JamiiTalks Mahojiano ya moja kwa moja na Mhe. Zitto Zuberi Kabwe katika JamiiForums

Status
Not open for further replies.
Mkuu Zitto you sound really really proud kuwa watokea Kigoma na changes zake pia. Inapendeza. Kwa mara nyingine tena NASHUKURU kwa majibu ya swali lililo pita.

Swali linalofuata;

E. Zitto na Maoni juu ya Tanzania


  1. Nini ni Dira ya Kabwe Zuberi Zitto kwa Tanzania?
  2. Kama leo ungechaguliwa kuwa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya katiba ya sasa ukiwa amekuta maadui wale watatu (ujinga, umaskini na maradhi) wakineemeka hasa wakiwa wamepata mwenzao ufisadi, ungetumia jeshi gani/mbinu gani kupambana na maadui hawa?
  3. Kwanini Tanzania ni Maskini? Mkakati gani wa anaouona kuwa unaweza kutambua vipaumbele vya kuondokana na umasikini wa Tanzania?
  4. Kama kijana, umetembea nchi kadhaa duniani, kwa muono wako ni wapi wananchi, viongozi, serikali na taifa kwa pamoja tunakosea katika kulisongesha gurudumu la maendeleo Tanzania?
  5. Ikiwa ndani ya uwezo wako i.e tuchukulie umepata urais; ni njia gani ambayo unaweza kutumia kufuta na kumaliza Udini ambao unaanza kujidhihirisha kwenye siasa za Tanzania?
 
Nini ni Dira ya Kabwe Zuberi Zitto kwa Tanzania?
Tanzania ambayo kila Mtu ana fursa sawa ya kujiendeleza na kuliendeleza Taifa bila vikwazo vyovyote. Tanzania yenye heshima mbele ya Mataifa ya dunia, wenye watu wanao thamini Utu wa binadam wote duniani, yenye watu werevu wanao tambulika nyumbani na kimataifa, na wenye siha njema. Mwono chanya kuhusu nchi yao na majirani wao. Napenda kuona Taifa imara na bora barani Afrika. Taifa lisilo na taswira ya ufisadi. Taifa la kujivunia. Inawezekana.
Kama leo ungechaguliwa kuwa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya katiba ya sasa ukiwa amekuta maadui wale watatu (ujinga, umaskini na maradhi) wakineemeka hasa wakiwa wamepata mwenzao ufisadi, ungetumia jeshi gani/mbinu gani kupambana na maadui hawa?
Kwanza kuibadili Katiba hiyo ingekuwa suala la kwanza maana huwezi kupambana na ufisadi kwenye Katiba ambayo ni mbaya.

Pili ningeimarisha sana miiko ya uongozi na kuweka bayana kwamba yeyote anayetaka uongozi wa Umma atumikie umma, biashara aweke pembeni. Hata nchi zilizoendelea zinafanya hivi (conflict of interest code). Hii ndio inaimarisha ufisadi.

Tatu, uwazi wa mali za viongozi, uwazi wa mikataba yote ya kunyonya rasilimali na uwajibikaji wa viongozi kwa wananchi.

Ukishaweka misingi hii na hasa misingi ya uwazi na uwajibikaji kazi ya kupambana na rushwa inakuwa rahisi sana. Hivi sasa tunashindwa kwa sababu hao wanaopaswa kupambana na rushwa wao wenyewe wana maslahi na wanazuia mabadiliko. I am anti status quo person all my life and we need just that.

Suala la mgongano wa maslahi nimeliandikia mara kadhaa na hata jana kuna makala kwenye RaiaMwema kuhusu suala hili. Pia niliandika muswada binafsi Bungeni kuhusu suala hili na niliuweka hapa JF napia kwenye blog yangu zittokabwe.com. Hili ni suala linahitaji sana msukumo ni kuondoa ufisadi nchini.
Kwanini Tanzania ni Maskini? Mkakati gani wa anaouona kuwa unaweza kutambua vipaumbele vya kuondokana na umasikini wa Tanzania?
Tanzania ni masikini kwa sababu viongozi wetu wamechagua tuwe masikini. Njia moja kubwa na ilio endelevu ya kutokomeza umasikini Tanzania ni kuwekeza walipo Watanzania wengi na kuwapa fursa za ajira na ujira, fursa za kuzalisha utajiri kwa kuongeza uzalishaji mali.

Umasikini wa Tanzania utaondoka kwa kuwa na Maendeleo Vijijini. Ili kupata rasilimali za kuwekeza vijijini ni lazima kuondokana na upotevu mkubwa wa rasilimali za nchi kutokana na matumizi mabaya (kama posho), ufisadi, wizi na udokozi, pia kuzuia ukwepaji mkubwa wa kodi. Kazi ndio kipimo cha Utu itakuwa ni kauli mbiu muhimu ili kurejesha ‘attitude' ya kufanya kazi badala ya kuwa Taifa la wanyemelea-kipato (rent-seekers).
Kama kijana, umetembea nchi kadhaa duniani, kwa muono wako ni wapi wananchi, viongozi, serikali na taifa kwa pamoja tunakosea katika kulisongesha gurudumu la maendeleo Tanzania?
Hatuna wivu wa maendeleo. Tumekata tamaa. Hatuna ‘ambition' za kuacha legacy kama walivyo kina Mahathir, kina Meles nk. Hatuna attitude ya maendeleo. Watu wenye madaraka hawana mawazo mapana, hawaoni mbali., na hawana constancy and consistency katika strategies zao za kuendesha nchi. Ukienda kwenye blog yangu soma a post imagine Tanzania utaona potential ya nchi hii.
Ikiwa ndani ya uwezo wako i.e tuchukulie umepata urais; ni njia gani ambayo unaweza kutumia kufuta na kumaliza Udini ambao unaanza kujidhihirisha kwenye siasa za Tanzania?
Udini ni state of mind. Tatizo Tanzania tumekuwa kwenye state of denial.

Malalamiko ya Udini katika nchi yameanza siku nyingi sana. Njia ni moja tu, Serikali kutoshughulika na masuala ya Dini na viongozi wa dini kutojiingiza kwenye siasa za vyama bila kupoka uhuru wao wa mawazo au wa kujiunga na vyama vya siasa. Ukiwa na Serikali inayotenda haki kwa watu wote bila kujali wana Sali au wanaSwali hapatakuwa na malalamiko haya.

Hii sio mara ya kwanza tunaona vurugu za kidini kwenye nchi. Kwani mmesahau suala la maduka ya nguruwe miaka ya tisini? Mmesahau suala la mwembechai la miaka hiyo hiyo? Mmesahau mauaji ya Arumeru? Muhimu ni Serikali kuwa imara kuhakikisha tunapiga vita ‘chuki' kisheria na kutenda haki kwa watu wote bila kujali dini zao. Udini ulivyo sasa ni kansa inayotutafuna kidogo kidogo. Nimeshuhudia mwenyewe udini mkali sana wakati wa kampeni mwaka jana Jimboni kwangu ulioendeshwa na dini zote kuu - Waislam na Wakristo kila mmoja kwa mwono wake.

Nimesoma jana makala ya MwanaKijiji kuhusu namna ya kushughulika na suala hili. Kuna haja ya kuzungumza kwa uwazi bila jazba suala hili. Ningekuwa ni Rais leo ningeunda Tume ya Ukweli na Maridhiano kujadili kwa uwazi na mapana yake suala la Udini. Tusipochukua hatua nchi hii itapasuka vipande. Haya mambo ya Gesi na Mafuta haya ndio yatatumika na maadui wa nchi yetu kutugawa.

Tuwe Makini sana. Tusione tu hizi vurugu kwa juu juu. Tuzungumze
 
Asante kwa majibu Mkuu Zitto. Hii quote speaks loads, kwa mtazamo wangu inabeba msingi wa KILA KITU cha kwa nini Tanzania na wananchi wake wengi ni maskini - "Tanzania ni masikini kwa sababu viongozi wetu wamechagua tuwe masikini".

Swali hili kipengele ni kimoja tu kama ifutavyo;


F. Zitto na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar


Viongozi wengi wanakwepa kujadili suala la muungano kwa kuogopa kuathirika kisiasa, lakini ni muhimu wananchi wakaanza kujua misimamo ya viongozi wao ni ipi ili waanze kuwapima kwa masuala na misimamo, badala ya personalities (sura, uwezo kifedha, kabila, dini, n.k); Isitoshe kuna viongozi waliothubutu kama Tundu Lissu ambaye anaitaka Tanganyika na hilo halijamshusha bali kumpandisha juu zaidi.

Tukiachana na hoja juu ya umuhimu wa wananchi wenyewe kuamua, je, wewe binafsi kama mmoja ya hao wananchi, unadhani mfumo upi ni bora ambao utaweza kusaidia pande zote mbili kuhisi zinafaidika na muungano?
 
Tukiachana na hoja juu ya umuhimu wa wananchi wenyewe kuamua, je, wewe binafsi kama mmoja ya hao wananchi, unadhani mfumo upi ni bora ambao utaweza kusaidia pande zote mbili kuhisi zinafaidika na muungano?
Kwanza kabisa niweke wazi kwamba mimi ni muumini wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Shirikisho la Afrika Mashariki na Mwanamajui wa Afrika (Pan Africanist). Lazima tuulinde muungano wetu kwa kuufanyia marekebisho makubwa sana ikiwemo kutoa uhuru mpana kwa pande za Muungano kufanya mambo yao. Muungano wenye Zanzibar na Tanganyika zenye Mamlaka ya kutosha (Kina ndugu Jussa wanasema Mamlaka kamili, ukisema mamlaka kamili ni sawa na kusema hakuna muungano). Baada ya utangulizi huu, ningependa muungano uwe na muundo gani?

Muundo wa Muungano uwe wa Nchi moja, Dola moja, Taifa moja. Serikali tatu. Kuwe na Rais wa Jamhuri ya Muungano ambaye ni Mkuu wa nchi na Mtendaji kwenye masuala ya Muungano tu ambayo yatakuwa machache kama Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, Sarafu, Sera za Fedha, Biashara ya Kimataifa, Kodi za kimataifa, usimamizi wa Rasilimali za Taifa, Uraia nk. Zanzibar watakuwa na Waziri Mkuu Mtendaji na Tanganyika hivyo hivyo. Chama chenye Wawakilishi wengi kwenye Baraza la Wawakilishi la Tanganyika kitatoa Waziri Mkuu na kuunda Serikali na Zanzibar hivyo hivyo. Bunge la Muungano litachagua wajumbe wake kutoka kwenye kila mkoa wa Tanzania wajumbe wawili. Maamuzi yataamuliwa kwa zaidi ya nusu ya kura kwa Wabunge kutoka kila upande wa Muungano.
 
Nashukuru Mkuu,

Swali linalofuata;

G: Zitto na Azimio la Arusha

Inazidi kuwa dhahiri kwamba tangia nchi iachane na Azimio La Arusha mwaka 1992, kama taifa, hatuna tena ‘ownership of the development agenda' (badala yake kwa kiasi kikubwa, tunafanyiwa maamuzi mengi muhimu na Benki ya Dunia, IMF n.k) na pia nchi haiongozwi tena kwa maadili.

  1. Kwa mtazamo wako kama Zitto, Je unadhani kuna mambo gani yaliyomo ndani ya Azimio la Arusha ambayo bado yanaweza kutusaidia katika kipindi hiki kigumu bila ya kujali itikadi za kisiasa?
  2. Kuna lingine la muhimu katika hili mkuu… Wengi wanaliponda Azimio La Arusha lakini ni mabingwa wa kukimbia kujadili kitu mbadala wa Azimio la Arusha; Wakibanwa, wanakimbilia Katiba Mpya; Hivi ni vitu viwili tofauti; Declarations mbalimbali ni muhimu sana kwa taifa katika kujipanga kimaendeleo. Unadhani kwanini?
 
Kwa mtazamo wako kama Zitto, Je unadhani kuna mambo gani yaliyomo ndani ya Azimio la Arusha ambayo bado yanaweza kutusaidia katika kipindi hiki kigumu bila ya kujali itikadi za kisiasa?
- Miiko ya Uongozi.
- Serikali kuwa msimamizi mkuu wa maendeleo ya nchi badala ya kuachia soko kila kitu.
- Msisitizo wa maendeleo vijijini.

Kuna lingine la muhimu katika hili mkuu… Wengi wanaliponda Azimio La Arusha lakini ni mabingwa wa kukimbia kujadili kitu mbadala wa Azimio la Arusha; Wakibanwa, wanakimbilia Katiba Mpya; Hivi ni vitu viwili tofauti; Declarations mbalimbali ni muhimu sana kwa taifa katika kujipanga kimaendeleo. Unadhani kwanini?
-Katiba sio mwarobaini wa matatizo ya nchi yetu. Unaweza kuwa na Katiba nzuri sana lakini fukara tu. Maazimio yanatoa mwelekeo wa nchi kutokana na nyakati. Katiba inaweka tu misingi ya mtajiongoza namna gani na kwa mipaka gani na maono. Azimio kama ilivyo Azimio la Arusha linaweka utaratibu wa kutekeleza katiba
 
Kwa mara nyingine Asante Mkuu.

Swali linalofuata;

H: Zitto na KATIBA Mpya


Mkuu Zitto tupo katika mchakato wa kupata Katiba Mpya, katiba ambayo viongozi mbalimbali wa chama tawala na Vyama vya pinzani, wanaharakati na watanzania wengi wanakubaliana kuwa Katiba ya sasa ina mapungufu mengi na hivyo haina budi kubadilishwa.

Katika hili eneo la Katiba kuna maswali kadhaa kwako:-

  1. Unazungumzia vipi suala la majina wajumbe wa kamati ya kukusanya maoni ya katiba mpya kuchaguliwa na rais?
  2. Ni kipengele/vipengele gani katika katiba ya sasa vina mapungufu makubwa zaidi kuliko vingine na una maoni gani?
  3. Unakubaliana na dhana ya kuwa Spika wa bunge amekuwa na madaraka makubwa mno hivyo kuna umuhimu wa kupunguza baadhi ya madaraka.
  4. Mkuu Zitto, ningependa kujua kitu kingine kutoka kwako. Katika Mabadiliko ya Katiba yanayokuja kuna uwezekano mkubwa wa MAWAZIRI wasitokane na nafasi za UBUNGE. Kwa muono mwingine wewe umetangaza kutogombea ubunge jimboni kwako. Hii inaweza kuchukuliwa kuwa unawinda UWAZIRI kwa kulifikiria hili?
  5. Je, utaratibu wa sasa wa bunge la JMT wa kupiga kura kwa kuuliza wanaosema NDIYO na wanaosema SIYO ni sawa na unakidhi matwaka ya kidemokrasia uendelee au ubadilishwe? Kwanini?
 
Unazungumzia vipi suala la majina wajumbe wa kamati ya kukusanya maoni ya katiba mpya kuchaguliwa na rais?
- Hili halina mjadala tena maana tume imeshaundwa na majina yameshatangazwa. Vyama vilipeleka majina kwa Rais na Rais akateua kutokana na orodha ambayo yama vimepeleka. Hili swali halina tija kwa sasa.
Ni kipengele/vipengele gani katika katiba ya sasa vina mapungufu makubwa zaidi kuliko vingine na una maoni gani?
Katiba nzima ina mapungufu na hivyo tunaandika upya kabisa. Katiba itakayo tufaa ni yenye kulinda maslahi ya taifa, sio vyama au watu binafsi. Katiba hiyo inatakiwa kuweka msingi ya Tanzania tunayo itaka.

Napenda Katiba ambayo itaimarisha sana Uwajibikaji. Kama Katiba ingekuwa ni neno moja tu basi mimi ningechagua neno hilo liwe 'UWAJIBIKAJI' yaani Accountability. Huu ndio msingi wa Taifa kwa wananchi kuwa na uwezo wa kuwawajibisha viongozi na viongozi kuwajibika kwa wananchi.

Ningependa kuona Katiba ambayo inaweka maliasili zote za nchi, zilizopo chini ya ardhi na juu ya Ardhi chini ya mamlaka ya Dola. Katiba Itamke kuwa Madini, Mafuta, Gesi Asilia, Ardhi na vilivyomo ni mali ya nchi na Katiba na Sheria itaweka utaratibu wa kuendeleza rasilimali hizo kwa faida ya wananchi wote.

Ningependa kuona Katiba ambayo inatupa matumaini ya Taifa tunalojenga. Katiba itakayotumikia wananchi na sio wananchi kutumikia katiba.

Napenda kuona katiba itakayoimarisha Utu wa Mtanzania. Katiba itakayoweka misingi ya dhati ya Utu, Uzalendo na Uadilifu wa wananchi kwa Taifa lao na wa viongozi kwa wananchi.
Unakubaliana na dhana ya kuwa Spika wa bunge amekuwa na madaraka makubwa mno hivyo kuna umuhimu wa kupunguza baadhi ya madaraka.
- Spika hana madaraka yoyote. Unaposema madaraka makubwa mno maana yake nini? Kazi ya Spika ni kusimamia mijadala tu Bungeni. Spika sio mtendaji wa Bunge. Jambo la msingi ni kuboresha kanuni za Bunge ili ziweze kuweka uhuru mkubwa zaidi wa mawazo ndani ya Bunge.
Mkuu Zitto, ningependa kujua kitu kingine kutoka kwako. Katika Mabadiliko ya Katiba yanayokuja kuna uwezekano mkubwa wa MAWAZIRI wasitokane na nafasi za UBUNGE. Kwa muono mwingine wewe umetangaza kutogombea ubunge jimboni kwako. Hii inaweza kuchukuliwa kuwa unawinda UWAZIRI kwa kulifikiria hili?
Duh, umewaza mbali hata mimi sikuwa nimewaza hivyo. CHADEMA ikishinda niwe au nisiwe Mbunge ninaamini nitakuwa Waziri ili kuweza kutekeleza mabadiliko tunayohubiri katika harakati.

Nimetangaza kutogombea Ubunge, kwanza kuomba ridhaa ya chama changu kuwa mgombea Urais na hilo lisipowezekana nitakuwa mpiga debe wa mgombea Urais. Sitaki itokee tena yaliyotokea mwaka 2010 ambapo mgombea Urais alibaki mpweke kwani kila mtu alikwenda kugombea Ubunge.
Je, utaratibu wa sasa wa bunge la JMT wa kupiga kura kwa kuuliza wanaosema NDIYO na wanaosema SIYO ni sawa na unakidhi matwaka ya kidemokrasia uendelee au ubadilishwe? Kwanini?
Kuna mashine ya ki elektroniki za kupiga kura ndani ya Bunge. Nadhani tuanze kutumia hizo ili pia kuweka rekodi za wabunge kuhusu kura zao. Itasaidia sana kujua misimoa ya watu kwenye masuala mbalimbali ya nchi.
 
- Spika hana madaraka yeyote. Unaposema madaraka makubwa mno maana yake nini? Kazi ya Spika ni kusimamia mijadala tu Bungeni. Spika sio mtendaji wa Bunge. Jambo la msingi ni kuboresha kanuni za Bunge ili ziweze kuweka uhuru mkubwa zaidi wa mawazo ndani ya Bunge.

Mkuu Zitto,

Kama Spika hana madaraka yoyote na kazi ni kusimamia tu mijadala ya bunge, mbona amekuwa aki 'play part' kubwa sana katika kutoa maamuzi ambayo huathiri baadhi ya malengo, matendo ya bunge na pia mara kwa mara kuweza kuzima mijadala ambayo saa nyingine inakuwa ni ya msingi? I mean, anaweza kuzima mjadala hivihivi!

OK:
Swali linalofuata nalo likiwa na kipengele kimoja;

I: VITI MAALUM:

Nini msimamo wako juu ya uwepo wa wabunge zaidi ya 100 wa viti maalum ambao kimsingi wanaligharimu taifa mamilioni ya fedha?
 
Mkuu Zitto,

Kama Spika hana madaraka yoyote na kazi ni kusimamia tu mijadala ya bunge, mbona amekuwa aki 'play part' kubwa sana katika kutoa maamuzi ambayo huathiri baadhi ya malengo, matendo ya bunge na pia mara kwa mara kuweza kuzima mijadala ambayo saa nyingine inakuwa ni ya msingi? I mean, anaweza kuzima mjadala hivihivi!

Muundo wa Bunge ndio unamfanya Spika aonekane ana mamlaka makubwa sana. Ikiwa Bunge litafikia angalau asilimia 40 ya Wabunge upinzani lazima Spika atasimamia vema kanuni.

Pia wakati mwingine wabunge ni mbumbumbu wa kanuni za wabunge na hivyo wanampa nafasi Spika kutumia vipengele vingine vya kanuni kuua hoja za wabunge.

Ni vizuri na sisi wabunge kusoma kanuni kikamilifu na kuzitumia kupenyeza hoja zetu. Mimi bianfsi nimefanya hivyo mara kadhaa nakufanikiwa. Kuna sheria kadhaa nimezifanyia marekebisho kupitia kamati ya Bunge zima kwa kutumia kanuni. Kwa mfano, Mkutano wa 8 wa Bunge nilifanya ammendment ya kufuta msamaha wa kodi ya VAT kwa kampuni za Madini kwa kupitia tricks za kanuni na ammendment yangu ikapita.

Vile vile ammendment ya sheria ya kulinda viwanda vya ndani vya maziwa na bidhaa za maziwa, licha ya kukataliwa kwenye kamati ya Fedha lakini niliweza kuipenyeza kwenye Kamati ya Bunge zima na kupita. ndugu Mnyika pia mara kadhaa amefanikiwa kupitisha amendments kadhaa Bungeni jambo ambalo ni gumu sana kwa mbunge wa upinzani.

Ni vizuri wabunge waige watu kama kina Mnyika kwa kuzisoma kanuni vizuri na kuzitumia kufanikisha kazi zetu. I admire John Mnyika for that and he has specialised on that and do it very well.
 
Nini msimamo wako juu ya uwepo wa wabunge zaidi ya 100 wa viti maalum ambao kimsingi wanaligharimu taifa mamilioni ya fedha?
Naunga mkono mfumo wa uchaguzi utakaohakikisha kuwa vyombo vya maamuzi vinakuwa na uwiano sawia wa wanawake na wanaume. Napinga mfumo wowote wa upendeleo maana inadhalilisha.

Hivyo Katiba mpya ifute mfumo wa viti maalumu na kuweka mfumo wa uchaguzi utakaohakikisha vyombo vya maamuzi vinakuwa na wanawake na wanaume kwa uwiano sawia. Mimi ni muumini wa mfumo wa Uwakilishi wa uwiano (Proportional Representation).

Nchi za scandinavia zina mfumo mzuri sana wa uwiano ambapo viti vya Bunge vinapatikana kutokana na uwiano wa kura ambazo kila chama kimepata. Sio lazima tufuate mfumo wao, tunaweza kuwa na mfumo mchanyato. Ujerumani wanafuata mfumo mchanyato na kuna wabunge wengi tu wanawake.

Rwanda pia imefanikiwa kuwa na wanawake wengi sana Bungeni ingawa inabidi kuwa makini kufuata mfumo wa Rwanda demokrasia yao ina mashaka kidogo. Hata hivyo kuja jambo la kujifunza.
 
Mkuu asante kwa udadavuzi juu ya nguvu ya Speaker na pia kwa H/W niliyopata ya kuangalia mfumo wao wa uongozi na uwakilishi (German, nchi za Scandinavia na Rwanda) upo vipi na namna wanawake wanavyojiwakilisha katika ulimwengu wao wa siasa. Much respect.

Swali lifuatalo;

J: Zitto na matumizi ya vyombo vya usalama wa taifa katika kulinda maslahi ya chama tawala

  1. Kuna taarifa kuwa CCM inatumia vyombo vya ulinzi na usalama katika kuudhoofisha harakati za vyama vya upinzani, na hasa CHADEMA. Mheshimwa Zitto, una mtizamo gani katika hili?
  2. Mhe, kuelekea uchaguzi wa mwaka 2010 gazeti la MwanaHalisi lilichapisha mawasiliano ya simu baina yako na ndg Jack Zoka wa TISS, mpaka leo sijasikia sehemu ukikanusha; kwakuwa hakuna kanusho toka kwako, unaweza kutueleza mazungumzo yenu yalihusu nini?
 
Kuna taarifa kuwa CCM inatumia vyombo vya ulinzi na usalama katika kuudhoofisha harakati za vyama vya upinzani, na hasa CHADEMA. Mheshimwa Zitto, una mtizamo gani katika hili?
Ni kweli kabisa. CCM inatumia sana vyombo vya dola kumaliza upinzani. Hata hii ya kugawa wanachama na kupakaza matope baadhi ya viongozi ni kazi ya usalama wa Taifa. Wanapandikiza chuki ili viongozi tusiaminiane. Viongozi vichwa maji wasiojua kazi ya usalama wa Taifa wanafurahia mambo haya kumbe wanatumika
Mhe, kuelekea uchaguzi wa mwaka 2010 gazeti la MwanaHalisi lilichapisha mawasiliano ya simu baina yako na ndg Jack Zoka wa TISS, mpaka leo sijasikia sehemu ukikanusha; kwakuwa hakuna kanusho toka kwako, unaweza kutueleza mazungumzo yenu yalihusu nini?
Naomba nikusahihishe kwamba MwanaHalisi walichapisha mawasiliano hayo baada ya uchaguzi. Suala hili nimeshalisemea sana.

Kwanza ni kweli mimi ninawasiliana na viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama wakiwemo TISS, Polisi, TAKUKURU na hata JWTZ. Kama kuna kiongozi yeyote wa nafasi kama yangu ambaye hafanyi mawasiliano na watumishi hawa wa Umma basi kiongozi huyo hafai kuwa Kiongozi.

I challenge mtu yeyote aseme kama kuna kiongozi yeyote wa vyama vya siasa ambaye hafanyi mazungumzo na watu wa usalama nk. Jambo la msingi ni mazungumzo mnayoyafanya yanahusu nini? Yanahujumu chama? Niliwaambia viongozi wangu wa chama kwenye vikao vya chama kuwa, kama kuna chembe ya hujuma kwa chama kwenye mazungumzo yangu na watu kama Zoka basi nitaachia nafasi zangu zote uongozi kwenye chama na Ubunge. Nikawaambia wale waliosema wanao ushahidi wa mazungumzo hayo wayaweke wazi. Sio MwanaHalisi wala washirika wa MwanaHalisi waliofanya hivyo.

MwanaHalisi ilikuwa inafanya kazi ya siasa za ndani ya chama. MwanaHalisi walikuwa na ajenda yao dhidi yangu. MwanaHalisi waliamua kunimaliza kisiasa. Hata hivyo kwangu mimi hayo yamepita, ni historia.

Mazungumzo yetu yalikuwa yanahusu nini? Yalikuwa yanahusu nchi. Watu wa Usalama wanasema tunawashambulia sana kwenye mikutano yao na wao sio wanasiasa kwa hiyo mara kwa mara wanajaribu kutusihi tusiwazungumze. Tusiwataje taje. Mara zote nawaambia tutawataja pale ambapo wao wanahusika na kwamba hawapaswi kuhusika na CCM maana wao wanapaswa kulinda dola na sio kulinda CCM.

Wakati nipo Mwanza mapema mwaka 2011 palitokea mauaji ya raia yaliyofanywa na polisi kule Arusha, viongozi wetu wakakamatwa. Mmoja wa waliokamatwa ni Mzee Ndesamburo, mzee wa zaidi ya miaka 75 na wakawa wanamweka katika mazingira mabaya, niliwapigia watu Usalama kuwaambia kuwa hayo ni makosa. Wamwache mzee yule na wanataka kumshikilia wamshikilie nyumbani kwake, sheria zinaruhusu.

Wakati mwingine watu wa usalama wana shida zao pia maana wao ni Watanzania kama sisi.

Kwa mfano, Mwaka 2009 tulikuwa tunapitisha sheria ya Baraza la Usalama wa Taifa. Wakaja kuniomba kuwa sheria ile mbaya na inajaza watu wengi kwenye chombo hicho. Tuka mobilise wabunge kuikataa. Haikukatiza kwenye floor. Mwaka 2008 waliomba sheria yao iboreshwe ili kuondoa kipengele kinachowazuia wao kukamata. Maana sheria ya sasa inasema wao kazi yao ni kushauri tu. Nakumbuka nilifanya kazi hiyo na MwanaKijiji, alinisaidia sana kutafiti na kuandika kwa uzoefu wake wa Marekani kipengele kipya. Hatukufanikiwa na hivi sasa TISS hawana meno!
 
Kwa mara nyingine tena nashukuru kwa ufafanuzi huo juu ya hio makala iliyokuwa imechapishwa na Mwanahalisi. Kuna members wengi hapa Jf na katika jamii huitumia sana kama reference na justification kwa baadhi ya arguments, hopefully imewafikia na itaendelea kuwafikia.

Mkuu Zitto swali lifuatalo;

K: Zitto na wabunge wanaokaa kwenye bodi za mashirika:

Mkuu Zitto katika utawala bora inaelekezwa kwamba kuwe na vyombo vya usimamizi yaani oversight institutions kama vile Bunge (na kamati zake) ili kusimamia executive (management). Hapa tunapata dhana ya governance na management. Kwa mujibu wa utaratibu wa corporate governance inabidi oversight institutions zisifanye kazi za kiuongozi ama kiusimamizi wa moja kwa moja wa taasisi za serikali kwani vitashindwa kukosoa.

Kwa sasa tunaona Wabunge wakiwa kwenye Bodi za Wakurugenzi wa Mashirika ya Umma hapa nchini. Hii inapingana na dhana ya utawala bora! Kumbukumbu zangu zinaonyesha ya kwamba uliwahi kulipigia kelele suala hili lakini sijui kama ulilifikisha mwisho.

  • Je, unaonaje kama utajiandaa kupeleka ‘Hoja binafsi' Bungeni ili Bunge liazimie kwamba ni marufuku kwa Wabunge kuwa Wajumbe wa Bodi za Wakurugenzi wa Mashirika ya Umma? Sina hakika kama Wabunge watakubali kwa kuwa ni wanufaika lakini kama utapeleka hoja yako kimahiri sina shaka litakubaliwa.
 
Je, unaonaje kama utajiandaa kupeleka ‘Hoja binafsi' Bungeni ili Bunge liazimie kwamba ni marufuku kwa Wabunge kuwa Wajumbe wa Bodi za Wakurugenzi wa Mashirika ya Umma? Sina hakika kama Wabunge watakubali kwa kuwa ni wanufaika lakini kama utapeleka hoja yako kimahiri sina shaka litakubaliwa.
Ushauri mzuri sana. Lakini suala hili sio tu hoja binafsi, suala hili nimewahi kuliandika muswada binafsi zaidi ya mara 4 Bungeni. Mtu yeyote anayefuatilia Bunge atakuwa anajua kuwa kwenye taarifa zote za Kamati ya Bunge ya POAC tumekuwa tukipeleka maazimio haya kwamba wabunge wasiwe wajumbe wa bodi za mashirika ya Umma. Miswada yangu yote ilipigwa chini isipokuwa nilifanikiwa kwenye muswada wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ambapo hoja yangu ilipitishwa na Bunge (sijui hawakujua maana sikupata upinzani kabisa).

Lakini nashukuru kuwa baadhi ya Mawaziri wametekeleza agizo la kamati yetu kuwa Wabunge wasiwe kwenye Bodi za Mashirika ya Umma. Waziri Muhongo Kaunda upya bodi ya TPDC, hakuna Mbunge. Waziri Mwakyembe Bodi ya TPA hakuna Mbunge. Waziri Kagasheki kuna Bodi Kaunda hakuna Mbunge.

Toka POAC ilipoanza juhudi hizi mwaka 2009, kuna mafanikio kidogo lakini tunahitaji kuhakikisha kuwa hili haliruhusiwi kabisa. Wabunge wabaki wabunge tu. Kwa hiyo nashukuru kwa ushauri ingawa tayari ushauri huu nimeshautekeleza sio kwa hoja binafsi, bali kwa muswada binafsi unaotunga sharia. Hivi sasa tuna muswada wa Sheria ya Ofisi ya Msajili wa Hazina na tumeweka kifungu hicho. Tutafanikiwa kuweka misingi ya utawala bora.

Ni kinyume na misingi yote ya utawala bora wabunge kuwa wajumbe wa Bodi za Mashirika ya Umma.
 
Mkuu asante kwa makala, kwa manufaa ya wengi itatafsiriwa kwa Kiswahili na kuambatanishwa katika post hiyo hiyo. Tutaomba wataalamu wa lugha na tafsiri wa Jf yeyote ataweza kujitolea kutafsiri tutashukuru saana kwa msaada huo.

L: Zitto na posho la wabunge:
Mkuu Zitto kuna hili suala la Posho mbalimbali ikiwemo posho za vikao. Nakumbuka hapo nyuma uliwasha moto juu ya hizi posho na ukaamua kutopokea posho za vikao vya bunge na hata walipokuambia kuwa utapokea tu kwa kuwa ulikuwa unasini daftari la mahudhurio bungeni, uliamua kutosaini.

Haikuishia hapo walikutishia kwamba utafukuzwa bungeni kwa mujibu wa kanuni kwa kuwa utaonekana kwamba hujahudhuria vikao/mikutano kadhaa lakini ulikuja na hoja ambazo naona ziliwazima.

Baada ya huo utangulizi naomba kuuliza maswali yafuatayo:

  1. Najua msimamo wa Chama chako juu ya posho ni kuzipinga, je Chama chako kinatekelezaje msimamo huo kwa vitendo?
  2. Je, katika suala hili ulipata ushirikiano wa kutosha toka kwa wapinzani wenzako bungeni?
  3. Je, ulipata ushirikiano wa kiwango gani toka kwa Wabunge wa CCM?
  4. Je, hadi sasa hupokei posho za vikao?
 
Status
Not open for further replies.
69 Reactions
Reply
Back
Top Bottom