Makala ya msimamo wa Obama juu ya uhusiano wa Tanzania na Marekani

Status
Not open for further replies.

Invisible

Robot
Feb 11, 2006
9,075
7,878
Obama apongeza ushirikiano kati ya Marekani na Tanzania
Na Carmen Rojas

Rais wa Marekani, Barack Obama, muda mfupi kabla ya kufanyika kwa Mkutano wa Kundi la Nchi 20 maarufu kama G20 Jijini London ambao yeye mwenyewe alihudhuria, aliandika makala iliyopewa kichwa cha habari “Ni Muda wa Mabadiliko kwa Dunia”, ambayo inatoa tahadhari kuhusu changamoto mbalimbali za kiuchumi zinazozikabili nchi duniani.

Madhumuni ya makala hiyo ni kuhamasisha nchi nyingine duniani kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Marekani katika kutafuta suluhu ya mgogoro wa kifedha ambao umezikumba benki za kimataifa na taasisi nyingine za kifedha na hivyo kuyumbisha ukuaji wa uchumi wa dunia na kuzorotesha ustawi wa jamii miongoni mwa mataifa ya duniani.

“Ujumbe wangu ni bayana: Marekani iko tayari kuongoza, na tunawahimiza washirika wetu ikiwemo Tanzania, kuungana nasi kwa kuzingatia dharura na dhamira ya pamoja. Kazi nzuri imekwisha kufanyika lakini mengi zaidi hayajafanyika”, amesema Rais Obama kwenye makala yake.

Lakini kinachovuta hisia zetu sisi Watanzania katika makala hiyo, ni jinsi Rais Obama alivyoitaja Tanzania kwa namna ya pekee kama mshirika wa Marekani. Kutajwa huko kwa Tanzania hakukuwa kwa kubahatisha tu kwa kuzingatia sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na ushirikiano wa kihistoria na wa muda mrefu kati ya Tanzania na Marekani tangu tupate uhuru mwaka 1961, na harakati zinazofanywa na serikali ili kujiletea maendeleo na ustawi wa watu wake.

Kwa muda mrefu, Tanzania imekuwa ikifanya jitihada kubwa ili kujiletea maendeleo katika nyanja za kijamii, kiuchumi na kisiasa kwa kutekeleza mabadiliko mbalimbali ya kiuchumi tangu wakati wa utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa kufufua Uchumi, yaani National Economic Survival Program (NESP); Mpango wa Kurekebisha Uchumi, Structural Adjustment Program (SAP) na Economic Recovery Programs katika miaka ya 80, hadi mipango ya sasa kama vile Mpango wa Taifa wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini maarufu kama MKUKUTA.

Ushirika wetu anaouzungumzia Rais Obama, unajionyesha vizuri katika jitihada za pamoja katika masuala ya demokrasia, maendeleo ya kiuchumi, utulivu wa eneo letu na afya. Kwa mfano kuanzia mwaka 1995 hadi mwaka 2000, uwekezaji wa moja kwa moja wa Marekani hapa nchini ulifikia Dola za Marekani 26 milioni ambapo makampuni ya nchi hiyo yaliwekeza katika sekta za mawasiliano, kilimo, uchimbaji wa madini na utalii.

Kwa namna alivyoitaja Tanzania, Rais Barack Obama anatukumbusha kwa mara nyingine tena alichowahi kusema Balozi wa zamani wa Marekani hapa nchini, Mark Green alipokuwa anahitimisha kipindi chake. “Uwepo wa Marekani hapa nchini ni mpana na wa kina na tunategemea utabakia kama ulivyo katika utawala mpya wa Obama. Hatua tunazochukua kupambana na umaskini, zinaendeleza ukuaji wa uchumi kupitia misaada katika uzalishaji, usalama wa chakula, maendeleo ya miundombinu na mambo mengine muhimu ambayo serikali ya Tanzania imetuomba kufanya”, alisema Balozi Green.

Jiitihada katika kuleta mabadiliko ya uchumi na mapambano dhidi ya rushwa, zimeifanya Tanzania kupata sifa ya kuingizwa katika mpango wa kusamehewa madeni nchi maskini na zenye madeni zaidi duniani uitwao Highly Indebted Poor Countries (HIPC) Initiative unaofadhiliwa na Marekani. Mpango huo ni kwa ajili ya nchi zinazochukua hatua katika kufanya mabadiliko ya kiuchumi na kuelekeza rasilimali zinazopatikana kutokana na kusamehewa madeni kwenye mahitaji ya kipaumbele kama vile afya na elimu.

Marekani pia inaisaidia Tanzania katika nyanja za mazingira, demokrasia na maendeleo ya sekta binafsi. Hapana shaka kwamba mafanikio ya Tanzania katika nyanja za utawala bora, hali kadhalika, yameleta mvuto na kuwajengea imani washirika wetu. “Serikali ya Awamu ya Nne itatekeleza majukumu yake ya kiutawala na maendeleo na itajikita zaidi katika utawala bora na uwajibikaji, utawala wa sheria na kuheshimu haki za binadamu kwa watu wote”, alibainisha Rais Kikwete mapema alipolihutubia kwa mara ya kwanza Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwezi Desemba, 2005.

Kuimarishwa kwa vita dhidi ya rushwa kunakofanywa na Serikali ya Awamu ya Nne ambako kunajionyesha kupitia hatua mbalimbali zilizokwisha kuchukuliwa ikiwa ni pamoja na kuwezesha kutungwa kwa sheria mpya , Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya mwaka 2007, kunathibitisha zaidi mwelekeo wa mafanikio katika nyanja za utawala bora.

Ni ukweli ulio wazi kwamba mahali popote ambapo rushwa imeshamiri, amani, utulivu, usalama, uhuru, usawa na haki vinakuwa hatarini. Vita dhidi ya rushwa hapa nchini inatekelezwa kupitia Mkakati wa Taifa wa Kupambana na Rushwa na Mpango wa Utekelezaji (NACSAP).

Katika mazingira ya sasa ambapo dunia inakabiliwa na mgogoro mkubwa wa kifedha, Tanzaania inafanya jitihada kubwa kuimarisha sekta ya fedha ambayo lengo lake mahsusi ni kuhakikisha kukua kwa kiwango cha utoaji wa mikopo cha sekta hiyo na kupunguza mfumko wa bei. Msisitizo, hali kadhalika, umeelekezwa katika kuendeleza utulivu katika mfumo wa mabenki kwa kuimarisha usimamizi hususan usimamizi unaozingatia tahadhari, kuimarisha mfumo wa malipo na kuendeleza ufanisi katika sekta ya fedha.

Ni kama ilivyotumwa kwetu toka kwa wakuu huko juu (mnajua wapi). Haija-haririwa!
 
Ukweli ubaki palepale na lazima tuujue kwamba hawa jamaa hawana Rafiki wala Adui wa kudumu, wapo kwa interest tu. Tanzania sasa tunaingia kwenye ramani ya dunia kwenye maswala ya uranium deposits and mining. Kwa hiyo nchi kama Marekani lazima awe karibu ili ana monitor hiyo uranium yote inaenda wapi na kufanya nini.

Pili kuna resource kubwa ya mafuta na natural gas hapa Tanzania ambazo pia ni kitu muhimu sana hasa kwa nchi za magharibi ambazo sasa zinaanza kupata ugumu ku-access hiyo energy source from nchi za kiarabu.

Dalili hizo za Marekani sio nzuri kabisa, ukiona hivyo ujue na vita imekaribia
 
Hii habari ni kweli inamaanisha au ndoto za mchana tu za hao watu toka juu. Maana inaonyeshwa imeandikwa na mtu aliye kuwa brain washed kabisa! Hii Tanzania ya 'Obama' ndio hii yetu kweli!
 
"Rais wa Marekani, Barack Obama, muda mfupi kabla ya kufanyika kwa Mkutano wa Kundi la Nchi 20 maarufu kama G20 Jijini London ambao yeye mwenyewe alihudhuria, aliandika makala iliyopewa kichwa cha habari “Ni Muda wa Mabadiliko kwa Dunia”, ambayo inatoa tahadhari kuhusu changamoto mbalimbali za kiuchumi zinazozikabili nchi duniani. "

Can we have a source to find this article (makala) please? Au ndo habari za kutunga hizi?
 
"Rais wa Marekani, Barack Obama, muda mfupi kabla ya kufanyika kwa Mkutano wa Kundi la Nchi 20 maarufu kama G20 Jijini London ambao yeye mwenyewe alihudhuria, aliandika makala iliyopewa kichwa cha habari “Ni Muda wa Mabadiliko kwa Dunia”, ambayo inatoa tahadhari kuhusu changamoto mbalimbali za kiuchumi zinazozikabili nchi duniani. "

Can we have a source to find this article (makala) please? Au ndo habari za kutunga hizi?
Mkuu,

Hii imetoka State House yetu... Imesambazwa kwa vyombo vya habari. Nikaiweka bila kuongeza wala kupunguza neno, nimerekebisha spellings tu!
 
Invisible,

..kwanini wasi-distribute makala aliyoandika Obama tuisome na kuipima wenyewe?
 
Wamarekani washukuru sana Kikwete kachukua nchi, angechukua Salim wangelia tu.
 
Status
Not open for further replies.
Back
Top Bottom