Madikteta, wezi wa Afrika kaeni chonjo, kwani hamjui siku wala saa

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Saturday, 13 August 2011 15:58


Ayub Rioba
LA kuvunda halina ubani. Historia inatuonyesha mifano mingi tokea zama za kale kuhusu viongozi waliolewa madaraka, wakabweteka na kujisahau. Na ukichunguza kwa makini, kila kiongozi mbaya, anayebweteka na kujisahau, pembeni mwake kuna majuha kadhaa anaowategemea kama wapambe au washauri wake.

Na mara nyingi washauri majuha humshauri kiongozi mbaya kile wanachojua, anapenda au anataka kusikia. Au kwa maneno mengine, washauri wale hubakia wakimchekeachekea, wakimsifu, kumpamba na kumweleza jinsi anavyopendwa na wananchi na jinsi nchi inavyoweza kuangamia bila yeye na jinsi ambavyo jua linasimama siku akiugua mafua, n.k.

“Mtukufu, Mheshimiwa, Mkuu wa wakuu, huwezi kuamini juzi ulipopatwa na hali ya mafua kidogo hakuna hata ndege mmoja aliruka angani katika miti ya nchi hii. Wote walisikitika na kukuombea upone haraka uje kusaidia watu wako,” ni maneno yaliyosemwa na mpambe wa kiongozi mmoja dikteta wa Afrika ambaye hata hivyo aliondolewa madarakani kwa nguvu ya umma na akakimbia kwa aibu kwenda kujifia ughaibuni miaka michache iliyopita.

Hakuna watu hatari kama wapambe wenye njaa ambao hawaamini katika kitu kingine chochote zaidi tu ya kupata mlo na kutuliza njaa zao.
Ni jambo dhahiri kuwa utapiamlo ni tatizo kubwa sana katika nchi zetu kiasi kwamba suala la kupata mlo ni tatizo la msingi kuanzia kwa mmachinga anayeuza nguo kadhaa za mtumba mkononi hadi kwa waziri wa serikali ya nchi.

Mmaachinga anapokuuzia shati au suruali ya mtumba anasisitiza: “Hapo natafuta pesa ya kula tu mjomba,” au unamsikia akisema: “Niongozee basi nipate hela ya kula.” Vivyo hivyo hata na waziri wetu anapokwenda kusaini mikataba (Kumbuka mikataba yote tuliyoingizwa mkenge, ukiwamo wa sasa wa Dowans) waziri wetu pia analia mbele ya yule anayeingia naye mkataba: “Na mie natafuta hela ya kula tu hapo ndugu mwekezaji,” au “Ongeza basi bei hapo nami nipate hela ya kula.”

Kwa vile tumezaliwa na kukulia katika nchi ambazo watu hukumbwa na baa la njaa na hata kufa, basi ni kama bongo zetu zimeandaliwa kufikiria namna ya kukabiliana na njaa muda wote. Ndiyo maana wakati mmachinga anatafuta shilingi 2,000/- kutwa nzima ili familia ile ivae na ijisitiri (katika chumba cha kupanga Manzese), vigogo wetu wanatafuta milioni 200 kwa siku ili familia zao zile (chakula sawa na cha Kempisky), zivae (nguo za wabunifu wa Ulaya kama Versace), na ziishi katika mahekalu ambayo maskini huyasoma katika hekaya za kufikirika.

Hizo tofauti tu siyo tatizo. Hakuna kokote duniani ambapo watu hulingana au kufanana kwa kila jambo. Tatizo ni pale watawala wwetu wanapotumia rasilmali za umma na kodi za wananchi kwa ajili ya anasa zao binafsi huku wananchi wengi wakiachwa kujitafutia chakula kama kuku wa kienyeji.

Na jambo muhimu ninalojaribu kulidadisi leo katika makala yangu ni tabia hii ya watawala na wapambe wao, kuhisi njaa muda wote na wakajisahau. Matokeo yake tumeyaona Tunisia hivi karibuni na tunazidi kuyaona Misri na katika nchi zingine.

Muhammad Bouaziz alikuwa amehitimu shahada ya kompyuta nchini mwake Tunisia. Lakini kutokana na mazingira yaliyojengwa na mfumo usiowajali vijana, hakupata kazi na aliishia kuwa mmachinga akiuza mbogamboga kwa toroli ili apate hela ya kula na kulisha familia yake.

Pamoja na Bouazizi kutafuta njia bora na “halali” ya kujiingizia kipato, bado alikumbana na nguvu za dola, akavumilia manyanyaso ya kila siku, hadi yalipomfika kifuani. Kazi aliyokuwa akiifanya Bouazizi ni halali japo wamachinga wa kule husumbuliwa na mgambo wa jiji kama ilivyo hapa kwetu.

Bouazizi akaamua kujiwasha moto (kujilipua) kudhihirisha hasira alizokuwa nazo dhidi ya mfumo. Maandamano yakapamba moto siyo tu kupinga uonevu aliokuwa ameonyeshwa Bouazizi bali pia kukataa mfumo uliosababisha mauti yake. Vijana wakafurika mitaani kuelezea hasira zao lakini serikali ya watawala waliojulikana kwa sifa ya ukatili na kujilimbikizia mali ikaamuru askari watumie nguvu za dola kuzima nguvu ya umma.

Mnadhimu wa Jeshi la nchi ile Rachid Ammar alipokataa kutii amri ya Rais Zile Al Abedine Ben Ali ya kuvunjilia mbali maandamano, aliondolewa na kuwekwa mwingine aliyekuwa tayari kutafuta hela ya kula kwa kunawa damu za watu.

Lakini ukweli umeanza kudhihirika. Kwamba viongozi wanaoingia madarakani kutafuta hela ya kula na wakauza rasilmali za nchi kwa manufaa yao binafsi na kusababisha madhila makubwa kwa wananchi wa kawaida siku zao zinahesabika.

Kama tulivyoona wimbi kubwa la mapinduzi ya kisiasa katika miaka ya mwishoni mwa 1980 na mwanzoni mwa 1990 wakati nchi nyingi zilivyolazimika kufuata demokrasia ya vyama vingi (bila watawala kutaka), wimbi la sasa ni la nguvu ya umma kwa watawala jeuri wanaoibia wananchi wao na kuwafukarisha kwa kutumia madaraka ya umma.

Tumeshuhudia ukweli kwamba askari na wanajeshi pia huchoshwa na utawala usiojali wananchi na unaotaka tu kutumia ubabe na ukandamizaji wakati mazingira yanayosababisha vurugu yanaandaliwa na watawala wenyewe.

Uzoefu wa Tunisia na Misri unaonyesha kuwa wakati mwingine vyombo vya dola vikiamua kuua waandamanaji si kwa sababu vinatii amri ya watawala; la hasha. Vinafanya hivyo kuwachochea wananchi wachukue hatua zaidi hadi tawala zile dhalimu zing’oke.

Ninachoweza kuwashauri watawala wa namna hiyo na wapambe wao ni kuaandaa ndege za kutosha kubeba masanduku ya almasi, dhahabu na vito vingine walivyoficha (kama alivyofanya Ben Ali wa Tunisia na mkewe) tayari kutoroka nchi zao kwa sababu hawatajua siku wala saa.

Imerudiwa kwa ombi la wasomaji

 
Hawezi kusikia kwa kuwa Mungu wako wewe aliyewapa walio wengi maono wao hayo maono hawana kwa hiyo hawana cha kupoteza kwa kuwa wao hawawezi kuona japo kwa hisia ni mpaka yatokee.Wanaamini kuwa haiwezi kutokea kwa kuwa huwa wanajaribu kuwachezesha shelea watanzania wanaona hawana uwezo huo na kwa kuwa kitabia watanzania tulio wengi mtu ama watu wenye nia njema nasi wakitufumbua macho uwa jamii inawabatiza majina machafu kama mbaguzi,mchochezi n.k.


Ila muda utaongea,Mungu amekifungua macho kizazi cha kayumba,hao ndio watakao leta mageuzi kwa kuwa kwa hivi sasa ndio wanamalizia wengine vyuoni na wengine wako street na shule za kata.Watakapo anza shughuri yao hakuna atakae simama.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom