RUCCI
JF-Expert Member
- Oct 6, 2011
- 1,701
- 1,713
Katika kuadhimisha siku ya haki za binadamu ulimwenguni, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu nchini (LHRC) kimesema hali ya haki za msingi za kiraia na kisiasa imezidi kuwa mbaya kwa wastani tangu kuisha kwa uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 kufuatia uanzishwaji wa sheria mpya ambazo huleta vikwazo vipya kwenye haki ya kujieleza na uhuru wa kutoa maoni pamoja na serikali kuzuia mikutano na mikusanyiko ya kisiasa hatua iliyozuia uhuru wa watu kukusanyika.
Wakati akisoma Ripoti ya Utafiti ya Mtazamo ya Haki za Binadamu na Kisiasa Tanzania iliyozinduliwa leo na LHRC, Mwanasheria na Mtafiti Paul Mikongoti amesema kwa mujibu wa utafiti huo inaonyesha kwamba asilimia 65 ya mikoa iliyofanyiwa utafiti nchi nzima, hakuna uhuru wa kukusanyika na maandamano kama ilivyokuwa kabla ya kipindi cha uchaguzi.
“Utafiti huu umefanyika mikoa yote nchini, kila mkoa uliofanyiwa utafiti unaonyesha kwamba haki za kiraia na kisiasa ni mbaya kwa wastani,” alisema.
Mikongoti alifafanua kuwa, kitendo cha kufanyika uchaguzi wa marudio visiwani Zanzibar mwezi Machi, 2016 bila ya chama kikuu cha upinzani kushiriki, na wanasiasa kuzuiliwa kufanya mikutano ya hadhara na maandamano kimesababisha haki ya kisiasa kuwa mbaya.
Kwa upande wa haki za kiraia, alisema hali imekuwa mbaya kwa wastani kufuatia mauaji na ukatili mikononi mwa vyombo vya dola, kujichukulia sheria mkononi na mauaji yanayotokana na imani za kishirikina.
Hata hivyo, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Hellen Kijo-Bisimba ameishauri serikali kupitia Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora pamoja na asasi za kiraia kutoa elimu na kuongeza uelewa wa haki za kiraia na kisiasa kwa jamii.
“Serikali inapaswa kuhakikisha sheria muhimu kama ya makosa ya mtandaoni, takwimu na huduma ya vyombo vya habari zinafanyiwa marekebisho kwa kuzingatia mapendekezo ya wadau ndani na nje ya nchi,” alisema.