahau utaifa," alisema Makinda.
Umeona alivyoelezea kama mtu anayefahamu maana hasa ya neno UFISADI?

sasa cheki ya leo
nijuavyo mimi ni kuwa fisadi ni mwanamume anayewachukua wanawake wa watu
sasa hii ina maana gani? Mwanzoni alisema anawafahamu mafisadi wa mali zetu sasa analeta definition hiyo na kuifanya haelewi definition ile ya kimazingira? Ni wazi fisadi ni mume anayekula mke wa mwenzie na vilevile kwa definition ya kimazingira ni anayekula mali za wenzie. Tumpe muda anaweza kufanya kazi vizuri na kutupa moyo!
 
Sasa kama aliyaongea haya mbona anatupa dfn mpya ya mafisadi
Uku akijua fika mafisadi ni akina nani?

Ndio politics hiyo politically right at that particular moment of time akiulizwa leo atasema waandishi walim misquote!!!
 
Ndio politics hiyo politically right at that particular moment of time akiulizwa leo atasema waandishi walim misquote!!!

Hajakanusha kwa miaka miwili sasa. Magazeti yakimbilie haraka archives zao na kupata video ya mwaka juzi alipokemea kutetewa mafisadi.
 
MUDA UTAZUNGUMZA. IMENIPA MATUMAINI KIDOGO Kwamba aliwahi kukemea Hata kama kwa wanakijiji.

NGULWA L.A
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom