MaxShimba
JF-Expert Member
- Apr 11, 2008
- 35,772
- 4,054
Tuesday, 20 September 2011 20:30 |
Nora Damian HATIMAYE Mkuu wa zamani wa Jeshi la Polisi (IGP), Omar Mahita amekubali kumhudumia mtoto aliyezaa na mtumishi wake wa ndani, Rehema Shabani. Hatua hiyo imefikiwa baada ya Mahita kulipa gharama za malimbikizo ya matunzo ya kumhudumia mtoto huyo kuanzia mwaka 2003 hadi siku ya hukumu. Jana, Mahita alilipa Sh9 milioni kati ya Sh12 milioni anazotakiwa kulipa na kuahidi kulipa nyingine katika kipindi cha siku 30. Fedha hizo zililipwa na Wakili wake, Charles Semgalawe kwa kampuni ya udalali ya Nasm Auction Mart ambayo ilipewa jukumu na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni kufuatilia fedha hizo. Kampuni hiyo ilitoa notisi ya siku 14 kwa Mahita awe amelipa fedha hizo, vinginevyo hatua ya kutumia nguvu kukamata mali zake ingetumika. Notisi hiyo ilikuwa inamalizika jana na kwa kuwa sehemu ya fedha hizo ilitolewa na kuhidi kumaliza kiasi kilichobakia ndani ya siku 30, hatua ya kutumia nguvu iliondolewa. Awali, Mahakama ya Kinondoni ilitoa hukumu ya kuidhinisha kuwa mtoto huyo ni wa Mahita hivyo kumtaka mstaafu huyo wa jeshi la polisi kutoa Sh100,000 kila mwezi kwa ajili ya kumhudumia pamoja na kulipa malimbikizo ya gharama za matunzo kuanzia mwaka 2003 hadi siku ya hukumu. Katika kesi hiyo, Mahakama ya Kinondoni ilijiridhisha kuwa mtoto huyo ni wa Mahita kutokana na ushahidi wa upande wa mlalamikaji uliowasilishwa mahakamani hapo, ukiwapo wa vipimo vya vinasaba (DNA). Hata hivyo, baada ya hukumu hiyo Mahita alikata rufaa ambayo ilitupiliwa mbali na Mahakama Kuu.Katika uamuzi wake, Jaji Dk Fauz Twaib alisema kuwa Mahakama ya Kinondoni ilikuwa sahihi na kumwamuru Mahita kulipa gharama za kesi hiyo. Jaji Twaib alisema kwa mujibu wa barua kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kwenda kwa Mahakama, mrufani hakuweza kufika kwa ajili ya uchunguzi huo mara sita kwa nyakati tofauti. Jaji Twaib pia aliunga mkono hoja za wakili wa mlalamikaji kuwa ingawa sheria inatamka fidia ya Sh100 lakini mahakama inaweza kuangalia hali ya maisha na uwezo wa mlalamikiwa na hivyo kuweza kuongeza kiwango hicho. Alisisitiza kuwa katika shauri husika, kiwango kilichoamuriwa na mahakama ya chini kilizingatia hali ya kiuchumi hususan gharama za maisha na uwezo wa mrufani kuweza kulipa. Mahita akubali kumlea mtoto aliyezaa na mtumishi |