Hashpower7113
JF-Expert Member
- Sep 26, 2011
- 1,353
- 2,137
TEARS OF THE SOUL (MACHOZI YA ROHONI)- 1
Mtunzi: Aziz Hashim (Hash Power)
NB: UNAWEZA KUIPATA SIMULIZI HII TAMU KUANZIA MWANZO
MPAKA MWISHO KWA MFUMO WA e-Book (PDF)
UTAKAYOISOMA KWENYE SIMU YAKO KWA SH. 5000/= TU
NICHEKI WHATSAPP 0719401968!
“Mke wangu!”“Abee mume wangu!”
“Jiandae leo nikitoka kazini nataka tutoke ‘out’!”
“Mh! Hata sijisikii kutoka leo mume wangu.”
“Kwa nini tena jamani?”
“Basi tu! Sijisikii kutoka!”
“Kwani yale ya jana bado hayajaisha mke wangu?”
“Aah! Yameisha lakini sijisikii tu kutoka.”
“Umepika nini leo.”
“Sijapika.”
“Sasa tutakula nini?”
“Nunua chipsi!”
“Vipi ule mzigo ulienda kuufuatilia?”
“Hapana! Sijaenda.”
“Kwa nini sasa hujaenda jamani?”
“Nimechoka! Sijisikii kufanya chochote leo!”
“Sasa, kwa nini hutaki tutoke mke wangu? Huoni itasaidia...” mlio wa simu upande wa pili ulisikika kuonesha kwamba simu ilikuwa imekatwa. Ilibidi nipige tena, simu ikaita kidogo kisha ikapokelewa.
“Kwa nini unanikatia simu wakati sijamaliza kuzungumza na wewe?”
“Sijakata!”
“Kumbe ni nini sasa?”
“Labda network!”
“Mh! Haya sawa! Basi baadaye...”
Nilikata simu na kubaki nimeishikilia, nikiitazama mithili ya mtu aliyekuwa anatazama kitu asichokijua. Ilikuwa ni simu ninayoitumia siku zote lakini hata sijui nini kilitokea, nikawa naitazama tu, hisia chungu zikipita ndani ya moyo wangu.
Why are doing this to me Joanna!” (Kwa nini unanifanyia haya Joanna!) nilijiuliza huku nikiwa bado naitazama ile simu.
Mabadiliko makubwa aliyokuwa nayo mke wangu kipenzi, Joanna yalisababisha niwe na huzuni kubwa ndani ya moyo wangu! Alikuwa amebadilika, hakuwa Joanna yule ambaye nilifunga naye ndoa takatifu miaka miwili iliyopita! Hakuwa Joanna yule ninayemjua, alibadilika mno na mabadiliko hayo ndiyo yaliyonifanya niwe na huzuni kubwa kiasi hicho ndani ya moyo wangu.
“Alex!” sauti ya mfanyakazi mwenzangu ndiyo iliyonizindua kutoka kwenye lindi la mawazo, nikakurupuka kutoka kwenye ile hali niliyokuwa nayo na kuanza kujifanya nipo bize kwenye kompyuta yangu.
“Machozi yanakutoka, una tatizo gani?”
“Aah! Nina matatizo ya macho Joel, nikiangalia kompyuta muda mrefu machozi yanatoka tu yenyewe,” nilimdanganya, uongo ambao aliukubali.
“Jitahidi kula karoti, zinasaidia sana na kama hali itaendelea hivi inabidi ufanye mipango ya kupata miwani.
“Sure! Hali inazidi kuwa mbaya,” nilimjibu huku nikijifuta.
“Jioni nina mtoko na shemeji yako, nilitaka kampani yako! Kama vipi mpigie shemeji tuungane, mimi na ‘wife’ na wewe na shemeji!
“Dah! Kuna wageni nyumbani, shemeji yako hawezi kutoka ila nitakupa kampani usijali!”
“Basi poa,” alisema Joel, tukagongesheana mikono ‘kishkaji’ kisha akatoka huku akiniambia kwamba nijiandae mambo yakiwa tayari atanishtua. Alipotoka nilishusha pumzi ndefu na kukaa vizuri kwenye kiti chake. Uragiki wangu na Joel ulikuwa umevika mipaka ya urafiki wa kawaida, alikuwa ni kama ndugu kwangu, nilimfahamu mkewe, alimfahamu mkewe na familia zetu zilikuwa na kawaida ya kujumuika pamoja mara kwa mara.
Mwenzangu yeye alitangulia kuingia kwenye ndoa kabla yangu na hata wakati naanza michakato ya kutaka kuingia kwenye ndoa, alikuwa ndiyo mshauri wangu mkubwa.
Nakumbuka mara kadhaa nilipomueleza kuhusu mipangoyangu ya kuingia kwenye ndoa na Joanna, alinishauri kwamba kama ni kweli nataka mwanamke wa kuishi naye, ni bora nifanye kama yeye, nikaoe mwanamke wa kijijini na kuja naye mjini lakini nilimkatalia! Nilikuwa nampenda sana Joanna na kwake nilikuwa kama kipofu! Sikuona wala sikusikia.
Hali hiyo ilisababisha sasa hata matatizo yaliyokuwa yakiendelea kunisibu kila siku ndani ya ndoa yangu, yabaki kuwa siri yangu. Nitamwambia nini wakati kuanzia mwanzo alishanishauri kwamba nikaoe kijijini lakini nikamkatalia mpaka ikafika kipindi tukataka kugombana?
Sijui ni sababu zipi zilizomfanya Joel ayapinge sana mahusiano yangu na Joanna siku za mwanzo kwani nakumbuka si mara moja au mara mbili alipokuwa akinipinga! Alishasema sana, alishanionya sana kuhusu uamuzi wangu wa kuanzisha mahusiano ‘serious’ na Joanna lakini kama unavyojua tena moyo unapopenda, unakuwa kama kipofu.
“Yataisha tu! Hili nalo litapita, nitakuwa sawa na Joanna, tutaendelea na maisha yetu kama kawaida,” nilijipa moyo. Kwa jinsi kichwa changu kilivyokuwa kimevurugika, sikuweza tena kuendelea kufanya kazi, niliinuka na kuzima kompyuta yangu, nikafungafunga mafaili niliyokuwa nayafanyia kazi na kutoka mpaka kwenye ‘kantini’ iliyokuwa nje, jirani na kazini kwetu.
Nikiwa pale kantini, angalau kidogo nilichangamka kutokana na mazoea ya kucheka na kila mtu niliyokuwa nayo! Mara huyu kanitania hili, yule kanitania lile, ilimradi burudani. Niliagiza juisi na kujumuika na watu kadhaa waliokuwa wakitazama runinga pale nje, stori za hapa na pale zikaendelea na kiukweli, nilisahau kwa muda kero zilizokuwa zinanikabili.
Mara simu yangu ilianza kuita, nilipotazama namba ya mpigaji, alikuwa ni Joel.
“Uko wapi Alex!”
“Nipo kantini hapa nje.”
“Nimekuja ofisini kukushtua kwamba muda wa kuondoka umefika naona patupu! Nakuja basi jiandae tuondoke,” aliniambia Joel na kukata simu.
Muda mfupi baadaye, alinifuata pale kantini, nikainuka na kuwaaga marafiki zangu tuliokuwa tukipiga stori, tukaongozana na Joel mpaka kwenye gari lake, mwenzangu yeye alishafanikiwa kununua gari dogo la kutembelea, Toyota Carina.
“Twende kwanza nyumbani tukampitie shemeji yako, nataka leo twende sehemu moja nzuri sana, tukale, kunywa na kufurahi!” alisema Joel huku akiendesha gari lake. Tulitoka Kurasini na kwenda moja kwa moja mpaka Tabata, nyumbani kwa Joel.
Hatukukaa sana, mkewe alishajiandaa na kupendeza, akaja tukasalimiana naye kisha akaingia kwenye gari, safari ya kuelekea mahali Joel alikokuwa amepanga ikaanza. Sikuwa najua tunaenda wapi.
Aliendesha gari mpaka Kinondoni, tukapita jirani kabisa na mahali nilipokuwa naishi.
“Kwani si tunampitia dada?” alihoji mke wa Joel, akimaanisha mke wangu, mumewe akawahi kumjibu kwamba alikuwa na wageni kwa hiyo hatajumuika nasi. Swali lake ni kama liliutonesha moyo wangu, nikatoa simu yangu na kutafuta namba yake.
Nilitaka nimtaarifu kwamba nitachelewa kidogo maana isije ikawa fujo tena baadaye nitakaporudi kama kawaida yake.
“Natoka na rafiki zangu, nitachelewa kidogo kurudi,” nilimtumia ujumbe mfupi, kisha nikashusha pumzi ndefu na kusubiri atakachokijibu.
“Niletee chakula kwanza, wewe hata kama unataka kwenda kulala hukohuko shauri yako.”
“Siwezi kukuletea chakula sasa hivi! Nipo mbali, kama ni chipsi si uagize hapo nje kwa wagosi?”
“Kwa hiyo umeamua kunishindisha na njaa si ndiyo? Sawa, nashukuru!” ilisomeka meseji yake.
Ikabidi nimtumie nyingine: “Nakushindisha na njaa kivipi wakati ndani kuna kila kitu, isitoshe nimekuachia fedha? Si suala la kuagiza tu hapo nje? Anyway ngoja nimpigie mimi simu mgosi akuletee, unataka chipsi na nini?”
“Sina haja! We endelea na mambo yako,” ilisomeka meseji ambayo ilinikata maini kabisa. Nikaamua kuachana naye.
“Vipi?” aliuliza Joel baada ya kuniona sipo sawa, nikamjibu kwa kifupi tu, safari ikaendelea. Tulienda mpaka Mikocheni, kwenye kiwanja kimoja tulichokuwa tunapenda sana kwenda, Glitters Grill. Hakikuwa kiwanja maarufu sana lakini kiukweli palikuwa pazuri sana.
Palikuwa na huduma nzuri ya vyakula, vinywaji, muziki laini na sehemu nzuri za kupumzikia. Nilifurahi sana kugundua kwamba kumbe safari yetu ilikuwa ikija kuishia hapo, nikamshukuru Joel kwa sababu nilikuwa na uhakika kwamba nita-enjoy kwelikweli na kusahau shida zote zilizokuwa zinanikabili.
Baada ya kupaki gari, tuliteremka na kupokelewa na wahudumu wachangamfu, wakatuchagulia sehemu nzuri ya kukaa, kwenye bustani za maua zilizokuwa zinatunzwa vizuri.
Cha kwanza ilikuwa ni kuagiza chakula, kila mtu aliagiza anachokitaka, mimi niliagiza ugali na makange ya kuku, chakula ninachokipenda sana. Shemeji yeye aliagiza chipsi kuku na Joel aliagiza ugali na samaki mzima.
Muda mfupi baadaye vyakula vililetwa, tukaanza kula huku stori za hapa na pale zikiendelea, nikijitahidi sana kujichangamsha lakini wapi!
“Shemeji leo umepooza, siyo kawaida yako! Sisikii zile stori zako zile,” alisema mke wa Joel na kusababisha wote tucheke. Nikiwa na furaha huwa napenda sana kupiga stori za kuchangamsha genge ambazo hufanya watu wanaonizunguka muda wote wawe wanacheka lakini siku hiyo ilikuwa tofauti.
Nilijitahidi kujichangamsha lakini huzuni iliyokuwa ndani ya moyo wangu haikufichika, ikabidi nisingizie kwamba nilikuwa na maumivu ya kichwa yanayotokana na matatizo ya macho yaliyokuwa yananiandama! Wote huo ulikuwa ni uongo, Joanna ndiye aliyesababisha niwe kwenye hali hiyo.
Basi Joel aliniunga mkono, wote wakawa wananishauri kula sana karoti na mbogamboga kwani husaidia kurekebisha matatizo ya macho.
Baada ya kumaliza kula, wenzangu walianza kupiga moja moto moja baridi! Joel na mkewe wote walikuwa wanywaji lakini mimi pombe zilikuwa hazipandi kabisa! Ikabidi niagize juisi na kwa sababu walishanizoea, hakukuwa na aliyehoji.
Hata hivyo, wakati naendelea kunywa juisi, wenzangu wakianza kuchangamka kwa kilevi, akili ilinituma na mimi kujaribu mbili tatu nikiamini pengine naweza kuwa na furaha kama wenzangu.
“Hata mimi nilitaka kukushauri hivyohivyo! Itakusaidia kupunguza maumivu ya kichwa, mhudumuuu!” aliita Joel ambaye hata sauti yake sasa ilishaanza kubadilika, akaja ambapo nilimuagiza kinywaji ambacho kabla sijaachanana mambo ya ulevi nilikuwa nikikipendelea.
Muda mfupi baadaye, mhudumu alikuja akiwa na chupa kubwa ya Bacardi, akaifungua na kuiweka mezani, kazi ikaanza.
Muda mfupi tu baadaye, tayari nilishaanza kulewa, uchangamfu wangu uliokuwa umepotea, ulianza kurudi kwa kasi ya ajabu, stori zikawa zinapigwa na kusababisha wote tuwe tunacheka sana.
Huwezi kuamini, nilisahau kabisa matatizo makubwa yaliyokuwa yananisibu, ikawa ni furaha kubwa kwelikweli utafikiri hakuna kilichotokea. Ilipofika majira ya saa tatu, ilibidi nimueleze Joel kwamba sitaweza kuendelea kujumuika nao, inabidi nirudi nyumbani.
“Mbona mapema?”
“Aah! Si unajua nyumbani kuna wageni, siwezi kurudi usiku sana, tena nikiwa nimelewa! Inaweza kuleta picha mbaya,” nilisema, basi ikabidi azungumze na mkewe na kwa pamoja, walikubaliana kwamba Joel anipeleke mpaka nyumbani kwangu kisha arudi waendelee ‘kula bata’.
Tulitoka na kwenda mpaka kwenye gari la Joel, tukawa tunaendelea kupiga stori za hapa na pale huku tukicheka kwa furaha. Nilijitahidi sana kuficha kilichokuwa ndani ya moyo wangu kwa sababu siku zote huwa nina kasoro moja, ninapokunywa pombe basi uwezo wa kutunza vitu moyoni huwa mdogo sana.
Siku hiyo nilijitahidi sana, hatimaye tukawasili Kinondoni, alinipeleka mpaka nyumbani kwangu, akaniteremsha kisha tukaagana. Huku nikipepesuka nilielekea kwenye geti dogo la kuingilia, kwa kuwa nilikuwa na funguo, nilifungua na kuingia ndani lakini hapohapo nikakumbuka suala la mke wangu kuhusu chakula.
Kwa jinsi nilivyokuwa namjua, endapo ningeingia nikiwa sina chakula chochote mkononi, halafu nimelewa, ugomvi mkubwa ungeweza kuibuka! Sikuwa nataka kugombana naye, sikuzoea kabisa maisha ya purukushani kwa hiyo niliamua kumpigia simu kijana aliyekuwa na kibanda cha chipsi jirani na hapo nyumbani.
Nikamuagiza chipsi kuku na soda huku nikimsisitiza awahishe! Sikutaka kuingia ndani, kwa hiyo nilisogea pembeni na kukaa kwenye kibaraza, nikiwa namsubiri kijana huyo aniletee chipsi ndiyo niingie ndani.
Basi nikiwa nimekaa pale kibarazani, nikiendelea kubofabofya simu yangu, mlango wa ndani ulifunguliwa! Alikuwa ni mke wangu.
“Vipi mwenzetu mbona umekaa nje?”
“Nasubiri chipsi nimemuagiza dogo hapo analeta.”
“Ndiyo ukae nje? Unanidanganya si ndiyo?”
“Nakudanganya nini tena mke wangu?”
“Yaani umetoka kwa wanawake zako huko, umeona haitoshi unafika nyumbani badala ya kuingia ndani unaanza kuchati hapa nje, hivi wewe mwanaume unanichukuliaje? Nakuuliza unanichukuliaje?” alisema Joanna huku akinisogelea mwilini. Ilibidi nisimame kwa lengo la kutaka kumuelewesha vizuri.
“Nachati na nani mke wangu, mbona unanihisi mambo mabaya bila sababu!”
“Halafu umelewa si ndiyo? Nakuuliza, umeenda kulewa tena si ndiyo?” alisema huku safari hii akiwa amenikwida shati nililokuwa nimevaa shingoni.
“Nimekunywa lakini sijalewa! Nilikwambia tutoke leo ukakataa, sasa ulitaka nifanye...” kabla sijamalizia kauli yangu, kengele ya getini iligongwa kuonesha kulikuwa na mtu, Joanna akaachia ‘msonyo’ mkali na kunisukuma!
Akatembea harakaharaka kuelekea kule getini, alikuwa ni yule kijana niliyemuagiza chipsi. Kwa kuwa sikuwa nimemlipa, ilibidi na mimi nisogee huku nikifungua waleti yangu kwa lengo la kutoa fedha.
“Nani amekuagiza?”
“Broo amenipigia simu,” alisema yule kijana wa chipsi, nikawa tayari nimeshafika.
“Mimi ndiyo nimemuagiza,” nilisema huku nikitoa noti ya shilingi elfu kumi na kumpa, akaipokea na kutoa chenji. Joanna wala hakuwa amempokea na kwa jinsi alivyokuwa amesimama na kuniziba, hata mimi nilishindwa kumpokea.
“Uliagiza kwa ajili ya nani?”
“Kwa ajili yangu na wewe, sijala na najua na wewe hujala.”
“Hapana! Mimi sitakula, sikia dogo, wewe umeshakula?”
“Hapana sista!”
“Basi hiyo moja ya kwangu utakula wewe sawa eeh!” alisema Joanna huku akisogea pembeni. Ikabidi nimpokee mfuko mmoja wa chipsi pamoja na chenji, sikutaka kuongeza neno, basi akaondoka akiwa amefurahi, nikafunga mlango huku nikiwa nimefedheheka sana ndani ya moyo wangu.
Joanna hakusema chochote, akawa ameuvuta mdomo kisawasawa na kutembea harakaharaka kuelekea ndani, na mimi nikawa namfuata. Tuliingia ndani, mimi nikakaa sebuleni, Joanna akapitiliza chumbani.
Sikuwa nimeagiza chipsi kwa ajili yangu, nilishashiba huko nilikotoka lakini sikutaka Joanna ajue kwamba nimekula ndiyo maana niliagiza sahani mbili kwa hiyo kitendo cha Joanna kukataa kuzipokea, tena mbele ya yule kijana, kilinifanya niishiwe nguvu kabisa.
Nikiwa nimekaa pale sebuleni, nikiwa hata sijui nifanye nini sasa, Joanna alitoka na kunisogelea, akionesha bado kutaka shari kwelikweli.
“Sikiliza nikwambie! Kuanzia leo kila mtu atakuwa analala chumba chake, nimechoshwa na maudhi ya kila siku.”
“Khaa! Mke wangu, kwa kosa lipi hasa mpaka ufikie uamuzi huo? Nimekufanyia nini kikubwa?”
“Ndiyo nimeshasema! Kama kuna kitu unataka kwenda kuchukua chumbani nenda, nataka nilale mimi,” alisema, nikamwambia sina cha kuchukua, basi akaelekea chumbani na kubamiza mlango kwa nguvu, nikasikia akiachia msonyo mkali.
Kwa kuwa nilikuwa nimekunywa, haukupita muda mrefu nikapitiwa na usingizi palepale kwenye sofa nilipokuwa nimekaa. Nilipokuja kuzinduka, ilikuwa ni usiku sana, majira ya kama saa nane, kwa mbali nikawa nasikia kama mtu anaongea na simu. Nilipotega masikio mazuri, niligundua kwamba alikuwa ni Joanna, mapigo ya moyo yakaanza kunienda mbio kwelikweli.
Niliinuka na kuanza kusogea upande wa chumba chetu cha kulala! Kweli alikuwa ni Joanna na ilionesha kama anazungumza na mwanaume maana nilimsikia mara kwa mara akimshukuru ‘asante baba’, na maneno mengine ya aina hiyo.
Joanna alikuwa na mapungufu mengi sana ambayo kwa mwanaume kumvumilia, ilikuwa inahitaji moyo kwelikweli lakini siku zote nilikuwa naamini kwamba ipo siku atakuja kubadilika. Sikuwahi kuhisi kwamba kwenye mapungufu yake hayo, pia ana tabia ya kunisaliti, sikuwahi.
Siku zote nilikuwa naamini kwamba mke wangu ni miongoni mwa wanawake waaminifu sana kwenye ndoa lakini kumbe nilikuwa najidanganya! Mapigo ya moyo yaliendelea kunienda kwa kasi kubwa, kijasho chembamba kikawa kinanitoka nikiwa naendelea kumsikiliza.
Nadhani mwenyewe hakuwa anajua kwamba namsikiliza, aliamini nitakuwa nimelala fofofo hasa ukizingatia kwamba nilikuwa nimepasha kidogo. Pengine hata uamuzi wa kuja kuniambia kwamba tunatakiwa kutengana vyumba, alikuwa anatafuta uhuru wa kufanya upuuzi wake bila kuulizwa chochote.
“Basi tuchati baba,” alisema kisha akakata simu. Nikiwa bado katika hali hiyo, wazo lilinijia kichwani mwangu kwamba nimgongee mlango ili ajue kwamba nimemsikia. Hata hivyo, upande mwingine wa nafsi yangu ulikataa, ningeweza kusababisha matatizo makubwa zaidi usiku huo, ikabidi nirudi pale kwenye sofa, safari hii machozi yalikuwa yananitoka kwa uchungu.
Sikupata usingizi tena mpaka kulipopambazuka. Akawahi kuamka kama kawaida yake na alipotoka, alinikuta nikiwa nimekaa kwenye sofa, nikiwa nimejiinamia. Hakunisemesha chochote, hata salamu yake hakutana kunipa, akanipita kama hajaniona na kwenda kufungua mlango mkubwa wa nje.
“Siku nyingine kama unajijua huwezi kula siyo kuniletea uchafu ndani kwangu, usafi huwa unafanya wewe?”
“Joanna!” nilisema kwa jazba huku nikisimama. Alipoona nasimama, na yeye aliacha kila alichokuwa anakifanya, akanisogelea kisharishari, tukawa tunatazamana.
“Ndiyo hivyo nimeshasema! Au unatakaje?”
“Nimekusikia usiku ukiwa unazungumza na simu, unaweza kuniambia ulikuwa unaongea na nani?” nilimuuliza huku nikitetemeka, basi akacheka kwa dharau na kuanza kunitazama kuanzia juu mpaka chini.
“Simu yangu, unataka kunipangia matumizi? Mbona wewe ukienda kwa hao malaya zako mimi sikuulizi chochote? Tena ukome kunifuatafuata, kila mtu ajue ustaarabu wake,” alinijibu kwa nyodo.
Sikuwahi kupandwa na jazba kama siku hiyo. Nilitamani nimkamate na kumfinyangafinyanga kwenye mikono yangu, nilitamani kumzibua kisawasawa, nilitamani hata nikachukue kisu na kumchinja kama kuku lakini kuna sauti ndani yangu ikawa inanituliza.
Itaendelea hapo chini!