Lishe ya mgonjwa wa vidonda vya tumbo

jamadari

JF-Expert Member
Feb 13, 2010
295
92
Ili kupunguza makali au kujiepusha kabisa na ugonjwa wa vidonda vya tumbo, unapaswa kujiepusha na tabia ya kula na kushiba kupita kiasi, kwa sababu kushiba sana huchochea uzalishaji wa asidi nyingi wakati wa usagaji chakula tumboni.

Mbali na hilo, vyakula vyenye mafuta na sukari nyingi na vyenye kiwango kidogo sana cha kamba lishe, imethibitika kuwa husababisha madhara mengi tumboni. Katika makala ya leo, tutaangalia aina ya vyakula anavyopaswa kula au kuviepuka mgonjwa ili kupata nafuu na kuishi bila kusumbuliwa nao:

VYAKULA VYENYE VIUNGO VINGI
Epuka ulaji wa vyakula vilivyopikwa na kuungwa viungo vingi vya aina mbalimbali, kama vile pilipili kali za aina zote na viungo vingine vyenye ladha ya ukali ambavyo hutiwa ndani ya mboga ama chakula ili kuongeza ladha.

POMBE NA KAHAWA
Pombe na kahawa au vinywaji vingine vyenye ‘caffeine’, vinaweza kuleta matatizo kwa mtu mwenye vidonda vya tumbo na kwa mtu asiye navyo anaweza kupatwa na tatizo, hivyo ni vyema kuepuka au kutumia kwa kiasi kidogo vinywaji hivi. Kimsingi vinywaji hivi huongeza asidi tumboni na hivyo vinaweza kusababisha vidonda au kuzidisha maumivu kwa anayeumwa.
ULAJI CHUMVI
Utafiti uliowahi kufanywa nchini Marekani umeonesha kuwepo kwa uhusiano kati ya ulaji chumvi na vidonda vya tumbo. Mgonjwa anashauriwa kuepuka ulaji wa vyakula vyenye chumvi nyingi, hususan vyakula vya kusindika ambavyo huwekwa chumvi nyingi ili visiharibike haraka. Pia jiepushe na kuongeza chumvi kwenye sahani wakati wa kula.

MAFUTA YA SAMAKI
Baadhi ya utafiti unashauri wagonjwa wa vidonda vya tumbo wale mafuta yatokanayo na samaki (Omega-3 fats) ambayo yameonekana kutoa ahueni kwa wagonjwa. Na kwa mtu ambaye si mgonjwa atakuwa anajiwekea kinga dhidi ya vidonda vya tumbo na magonjwa mengine ya tumbo.

VITAMINI NA MADINI
Ulaji wa vyakula vyenye madini na vitamini kwa wingi husaidia sana kuleta ahueni kwa mgonjwa wa vidonda vya tumbo na kutoa kinga kwa wale ambao hawajaathirika. Wataalamu wa lishe wanashauri kupenda kula matunda na mboga za majani kama vile karoti, juisi ya kabeji, ndizi mbivu, na matunda mengine yenye vitamin C, halikadhalika maziwa ya mbuzi, jibini na cream za maziwa huleta ahueni.
STAILI YA MAISHA NA VIDONDA VYA TUMBO
Licha ya kusabisha Saratani, uvutaji sigara pia huongeza hatari ya mtu kupatwa na ugonjwa wa vidonda vya tumbo, hivyo ni sababu tosha ya kuacha uvutaji sigareti. Japo msongo wa mawazo unaweza kuwa vigumu kuuhusisha moja kwa moja na vidonda vya tumbo, lakini maisha ya wasiwasi, ukichangaya na ulaji mbovu, huweza kusababisha ugonjwa huu, hivyo kama unataka kujiepusha au kupunguza makali ya ugonjwa huu, ni muhimu kuzingatia ulaji sahihi na kuishi maisha ya furaha.
 
Back
Top Bottom