JamiiTalks Mahojiano ya moja kwa moja na Mhe. Zitto Zuberi Kabwe katika JamiiForums

Status
Not open for further replies.
Najua msimamo wa Chama chako juu ya posho ni kuzipinga, je Chama chako kinatekelezaje msimamo huo kwa vitendo?
Naomba swali hili aulizwe Msemaji wa Chama Bungeni ambaye ni Kiongozi wa Upinzani Bungeni. Mimi ninajisemea binafsi. Ninatekeleza msimamo huu kivitendo. Sipokei posho za vikao Bungeni na mahala popote ambapo ninahudhuria vikao kama sehemu ya kazi yangu. ( huu ni mfano wa namna ninavyokataa posho #1 Say NO to Posho! « Zitto na Demokrasia)

Posho za vikao ni wizi wa fedha za umma. Posho za vikao ni moja ya dalili za mfumo unaoitwa ‘rent seeking ' au Pato-nyemelea. Huu ni mfumo wa kujipatia kipato bila kufanyia kazi. Wabunge wamechaguliwa kwa kazi maalumu na tunalipwa mshahara na marurupu mengine kwa kazi hii. Kulipwa posho ya kukaa kitako ni kujipatia kipato bila kufanyia kazi. Wabunge wanakuwa kama genge la majambazi yanayovamia benki na kuiba! Kwa kuwa mfumo unatoa nguvu kwa wabunge, basi hawatumii silaha, bali wanatumia mfumo kujilimbikizia mali. Sitting allowances ni uporaji.
Je, katika suala hili ulipata ushirikiano wa kutosha toka kwa wapinzani wenzako bungeni?
Ndio maana tulikaa kikao na kuamua kuandika barua kwa Spika ili atupe fomu nyingine za mahudhurio na nyingine za posho. Hajafanya hivyo na mimi siandiki mahudhurio. Mimi kama Waziri kivuli wa Fedha nilikuwa nazungumzia na kutekeleza msimamo wa kukataa posho kama sehemu ya kazi yangu. Ndio mandate yangu. I walked the talk. Wengine watajisemea wenyewe maana mimi sio msemaji wao na wala sio msemaji wa Wabunge wa upinzani.

Je, ulipata ushirikiano wa kiwango gani toka kwa Wabunge wa CCM?
Mbunge pekee wa CCM aliyekuwa na msimamo kama wangu ni ndugu Januari Makamba. Alishambuliwa sana kwenye chama chake lakini alisimama kidete. Nafurahi kuona wabunge vijana kama hawa ambao wanaleta aina mpya ya siasa. Ninamtakia kila la kheri. Ndugu Filikunjombe alinipa moyo sana kuhusu suala hili lakini sikumbuki kama naye aliacha kuchukua posho. But he was on my side all the time. January najua alikataa kuchukua posho. Wengine sijui.
Je, hadi sasa hupokei posho za vikao?
Sipokei posho ya kikao (sitting allowances) na sitapokea posho hiyo katika kipindi chote ambacho mimi ni Mbunge. Nikiwa Rais moja wa uamuzi wangu wa kwanza utakuwa ni kufuta posho za aina hii kwenye Serikali nzima. Nisipokuwa Rais nitamshawishi Rais atakayekuja afute posho hizi na kuelekeza fedha tutakazookoa kwenye kuondoa umasikini vijijini.
 
Duh.. Genuinely nijuavyo mimi ni kuwa ulishawahi wakilisha suala la ku ‘bannish' posho, ila sikujua wala sikutegemea kuwa toka hapo HUJAWAHI na wala HUCHUKUI Posho.

Nashauri viongozi wote wa CDM mliangalie hili kwa undani, itatia moyo kuwa bado kuna viongozi Wazalendo

Swali lifuatalo ni eneo lako of Great Interest tokana na jitihada zako hapo;

M: Umeme na Gesi


  1. Una maoni gani kuhusiana na hali ya umeme nchini kwa wakati huu? Itaichukua Tanzania miaka mingapi kuwa na uhakika wa upatikanaji wa nishati ya umeme?
  2. Pia uliposema mikataba iwekwe wazi, ulikuwa na maana gani? Ulimaanisha ikiwekwa wazi hata sisi wananchi wa kawaida tutaweza kuiona ama ulimaanisha iwe wazi kwa wabunge peke yake?
  3. Una maoni gani juu ya sera ya Nishati ya Gesi kutafsiriwa kwa Kiswahili?
 
Una maoni gani kuhusiana na hali ya umeme nchini kwa wakati huu? Itaichukua Tanzania miaka mingapi kuwa na uhakika wa upatikanaji wa nishati ya umeme?
Nimekuwa nikitoa maoni yangu kuhusu suala la nishati ya Umeme nchini toka nimekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya POAC. Suala hili wakati mmoja lilitaka kunimaliza kabisa kisiasa kwani msimamo niliochukua niliamua ni msimamo mzuri lakini haukupendwa na wengi ( Sakata la Ununuzi wa Mitambo ya Dowans: Barua ya Zitto kwa Watanzania ).

Bila nishati ya umeme ya uhakika hatuwezi kabisa kukuza uchumi na kuondoa umasikini nchini. Serikali ikiamua baada ya miaka 3 hatutakuwa na tatizo la umeme. Serikali itulize akili kuhakikisha miradi ya Kiwira, mchuchuma na Liganga na mradi wa bomba la gesi unakamilika. Lakini pia Serikali isiwe kigingi cha players wengine kwenye sekta ya umeme na hasa uzalishaji. Serikali ingejikita sana kwenye kusamabza miundombinu na kuruhusu watu binafsi kuzalisha umeme mwingi. Hata hivyo suala la mikataba ya kununua umeme (PPAs) inabidi kuangaliwa vizuri maana mingi inanyonya nchi. Huko tuendako mikataba yote ya aina hii iwekwe wazi kama njia ya kuepuka ufisadi na kuimarisha uwajibikaji. Tanzania inaweza kuwa net energy exporter in the region. Uamuzi ni wetu.

Pia uliposema mikataba iwekwe wazi, ulikuwa na maana gani? Ulimaanisha ikiwekwa wazi hata sisi wananchi wa kawaida tutaweza kuiona ama ulimaanisha iwe wazi kwa wabunge peke yake?

Mikataba iwe wazi kwa wananchi kuweza kuona wakati wowote. Pia itengenezwe nakala za lugha rahisi ili wananchi wa kutoka kwenye maeneo yenye gesi wajue ni nini haki zao na nini wajibu wao. Uwazi wa Mikataba ni silaha kubwa sana ya kupambana na uporaji wa mali asili ya nchi. Uporaji mbaya zaidi ni uporaji dhidi ya kizazi kijacho. Sitaki watoto wetu waje kwenye makaburi yetu kutulaani bali kutuombea dua. USIRI unalea ufisadi.

Kama ni wabunge peke yake ndio waone mikataba hii, hilo litaleta utofauti gani kwenye bunge ambalo wabunge wake wanapiga kura za maamuzi kutokana na chama na si maslahi ya taifa?

Una maoni gani juu ya sera ya Nishati ya Gesi kutafsiriwa kwa Kiswahili?
Tulitoa kauli kupitia Waziri wetu kivuli wa Nishati kuwa Sera ya Gesi iwekwe kwa lugha ya Kiswahili. Imewekwa. Natoa wito kwa watanzania wajadili na kutoa maoni namna ya kuhakikisha kuwa gesi inakuwa kwa maendeleo ya nchi na sio kwa ajili ya watu wachache.

Kwa ujumla nimeandika sana kuhusu suala la mafuta na gesi. Makala hii ( https://zittokabwe.wordpress.com/tag/tanzania-oil-and-gas-sector-2/) inaweza kusaidia ufahamu wa sekta hii na mwono wangu kama Mtanzania. Pia unaweza kwenda kwenye blog yangu utakuta blogposts nyingi sana kuhusu suala hili.

Napenda kuona Tanzania inakuwa nchi ya kupigwa mfano duniani kwa namna ilivyotumia utajiri wake wa gesi na Mafuta. Sitaki turudie makosa tuliyoyafanya kwenye sekta ya Madini. Nitaendelea kufuatilia kwa karibu sana sekta ndogo ya gesi na nitakuwa muwazi sana ili kuzuia 'a nigeria' in Tanzania.
 
Mkuu Zitto asante kwa majibu, swali linalofuata lina wadau wengi sana waliouliza na wana interest ya kujua kwa hamu kabisa, idadi ya JF members waliowakilisha ikitoa picha ni kwa kiasi gani.

N: Zitto katika Uongozi/Ubunge na Urais 2015


Katika kipengele hiki, kinachogusa watanzania ni nia yako ya kugombea urais ambapo tayari katika vyombo mbalimbali umeshanukuliwa ukitoa msimamo wako juu ya kuwa na nia ya kugombea Urais (kwa tiketi ya CHADEMA?) 2015. Inaaminika pia wewe ni mmoja wa Wabunge waliokubaliana na mapendekezo ya moja ya kipengele kati ya vipengele vilivyowasilishwa na wabunge mapema mwezi huu wa Novemba kwa tume ya katiba juu ya kushusha umri wa kugombea urais na kuwa kati ya miaka 35-40 kati ya mengine mengi yaliowakilishwa.

Umesikika pia kwa kunukuliwa na vyombo vya habari juu ya niya yako ya kutokuwa na nia tena ya kugombea Ubunge 2015 Kigoma ama popote pale.

Kwa maelezo hapo juu, naomba ujibu maswali yafuatayo:

  1. Naomba kujua ni kwanini hasa umekuwa na uamuzi wa kuachana kabisa na Ubunge na kutogombea tena; na kama hayo ni maamuzi yako na hujaeshinikizwa na kitu ama mtu yeyote. Je utaendeshaje maisha yako ya kisiasa nje ya Bunge na nje ya taasisi ya Urais?
  2. CHADEMA kina utaratibu gani wa kutangaza nafasi za wagombea katika ngazi mbali mbali hasa ya urais?
  3. Katika moja ya ‘school of thought', inasemekana umetangaza haraka nia ya kugombea Urais kwa misingi ya kuwa Dr. Slaa hana tena mpango huo na kwamba nje ya Slaa huoni zaidi yako ambaye anaweza wakilisha vema. Unalizungumziaje hili mkuu?
  4. Ikitokea kuwa hujateuliwa na chama chako (CHADEMA) kugombea Urais 2015 kwa tiketi ya chama hicho, una nia ya kutafuta chama kingine kitakachokuruhusu kugombea nafasi hii ya Urais?
  5. Kabla ya uchaguzi wa 2010 ulishawahi tangaza kutogombea tena ubunge 2010; ni kitu gani kilifanya ubadilishe huo msimamo?
  6. Tokana na kauli yako hivi karibuni kuhusu kwamba Uongozi wa nchi hautakiwi kuwa mikononi mwa watanzania waliozaliwa kabla ya uhuru; Je kulikuwa na ulazima kutamka haya? Huoni kwamba iwapo utafanikiwa kuwa rais wa nchi yetu, urais wako unaweza kuja kutuletea generational conflicts (misuguano/migongano/mifarakano ya vizazi)?
 
Mkuu Zitto asante kwa majibu, swali linalofuata lina wadau wengi sana waliouliza na wana interest ya kujua kwa hamu kabisa, idadi ya Jf members waliowakilisha ikitoa picha ni kwa kiasi gani.

Zitto katika Uongozi/Ubunge na Urais 2015


Katika kipengele hiki, kinachogusa watanzania ni nia yako ya kugombea urais ambapo tayari katika vyombo mbalimbali umeshanukuliwa ukitoa msimamo wako juu ya kuwa na nia ya kugombea Urais (kwa tiketi ya CHADEMA?) 2015. Inaaminika pia wewe ni mmoja wa Wabunge waliokubaliana na mapendekezo ya moja ya kipengele kati ya vipengele vilivyowasilishwa na wabunge mapema mwezi huu wa Novemba kwa tume ya katiba juu ya kushusha umri wa kugombea urais na kuwa kati ya miaka 35-40 kati ya mengine mengi yaliowakilishwa.
Umesikika pia kwa kunukuliwa na vyombo vya habari juu ya niya yako ya kutokuwa na nia tena ya kugombea Ubunge 2015 Kigoma ama popote pale.
Kwa maelezo hapo juu, naomba ujibu maswali yafuatayo:

  1. Naomba kujua ni kwanini hasa umekuwa na uamuzi wa kuachana kabisa na Ubunge na kutogombea tena; na kama hayo ni maamuzi yako na hujaeshinikizwa na kitu ama mtu yeyote. Je utaendeshaje maisha yako ya kisiasa nje ya Bunge na nje ya taasisi ya Urais?
  2. CHADEMA kina utaratibu gani wa kutangaza nafasi za wagombea katika ngazi mbali mbali hasa ya urais?
  3. Katika moja ya ‘school of thought', inasemekana umetangaza haraka nia ya kugombea Urais kwa misingi ya kuwa Dr. Slaa hana tena mpango huo na kwamba nje ya Slaa huoni zaidi yako ambaye anaweza wakilisha vema. Unalizungumziaje hili mkuu?
  4. Ikitokea kuwa hujateuliwa na chama chako (CHADEMA) kugombea Urais 2015 kwa tiketi ya chama hicho, una nia ya kutafuta chama kingine kitakachokuruhusu kugombea nafasi hii ya Urais?
  5. Kabla ya uchaguzi wa 2010 ulishawahi tangaza kutogombea tena ubunge 2010; ni kitu gani kilifanya ubadilishe huo msimamo?
  6. Tokana na kauli yako hivi karibuni kuhusu kwamba Uongozi wa nchi hautakiwi kuwa mikononi mwa watanzania waliozaliwa kabla ya uhuru; Je kulikuwa na ulazima kutamka haya? Huoni kwamba iwapo utafanikiwa kuwa rais wa nchi yetu, urais wako unaweza kuja kutuletea generational conflicts (misuguano/migongano/mifarakano ya vizazi)?

Najua kuwa swali hili linasubiriwa na wengi sana na kila mtu anasema yake. Nitakayoyasema sio mapya sana. Lakini niyajibu tu.
 
Naomba kujua ni kwanini hasa umekuwa na uamuzi wa kuachana kabisa na Ubunge na kutogombea tena; na kama hayo ni maamuzi yako na hujaeshinikizwa na kitu ama mtu yeyote. Je utaendeshaje maisha yako ya kisiasa nje ya Bunge na nje ya taasisi ya Urais?

Wakati nagombea Ubunge mwaka 2005 niliwaambia wapigakura wangu kuwa nitakuwa Mbunge wao kwa vipindi viwili tu. Niliwaambia nina ndoto za kuja kuwa Rais wa nchi yetu baadaye. Hivyo haya ni makubaliano yangu na wapigakura wangu. Nia yangu ni kupisha wengine nao wakimbize kijiti cha maendeleo ya Jimbo letu na Mkoa wetu. Nimesema mara kwa mara kwamba ukiachana na siasa kazi ninayoipenda zaidi ni ualimu. Nitakapomaliza Ubunge na Urais nitakwenda kufundisha. Ninajiandaa vilivyo kwa suala hilo. Nitapenda kufanya tafiti, kusoma, kuandika na kufundisha. Hivi sasa tunaandaa mpango wa kuanzisha Chuo Kikuu cha Ziwa Tanganyika (Lake Tnaganyika University) mkoani Kigoma. Nitafurahi kama nitakuwa mmoja wa wahadhiri wa mwanzo wa chuo hiki kufundisha Watanzania Uchumi wa Rasilimali.


Sina wasiwasi pia wa kuendesha maisha maana mimi ni mwanachama wa NSSF, ninajichangia kwa hiari toka nilipoacha kazi katika Shirika la FES mwaka 2004. Ikifika mwaka 2015 nitakuwa nimetimiza &[HASHTAG]#8216[/HASHTAG];points' za kulipwa pensheni. Nashukuru kwamba nilikwepa ushawishi wa kujitoa kwenye mafao. Naamini nitaendesha maisha yangu kwa kazi za kufundisha, kuuza vitabu, consultancies na pensheni niliyojiwekea akiba.


CHADEMA kina utaratibu gani wa kutangaza nafasi za wagombea katika ngazi mbali mbali hasa ya urais?

Chama chetu hakina utaratibu wowote hivi sasa wa kutangaza nia za watu kutaka kugombea nafasi yeyote. Juzi tumekutana Morogoro na kukubaliana kuwa tutatengeneza utaratibu wa watu kutangaza nia zao wanapootaka kugombea nafasi yeyote ya uongozi. Nadhani huu ni uamuzi mzuri wa chama maana kuna watu wana wasiwasi usio na msingi kabisa kuwa kuwa na wagombea wengi kwenye chama ni kuvuruga chama. Lakini watu hao hao wanashangilia kweli wakiona demokrasia inavyotekelezwa kwenye nchi nyingine kama Marekani. Watanzania wanapenda kuona demokrasia inatekelezwa lakini wanaogopa kuitekeleza wao. Uamuzi wa Morogoro kuhusu mwongozo kwa wagombea utatusaidia sana kuondoa mashaka kama haya.


Katika moja ya &[HASHTAG]#8216[/HASHTAG];school of thought', inasemekana umetangaza haraka nia ya kugombea Urais kwa misingi ya kuwa Dr. Slaa hana tena mpango huo na kwamba nje ya Slaa huoni zaidi yako ambaye anaweza wakilisha vema. Unalizungumziaje hili mkuu?

Slaa hakuwahi kutangaza nia ya kugombea Urais wakati wowote ule wa maisha yake. Mwaka 2010 Tulimwomba kama chama. Chama kinaweza kumwomba tena na tukifikia mwafaka ndio atakuwa huyo na sote lazima tumwunge mkono. Mimi nimetangaza kwa kuwa ninautaka Urais na hivyo nakiomba chama kiniteue. Pia chama kina viongozi wengine wazuri tu. Tundu Lissu na Mnyika wamesema hawautaki Urais. Ndugu Mbowe yeye hajasema kama anautaka au la. Kumbuka hata mwaka 2005 Mbowe tulimlazimisha, yeye alitaka aendelee kuwa Mbunge wa Hai. Sisi tukamwambia kuwa lazima abebe chama. Nakumbuka mimi binafsi niligombana naye maana aliposema yeye atagombea Hai, nikamwuliza kwa chama gani? Maana kama hutaki kukibeba chama kwenye Urais tutachukua kadi yetu. Ndio! Nilimwambia hivyo kwenye secretariat ya chama. Akakasirika kweli, lakini baadaye alinielewa na mafanikio tuliyoyapata ni makubwa sana baada yeye kugombea. Kwa hiyo hiyo School of Thought ni hisia tu za watu. CHADEMA ina watu wengi sana wenye uwezo wa kuwa maRais. Kitila Mkumbo mnamwonaje? Au mpaka watu wawe Bungeni. Huyu ni hazina ya chama na nchi. Chama kinaweza kusema, Zitto hapana, mwunge mkono Kitila. Nitafanya hivyo. The Party deploys for or against your wishes and every member must oblige a JUST deployment. I will.


Ikitokea kuwa hujateuliwa na chama chako (CHADEMA) kugombea Urais 2015 kwa tiketi ya chama hicho, una nia ya kutafuta chama kingine kitakachokuruhusu kugombea nafasi hii ya Urais?

Nisipoteuliwa na chama kugombea Urais nitamfanyia kampeni mgombea atakayeteuliwa na chama. Siamini katika kuhama vyama ili kutimiza malengo ya kisiasa na ndio maana mimi sijawahi kuwa chama kingine chochote zaidi ya CHADEMA maisha yangu yote. Mwanasiasa anayehama vyama ili kupata uteuzi anafuata vyeo na sio muumini wa sera ya chama husika.Vile vile Urais kwangu mimi sio an end in itself, it is a means ya kuleta mabadiliko ya hali ya maisha katika nchi yetu. Kama ilivyokuwa kwa Ubunge, ambapo nimehudumia wananchi na kuleta mabadiliko makubwa sana ndani ya muda mfupi na sasa nataka kuachia wengine, Urais nao ni hivyo hivyo, kutaka kufanya transformation ya nchi yetu, radical transformation katika uchumi, siasa na jamii. Nataka kuionyesha dunia kuwa tunaweza kuondokana na umasikini in our life time. Sasa kama chama kina mtu mwingine mwenye mwona kama huu, mimi nitamuunga mkono na kumsaidia kuifanya kazi hii.

Kabla ya uchaguzi wa 2010 ulishawahi tangaza kutogombea tena ubunge 2010; ni kitu gani kilifanya ubadilishe huo msimamo?

Mwaka 2009 niliamua kuwa ni bora niache ubunge ili nifanye shahada yangu ya uzamivu na kasha nifanye machapisho. Unajua niliingia Ubunge nikiwa na umri wa miaka 29 tu. Kazi niliyofanya kwenye Bunge la Tisa ilikuwa inanizidi kimo kwa kweli. Nilikuta Bunge limelala sana. Lilikuwa Bunge la status quo. Halikuwa Bunge vibrant kabisa. Siku ya kwanza tu nimeingia Bungeni sikulipenda. Hamu iliniisha. Lakini nikasema ngoja nibadili modus operandi ya Bunge. Nikaanza kutoa hoja kali kali Bungeni na hatimaye nikasimamishwa Bunge. Nafurahi kwamba Wabunge wengine walifuata kasi yangu. Mnakumbuka kuna wabunge walikuwa wanasema &[HASHTAG]#8216[/HASHTAG];hatuwezi kumwachia Zitto Kabwe peke yake kazi ya kuibua ufisadi' nk. Sasa baada ya kuona nimefanikiwa nikasema basi term moja inatosha. Badaye nikapata ushawishi kuwa hapana, nenda Geita au Kahama au Kinondoni. Nikafanya utafiti wangu nikaona mwenyewe kuwa niende Geita. Viongozi wa chama kutoka Geita wakaenda kuwaona wenzao Kigoma wakakataliwa. Wazee wakanikumbusha kuwa, makubaliano yetu yalikuwa mihula 2. Ikabidi nitimize ahadi hiyo ya mihula 2. Haikuwa matakwa yangu. Mpaka sasa nime abandon PHD yangu maana sina muda na siasa zangu mimi huwa naacha kila kitu kinacho weza kuni divert, hivyo nakosa muda wa kusoma na kuandika.


Tokana na kauli yako hivi karibuni kuhusu kwamba Uongozi wa nchi hautakiwi kuwa mikononi mwa watanzania waliozaliwa kabla ya uhuru; Je kulikuwa na ulazima kutamka haya? Huoni kwamba iwapo utafanikiwa kuwa rais wa nchi yetu, urais wako unaweza kuja kutuletea generational conflicts (misuguano/migongano/mifarakano ya vizazi)?

Mimi ninaamini kabisa kuwa Rais ajaye wa Tanzania ni lazima atokane na kizazi cha baada ya uhuru. Nchi inahitaji a fresh start. Misuguano ndio huleta maendeleo. Hebu tazama nchi hii, Asilimia 70 ya Watanzania wapo chini ya umri wa miaka 29! Asilimia 65 ya wapiga kura wapo kati ya umri wa miaka 18 &[HASHTAG]#8211[/HASHTAG]; 40. Hili ni Taifa la vijana. Nusu ya Watanzania wapo chini ya umri wa miaka 17! Unaweza kusema hili ni Taifa la watoto. Hawa wazee wetu walipokuwa wanachukua nchi walikuwa vijana. Mwalimu alikuwa Waziri Mkuu akiwa na miaka 39, Mzee Kawawa alikuwa Waziri Mkuu akiwa na miaka 37. Waziri Mkuu wakati huo ndio alikuwa Mkuu wa Serikali maana Mkuu wa nchi alikuwa Malkia wa Uingereza. Angalia mafanikio ya Mwalimu Nyerere na Kawawa kati ya mwaka 1961 na 1971 halafu pima na baada ya hapo mpaka wanastaafu. Tusibwabwaje tu bila evidence. Ndio maana leo Marekani Rais wao ni kijana. Uingereza Waziri Mkuu wao kijana ingawa mataifa haya yana wazee wengi zaidi kuliko sisi. Ninaweza kutamba kwamba mimi ni mmoja wa wanasiasa ambao ninaheshimu sana wazee. Uliza wazee waliopo na waliokuwapo Bungeni ni mwanasiasa gani kijana anatumia muda mwingi nao. Mwulize mzee Sarungi, bahati mbaya mzee Makwetta amefariki. Mwulize dokta Salim, mwulize Mzee Warioba. Wao pia wananiambia, Zitto huu ni wakati wenu. Sisi tulifanya yetu.


Kuna watu lazima watafsiri chochote atakachosema Zitto. Hata hili ninaloandika hapa mtasikia, watasema tu. Kuna watu wanaumwa ugonjwa wa zittophobiasis ni lazima waseme. Mtasikia tu wanasema hivi sasa. Sasa wanaotaka kutafsiri kauli yangu wana mambo yao, lakini ninaamini kabisa kuwa changamoto za sasa za Taifa zinahitaji Rais wa kizazi cha baada ya Uhuru. Wazee watatupa ushauri. This country has to move very fast. We need an ambitous young man, visionery and focused to transform this country. Tunaweza kuwa na Spika mzee ili adhibiti kasi kama inakwenda sana, lakini sio CEO wa nchi. How Old was Lumumba? How old was Kagame? How old is Kabila?


Let us be serious guys. Mnataka tutambae? Wazee wameishi maisha yao. Wameishi yetu na sasa tunataka kuwakopesha maisha ya watoto wetu?
 
Let us be serious guys. Mnataka tutambae? Wazee wameishi maisha yao. Wameishi yetu na sasa tunataka kuwakopesha maisha ya watoto wetu?

Ha ha ha! Hapa nimecheka literally! So funny in a sad way...

Mkuu Zitto swali linalofuata matata pia;

Zitto na "Ufisadi na Malimbikizi ya Mali" & "Pesa Uswisi
"

Hivi karibuni katika kikao cha bunge lililopita, ulitoa hoja ya msingi na nzito ya kulitaka bunge letu tukufu liunde tume kuchunguza tuhuma zinazowahusisha Watanzaia kuficha MABILIONI nchi za nje kinyume na utaratibu wa sharia za nchi yetu. Kufumba na kufumbua kuna taarifa iliyosikika katika vyombo mbalimbali na hata hapa hapa JF.

Serikali ya Uswisi ikitoa masharti kwa serikali ya Tanzania ili iweze kupatiwa orodha ya Watanzania wenye mabilioni katika nchi hiyo. Suala la fedha za Uswizi ni moja ya entity ambayo huleta changamoto sana katika fikra na namna ya kupokea kwa habari hizo dhidi ya wananchi, viongozi, vyombo vya habari na sekta mbali mbali. Kumekuwa na wale wanao kutetea kwa hatua yako ya kutotaja majina ya walio na fedha Uswizi na kuli-justify kwa kusema ni juhudi zako binafsi za kuyapata majina hivyo usihukumiwe/laumiwe kwa kwa kushindwa huko.

Juu ya hilo wewe mweyewe inasemekana ulishasema kuwa kupatikana kwa majina hayo ni jitihada zako binafsi kwa kigezo kuwa yalikuwa yakiuzwa kwa bei ya ghali kwenye CDs.

Na pia kwa kuongezea kuna wale ambao wametetea kuwa umetaja vyeo na nyakati za utawala wa hao wanao husishwa moja kwa moja na kashfa hiyo hivo ni sawa na kuwataja. Hili Mkuu Zitto ni moja ya eneo ambalo wengi wa members waliopo hapa JF kufuatilia huu mjadala wanataka sana majibu.

Tokana na hapo juu, nina maswali kadhaa kama ifuatavyo:-

  1. Unaposema kuwa ni jitihada zako mwenyewe za kupata hayo majina ya mafisadi wa Uswisi si inakuwa sawa na kuwa una maslahi yako binafsi kama vile kutaka kuyauza hayo majina kwa wale ambao wapo kwenye list?
  2. Unachukuliaje mawazo/kauli ya baadhi kuwa kuwasilisha kwako hoja hiyo ya fedha za Uswizi bungeni bila kutaja majina ni moja ya njia ya kujisafisha katika uvumi/tetesi ya kuwepo katika list hiyo ya wenye fedha Uswizi?
  3. Kuna ukweli wowote kuwa taarifa ile ya USWISI kuiwekea masharti Tanzania, ilitoka ndani ya serikali ya USWISI au ni mkakati wa mafisadi hawa kuzima jaribio la kurejesha pesa hizo?
  4. Je, kuna nafasi ya nchi yetu kufanikiwa kuyarejesha mabilioni hayo ambayo ni kodi ya wanachi?
  5. Ikumbukwe kuwa, tangu nchi hii itumbukie ktk ufisadi mkubwa, chombo chetu TISS kipo kama hakipo, na kama kipo basi ni kwa msaada wa mafisadi tu, Katika mtazamoo na tafsiri ya ripoti yako, taasisi ya Usalama wa Taifa (TISS) Unaiweka katika mizani ipi au haihusiki katika hili?
  6. Kwanini umependekeza kuundwa kwa tume, na kuendelea kumaliza pesa za watanzania wakati kimantiki ripoti yako ilikuwa ni ya kuiwasilisha vyombo vya dola tu, na ikiwa hawajaridhika, TAKUKURU kwa utaratibu wao wa ndani waendeshe uchunguzi na kuchukua hatua?
  7. Huku ukijua serikali haina nia ya kuwataja walioficha fedha mabenki ya nje huku wewe ukiwa na majina; unayashikilia hadi sasa ili nini na kwa faida ya nani?
  8. Yale majina ya baadhi ya watanzania unaowatuhumu kumiliki fedha haramu/halali (nyingi) nje ya nchi kwanini huyaweki bayana kwa umma? Wewe kama Mtanzania mzalendo na nchi yako kwanini umeshindwa (na chama chako) kuwapeleka mahakamani na kuwafungulia mashitaka?
  9. Kulikuwa na tetesi kuwa nawe umeficha fedha nje. Hii inaweza kulenga kukuchafua ili uwagwaye waliofanya hivyo, je huoni kuwa hii ni nafasi adimu ya kuondoa shaka? Tuondoe wasiwasi katika hili…
  10. Kwanini ulipeleka hoja binafsi ndani ya bunge na si kupitia uwakilishi wa upinzani? Je, umefanikiwa kwa kile alichotaraji kutokana na hoja hii? Uliungwa mkono na chama?
  11. Vipi, unauongeleaje ujenzi wa bandari ya Bagamoyo?
 
Unaposema kuwa ni jitihada zako mwenyewe za kupata hayo majina ya mafisadi wa Uswisi si inakuwa sawa na kuwa una maslahi yako binafsi kama vile kutaka kuyauza hayo majina kwa wale ambao wapo kwenye list?
Nadhani hivi ndivyo ungefanya wewe maana wakati mwingine watu hudhani vyao kwa wengine.

Unachukuliaje mawazo/kauli ya baadhi kuwa kuwasilisha kwako hoja hiyo ya fedha za Uswizi bungeni bila kutaja majina ni moja ya njia ya kujisafisha katika uvumi/tetesi ya kuwepo katika list hiyo ya wenye fedha Uswizi?
Kwangu mimi suala hili ni pana na majina ni sehemu tu ya suala hili. Nimeshasema mara kadhaa kwamba, nina akaunti mbili hapa nchini, CRDB na NMB. CRDB kwa ajili ya mshahara wangu na NMB kwa ajili ya fedha za kujikimu ninazolipwa na Bunge. Sio tu Uswisi, hapa Tanzania sina akaunti benki nyingine yeyote ukiachana na kuwa signatory kwenye akaunti za chama au za kifamilia.

Sina biashara yeyote hapa nchini au nje ya nchi. Naishi kwa mshahara na siwezi kuupeleka mshahara Uswisi. Waliosema mimi nina fedha huko Uswisi walikuwa na lengo la kufifiza hoja yangu kwa malengo yao. Ni watu waliotumwa na usalama wa Taifa au na wenye fedha ili niogope. Watu wa aina hii ni wapuuzi, wapumbavu na hatari sana kwenye vita dhidi ya ufisadi. Tena watu hawa mnawajua na mnawachekea. Hawa watu ni vibaraka wa watu fulani. Tena nasikia wametengeneza na orodha yao ya wenye fedha nje. Hawa ndio wagonjwa wa zittophobiasis. Nasikia wengine walisema kuwa hii hoja akiachiwa Zitto itampa umaarufu. Wapuuzi wanawaza umaarufu tu badala ya kuwaza nchi yetu.

Suala la utoroshwaji wa fedha kwenda nje ni kubwa sana. Tanzania imepoteza dola bilioni 11 toka mwaka 1970 mpaka sasa (ukiongeza na riba kwenye fedha hizo). Halafu kuna wapuuzi fulani wanaleta uzezeta kwenye masuala ya msingi ya nchi. Wanajijua ninaowasema hapa. Waache ujinga. Kama humpendi Zitto basi penda afanyacho kwa maslahi ya nchi yetu.

Kuna ukweli wowote kuwa taarifa ile ya USWISI kuiwekea masharti Tanzania, ilitoka ndani ya serikali ya USWISI au ni mkakati wa mafisadi hawa kuzima jaribio la kurejesha pesa hizo?
Nimetoa kauli jana kuhusu suala hili. Nimesema Watanzania tusiwe mazezeta. Kauli hizi ndio ambazo hata Marekani waliambiwa. Hata Ujerumani waliambiwa. Sisi kuzishabikia badala ya kufanya uchunguzi wetu kwa njia zetu ni dalili za kutaka kuua hoja hii. Hoja hii haitakufa. Tutaisimamia mpaka mwisho.

Je, kuna nafasi ya nchi yetu kufanikiwa kuyarejesha mabilioni hayo ambayo ni kodi ya wanachi?
Tunaweza kurejesha. Kuna Azimio la Bunge na nitahakikisha Azimio la Bunge linatekelezwa. Senegal wanafanikiwa sana. Kenya walifanikiwa kwa kutumia wachunguzi binafsi. Kama Serikali ya CCM itashindwa kufuatilia suala hili, Serikali ya CHADEMA itafanya hivyo. Hawana pa kujificha katika dunia ya sasa.

Ikumbukwe kuwa, tangu nchi hii itumbukie ktk ufisadi mkubwa, chombo chetu TISS kipo kama hakipo, na kama kipo basi ni kwa msaada wa mafisadi tu, Katika mtazamoo na tafsiri ya ripoti yako, taasisi ya Usalama wa Taifa (TISS) Unaiweka katika mizani ipi au haihusiki katika hili?
Idara ya Usalama wa Taifa ni lazima isaidie nchi kwenye masuala kama haya, vinginevyo hawapaswi kuwepo. Sheria ya TISS ya mwaka 1996 inawazuia kuchukua hatua fulani fulani. Tutarekebisha sheria hiyo. CCM wasiporekebisha sisi CHADEMA tutapata ridhaa ya wananchi kuiandika upya sheria ya Usalama wa Taifa. Tunataka usalama wa Taifa na sio usalama wa viongozi au vyama vya siasa.

Kwanini umependekeza kuundwa kwa tume, na kuendelea kumaliza pesa za watanzania wakati kimantiki ripoti yako ilikuwa ni ya kuiwasilisha vyombo vya dola tu, na ikiwa hawajaridhika, TAKUKURU kwa utaratibu wao wa ndani waendeshe uchunguzi na kuchukua hatua?
Uzuri wa Kamati Teule ya Bunge ni kwamba kila kitu huwa wazi kwenye hansards za Bunge na hivyo ni rahisi kufichua uchakachuaji. Pia ngoja niwamegee siasa za Bunge kidogo. Bungeni unapokuwa na hoja unaingia na hitaji kubwa sana wakati unajua fall back ni nini. Tulijua kwa hatua ya sasa hawatakubali kuundwa kwa kamati teule, tulitaka hoja ipite ili kujenga msingi wa kupanua uchunguzi siku za usoni. Tukafanikiwa. Tulitumia approach hiyo hiyo kwenye hoja ya ndugu Halima Mdee. Ni mikakati tu. Sisi tumekuwa ni Bunge la kwanza katika eneo la SADC kutoka na Azimio kuhusu 'illicit money flows'. Sasa tunapaswa kuhakikisha Azimio linakuwa enforced na kisha a public inquiry....

Huku ukijua serikali haina nia ya kuwataja walioficha fedha mabenki ya nje huku wewe ukiwa na majina; unayashikilia hadi sasa ili nini na kwa faida ya nani?
Kwa faida ya uchunguzi. Lazima Serikali ijenge uwezo wake wa kuchunguza na kuweka mambo sawa baada ya uchunguzi. Sasa ikiwa mimi kama mbunge nitatoa jina la walio torosha pesa kwa sasa, nani atatoa majina hapo kesho? Mbunge mpya wa Kigoma kaskazini?

Yale majina ya baadhi ya watanzania unaowatuhumu kumiliki fedha haramu/halali (nyingi) nje ya nchi kwanini huyaweki bayana kwa umma? Wewe kama Mtanzania mzalendo na nchi yako kwanini umeshindwa (na chama chako) kuwapeleka mahakamani na kuwafungulia mashitaka?
Uchunguzi bado unaendelea

Kulikuwa na tetesi kuwa nawe umeficha fedha nje. Hii inaweza kulenga kukuchafua ili uwagwaye waliofanya hivyo, je huoni kuwa hii ni nafasi adimu ya kuondoa shaka? Tuondoe wasiwasi katika hili…

Sina fedha za kuficha nje. Nazitoa wapi? Sina biashara naishi kwa mshahara wa ubunge, natoa wapi fedha za kuficha nje?
Kwanini ulipeleka hoja binafsi ndani ya bunge na si kupitia uwakilishi wa upinzani? Je, umefanikiwa kwa kile alichotaraji kutokana na hoja hii? Uliungwa mkono na chama?
Sijaelewa swali lako. Mimi ndio Waziri kivuli wa Kambi ya Upinzani kuhusu Fedha. Upinzani gani tena? Unadhani chama makini kama CHADEMA kinaweza kuacha mbunge wake apeleke hoja bungeni bila kuungwa mkono na chama? Wale wabunge waliosimama kuunga mkono niliposema 'naomba kutoa hoja' ni wabunge wa CHADEMA wale(isipokuwa ndugu Kessy na Kangi Lugola ambao ni CCM).

Vipi, unauongeleaje ujenzi wa bandari ya Bagamoyo?
Ni wazo zuri lakini lifuate mpango wa Ports Masterplan. Sio suala jipya hili.
 
Nimetoa kauli jana kuhusu suala hili. Nimesema Watanzania tusiwe mazezeta. Kauli hizi ndio ambazo hata Marekani waliambiwa. Hata Ujerumani waliambiwa. Sisi kuzishabikia badala ya kufanya uchunguzi wetu kwa njia zetu ni dalili za kutaka kuua hoja hii. Hoja hii haitakufa. Tutaisimamia mpaka mwisho.

Kwa wale ambao hawajaona hii makala iliyoguswa kipengele hiki naomba fuata hii Link kwa hisani ya Mkuu n00b https://www.jamiiforums.com/jukwaa-...ilioni-ya-uswisi-%96-tusigeuzwe-mazezeta.html

Mkuu kwa mara nyingine Asante kwa majibu yako. Swali linalofuata;

P: Zitto katika Maswali Mchanganyiko


  1. Nini uelewa wako kuhusu familia? Umeoa? Maana Kuishi au kuwa na mke siyo jambo jepesi, linahitaji uvumilivu na busara nyingi sana, kama vile ilivyo kuishi na mume. Kama hili limekushinda, vipi utaweza kuwaongoza watanzania wote wake kwa waume?
  2. Mkuu Zitto is there any chance unajua mshahara wa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mshahara wa makamu wa rais wa JMT, na ule wa rais wa Zanzibar? Ni mahala gani pa kwenda kufuatilia hizo data kwa yeyote yule anayetaka kufahamu hayo? Pia katika hili unadhani ni kwanini hiyo mishahara inawekwa siri sana kwa wananchi hali kimantiki wananchi ndio waajiri wao?
  3. Mkuu unadhani unakubaliana na mfumo wa Uongozi wa serikali uliopo sasa? Kama HAPANA unadhani ni mfumo upi ambao ni mzuri na unafaa kwa kupata viongozi wa vyama vyetu kwa ngazi za juu kama M/Kiti, Makamu M/Kiti na Katibu Mkuu – Ule wa kuteua na kupigiwa kura za wajumbe au kugombea na kupigiwa kura na wajumbe na kwanini?
  4. Ni ukweli kuwa wewe ni mshauri wa uchumi wa Ujerumani. Kama ni kweli, je ni kitu gani kilichokutambulisha hadi kufikia kupewa hiyo nafasi?
  5. Umewahi kuanika utajiri wako (vitu unavyomiliki); unaweza walau kutufafanulia unamiliki magari mangapi, nyumba ngapi n.k?
  6. Unazionaje shughuli za kisayansi za watanzania? Je, kuna sera yeyote Tanzania inayompa kijana wa kitanzania nafasi ya kuwa mbunifu?
 
Nini uelewa wako kuhusu familia? Umeoa? Maana Kuishi au kuwa na mke siyo jambo jepesi, linahitaji uvumilivu na busara nyingi sana, kama vile ilivyo kuishi na mume. Kama hili limekushinda, vipi utaweza kuwaongoza watanzania wote wake kwa waume?
Ninaamini katika familia imara na ni mwumini wa familia ya kiafrika ambapo familia sio tu ni mke, mume na watoto bali pia ndugu na jamaa mbalimbali. Ndio maana ninaishi na ndugu zangu, nimelea wadogo zangu na wazazi wangu na hivi sasa ni nguzo katika ukoo wetu mkubwa sana ambao kuuweka pamoja kunahitaji uvumilivu na busara nyingi sana kuliko hata busara inayohitajika kwa mke na watoto. Mimi sijaoa. Muda ukifika nitaoa. Sitaoa kwa sababu ya kuonekana kiongozi ameoa. Nitaoa pindi nitakaporidhika na huyo mwenzangu ambaye nitafunga naye ndoa. Historia inatuonyesha viongozi wengi sana ambao wameoa na wameshindwa kuongoza nchi zao. Vilevile tuna viongozi wengi sana ambao hawana wake au waume na waliongoza nchi zao vizuri sana.

Indira Gandhi hakuwa ameolewa kipindi chote akiwa Waziri Mkuu wa India. Baba yake Indira, Nehru naye alikaa miaka zaidi ya 30 bila mke. Rais Khama wa Botswana hana Mke wala mtoto, hajapata kuoa lakini anaendesha nchi yake kwa mafanikio makubwa sana kuliko King Mswati mwenye wake zaidi ya 12. Rais Nkrumah alioa mwanamke ambaye hakuwa anamjua akiwa tayari ni Waziri Mkuu wa Ghana, tena aliletewa mke na Rais Nasser wa Misri. Hakuna mahusiano yeyote ya kisayansi kati ya kuoa na uongozi mzuri ingawa kuoa ni muhimu sana. Sidhani kama kuoa itakuwa kikwazo katika uongozi wangu kama itafikia uchaguzi sijaoa maana tumeona viongozi kadhaa wakiamua kuoa baada ya chaguzi. Hata hivyo nitafurahi zaidi kuoa kabla sijawa Rais, lakini ikibidi nitaoa nikishakuwa Rais. Sitalazimisha ndoa kwa ajili ya Urais. Nitaoa nitakapopenda kuoa.

Mkuu Zitto is there any chance unajua mshahara wa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mshahara wa makamu wa rais wa JMT, na ule wa rais wa Zanzibar? Ni mahala gani pa kwenda kufuatilia hizo data kwa yeyote yule anayetaka kufahamu hayo? Pia katika hili unadhani ni kwanini hiyo mishahara inawekwa siri sana kwa wananchi hali kimantiki wananchi ndio waajiri wao?
Sijui mshahara wa Rais na naamini ni katika vitu ambavyo walipa kodi wanatakiwa kujua. Mshahara wa Rais hautakiwi kuwa siri kwa mtanzania yeyote. Inapaswa kuwa wazi kabisa na kila Raia ajue. TRA watakuwa wanajua kama sio tax exempt. Nadhani tukifatilia kupitia Utumishi tunaweza kupata hizo data. Hebu ngoja nipeleke swali Bungeni kuhusu jambo hili ili lijibiwe Mkutano ujao wa Bunge. Haya ni mambo ambayo tuna overlook sana.

Mwaka 2008 wakati tunapitisha sheria ya Utawala wa Bunge (National Assembly administration act) niliwasilisha ammendment kuwa mishahara ya wabunge na mawaziri iwe wazi na iwekwe online watu waweze ku access. Nikajibiwa ni siri ya mtu. Rais ni mtu ndio, lakini sio mtu kama mtu mwingine. Ni mtu mwenye maamuzi kuhusu mwelekeo wa Taifa. Ni vizuri kujua tunamlipaje. Ngoja na mimi niwaulize, Nani anajua mshahara wa Mbunge wa Jimbo lake hapa?

Mkuu unadhani unakubaliana na mfumo wa Uongozi wa serikali uliopo sasa? Kama HAPANA unadhani ni mfumo upi ambao ni mzuri na unafaa kwa kupata viongozi wa vyama vyetu kwa ngazi za juu kama M/Kiti, Makamu M/Kiti na Katibu Mkuu – Ule wa kuteua na kupigiwa kura za wajumbe au kugombea na kupigiwa kura na wajumbe na kwanini?
Sina maoni

Ni ukweli kuwa wewe ni mshauri wa uchumi wa Ujerumani. Kama ni kweli, je ni kitu gani kilichokutambulisha hadi kufikia kupewa hiyo nafasi?
Nilikuwa kwenye jopo la Rais Kohler kuhusu Afrika. Nilimaliza kazi hiyo mwaka 2009. Niliteuliwa tu na Rais Kohler wa Ujerumani

Umewahi kuanika utajiri wako (vitu unavyomiliki); unaweza walau kutufafanulia unamiliki magari mangapi, nyumba ngapi n.k?
Nimewahi kusema ninamiliki nini ili kufuta uzushi unaoenezwa kuwa mimi nina ukwasi wa kutisha. Nina gari 2, moja Freelander na nyingine Toyota vista. Ninajenga nyumba Kigoma, kijijini Mwandiga. Nina shamba lenye mikorosho 400 Mtwara, Nina shamba la ekari 3 eneo la Mbutu, Kigamboni. Ninadaiwa na CRDB milioni 120 nilizokopa kwa ajili ya kununua vitu hivyo. Nina mkopo wa Bunge wa kununua gari wa tshs 90 milioni ambao tunalipa nusu yake! Nina exemption ya kodi ya kuingiza gari lakini nimekataa kuitumia kwa sababu mimi kama Waziri kivuli wa Fedha ninapinga tax exemptions na hivyo nimeamua ku walk the talk. Sijaitumia na sitaitumia exemption hiyo.

Nimeamua kuwa ifikapo Mwezi January, mara baada ya kujaza fomu zangu za Maadili na kuziwasilisha nakala ya fomu hiyo ya Mali na Madeni nitaiweka online kwenye blog yangu ili kila mtu aone nimetangaza nina miliki nini na yeyote mwenye mashaka aweze kuniumbua kwa kusema mbona hili umeacha, mbona lile umeacha. Njia pekee ya kumaliza uzushi na majungu ni uwazi. Shaurini wabunge wenu wafanye hivyo pia ili kupambana na ufisadi.

Unazionaje shughuli za kisayansi za watanzania? Je, kuna sera yeyote Tanzania inayompa kijana wa kitanzania nafasi ya kuwa mbunifu?
Kuna sera na sheria za kusaidia ubunifu wa kisayansi. Tatizo ni kwamba Tanzania hatuheshimu sana R&D issues na matokeo yake tumekuwa watumiaji wa ugunduzi wa watu wengine. Kwenye eneo la ICT nimeona vijana wameanzisha The Kinu, tutawasaidia. Hii platform hapa tunayotumia JF imetengenezwa na Mtanzania Maxence, lazima tumsaidie ili iweze kudominate eneo lote la maziwa makuu.
 
Nimeruka swali moja la mwisho uzuri halikuwakilisha member yoyote hakuna niliemnyima haki... Naona turukie hapa kabla hujanikimbia.

MWISHO: On JamiiForums

  1. Hatuwezi kuwa sahihi katika kila nyanja, vipi umeridhika na namna mdahalo huu ulivyoenda?
  2. Unaiongeleaje JamiiForums na ungepata nafasi ya kukutana na wahisani ungewashauri waisaidieje?
  3. Wewe ni mmoja kati ya wanasiasa wachache wenye 'guts' za kujibu kero za wananchi hata mitandaoni (hasa JF), tunakupongeza kwa hili; unaweza kuwashawishi wanasiasa wengine kufanya hivi?
 
Hatuwezi kuwa sahihi katika kila nyanja, vipi umeridhika na namna mdahalo huu ulivyoenda?
Ni hatua nzuri sana na nadhani mtatoa fursa kama hii kwa watu wengine watakao tayari kujiweka wazi. Wasiwasi wangu ni kwamba maswali ni mengi sana inabidi mtu kukaa siku nzima kwenye KOMPYUTA kujibu maswali. Sio kila mtu atakuwa na muda kiasi hiki. Ninachoshauri ni kuwa na maswali machache muhimu au kuna na maswali na kumwuliza mapema interviewee na yeye ku-paste majibu yake na mjadala uwe kwenye majibu hayo kwa muda maalumu ambapo kila member ataweza kuuliza na MODs kuratibu zoezi hilo. Nitafurahi kuona wanasiasa wengine wakihojiwa hapa. Nafurahi kufungua dimba.

Unaiongeleaje JamiiForums na ungepata nafasi ya kukutana na wahisani ungewashauri waisaidieje?
Jamiiforums ni mtandao wa kijamii ambao umepata sifa kubwa sana. Kuna watu ambao kila kinachoandikwa JF wao wanaona kweli. Utasikia wanasema, ndio nimeona JF. Kwa hiyo mmepata kuamianiwa sana. Sasa uaminifu huu lazima muutumie vizuri. Kuna watu wanaleta maneno ya uwongo hapa, uwongo mwingine ni wa dhahiri kabisa unaachwa. Kuna watu wanaleta habari za kweli kabisa lakini zinatolewa. Ni lazima Wanachama wa JF wawe makini kwa kile wanachoandika na MODs wawe makini zaidi kuhakikisha masuala ambayo uhakika na yanaharibu reputation za watu yasiruhusiwe.

JF lazima ijiepusha na hali yeyote ya kuonekana kuwa ni chombo cha chama fulani cha siasa. Hii inaharibu objectivity ya forum. Itakuwa ni raha sna kama wanachama wa vyama vyote vya siasa watakuwa na uhuru kutumia jukwaa hili. Sisi CHADEMA tunafurahi kwamba wanachama wetu wengi wapo humu na wanafanya kazi nzuri kulinda heshima ya chama chetu. Najua kuna wana CCM humu, nao waje na hoja zao pia. Najua kuna CUF humu waje na hoja zao pia. NCCR nk waje na hoja zao pia. Tujenge uvumilivu wa kisiasa. Matusi yanaharibu kabisa heshima ya jukwaa na kwa kweli matusi yasivumiliwe kabisa. Hoja zijibiwe kwa hoja.

JF iwe ni chombo cha kila Mtanzania kuwa huru kusema atakacho bila kuogopa atahojiwa na nani kwa nini. Ninaamini tutafika huko.

JF inapaswa kusaidiwa na Watanzania wenyewe kwa kuwa na huduma za kununua na pia matangazo. Nasisitiza sana matangazo. Mashirika na Taasisi za Serikali zisiogope kutangaza huduma zao JF kwani Watanzania wengi watapata habari za huduma zao. Mashirika ya Umma yasioope kuambiwa wanafadhili chombo kinachoinanga Serikali, hapana. Kampuni binafsi pia zitoe matangazo yao hapa. JF ni muhimu sana katika kukuza demokrasia hapa nchini kwetu.

Wewe ni mmoja kati ya wanasiasa wachache wenye 'guts' za kujibu kero za wananchi hata mitandaoni (hasa JF), tunakupongeza kwa hili; unaweza kuwashawishi wanasiasa wengine kufanya hivi?
Yataka moyo sana. Mimi hutumia JF kama kioo hivi. Kuna mambo mengi mazuri sana humu. JF hutusaidia kupata taarifa kwa haraka badala ya kusubiri magazeti siku ya pili. Hata hivyo Najua kuna mengi sana ya uwongo yanasemwa humu lakini kwa kuwa najua ni uwongo hainisumbui sana. Wakati mwingine hata huyo msema uwongo huwa anajijijua kuwa anasema uwongo. Tukikutana mitaani wengine wanaona aibu na hata kuomba radhi. Kuna wakati mpo kwenye kikao na mtu anaandika suala la kikao hicho JF kwa kutwist ukweli na wakati mwingine unamjua na unamwona anavyohangaika. Wakati mwingine mtu ni rafiki yako kabisa lakini ukimpa kisogo tu anapost kitu JF cha uwongo. I don't take anyting personal. Hapana ninakomazwa zaidi maana najua huko mbele criticism zitakuwa nyingi sana. Ninashauri wenzangu wapite katika kikaango hiki. Mimi sina la kuficha ndio maana nipo wazi kabisa kuja hapa na kujibu hoja zinazonihusu. Nitaendelea kushiriki mijadala Jamiiforums.

Nashukuru sana
 
Sijasoma hata hio post vizuri ila whatever the case naomba Maxence Melo, Mike McKee, Invisible, moderators woote na members woote wasome hio post kwa makini zaidi sababu naamini inatugusa kila mmoja wa anaetumia huu mtandao...

Mheshimiwa Zitto, RESPECT kwako. Mwenyezi Mungu azidi kukuneemesha, kukubariki, kukujaaliya katika kila mema utendayo hasa yanayogusa Watanzania na watu wako wa karibu. Umetumia siku nzima hapa, sio suala dogo na hakuna namna zaidi ya hii mimi na my fellow members tunaeza kushukuru. Najua lazima kuna mapengo kwa wengine... Ila bado ukweli unabaki huwezi kurithisha kila mmoja wetu.

Kwa mara nyingine nasema "ASANTE SAANA" Mkuu na I am humbly humble to have gotten this chance.

Nina Ombi kwako:

Kwa leo na dakika hii najivisha kwa lazima u'JF ambassador ( Mike McKee naazima hiki cheo) katika kuhakikisha JF inazidi kusonga mbele na kufanyiwa wepesi. Hivo mkuu kama hutojali naomba mchango wako wa kuchangia JF kwa kiasi chochote kilicho ndani ya uwezo wako. Naomba TAFADHALI ukubaliane na hili ombi langu na uniahidi utachangia kiasi gani...


Pamoja Saana,

AshaDii.
 
Wana JF,

Maswali yote yaliyowakilishwa na wana Jf hadi pale deadline yameulizwa yote, nilijitahidi kuwa makini sana, nikashirikisha na kupata assistance na fellow Jf member kupitia kama nimeruka na tukaridhika yoote yapo. I pray kuwa hakuna niliyeruka swali lake na kuwa sijamuwakilisha. Natanguliza kwa kuomba Samahani iwapo itatokea hivo.

Shukrani za dhati ziwaende wooote! Kwa kweli NASHUKURU kwa uwepo wenu. Nikiliongelea kwa upande wangu it is quite an achievement, ni mambo mengi nilitaka ( naamini kama ilivyo miongoni mwa wengi wa members wenzangu) kujua na kupata na nimeyapata, na nitayapata vema nikitulia na kusoma upya. Nikikiri kuwa leo kwangu ni furaha ilioje kwa kuweza timiza hili. Imechukua takribani wiki 6, a face to face meeting, rafiki wa karibu, assistance ya karibu ya Maxence Melo, Members wa Jf, uwepo wa Mheshimiwa Zitto, Ushirikiano wa JF Utawala, Usimamizi wa Invisible and the crew kuweza fanikisha hii Interview. Shukrani kwenu woote, I humbly appreciate wakuu…

Zitto Zuberi Kabwe ni moja wa viongozi wa siasa ambao wana ‘qualify' kuitwa machachari katika anga hiyo na naweza sema kwa ‘confidence' kuwa ni moja ya Kiongozi ambaye huleta utata mwingi sana. Matumaini yangu ni kuwa kwa mjadala huu, kila mmoja awe amepata kipya, hata kama sio yote lakini kwa kiasi. Na kuwa ile quote ya Mchambuzi wa Jf kuwa " Masuala Mazito juu ya Zitto huangaliwa kwa hoja nyepesi katika masuala yaliyo Mazito" kutabadilika kwa uzuri kwa kiasi Fulani.

Niya nyingine ilikuwa kuwa hii thread ijibu mengi juu ya Zitto hivo kwa Muktadha huo naambatanisha Threads zingine mbali mbali juu ya Mheshimiwa Kabwe katika masuala mbali mbali. Kwa muktadha huo nitajitahidi hii post kuweka thread zote za muhimu zinazo mgusa Zitto moja kwa moja .

Thread zote alizowahi rusha Mkuu Zitto akiwa kama member wa Jf - Search Results - JamiiForums | The Home of Great Thinkers

Kuna threads mbali mbali ambazo Zinamgusa Zitto MOJA KWA MOJA nitaorodhesha hapa pia, kwa sasa naweka chache maana mwili unagoma. Na pia naomba Paw, Fang, Roulette, PainKiller ama mod yeyote kwa mda wake akiweza anisaidie kwa hili NITASHUKURU.

https://www.jamiiforums.com/jukwaa-la-siasa/337716-uzito-wa-zitto-wepesi-wa-hoja-kwa-suala-zito.html

https://www.jamiiforums.com/jukwaa-...a-binafsi-juu-ya-walioficha-fedha-uswiss.html

https://www.jamiiforums.com/jukwaa-...5-ni-kwa-tiketi-ya-chadema-habib-mchange.html

https://www.jamiiforums.com/jukwaa-...abilioni-nje-chadema-itawataja-hadharani.html

https://www.jamiiforums.com/jukwaa-...atanicheka-watapambana-lakini-nitashinda.html

https://www.jamiiforums.com/jukwaa-...ge-2015-nitagombea-urais-kupitia-chadema.html

https://www.jamiiforums.com/great-thinkers/169603-mh-zitto-kuna-ukweli-gani-katika-report-hii.html

Ushauri wangu kwa Zuberi Zitto Kabwe




Pamoja Saana,


AshaDii.
 
Status
Not open for further replies.
69 Reactions
Reply
Back
Top Bottom