Mafuriko yaliyotokea Ulaya na China yanatukumbusha umuhimu wa kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,034
VCG111339939580.jpg


VCG111340071968.jpg


Mwezi huu wa Julai umekuwa ni mwezi wenye matukio mengi yanayohusiana na mabadiliko ya tabia nchi. Karibu nchi zote kubwa duniani zimekumbwa na matukio yanayothibitisha kuwa mabadiliko ya tabia nchi ni hatari ya kweli, na sio “jambo la kufikirika” kama inavyoelezwa na baadhi ya wanasiasa wa nchi za magharibi, na makundi ya “wataalamu” wanaokanusha kuwepo kwa mabadiliko ya tabia nchi.

Matukio mengi ya hali ya hewa ambayo yanatajwa kuwa hajayawahi kutokea katika miaka 50 iliyopita yameripotiwa katika nchi mbalimbali. Tumesikia mafuriko makubwa yaliyotokea Ulaya na kusababisha vifo na hasara kubwa ya mali, tumesikia wimbi kubwa la joto kali magharibi mwa Marekani na Canada lililosababisha vifo vya watu zaidi ya 130 nchini Canada, na moto wa misituni unaoendelea kutokea magharibi mwa Marekani, nchini China katika mji wa Zhengzhou watu pia wameathiriwa vibaya na kupoteza maisha, na barani Afrika mamlaka za hali ya hewa katika nchi mbalimbali zimesema baridi katika baadhi ya maeneo kwa mwaka huu, imekuwa kali kuliko kawaida.

Matukio haya yameonyesha kuwa mabadiliko ya tabia nchi si jambo la kufikirika tena kama ambavyo baadhi ya wanasayansi na wanasiasa wanavyotaka tuamini. Lakini jambo la muhimu kwa sasa, ni kuangalia nini kinafanyika kukabiliana na hali hiyo, na serikali zinafanya nini kukabiliana na hali hiyo.

Tukiziangalia nchi kubwa, tunaona kuwa Marekani kama nchi bado haieleweki vizuri ina msimamo gani kuhusu jambo hili. Rais aliyepita Donald Trump ni mmoja kati ya watu wanaopinga uwepo wa mabadiliko ya tabia nchi, na alifikia hata hatua ya kuitoa Marekani kwenye makubaliano ya Paris yanayoratibu juhudi za dunia nzima kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi, lakini Rais wa sasa Bw. Joe Biden ameirudisha tena Marekani kwenye makubaliano hayo. Ingawa ni jambo zuri, lakini bado hakuna uhakika kama sera za kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi kwa Marekani, ni jambo la uamuzi binafsi wa Rais wa Marekani au ni jambo la sera za taifa.

Tukiangalia China jambo moja tunaloliona ni kuwa, inakiri wazi kuwa mabadiliko ya tabia nchi ni changamoto ya dunia nzima, na nchi zote zinatakiwa kushiriki kwa mujibu wa uwezo wake kwenye kukabiliana na tatizo hili. Jambo la pili ni kuwa China imeweka mpango madhubuti wa kisera wa taifa, ambao ni wa muda mrefu wa kupunguza uchafuzi unaosababisha mabadiliko ya tabia nchi.

Hivi karibuni China pia ilitanganza kuwa utoaji wa hewa ya carbon utafikia kilele mwaka 2030 na kuanza kupungua baada ya hapo. Hii ni ahadi muhimu ambayo bado haijasikika kutoka kwenye nchi nyingine kubwa.

Lakini pia tunatakiwa kukumbuka kuwa kwa sasa China ni moja ya nchi zilizo mstari wa mbele duniani katika kuuza bidhaa zinazohimiza matumizi ya nishati mbadala duniani, na kupunguza utoaji wa hewa ya ukaa.

Tulichokiona mwezi huu kimetukumbusha kuwa mabadiliko ya tabia nchi ni changamoto. Safari hii wahanga wa joto kali na mafuriko ni nchi zenye nguvu kubwa za kiuchumi, huenda madhara yake si makubwa sana kama hali hii ingetokea kwenye nchi za dunia ya tatu, ambazo uwezo wake wa kukabiliana na majanga hayo si mkubwa. Kama hatua hazitachukuliwa mapema, ifikapo majira ya mvua kubwa katika nchi za Afrika, huenda kukawa na changamoto kubwa.
 
Back
Top Bottom