Luteni
JF-Expert Member
- Jan 9, 2010
- 2,274
- 301
Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa (CCM) na Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz (CCM), ni miongoni mwa wabunge wanne, ambao wametajwa kwamba, hawajawahi hata mara moja kuchangia mijadala kama wabunge tangu Bunge la sasa lianze mikutano yake mwaka 2005.
Katika orodha hiyo, wamo pia Mbunge wa Kwahani, ambaye pia ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Dk. Hussein Mwinyi (CCM) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema.
Aidha, Mbunge wa Karatu, Dk. Willibrod Slaa (Chadema), ametajwa kushika nafasi ya kwanza ya utendaji bungeni kati ya wabunge wote 320 wa Bunge la Tanzania akifuatiwa na Mbunge wa Iramba Mashariki, Mgana Msindai (CCM) na Mbunge wa Mpwapwa, George Lubeleje (CCM).
Hayo yamo kwenye muhtasari ulioandaliwa na asasi ya Uwazi Infoshop, ambao umebainisha kuwa wabunge hao wamewekwa katika makundi hayo, baada ya kupima kiwango cha ushiriki wao katika vikao rasmi vya Bunge na kugundua tofauti kubwa ya viwango vya ushiriki huo miongoni mwao.
Muhtasari huo wenye kichwa cha maneno: Je, wanafanya kazi kwa ajili yetu?, unapima utendaji wa wabunge kwa kuzingatia namna walivyoshiriki katika vikao vya Bunge. Kipindi kilichopitiwa ni mikutano 17, kuanzia mwaka 2005 hadi 2009 bila kujumuisha mkutano wa 18 wa Bunge wa sasa ulioanza Januari 26, mwaka huu.
Muhtasari huo pia umechambua mambo manane kuhusu Bunge la Tanzania kwa kutumia Mfumo wa Mtandao wa Taarifa za Bunge kwa Umma (POLIS) kwenye tovuti ya Bunge, zilizopatikana Januari, mwaka huu.
Mambo hayo, ni pamoja na Bunge la Tanzania kuwa wazi, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa chama kinachochangia zaidi bungeni, wabunge wa upinzani kushiriki zaidi kuliko wa chama tawala na wabunge waliochaguliwa wanachangia zaidi kuliko walioteuliwa.
Mengine ni wabunge wanaume kushiriki zaidi kuliko wanawake, wabunge 72 hawajawahi kuuliza swali la msingi hata moja, Dk. Slaa, Msindai na Lubeleje wanaongoza kushiriki bungeni, na Lowassa na Rostam wako mwisho katika ushiriki bungeni.
Bunge lina wabunge watatu wa kuchaguliwa ambao hawajawahi kuchangia mijadala ya vikao hata mara moja kwa mujibu wa POLIS. Hawa ni Dk. Hussein Mwinyi, Edward Lowassa na Rostam Aziz, ilieleza sehemu ya muhtasari huo.
Ikumbukwe kwamba hiki ni kiashiria kimoja tu cha utendaji wa wabunge; wajibu mwingine muhimu wa wabunge ni pamoja na kufanya kazi kwenye Kamati za Bunge na kushirikiana na wananchi kwenye majimbo yao, uliongeza.
Hata hivyo, muhtasari huo umemtetea Jaji Werema, ambaye hajawahi kuchangia mijadala kwa vile aliteuliwa hivi karibuni (Oktoba, 27, 2009), kama mbunge kutokana na cheo chake (Mwanasheria Mkuu wa Serikali).
Katika uchambuzi wake, muhtasari huo umewaelezea Lowassa, Rostam na Mwinyi kwamba, wamefungana kwa kushika nafasi ya mwisho kabisa (ya 319) ya utendaji bungeni; kwa kila mmoja kupata sifuri katika uzito wa ushiriki, maswali ya msingi, maswali ya nyongeza na michango bungeni.
Muhtasari huo umebainisha kuwa, anayeshika mkia katika kundi la wabunge wote, ni Dk. Mwinyi, akitanguliwa na Lowassa kabla ya Rostam.
Aliyemtangulia juu Rostam, ni Mbunge wa Bagamoyo (CCM), ambaye pia ni Waziri wa Miundombinu, Dk. Shukuru Kawambwa akiwa na mchango mmoja, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda (1), Ali Haroon Suleiman (Baraza la Wawakilishi-CCM- 2), Mohamed Seif Khatib (Uzini-CCM-2), Dk. John Magufuli (Biharamulo Mashariki-CCM-3), Mohamed Aboud Mohamed (Kuteuliwa-CCM-3), Zakia Meghji (Kuteuliwa-CCM-3) na Yusufu Makamba (Kuteuliwa-CCM-4).
Kwa mujibu wa uchambuzi huo, Dk. Slaa ameshika nafasi ya kwanza kwa kujizolea jumla ya ushiriki 268, maswali ya msingi (33), maswali ya nyongeza (106) na michango (129) bungeni.
Wa pili, ni Msindai, mwenye jumla ya ushiriki 256, maswali ya msingi (58), maswali ya nyongeza (109) na michango (89), huku Lubeleje akishika nafasi ya tatu kwa kupata jumla ushiriki 225, maswali ya msingi (46), maswali ya nyongeza (98) na michango bungeni (81).
Wanaofuatia kwenye mlolongo huo, na jumla ya ushiriki wao kwenye mabano ni Diana Chilolo (Viti Maalum-CCM- 214), William Shellukindo (Bumbuli-CCM- 208), Zitto Kabwe (Kigoma Kaskazini-Chadema- 199), Godfrey Zambi (Mbozi Mashariki-CCM- 192), Juma Killimbah (Iramba Magharibi-CCM- 186), Jenista Mhagama (Peramiho-CCM-185), Suzan Lyimo (Viti Maalum-Chadema-179), Michael Lekule Laizer (Longido-CCM-168), Lucas Selelii (Nzega-CCM-163) na Job Ndugai (Kongwa-CCM- 161).
Wengine ni Profesa Raphael Mwalyosi (Ludewa-CCM-152), Mohamed Rished (Pangani-CCM-150), Hamad Rashid Mohamed (Wawi-CUF-149), Said Arfi (Mpanda Kati-Chadema-149), Siraju Kaboyonga (Tabora Mjini-CCM-149), Esther Nyawazwa (Viti Maalum-CCM-149), Ruth Msafiri (Muleba Kaskazini-CCM), Raynald Mrope (Masasi-CCM-148) na Mohamed Mnyaa (Mkanyageni-CUF-144).
Wengine ni Chrisant Mzindakaya (Kwela CCM- 144) na Hebert Mtangi (Muheza- CCM- 144). John Cheyo mbunge pekee wa UDP kwa jimbo la Bariadi Mashariki amechangia mara 142. Wabunge wengine wanafuatia chini ya hapo.
Muhtasari huo uliosambazwa kwenye mtandao wa kompyuta, unatoa picha muhimu kwa umma kujadili namna wabunge wanavyowakilisha maslahi ya wananchi.
Pia, unatoa fursa kwa kila chama cha siasa na kila mbunge kujitathmini zaidi namna ambayo wamekuwa wakihudumia maslahi ya wananchi kwenye majimbo yao.
CHANZO: NIPASHE