Madalali wa Nyumba: Hali ngumu, wateja wengi wa kupanga walikuwa "nyumba ndogo" za Waume wa watu

Ngaliba Dume

JF-Expert Member
Oct 6, 2010
1,710
3,669
Kilio cha hali ngumu ya maisha kwa Januari kimeendelea kupamba moto na safari hii kimewafikia madalali wa nyumba ambao walikuwa wakitengeneza pesa chekwa hususani mwanzoni mwa mwaka.

Tofauti na ilivyokuwa miaka mingine, inadaiwa kuwa biashara ya nyumba za kupanga mwaka huu imedorora kutokana na kukosekana kwa wateja.

Mwananchi ilizungumza na wenye nyumba na madalali kadhaa wa jiji la Dar es Salaam, Mbeya, Tanga na Iringa ambao walieleza kuwa hali imekuwa tofauti kwa mwaka huu na sababu kubwa ikitajwa kuwa ni hali ngumu ya maisha.

Madalali hao walilalamika kuwa hali hiyo imesababisha maisha kuwa magumu kutokana na kutegemea kazi hiyo kuwaingizia kipato.

Mmoja wa madalali hao, Juma Kinole ambaye anafanya shughuli zake Tabata, alisema mwaka huu umeanza vibaya kwao na mambo yatakuwa mabaya zaidi endapo hali itaendelea kuwa hivyo.

Dalali huyo alieleza kuwa, awali alikuwa akipangisha nyumba mbili hadi tatu kwa siku lakini sasa hivi anaweza kumaliza wiki bila kupata mteja.

“Wateja wengi walikuwa ‘nyumba ndogo’ (vimada) na ndiyo walikuwa wanatupa kazi lakini sasa mambo yanaonekana kuwa tofauti. Hakuna wateja, inawezekana waliokuwa wanawapangishia wamejitoa kutokana na hali ngumu ya maisha.”

Kinole alisema kwa kiasi kikubwa hali hiyo imewasababisha watu waliokuwa wakijenga kuhamia hata kabla ya nyumba zao kukamilika.

“Mtu anaona bora ahamie kwenye banda lake hata kama halijaisha ili kukwepa kodi. Ukitembea sasa hivi nyumba nyingi hazina wapangaji kilio kikubwa kimekuwa pesa.”

Kando na hilo, Kinole alisema wapo wapangaji ambao wamehama nyumba kubwa na kwenda kupanga chumba au vyumba viwili kwa lengo la kupunguza gharama za kodi.

Kauli hiyo inaungwa mkono na dalali wa Ubungo, Salum Salehe anayeeleza kuwa kuna idadi kubwa ya nyumba ziko wazi hazina wapangaji na nyingine zikitakiwa kuuzwa.

“Nyumba zimekuwa nyingi hakuna wateja. Yaani nyumba ya kupanga inaweza kukaa muda mrefu bila kupata mpangaji hali haikuwa hivi. Hata kwa nyumba zinazouzwa mambo yamekuwa magumu, watu wanatangaza kuuza lakini hakuna wateja.”

Bei ya kupanga katika nyumba zilizopo Tabata Segerea zimeendelea kushuka. Zilizokuwa zikipangishwa kwa Sh200,000 zimeshuka hadi kati ya Sh170,000 na Sh150,000 kwa mwezi.

Baadhi ya wapangaji ambao walimudu kupanga nyumba nzima wameanza kupunguza matumizi kwa kuhamia katika vyumba vichache ili kuendana na hali ya kiuchumi.

Mkazi wa Tabata Segerea aliyejitambulisha kwa jina moja la Winnie alisema amelazimika kuhamia katika nyumba ya rafiki yake baada ya kukubaliana ili walipe nyumba ya pamoja ya Sh250,000 kwa mwezi akihama katika nyumba ya Sh400,000 aliyokuwa akilipiwa na mpenzi wake.

“Tunaishi marafiki watatu, wote tulikuwa tukilipiwa na marafiki zetu wa kiume lakini wote kwa sasa wamesema hawana fedha na kodi zimeisha, imebidi tukubaliane kuchangishana fedha na kupanga angalau nyumba aliyokuwa akiishi mwenzetu kwa gharama ya chini ili maisha yaendelee,” alisema Winnie.

Mbeya

Madalali wa vyumba jijini Mbeya nao wanalia hali ngumu kutokana na wapangaji wengi kushindwa kumudu gharama za kodi hivyo kutafuta nyumba zenye unafuu.

Wamesema hali imekuwa ya tofauti kwani baadhi ya watu waliokuwa wanaishi nyumba ya kupanga na kulipa kodi ya Sh500,000 kwa mwezi wameamua kuhama na kutafuta nyumba ya Sh300,000, waliokuwa wanalipa Sh300,000 wanakwenda kwenye nyumba ya Sh150,000 kutokana na mambo kubana.

Dalali wa nyumba na viwanja jijini Mbeya, Venance Mwamengo, ambaye ofisi yake ipo eneo la Mama John alisema hali sasa si nzuri kwani wapangaji wengi wanatoka kwenye nyumba na kutafuta vyumba au nyumba za bei ya chini zaidi.

“Kwa ufupi hata mimi ni dalali lakini pia mpangaji, tutakuwa na hali ngumu zaidi siku za usoni,” alisema dalali huyo.

Dalali anayefanya shughuli zake eneo la Ilomba, Kenneth Kaunda maarufu kwa jina la ‘Dalali Kidevu’ alisema hali imekuwa ngumu kwa madalali kwani wanaweza kukaa mwezi mzima bila kupata mteja wa chumba.

Kidevu alisema, “Kwanza wateja hawapatikani na hata ukimpata muda mwingine ni kama vile anakuwa anapeleleza tu kwani unaweza kuzunguka naye hata nyumba 10 lakini akiangalia chumba au nyumba nzima akilinganisha na bei, anakuambia hapana, hivyo hata sisi madalali tuna hali ngumu.”

Mmoja wa wamiliki wa nyumba za kupanga wa Soweto, aliyejitambulisha kwa jina moja la Huruma alisema kwa sasa wamiliki wengi hususan wanaopangisha nyumba nzima wamekuwa na wakati mgumu kutokana na wapangaji kugoma kuingia kwa vile bei zao zinaonekana kuwa juu licha ya kwamba zimekuwapo kwa muda mrefu.

Tanga

Ugumu huo wa biashara ya nyumba pia umeelezwa kulikumba jiji la Tanga. Dalali wa siku nyingi katika jiji hilo, Hamdani Bakari alisema hali sasa ni ngumu tofauti na zamani kwa kuwa wapangaji wengi waliokuwa wakiishi nyumba nzima sasa wanaamua kujibana na kuhamia kwenye chumba na sebule licha ya nyumba nzima kushushwa bei.

Bakari alisema sasa, nyumba nzima hazina soko na wakipewa kuzitafutia wateja wakati mwingine kukaa hata miezi mitatu bila ya kupata mpangaji tofauti na ilivyo kwa chumba kimoja kimoja au chumba na sebule.

Mtwara

Licha ya mji wa Mtwara kuanza kuchangamka kutokana na fursa ya gesi, bei ya nyumba imeanza kushuka kutokana na wamiliki kukosa wapangaji huku baadhi ya wapangaji waliopanga nyumba za gharama nao wakihamia kutokana na kushindwa kumudu gharama.

“Baada ya ujio wa gesi, nyumba zilipanda sana, pia wanafunzi nao walikuwa ni wengi sasa wamerudi kukaa hosteli hivyo nyumba zinabaki tupu inabidi sisi tuanze kazi ya kutafuta wapangaji,” alisema dalali wa nyumba mjini hapa,” Hamis Haule na kuongeza:

“Nyumba ya vyumba vinne unaipata kwa Sh300,000 lakini sasa hivi wengi wanachangia nyumba, tofauti na zamani tulikuwa tukipata mtu mmoja,” alisema.

Chanzo: Gazeti la Mwanachi
 
Mzunguko wa Fedha ukiwa mdogo utasababisha mdororo katika ukuaji wa uchumi.
Wewe na elimu yako ya social science na uchumi wapi na wapi.
Tunaongelea madalali kulia hakuna wateja na nyumba zimeshuka kodi,huoni kuwa ni nafuu?
Tunapoelekea kodi itakuwa inalipwa mwezi kwa mwezi,ukipokea mshahara unalipa kodi ya watu
 
  • Thanks
Reactions: mps
Huu mwendo katika hili naunga mkono 100%. Tuliamua kujiingiza katika maisha ya kideoni wakati sie ni kapuku tu, unaona sasa maisha yanavyotuhaibisha.

Kila mtu aishi maisha yake harisi
 
Wenye nyuma sasahivi wanataka kodi ya mwezi mmoja na si miez sitta tena kama zamani.Na ukimcheleweshea hakubughudhi kabisa
 
Back
Top Bottom