Makala Ndani ya RAIA MWEMA: "Ndimi mbili za Zitto na kisa cha mkata kuti alilokalia"

Mzalendo_Mwandamizi

JF-Expert Member
Dec 12, 2007
1,117
4,764
Ndimi mbili za Zitto na kisa cha mkata kuti alilokalia

Evarist Chahali

Uskochi
Toleo la 262
10 Oct 2012


MIONGONI mwa faida ninazopata kutokana na uandishi wa makala katika jarida hili maridhawa, ni mawasiliano ya kila wiki na baadhi ya Watanzania wenzangu. Wengi wa ninaowasiliana nao, ni wasomaji ambao kwa namna moja au nyingine huwa wameguswa na mada ninazoongelea. Kuguswa huko hufuatiwa na ama pongezi au kukosolewa. Wakati mara nyingi pongezi huandamana na maneno ambayo si tu yananipa moyo na ujasiri zaidi wa kuendelea na uandishi wa makala hizi, mara nyingi kukosolewa huambatana na maneno yasiyopendeza kuyasoma au kuyasikia popote pale.

Baadhi ya wanaopongeza safu hii hudiriki kwenda mbali zaidi na kushauri labda nifikirie kuingia kwenye siasa. Mara zote jibu langu huwa lile lile. Najisikia fahari kuwatumikia Watanzania wenzangu kupitia uandishi wa makala, huku nikiamini kuwa si lazima kuwa mwanasiasa ili uweze kutekeleza jukumu hilo ipasavyo.

Lakini kwa upande mwingine, baadhi ya wanaonikosoa huenda mbali zaidi na kunituhumu kuwa uandishi wangu umeelemea kwenye chuki binafsi, husda na vitu kama hivyo. Jamaa mmoja alifikia hatua ya kudai kuwa makala zangu ni sehemu tu ya mikakati wa dini yangu dhidi ya utawala unaoongozwa na mtu anayetoka dini tofauti na yangu.

Kama ambavyo ninaridhishwa na pongezi kuhusu safu hii, huwa ninajifunza jambo moja au jingine kutoka kwa wakosoaji wangu (wengi wao hupenda kuhifadhi majina yao halisi). Kukosolewa huko, kunanisaidia kwa kiasi fulani, na hasa tukizingatia ukweli kwamba ukiona unamwagiwa sifa tu pasipo kuelezwa japo kasoro kidogo, basi yayumkinika kuhisi kuwa kuna mushkeli mahala fulani.

Nimelazimika kuandika hayo kutokana na ukweli kwamba makala yangu katika toleo lililopita ambayo pamoja na mambo mengine ilimzungumzia mbunge wa Kigoma Kaskazini kupitia CHADEMA, Zitto Zuberi Kabwe, imetafsiriwa na baadhi ya wasomaji wangu kama sehemu ya kampeni zangu za kumkwamisha kuingia ‘Ikulu.’

Nimeshaeleza mara kadhaa katika baadhi ya makala zangu zilizopita kuwa mimi si mwanachama wa chama chochote kile cha siasa, na nimekuwa hivyo kwa miaka kadhaa, tangu nikiwa huko nyumbani. Wakati, kwa kiasi kikubwa nilipokuwa huko nyumbani sheria ilikuwa inanikataza kuwa mwanachama wa chama chochote cha siasa, kwa sasa uamuzi wangu wa kuwa neutral unachangiwa zaidi na imani yangu kuwa itikadi bora zaidi kwa mwananchi ni uzalendo na kuitumikia jamii kwa hali na mali.

Moja ya sifa kuu za sheria, ni kwamba iwe mbaya au nzuri, inabaki kuwa sheria hadi itakaporekebishwa au kuondolewa. Kuna nyakati tunalazimika kufuata sheria zinazokinzana na haki zetu (kimsingi sheria inapaswa kuendana na uwiano kati ya haki na wajibu), lakini tunalazimika kuzifuata kwa vile ndizo sheria zinazotawala.

Ni kwa mantiki hiyo, ninarejea tena kutofautiana na Zitto katika dhamira yake ya kutaka kuwa Rais wa Tanzania, kwa sababu kwa mujibu wa sheria tulizonazo, hatokuwa na sifa ya urais hapo mwaka 2015 kutokana na kuwa na umri pungufu ya ule unaotajwa kwenye sheria mama ya nchi, yaani Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Ninaafikiana na Zitto kwamba sheria hii ni ya kionevu kwa sababu kama inawezekana kwa mtu wa miaka 40 kuwa Rais kwanini ishindikane kwa mtu mwenye miaka 39?

Hata hivyo, napenda kumfahamisha kuwa hadi hapo sheria hiyo itakaporekebishwa au kubadilishwa, pamoja na ‘ubaguzi’ inaoubeba, itaendelea kuwa sheria inayopaswa kufuatwa. Na kwa vile kwa mazingira ya kawaida tu inatarajiwa Rais kuwa miongoni mwa vinara wa si tu kufuata sheria, bali pia kuzilinda, itakuwa ni ‘utani mbaya’ kwa mtu anayetaka kuwa Rais kudhamiria kuvunja sheria kama hiyo inayokataza walio chini ya miaka 40 kugombea urais.
Nimesema ninamuunga mkono Zitto kwamba sheria hiyo ni ya kibaguzi. Lakini kama tunachukia ubaguzi kwenye sheria, basi pia tunapaswa kuchukia ubaguzi kwenye kila eneo, iwe kwenye jinsia, imani, asili, rangi na hata kundi la mtu katika jamii. Siku chache zilizopita, kulikuwa na taarifa za kwamba Zitto aliongea na kituo kimoja cha redio jijini Dar es Salaam na kutamka maneno yafuatayo:

“Wazee wetu walitusaidia sana kutupatia maendeleo ya kisiasa, sasa ni jukumu letu kuleta maendeleo ya kiuchumi. Ila naomba nisisitize kuwa jukumu hilo haliwezi kutekelezwa na mtu yeyote aliyezaliwa kabla ya uhuru, na ninatangaza nitagombea urais mwaka 2015.”

Binafsi, ninahitimisha kuwa kauli hiyo ni ya ubaguzi wa mchana kweupe. Lakini pia, licha ya ubaguzi, inaonekana kichekesho kwani imetoka kwa mwanasiasa (Zitto) ambaye hajawahi kuficha hisia zake dhidi ya ubaguzi wa watu kwa vigezo vya umri. Tukiweka kando taratibu za ndani ya CHADEMA kupata mgombea wake, moja ya sababu kuu zinazoonekana kama kikwazo kwa dhamira ya Zitto kuwa Rais, ni hiyo tuliyoiongelea hapo juu ya kutotimiza umri wa miaka 40 mwaka 2015 kama inavyotajwa kwenye Katiba.

Tunaomsapoti Zitto katika hoja yake hiyo, tunazingatia ukweli kwamba japo nchi haiwezi kuongozwa na mtoto wa miaka mitano, kwa mfano, mtu yeyote mzima (kiumri) anaweza kuiongoza nchi yetu pasipo umri wake kuathiri utendaji kazi wake. Utu-uzima si umri maalumu bali masafa (range) ya umri. Utu-uzima unaendana zaidi na uwezo wa mtu kutambua wajibu wake na kumudu kuutekeleza.

Wajibu huo unaweza kuwa katika ngazi ya familia (kama vile kuoa/kuolewa) au katika jamii pana, kama vile kushika dhamana ya uongozi.

Kwa hiyo, kimsingi, kama Zitto amemudu kuwatumikia wapigakura wa jimbo la Kigoma Kaskazini kwa mihula miwili sasa, sambamba na kulitumikia taifa kupitia uenyekiti wake kwenye Kamati ya Bunge, basi hakuna sababu ya msingi kwa umri wake kuwa kigezo cha kumzuwia kugombea urais mwaka 2015 hata kama atakuwa hajatimiza miaka 40. Ndiyo. Katiba inazuwia, lakini ukweli ni kuwa inazuwia kiuonevu!

Sasa wakati tunaafikiana na Zitto kupingana na uonevu huo wa Katiba, inakuwaje tena anatumia kigezo cha umri kuwabagua ‘wazee’ anaodai hawawezi kutuletea maendeleo ya kiuchumi? Busara ndogo tu ingeweza kumfahamisha Zitto-kama msomi-kuwa siasa na uchumi ni maeneo yanayotegemeana. Kama wazee waliozaliwa kabla ya Uhuru walimudu kutuletea maendeleo ya kisiasa, kwanini washindwe kwenye maendeleo ya kiuchumi?

Kama yeye aliyezaliwa baada ya Uhuru ameweza kufanya kazi nzuri kabisa katika uongozi wake wab kisiasa, ni kigezo kipi anachotumia kuwaona wazee waliozaliwa kabla ya Uhuru kuwa hawatoweza harakati za kuleta maendeleo yetu? Kwa hakika kabisa, huu ni ubaguzi, na kamwe mtu mwenye hisia za ubaguzi hapaswi japo kufikiriwa kuongoza nchi yetu.

Ninasema hivyo kwa sababu kama alivyotuusia Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ubaguzi huzaa ubaguzi. Leo itakuwa “wazee waaliozaliwa kabla ya Uhuru hawawezi kutuletea maendeleo ya kiuchumi,” kesho itakuwa “Wakristo/Waislamu hawawezi kufanya hili,” “Wapogoro hawawezi kufanya lile,” au “wanawake hawawezi jukumu Fulani na kadhalika.

Naomba nimpe darasa dogo tu Mheshimiwa Zitto kuhusu kikwazo halisi cha maendeleo yetu. Uhaba unaozidi kukua katika uzalendo wa Mtanzania. Uzalendo hauna umri. Historia inatufundisha mengi tu kuhusu mchango wa wazee katika maendeleo ya sehemu zao husika. Mwalimu Nyerere, Nelson Mandela, Mahatma Ghandhi na kadhalika.

Binafsi, niliwahi kupishana kimtizamo na Zitto kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter, ambapo katika hali ya kuchokoza mjadala, nilitamka kuwa muundo wa Tume ya Kuratibu Maoni ya Katiba haukuzingatia uwiano kati ya Wakristo na Waislam. Zitto alikerwa sana na hoja yangu hiyo aliyoiita ya kibaguzi. Alisisitiza kuwa tunapaswa kuangalia wasifu wa wajumbe kwa kigezo cha uwezo na uzoefu wao na si imani zao za kidini.

Cha kushangaza, ndani ya miezi michache tu, mtu huyo huyo aliyekemea vikali virusi vya ubaguzi (wa dini), amegeuka mfuasi wa ubaguzi wa umri. Kama tunapojadili teuzi mbalimbali tunapaswa kuangalia uwezo na uzoefu wa mteuliwa, kwanini basi wazee waliozaliwa kabla ya Uhuru wasitizamwe kwa uwezo na uzoefu wao kutuletea maendeleo ya kiuchumi, badala ya kuwahukumu kwa umri wao?

Ninaibua changamoto kama hiyo ya ‘ubaguzi’ kwa minajili, si ya kukwaza dhamira ya Zitto kuingia Ikulu mwaka 2015, bali kumsaidia kuamsha tafakuri yake iwapo utekelezaji wa dhamira hiyo utakuwa na manufaa kwake na kwa chama chake, au utaishia kuwa njia ya mkato kwa CCM kurejea madarakani huku CHADEMA ikiishia kuonekana chama cha mapambano kati ya vijana na wazee kukimbilia Ikulu.

Nimalizie makala haya kwa kukumbushia tena kauli ya Baba wa Taifa, ya kwamba yatupasa kuwaogopa kama ukoma wale wote wanaokimbilia Ikulu. Kama sisi wengine tunaweza kuitumikia nchi yetu kupitia makala zetu, huku wanasiasa kama Zitto wakimudu kututumikia kama wabunge, kisa cha kukimbilia Ikulu ambako Mwalimu alituasa kuwa anayefanya hivyo aogopwe kama ukoma, ni cha nini?

Simshawishi Zitto aachane na ndoto zake za urais kwani ninatambua hiyo ni haki yake ya kidemokrasia. Hata hivyo, ni muhimu kwa mwanasiasa huyo kijana kutambua kuwa wapenda mabadiliko ya kweli watamwona kama msaliti pindi ndoto zake hizo zitakapoishia kuwa kikwazo kwa CHADEMA kuing’oa CCM madarakani. Japo busara zinatueleza kuwa na ndoto pekee haitoshi, bali ni muhimu kutekeleza ndoto hizo kwa vitendo, ukiota unakata kuti unalokalia, na ukiamka ukaamua kulikata, sote tunajua matokeo yake.








 
Umempa kweli ila zzt atapingana na wewe kwa kile anachokiita hoja yako ni dhaifu tena dhaifu sana.
 
Ubaguzi wa zitto, ni kuishiwa ajenda na kuanguka kisiasa. Chadema wapo ktk mapambano ya kuishambulia ccm, cha ajabu wanatokea watu miongoni wanaanza kuwashambulia. Kwa hila na pesa wanasahau walipoanzia safari.
 
Naamini kwa %100, zzt anatumika na magamba anajua kabisa akileta chokocho za kugombea urais ataleta makundi ndani ya chama hivyo kukisambaratisha.
 
kweli ni haki ya zito kutangaza nia, ila ikiwa anahiden agenda atakuwa anakosea sana na atarudisha nyuma harakati za CHADEMA kupigania mackini. bro zito fikiria sana kuhusu haya
 
kweli ni haki ya zito kutangaza nia, ila ikiwa anahiden agenda atakuwa anakosea sana na atarudisha nyuma harakati za CHADEMA kupigania mackini. bro zito fikiria sana kuhusu haya

Mimi kuna kitu sikielewi, nguvu za kumpinga Zitto in running for Presidency zinatumika kubwa sana kuliko kawaida. Kuna vitu Zitto alistipulate ktk ambition yake kama nakumbuka vzr, among others alisema, "Endapo Chama chake (CHADEMA) kitampa ridhaa ya yeye kupeperusha Bendera hiyo". Nikienda mbali zaidi alisema pia asipopewa hiyo ridhaa he won't mind, atampigia kampeni atakayesimamishwa kugombea huo Urais... Sasa, kwanini tusikiachie chama kiamue na wanachama wake? Why are we putting a lot of efforts kwa kumshambulia? Mbona hatuongelei hizo issue zingine alizozitoa? Maana ni conditional ambition ambayo yeye ameitoa.
Demokrasia ina pillars kadhaa, mojawapo ni ya media kuandika na kupeleka habari kwa wananchi. Media tukiitumia vby ina implications zake as well. Tutumie media kwa vitu ambavyo vinamatter zaidi kwa wakati huu. Kuna issues nyingi sana wananchi hawazijui, tuwaelimishe haki zao wazijue, tuwaelimishe katiba iliyopo, na ikiwezekana tuichambue vzr kabisa paragraph by paragraph, tuwasaidie waparticipate vzr katika mchakato wa katiba mpya maana hata hawaifahamu hiyo ya zamani. Na vitu kama hivyo. Nawasilisha hoja.
 
Nimechoka na habari za ZITTO,ZITTO,kila siku,si mumfukuze kama hamumtaki? Wachaga bana!! Ningewaona wamaana sana tungepigania ktk KATIBA kupunguzwa kwa adhabu kwa wale wanaofumaniwa manake wana toza mapesa mengi na ng'ombe wengi.tunaumia.
 
Nimeipenda makala hii,lakini ninavyoamini mimi,ni kwamba sheria ya kuwa na 40 years kabla ya kugombea urais,sidhani kama iliwekwa kwa misingi misingi ya ubaguzi,lakini ninaamini kwamba kauli ya Zitto ndiyo ilikuwa ya kibaguzi.
 

Similar Discussions

2 Reactions
Reply
Back
Top Bottom