Lissu, Zitto na Magufuli ni wazalendo wa kweli wa nchi hii..

Interest

JF-Expert Member
Apr 11, 2015
3,433
7,055
NAMPENDA RAIS MAGUFULI

Ni Rais mzalendo kwa nchi yake. Ana uchungu sana kuona watu wanatajirika kwa rasilimali za umma. Ni kiongozi ambaye anataka kuona watu wananufaika kwa jasho halali na siyo upigaji.

Ni Rais jasiri mno. Anaweza kuingia kwenye anga ngumu na kuzitikisa. Kujenga nchi yenye heshima unahitaji kiongozi mkuu mwenye uthubutu kama Magufuli a.k.a John The Iron 'Chuma'.

Ni Rais ambaye yupo tayari kuingia kwenye mgogoro wowote wa ama ndani au nje, mradi tu asimamie kile ambacho anakiamini.

Iwe yupo sahihi au anakosea, ikiwa yeye anajiona yupo sahihi, Rais Magufuli huwa hapindi. Husimamia anachokiamini kwa nguvu zote.

Si mnafiki, si mwoga, si wa nyekundu na njano au nusu kwa nusu, akisema nyekundu, keshokutwa utamkuta na nyekundu yake. Hana ndimi mbili.

NAMPENDA TUNDU LISSU

Siku zote hutafuta makosa ya Serikali na kuyaweka wazi. Hata pale ambapo kila mtu huamini Serikali imepatia na kuishangilia, Lissu akiibuka utampenda tu.

Anafahamu mantiki ya kuwa mpinzani kwa nchi za Afrika hususan Tanzania. Anatambua kuwa yeye si sehemu ya watu wanaopaswa kuiimbia mapambio Serikali inapofanya vizuri. Anajua kuwa uhai wa upinzani ni makosa ya Serikali na Chama Tawala, kwa hiyo anakosoa tu.

Uzuri wa Lissu ni kwamba hakosoi ilimradi aonekane anakosoa, isipokuwa hukosoa kwa hoja na vielelezo yakinifu. Lissu akizungumza, hata kama sauti yake na maneno yake yanakera lakini wewe sikiliza ujumbe, hutaambulia sifuri.

Ukiona Lissu anafungua kinywa ujue amejipanga. Japo yapo maeneo mengi huonekana mpiga kelele lakini ukiona analibebea bango jambo ujue ana hoja za msingi.

Ni faida kubwa kuwa na Lissu katika nchi hii, maana haogopi kukosoa. Haogopi nafasi ya anayemkosoa.

Katika nchi ambayo watu wengi wanaogopa kufunua vinywa vyao kumkosoa Mkuu wa Nchi, angalau sauti ya Lissu itasikika ikikosoa. Akiwa bungeni au nje ya Bunge, msamiati unaoitwa woga, haumo kichwani kwa Lissu.

Unamhitaji Lissu kumfanya mtawala asibweteke. Hata kama mtawala anafanya vizuri, uwepo wa Lissu husaidia kuchokonoa hata makosa madogo yenye kujificha na kuyaweka wazi. Katika nchi ni hasara kubwa kukosa watu wa kuikosoa Serikali.

NAMPENDA ZITTO KABWE

Mwanasiasa muungwana na mzalendo kwa nchi yake. Si mtoa lugha za kushambulia, isipokuwa hujikita katika kujenga hoja zenye kuifaa nchi.

Ni mpinzani lakini Serikali inapofanya sawa husifia. Serikali inapokosea husimama na kukosoa bila woga.

Kila jambo linalofanyika kwa masilahi ya umma hutakosa kauli ya Zitto. Kauli yake inaweza kuwa chanya au hasi kulingana na mapokeo yake.

Tabia yake ya kuisifu Serikali inapofanya vizuri na kuikosoa inapofanya vibaya, humfanya wakati mwingine ajikute anapokea mashambulizi kila upande; kutoka Chama Tawala, vilevile kwa wapinzani wenzake.

Zipo nyakati Zitto hujikuta anatofautiana na wapinzani wenzake pale anapoona hawapo sawa. Ndiye mpinzani anayeongoza kwa kushambuliwa na wapinzani wenzake, wakati huohuo akishambuliwa na watu wa utawala.

Ni mwanasiasa mwenye maono makubwa. Hoja zake si za kukosoa tu, isipokuwa hukosoa, husahihisha na kuelekeza njia ya kufikia jawabu.

Akisimama bungeni huwa hasemi "Serikali imeshindwa", bali husema " Serikali inatakiwa ifanye haya ili ifanikiwe", daima hutoa hoja zenye thamani kubwa. Hutoa hoja za dhahabu. Zitto si mlalamikaji, ni mtoaji wa ufumbuzi kisha husherehesha ufumbuzi wake.

Wakati mwingine hoja zake na namna ambavyo huzitoa kwa uchambuzi wa kina, huwafanya watu waone anajifanya anajua. Kiukweli Zitto ni fundi hasa katika kujenga hoja.

Muogope sana Zitto akizungumzia jambo baada ya kitambo japo kifupi. Hapo ujue tayari ameshasoma na ameshakuwa na pointi nyingi kichwani.

Unamhitaji Zitto kwa ajili ya kupata sura ya pili, maana anapokosoa sura ya kwanza, huja na uchambuzi wa kina kuhusu faida za sura ya pili. Ndiye kiongozi mwenye hoja mbadala.

Ni tunu kwa nchi kuwa na Zitto Kabwe. Ni kiongozi ambaye huwa hafichi hisia zake. Akiumizwa huwa hanyamazi.

HITIMISHO

Tunamhitaji Rais Magufuli kwa nafasi yake na utashi wake wa kizalendo.

Tunamhitaji Lissu kwa jicho lake la kuyasaka makosa ya Serikali na kuyaweka wazi.

Tunamhitaji Zitto kwa maono mapana na hoja mbadala zenye tija kwa taifa.

Mwisho kabisa, Rais Magufuli, Lissu na Zitto wote ni Watanzania na wanaipenda sana nchi yao. Hilo ndilo ambalo naliona kwa wote hao.

Rais Magufuli anataka mabadiliko makubwa kwenye nchi ili taifa linufaike kwa rasilimali zake, hii ni kwa sababu Rais Magufuli anaipenda sana Tanzania yake.

Lissu anakosoa mbinu ambazo Rais Magufuli anazitumia kwa sababu anaona zinaweza kuigharimu nchi. Lissu anajua kuwa nchi haiwezi kubeba gharama bila yeye kuathirika. Hii ni kwa sababu Lissu anaipenda sana Tanzania yake.

Zitto anatoa hoja za utatuzi wa changamoto za sekta ya madini, akisahihisha hatua za Rais Magufuli kwa sababu anaamini kwamba Rais Magufuli hapaswi kuachwa peke yake kwenye vita hii ya uchumi kupitia madini ya Tanzania. Hii ni kwa sababu Zitto anaipenda sana Tanzania yake.

Nawapenda sana hawa wazalendo wa nchi hii. Kila mmoja ana nia njema. Ni vizuri kusikilizana na kukopeshana kama siyo kuazimana mawazo ili kufikia mafanikio ya pamoja kama nchi.

Tanzania haina malaika, kwamba akifanya jambo asikosolewe hata kama ni jema kiasi gani. Wanaokosoa nao ni Watanzania wazalendo. Vema kusikilizana. Mwisho kabisa wote wanaipenda Tanzania.

Wasioipenda Tanzania wote wapo kimya, hawana maoni, wala hawawezi kuingia kwenye malumbano, maana wanaogopa 'kuamsha dude', wakifunua vinywa watakumbushwa usaliti wao kwa nchi na wizi waliofanya.

Kila mtu aachwe huru kutoa maoni yake. Nchi inawahitaji Rais Magufuli, Lissu na Zitto kwa wakati mmoja.

Imeandikwa na Luqman MALOTO
-----------

Mtazamo wangu: Zitto ni mchumi mzuri, Lissu ni mwanasheria mzuri na Rais Magufuli ni mtendaji na msimamia UKWELI.

Kwa maslahi mapana ya nchi, hawa watu watatu ni watu muhimu sana wakifanya kazi kwa mwendo huu huu kwa kuwa najua hawawezi kufanya pamoja..

Nchi yetu tamu sana..
 
Magufuli angekuwa nje ya system ya CCM angefanya vizuri zaidi ya hivi, tatizo ni CCM ambao wanamchelewesha na watafanya Magufuli asifanye vizuri zaidi, kwa kuwa muda mwingi anautumia kwa kurekebisha makosa yao wakati mwingine ana lazimika kutumia muda mwingi kuwalinda CCM ili wasiishie jela,maana yake akiamua kufanya kazi kwa weledi hasa kwa kufuata taratibu na sheria nusu ya CCM Kama siyo wote wataishia jela,kwa hiyo mchawi wa maendeleo na Magufuli ni CCM wenyewe.
 
andiko lenye mizani, sio kila mara lazima tufikirie kichama chama ,safi sana mie naona Magufuli anauthubutu tatizo maono kwake ni tatizo hapo anahitaji watu kama Zitto na Lissu na wengine wenye uono wamsaidie njia ya kwenda nae ni mzuri wa kusimamia watu waende wapi
 
Kwa tindu lissu hapo nakataa lissu sikuzote ni mshambuliaji tu way chama tawala hata akimsifia magufuli Leo atamtukana kikwet au mkapa hapo hapo ili kusafisha chama chake....

Nakubali umeandika Uzi mantinki sana
 
Analysis yako ni nzuri sana, hao wote ni wazalendo wa kweli.

Magufuli ni mzalendo, ana nguvu za dola, ni Amir kesho mkuu, lakini uzalendo wake hautatufikisha salama tuendako. Amedai hafukui makaburi, hapa uzalendo wake unaingia mashakani. Uzalendo wake hautatufikisha kule watanzania wanapopatamani kwa kuwa mbele anafika anagonga mwamba. Na kwa kweli kwa kuwa ndani ya ccm tayari namwona mzalendo aliyeshindwa.

Tundu Lisu ni mzalendo nakubaliana nawe. Uzalendo wake unakosa nguvu kwa kuwa upande wa mzalendo mwingine Magufuli wenye nguvu za dola unamkandamiza na kumnenea kila lililo baya. Lisu ana uchungu na nchi yake, mpaka Mimi ninatamani kuwa kama yeye. Wenzake wa UKAWA ni waoga, hawana ujasiri kama wake ndiyo maana inaonekana kana kwamba ni one man show. Magufuli asipotoshe umma kuhusu Lisu, anatakiwa awe jasiri kuueleza umma kuwa Lisu ni mzalendo na achukue ushauri wake ili nchi isonge mbele.

Zitto ni mzalendo kweli na ana uwezo mkubwa sana wa kujenga hoja. Nampenda sana Zitto, no wonder Magufuli ameamua kukibomoa Chama chake kwa kuwateua watu aliokuwa anawategemea sana. Magufuli anamuogopa sana Zitto isipokuwa kwa sababu ya hoja zake za kistaarabu anashindwa kumuweka ndani kama anavyofanya kwa Lisu. Uzalendo wa Zitto hauna shaka na una nia njema na nchi yetu.

Magufuli aachane na u ccm kama ana nia njema na nchi yetu. Atambue kuwa hata wapinzani ni watanzania wa nchi hii, wana shauku ya kuona tunafanikiwa, awatumie akina Lissu na Zitto sio kwa kuwapa vyeo kama Kitila na Anna, la ila kwa kupokea mawazo yao na kuyafanyia kazi. Magufuli akubaki kukosolewa ili uzalendo wake uwe imara. Magufuli aruhusu mikutano ya vyama vya siasa kama katiba inavyoelekeza ili watu wewe huru. Uzalendo wa Magufuli upo katika vipimo, tusubiri wakati utatupatia majibu.
 
Lissu hawezi kuwa kwenye listi moja na Zitto. Zitto alikuwa na kelele kabla hajaonjeshwa utamu. Baada ya kulamba utamu wakati wa tume ya Bomani, ametulia. Siku zote ni mtu wa kuuma na kupuliza.
 
Umeandika kama mwanaharakati na siyo mshabiki wa chama.
Hupo sahihi sana. Wapo watakaokupinga ambao kwao wao mahaba ndiyo tatizo.

Wote hawa kila mmoja ana mapungufu na udhaifu wake, lakini kimsingi ni watu ambao taifa linapaswa kuwatumia ili lipige hatua.


Kwa nini unatumia nguvu kutujulisha hilo? Mzalendo hajitangazi, tungemjua tu na kumkubali!
 
25 Reactions
Reply
Back
Top Bottom