Mafanikio, changamoto za 2011 zituongoze kusonga mbele zaidi si kurudi nyuma

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,293
33,078
Na Gadi Solomon
NDUGU msomaji yatupasa kumshukuru Mwenyezi Mungu hata kwa kile kidogo ama kikubwa alilochotujalia katika mwaka mzima 2011.
Pia, tuwaombee wenzetu waliofikwa na maafa ya mafuriko katika maeneo mbalimbali jijini Dar es Salaam.
Vilevile, pongezi kwa Mhariri wa Makala, Ndyesumbilah Florian na timu nzima ya Mwananchi kwa kutoa fursa kwa wana

Kiswahili kupata uwanja wa kupashana na kujadili mambo mbalimbali yanayohusiana na lugha ya Kiswahili ulimwenguni kote.

Safu hii inawashukuru wote waliochangia kwa kipindi cha mwaka, mzima mada zilizokuwa zikitoka kila ijumaa na waendelee kusoma safu hii kwa manufaa yao na wengine, ambapo maarifa wanayoyapata japo kwa uchache, naamini wamekuwa

mabalozi wazuri kwa kufikisha ujumbe kwa wengine katika kuhimiza jamii kuzingatia matumizi sanifu ya lugha ya Kiswahili.

Haitakuwa rahisi kuwataja wasomaji wote, lakini kuwataja wasomaji wachache kama vile Mzee John Nchimbi, wana-Chawakama Tanzania na wadau wengine wa Kiswahili katika nje ya mipaka ya nchi yetu kupitia njia ya mtandao wa kompyuta.

Wapo waliojitoa kutuma maoni kwa njia ya baruapepe na njia ya ujumbe mfupi wa maneno kwa simu, hiyo ni namna ya kuonyesha uzalendo wao katika kutetea lugha ya Kiswahili na utamaduni wa Kiswahili kwa ujumla.
Vilevile, Baraza la Kiswahili la Taifa (Bakita) halikuwa nyuma katika kutoa mchango wake kwa ushauri na nakala za vitabu

katika kujipatia maarifa mbalimbali ili kuweza kutoa taarifa sahihi kwa jamii na wapenzi wa lugha ya Kiswahili.

Ni matumaini yangu kuwa tutaendelea kuwa bega kwa bega katika kuhakikisha gurudumu la maendeleo katika uga wa Kiswahili,maendeleo yanapatikana na yanakuwa endelevu ili tuzidi kujadili na kukumbushana au kupeana taarifa mbalimbali

zinazohusu uga wa Kiswahili.

Wapo wasomaji waliotaka kufahamu tofauti ya kolamu hii ya Tunu Yetu na ile ya mwandishi Stephen Maina ambapo kwa faida ya wasomaji wengine ni kwamba wote tunaandika kuhusiana na lugha ya Kiswahili, ambapo mwandishi wa kolamu hiyo

hujikita zaidi katika kuchambua makosa mbalimbali yanayojitokeza katika lugha ndani ya vyombo vya habari vinavyotumia Kiswahili hasa magazeti, runinga redio na kujaribu kutolea ufafanuzi wa kina katika kurekebisha miundo mbalimbali ya sentensi za Kiswahili.


Hakika safu hizi zimekuwa hazina kubwa kwa walimu na wanafunzi wa Kiswahili kwa ngazi mbalimbali kuanzia elimu ya msingi mpaka chuo kikuu, kulingana na mada zinazojadiliwa.

Vilevile, tumeshuhudia kukua kwa matumizi ya Kiswahili katika vyombo vya habari nchini na nje ya nchi kwa kuwa na idhaa

nyingi zaidi za Kiswahili ulimwenguni, ambazo zimekuwa zikiuhabarisha ulimwengu matukio mbalimbali yanayojiri ulimwenguni na kuwafanya watu kuendelea kukifahamu zaidi Kiswahili.
Changamoto kadhaa tulizokutana nazo kwa mwaka huu, ni vyema idara husika zikazifanyia kazi na kuhakikisha Kiswahili

kinatumika kama bidhaa, ambayo tutaweza kuiuza na kupanua wigo wa rasilimali ambazo zinaweza kulilete a taifa letu maendeleo.

Nao wanafunzi walioko shuleni na vyuo vikuu watumie mwaka ujao kujipanga na kusoma walau lugha moja ya kimataifa kulingana na mahitaji yao, ili kuwa na wigo mpana nwa mawasiliano na wazungumzaji wengine ulimwenguni.

Ukiacha Kiingereza ambacho ni lugha ambayo inatumika kama lugha ya mawasiliano katika ngazi ya elimu sekondari na vyuo, Kiswahili sasa ni lugha kuu ya mawasiliano.

Watanzania katika mwaka huu tumeandika historia kwa kushuhudia tukio la maadhimisho ya miaka 50 ya Uhuru wa

Tanganyika (Tanzania Bara), huku tukijivunia lugha ya Kiswahili ambayo ilitumika katika harakati za ukombozi wa taifa letu, hivyo kuweza kuyaunganisha makabila zaidi ya 120, kuishi kwa amani na upendo, jambo ambalo linasifiwa na mataifa mbalimbali hasa nchi kama Kenya na Uganda.

Kiswahili kimeendelea kuwa chachu ya maendeleo katika ukanda huu wa Afrika Mashariki kwa kutumika katika uhusiano wa biashara pia hata wageni kutoka nchi kama China.

Kwa upande mwingine tulishuhudia ripoti ya taasisi isiyo ya kiserikari ya Uwezo ikianika kwamba, idadi ya wanafunzi wa wasiojua kusoma Kiswahili katika shule za msingi yanaongezeka nchini ukilinganisha na Kenya.

Pamoja na mambo mengi, kuna kila sababu ya kumshukuru Rais Jakaya Kikwete na Serikali yake katika wazo la kuongeza wataalamu wa kati wa Kiswahili katika vyuo vikuu nchini, hasa katika Chuo Kikuu cha Dodoma(UDOM), ambapo hivi sasa kuna ongezeko la wataalamu wa Kiswahili ukilinganisha na miaka ya nyuma, ambapo changamoto imebaki katika kutengeneza fursa za ajira.


Kwa mfano, katika kipindi cha mwaka huu tulisikia kuhusu Gabon ambako Kikwete alikwenda kuhudhuria mkutano mmojawapo kiserikali na kutuletea habari njema ya kuhitajika kwa wataalamu wa Kiswahili katika kusaidia kuunda mtalaa wa Kiswahili, jambo ambalo utekelezaji wake haujazaa matunda mpaka sasa na kuzua maswali mengi, iwapo tuna dhamira ya

kweli na dhati ya kukiuza Kiswahili hasa katika kipindi hiki cha utandawazi.

Kwa jumla, tumesikia kupatikana kwa maendeleo katika Kiswahili kwa kuongezeka kwa kamusi nyingine, iliyotangazwa ndani na nje ya Afrika Mashariki, inayojulikana kama Kamusi Kibindo kutoka Kenya ambapo ilihusisha wataalamu wengine wa

Kiswahili kutoka nchi hiyo pia itaendelea kusaidia watu wa mataifa mbalimbali katika kujifunza msamiati na istilahi mbalimbali za lugha ya Kiswahili.


Pia, Waziri wa Habari, Utamaduni,Vijana na Michezo, Dk Emmanuel Nchimbi amekuwa mstari wa mbele katika kusaidia juhudi mbalimbali katika kuendeleza Kiswahili, ambapo mwaka huu alijumuika na vijana wa vyuo vikuu vya Afrika Mashariki kwa nchi tano ikiwamo Kenya, Rwanda, Burundi, Uganda na mwenyeji Tanzania katika kujadili mustakabali wa Kiswahili Afrika Mashariki.


Akiwakilishwa na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Utamaduni katika mkutano uliofanyika mjini Dodoma Dk Nchimbi aliahidi kuendelea kusaidia shughuli mbalimbali za kukuza na kuendeleza utamaduni wa lugha.
Nawatakia kila la heri Mwaka Mpya wenye baraka.

Chanzo. Mafanikio, changamoto za 2011 zituongoze kusonga mbele zaidi si kurudi nyuma
 
Silipendi neno changamoto, neno hili linapofusha moyo uone matatizo makubwa ni madogo
 
Back
Top Bottom