Kwa “nonsense” ya Sukari, Rais Samia anastahili pongezi. Je, tuishie kwenye "nonsense" ya Sukari tu au tuangazie na "nonsense" nyingine zote?

Pascal Mayalla

Platinum Member
Sep 22, 2008
50,337
113,180
Nonsense ya Sukari.png


Wanabodi,

Hili ni bandiko lililotokana na makala yangu hii, kwenye Safu yangu ya "Kwa Maslahi ya Taifa", kwenye gazeti la Nipashe kila siku za Jumapili. Kila nipatapo muda, huja na hizi makala zangu za "Kwa Maslahi ya Taifa" ambazo huja kwa mtindo wa swali, halafu jibu utatoa wewe msomaji mwenyewe.

Makala ya leo, ni makala ya pongezi kwa Rais Samia, kwa “nonsense” ya sukari, Rais Samia, anastahili pongezi za dhati, swali ni jee tuishie kwenye nonsense ya sukari tuu, au tuangazie na nonsense nyingine zote tuziache tusonge mbele? .

Naomba kuanza mada yangu ya leo, kwa kufundisha lugha kidogo, neno “nonsense” ni neno la kizungu lenye kumaanisha “ujinga”, hivyo uamuzi wowote unaoitwa “nonsense” ni “uamuzi wa kijinga”, Baba wa Taifa, alilitumia sana neno hili “nonsense”, ila yeye Baba wa Taifa, haikuishia tuu kwenye kulaumu maamuzi ya kijinga, “nonsense”, bali pia aliwaita watoa maamuzi hayo ni “wajinga”, ninanayo mifano mingi ya Mwalimu Nyerere kutumia neno “nonsense”

Mfano mzuri kabisa ni wakati Mwalimu Nyerere anaaga na kung'atuka kwenye urais, alikiri serikali yake imefanya makosa mengi tuu , akakiri kuna baadhi ya maamuzi yalikuwa ni “nonsense”, makosa, lakini pia akasema “kufanya kosa sii kosa, kosa kurudia kosa”.

Wakati tukijiandaa kwa uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi, ile 1995, Mwalimu alizungumza na sisi waandishi wa habari, kwenye ukumbi wa Hoteli ya Kilimanjaro, na mimi nilikuwepo, akizungumzia ubinafsishaji wa benki ya NBC, Mwalimu akaishangaa serikali kukubali masherti ya nchi mabeberu, kuwa NBC ni li benki likubwa sana, lenye nguvu sana, lazima livunjwe, ndipo turuhusu ushindani wa mabenki, Mwalimu akauliza, NBC ina ukubwa gani?, “a mere NBC?!, this is “nonsense”.


Hata hapa, kwenye video hii Mwalimu amezungumzia nonsense!.

kwa hisani ya Dada yangu, Maria Sarungi, Baba wa Taifa alitumia neno nonsense.

Mtu kuambiwa mjinga, ni kweli umetukanwa lakini ujinga sio tusi, ni kutojua tuu, mtu mjinga akiisha elimishwa, ujinga unamtoka, anakuwa mwerevu. Mtu mjinga akiisha elimishwa, ujinga usipomtoka, huyo sasa sio mjinga, huyo ni mpumbavu!.


Rais Mkapa wakati wa uzinduzi wa kampeni za CCM kwa uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, aliwaita watu fulani “malofa na wapumbavu”,
na haikuwa habari kubwa.

Rais Magufuli, aliwahi kumuita mawaziri fulani “mpumbavu” na haikuwa habari kubwa.


Juzi kati katika ziara za Rais Yoweri Museveni nchini Tanzania, katika kuzungumzia hoja ya sukari, Rais Samia pia alitumia neno “nonsense”.

Matumizi haya ya neno nonsense kutumiwa na Mama Samia, inamaanisha sasa Mama Samia huko anakoelekea, anakwenda kuwa kama Nyerere!.

Baada ya kutumika kwa neno hilo, huku kwenye mitandao ya kijamii kukalipuka “Rais Samia Katukana”, aliyetoa msimamo kuwa Tanzania hatutanunua sukari ya Uganda ni Waziri wa Kilimo, Prof. Adolf Mkenda. Baadhi ya mitandao ya kijamii ikamchagiza Prof. Mkenda kuwa asikubali kutukanwa hadharani, bora ajiuzulu kutunza heshima yake na asipojiuzulu atatumbuliwa!.

Sio mara moja nimeongea katika makala zangu, kuwa media ya Tanzania, hatuna watu wazuri wa kufanya uchambuzi wa habari, “news analysis”, Rais Samia alipotumia neno “Nonsense”, hakumtukana Waziri Prof. Mkenda ni “nonsense”, ameushangaa uamuzi ule wa kugomea sukari ya Uganda kwa kisingizio cha kulinda viwanda vya ndani, hivyo lile neno “nonsense” ni neno kwa ajili ya uamuzi ule na sio kwa ajili ya kumlenga mtu Prof. Mkenda. (emphasis mine)

Ukimsikiliza kwa makini, Waziri wa Kilimo, Prof. Adolf Mkenda, kwenye hoja ya sukari

Utakubaliana na mimi, hiki ni kichwa cha ukweli, na hawezi kuwa nonsense!.

Naomba tukubaliane, kama neno “nonsense” ni kwa uamuzi ule wa kugomea kuagiza sukari kutoka nchini Uganda, au uamuzi wa kugomea kuagiza bidhaa zozote kwa nia njema na lengo zuri la kulinda viwanda vya ndani, uamuzi kuhusu sukari, haukutolewa na Waziri Prof. Mkenda kusema ni uamuzi wake binafsi, pia nilimsikia Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa akiuzungumza. Huu ni uamuzi wa Baraza la Mawaziri lililopita, hivyo kauli ya rais Samia haimlengi mtu, inalenga uamuzi wa kugomea kuagiza sukari ya jirani Uganda.

Sasa twende kwenye ukweli wenyewe wa alichokisema Rais Samia uamuzi ule kweli ni “nonsense”. Hii maana yake ni kile niliwahi kukisema katika makala zangu za nyuma, kuwa viongozi wetu sio malaika, ni binaadamu, hivyo wanaweza kabisa kufanya makosa na kutoa muuamuzi “nonsense”, kama baraza la mawaziri limeweza kupitisha uamuzi kama huo, hili la sukari ni uthibitisho tuu wa uwezokano serikali yetu kufanya maamuzi mengi tuu “nonsense”.

Mimi kama Mwandishi wa habari, Mtanzania na Mzalendo wa kweli, kila ninapoona jambo ambalo kwa mawazo yangu sio sawa, kazi yangu huwa ni kuhoji tuu, hivyo kuna vitu vingi nilihoji, na baadaye vikaja kuthibitika I was right.
Baadhi ni hivi
Kupata Maendeleo ya Kweli, Tanzania Inahitaji Systems Not Dramas, Ze Comedy na One Man Shows!.

Jee Maendeleo ya Kweli ni Maendeleo ya Watu au Vitu?- Wachumi Tusaidieni, Magufuli Analisaidia Taifa au Ataliangamiza?.

Maendeleo ya kweli TZ Yataletwa na Elimu na Ukweli. Tusidanganye, Tusidanganywe, Tusidanganyike!
Nonsense Kubwa Kuliko ya Sukari ya Uganda, ni Nosense ya Sukari ya Zanzibar!.
Tena nonsense kubwa kuliko ya sukari, sio kwa serikali yetu kugomea kuingiza nchini sukari ya jirani zetu wa Uganda, serikali yetu iligomea kuingiza Tanzania Bara sukari kutoka Zanzibar!. Wakati huku bara tuna uhaba wa sukari, kulikopelekea kupanda kwa bei ya sukari kutoka shilingi 1,800 kwa kilo, hadi shilingi 2,500 kwa kilo. Kule Zanzibar bei ilibaki 1,500 hadi 1,800.

Kiwanda cha sukari Zanzibar, kilikuwa na sukari ya kutosheleza kabisa kumaliza upungufu wa sukari huku bara, hivyo kikaomba kuleta sukari yake Bara kukabili upungufu, haswa kwa kuzingatia bei ya huku Bara imechangamka kidogo kuliko bei ya Zanzibar, ilikataliwa!. That was nonsense!.

Waziri wa Viwanda na Biashara wa Zanzibar, Amina Salum Ali, akavuka bahari, kuja bara kusemezana na waziri mwenzake…lakini wapi, alikataliwa!. Waziri Amina Salum Ali akaigeukia taasisi ya TradeMark East Afrika inayoshughulika na kuondoa vikwazo vya kibiashara visivyo vya kikodi (non tariff barriers), na kukiripoti hicho kikwazo cha sukari.

Yaani Tanzania bara inakabiliwa na uhaba wa sukari, Zanzibar inayo sukari ya ziada bwelele, Zanzibar inakataliwa kuingiza sukari yake bara, na badala yake, wenye viwanda ndio wanaoruhusiwa kuagiza sukari ya bei chee kutoka ng’ambo, kufidia huo upungufu!, kwa uamuzi kama huu, ni neno gani zuri zaidi ya kulitumia zaidi ya neno “nonsense?”.

Nampongeza sana rais Samia kwa kukemea na kukomesha hii nonsense ya kwenye sukari, na sasa nitoe wito kwa rais wetu Mama Samia, hizi nonsense za kwenye sukari, zisiishie tuu kwenye sukari, twende na kwenye nonsense nyingine zote za uondoshaji wa vikwazo vya uingizaji nchini bidhaa muhimu ambazo viwanda vya ndani vimeshindwa kutosheleza mahitaji ya bidhaa hizo kushibisha soko la ndani.

Kwa sasa taifa linakabiliwa na upungufu wa sementi, mfuko wa sementi ya Tanzania kwa mikoa ya pembezoni, kama Arusha, na Moshi, imefikia bei ya shilingi 24,000 kwa mfuko. Sementi ya Kenya ni shilingi 12,000 kwa mfuko mpaka inafika dukani Tanzania. Watu wanahitaji sementi haipo, hapo kwa jirani yetu sementi bwelele, bei chee, lakini hairuhusiwi kuingia Tanzania, kwa lengo la kulinda viwanda vya ndani. Hii pia ni nonsense!. Hivyo baada ya hii nonsense ya sukari, twende kwenye nonse nyingine zote za vikwazo vya uingizaji bidhaa.

Angalizo: Kuunga mkono huu msimamo wa rais Samia kuondoa nonsense ya sukari, na kutaka nonsense nyingine zote ziondoshwe, namaanisha kufungua milango ya soko huria kwa zile bidhaa tuu za muhimu ambazo viwanda vyetu vya ndani, vimeshindwa kuzalisha kukidhi na kutosheleza mahitaji ya soko la ndani, na sio soko holela. Viwanda vya ndani vikifanikiwa kuzalisha kutosheleza soko, tuendelee kuvilinda, hata kama ulinzi huo utatuumiza sisi wananchi kulazimika kununua bidhaa zetu zinazozalishwa nchini kwa bei kubwa, huo ndio uzalendo wenyewe, na ndiko kujenga nchi kwenyewe na sio kukimbilia cheap imports kwasababu tuu ni cheap!.

Wasalaam.

Paskali.
 
Kuna na " nonsense" ya mafuta ya kula na ya mitambo( petroli, diesel)! Hii nonsense inaua kasi ya ukuaji wa uchumi wetu!

Mkuu mleta mada umeshiriki kunishawishi nitumie neno nonsense, kwa kigezo kuwa si neno la kuudhi bali la kuhimiza watu waache ujinga. Naliweka wazi hili kwa sababu sipendi kutumia maneno ya kuudhi popote!
 
Asante kwa makala na ufafanuzi uliokaa vizuri, inamfanya hata wa la 7 aelewe. Najuwa wako wanaoishi kwa kukariri na watakuponda kama kawaida.

Mama aliongea kwa staha sana. Inakuwaje uliyempa leseni ya kuzalisha sukari ndiye unampa leseni ya kuagiza nje? Halafu bado unatuambia wakulima wa miwa wa bonde la Kilombero kwa mwaka wanashindwa kuuza miwa yao kiwandani? Hiyo ndiyo NONSENSE
 
Umejikita zaidi kuonesha matumizi ya neno nonsense kama ambavyo lilitumiwa na Hayati Mwalimu, hujaonesha justification wa Raisi Samia kuita maamuzi ya Waziri wa Kilimo "nonsense". Waziri wa Kilimo alikataa kutoa vibali vya sukari kwa msimamo wa kulinda wazalishaji wa ndani. Raisi naye kwa uelewa wake inaonekana hakubaliani na waziri wake kwa sababu kuna upungufu wa sukari ambao lazima ujazwe kwa kuagiza sukari nje. Nafikiri kinachogomba hapa ni usimamizi wa hiyo biashara
 
17 Reactions
Reply
Back
Top Bottom