Kwa heri Kamanda Philip Magadula Shelembi"- WASIFU UNAOISHI...

mwana wa mtu

JF-Expert Member
Mar 5, 2008
220
53
Samson Mwigamba

KIFO chake kimetokea ghafla sana lakini hatuna zaidi ya kumwachia Mungu ambaye ndiye hupanga nani atangulie na nani afuate.

Hii leo Jumatano Aprili 27, 2011 niko mkoani Shinyanga nikihudhuria mazishi ya Kamanda Philip Magadula Shelembi aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA Mkoa wa Shinyanga.

Nikiwa Mwenyekiti wa Mkoa jirani wa Arusha nimekuja kuuwakilisha mkoa kwenye mazishi ya Kamanda huyu ambaye hatasahaulika kwa jinsi alivyoijenga CHADEMA katika Mkoa wake wa Shinyanga hata kabla ya kugawanywa na kupatikana Mkoa mpya wa Simiyu, ambao Mwenyekiti wake, Erasto Tumbo pia tunaye kama mwenyekiti wa mkoa jirani.

Kwa mara ya kwanza nilikutana na marehemu Shelembi jijini Dar es salaam, akiwa tayari ni mwenyekiti wa Mkoa wa Shinyanga. Tulionana tukiwa naye kwenye kugombea ujumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA.

Nakumbuka kwenye kundi la Tanzania Bara wanaume, tulikuwa wagombea 19 wakati nafasi zilizokuwepo zilikuwa ni tatu. Ilikuwa ni patashika nguo kuchanika. Wakati Shelembi anajieleza na kuomba kura mbele ya wajumbe wa Baraza Kuu la chama, mimi nilikuwa tayari nimekwisha kujieleza na kuomba kura na hivyo wakati huo nilikuwa nimeketi ndani ya ukumbi.

Alijieleza kwa dakika mbili tu, muda ambao wagombea wote tulipewa, lakini mpaka anamaliza dakika zake mbili wajumbe walikuwa wamekwisha kucheka karibu ya kuvunja mbavu.

Hata sisi wagombea wenzake tulijikuta tunacheka. Hata alipokuwa anaulizwa maswali mawili majibu yake yalijaa vichekesho, lakini yakiwa yamebeba ukweli mwingi.

Nakumbuka swali mojawapo aliloulizwa lilikuwa ni kwamba yeye kama mwenyekiti wa mkoa anayegombea ujumbe wa kamati kuu, je, mkoani mwake amehakikisha kwamba ameshafanya kazi ya kukitandaza chama mpaka ngazi za chini kabisa? Jibu alilolitoa Shelembi lilikuwa ni kwamba kazi hiyo alishamaliza na kuisahau. Matokeo yalipotoka Shelembi aliongoza akifuatiwa na Prof. Mwesiga Baregu na Dk. Kitila Mkumbo. Kweli alistahili.

Kustahili huko kwa Shelembi kulikuja kuonekana mara baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka jana.

Mkoa wa Shinyanga wa zamani ambao ndio ulifanyiwa kazi na Shelembi ulitoa wabunge wanne kupitia chama chake wakiipita mikoa ya Mwanza na Kilimanjaro ambayo ilitoa wabunge watatu kila mmoja na kufuatiwa na mikoa iliyotoa wabunge wawili wawili kama Arusha, Dar es Salaam na Mbeya.

Na hii ni pamoja na kuchakachuliwa kwa matokeo kwa hali ya juu mno, ambapo Shelembi mwenyewe anaaminika alishinda lakini akachakachuliwa.

Shelembi aligombea ubunge na udiwani kwa pamoja katika Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga. Alikuwa ana uwezo mkubwa wa kuongea na kushawishi watu.

Hakuwa tajiri lakini majuzi tulipokutana makao makuu ya CHADEMA mjini Dar es salaam aliniambia, “Mwigamba mimi sina pesa. Pesa yangu ni hii hapa”, aliniambia Shelembi akiwa ananyoosha kidole chake kwenye kinywa chake akimaanisha kwamba mdomo wake na maneno yatokayo humo ndiyo pesa yake.

Wale waliojaribu kufuatilia kampeni za uchaguzi mkoani Shinyanga watakuwa mashahidi wa umati wa watu waliokuwa wakimshangilia Shelembi wakitaka awe mbunge wao na diwani wao. Alizungumza kwa kujiamini na kumwaga sera za chama chake kwa ustadi mkubwa. Alitoa ahadi zinazotekelezeka akigusa shida za moja kwa moja zinazowagusa wananchi wake wa Shinyanga ambao wengi ni wakulima na wafugaji.

Mwisho wa siku Shelembi akaonekana anashinda uchaguzi na kuwa mbunge na diwani aliyeshinda vyote katika uchaguzi mmoja na kuweka rekodi kama ile iliyowekwa na marehemu Chacha Zakayo Wangwe kupitia CHADEMA pia. Alitangazwa kuwa diwani mapema kabisa lakini kutangazwa kuwa mbunge ikawa ngoma kama ilivyokuwa ngoma kwenye majimbo mengi tu ambako ilisadikika chama cha upinzani kilishinda.

Baada ya muda mrefu wa nguvu ya umma kudai matokeo, hatimaye msimamizi wa uchaguzi mteule wa rais ambaye pia ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga alimtangaza mgombea wa CCM kuwa mshindi akimpita Shelembi kwa kura moja.

Cha kustaajabisha ni kwamba mara tu baada ya kutangaza matokeo yale, msimamizi yule alikimbia na kutoweka mjini Shinyanga kwenye kituo chake cha kazi na alikuja kuonekana baada ya miezi mitatu.

Hiyo peke yake ilitosha kuonyesha namna ya hila iliyokuwa inafanywa ndani yake. Shelembi alifungua kesi Mahakama Kuu na mpaka mauti yanamkuta alikuwa anaendelea na kesi yake ambayo tulipokutana Dar es Salaam Aprili 4 mwaka huu aliniambia ana uhakika wa kushinda na hatimaye kugombea uchaguzi mdogo na kuchukua ubunge wake alionyang’anywa. Hayo yalikuwa ni maneno yake mwenyewe Shelembi wiki chache tu zilizopita.

Nilimuuliza Shelembi kwamba nini kinampa ujasiri na matumaini makubwa kiasi hicho kwamba uchaguzi mdogo ukitokea tu atashinda. Alinijibu kwamba amekwishaibadilisha Shinyanga kuwa ngome ya CHADEMA. Aliniomba kukumbuka maandamano ya Shinyanga yaliyoitishwa na chama hicho kwa ajili ya kupinga malipo ya Dowans, kudai uchaguzi wa umeya Arusha kurudiwa, kudai utawala bora, Katiba mpya na mengineyo.

Alinikumbusha pia wakati CCM walipofanya mkutano mkuu wa mkoa hivi karibuni. Aliniomba nikumbuke jinsi ilivyoripotiwa kwenye vyombo vya habari kwamba wajumbe wa mkutano ule walitoka majumbani kwao wakiwa wamevaa nguo za kawaida na kubadilisha na kuvaa sare za CCM wakiwa ndani ya ukumbi.

Baada ya mkutano kumalizika walibadilisha tena nguo na kuvaa nguo za kawaida kabla ya kutoka ukumbini. Baadhi yao walipoulizwa walidai kwamba wanaogopa kuvaa sare za CCM ndani ya mji wa Shinyanga kwa sababu CCM haikubaliki tena na ukivaa sare katikati ya mji utaambulia kuzomewa na wananchi.

Chini ya uongozi thabiti wa Kamanda Philip Magadula Shelembi, Shinyanga imekuwa ngome halisi ya CHADEMA. Alikuwa ni mcheshi na mzungumzaji. Ukimpatia dakika tano za kuzungumza na wewe utajikuta unamsikiliza kwa nusu saa bila kuchoka.

Alizungumza kwa lugha rahisi iliyochanganyika na lafudhi ya Kisukuma huku akitoa mifano na vichekesho kiasi kwamba huwezi kuchoka kumsikiliza. Alifanya kazi nyingi kwa wakati mmoja na hakuchoka kusafiri, kuzungumza, kutembea na kufanya lolote kwa ajili ya chama. Watu wake walimpenda na viongozi wenzake tulimpenda ndani ya chama.

Ndiyo maana alikuwa mwenyekiti wa mkoa na mjumbe wa kamati kuu taifa, ujumbe ambao ulimfanya kuwa moja kwa moja mjumbe wa Baraza Kuu na Mkutano Mkuu Taifa. Kama angetangaziwa ushindi wake wote, leo angekuwa pia diwani na mbunge.

Shelembi alikuwa na msimamo na hakusita wala kuogopa kutoa maoni yake. Kwenye vikao vya chama atakumbukwa kwa kusimamia yale aliyoyaamini lakini pale maamuzi ya vikao yanapotokea kuwa kinyume na maoni na misimamo yake, aligeuka na kuwa sehemu ya maamuzi hayo.

Ni kwa sababu hiyo hakuwahi hata siku moja kusigana na viongozi wenzake wa ngazi yoyote ile yenye vikao alivyokuwa anashiriki. Alikipenda chama na kwake chama kilikuwa zaidi ya mtu mmoja mmoja. Alipenda kudumisha umoja ndani ya chama na kukifanya chama kiendeshwe kama taasisi na si kama mtu mmoja mmoja.

Kutokana na ujasiri wa Shelembi alidiriki kumvimbia mkuu wa mkoa wake kwenye kikao cha Baraza la Madiwani. Baadhi ya matamshi yake hayakumpendeza mkuu wa mkoa ambaye alitishia kumshughulikia Shelembi. Lakini Shelembi alimjibu kwamba anazifahamu sheria na akiwa ndani ya ukumbi wa Baraza la Madiwani hakuna mwenye uwezo wa kumkamata.

Alimweleza bayana mkuu wa mkoa kwamba yeye ndiye si mjumbe wa baraza hilo na kwa hiyo akichafua hali ya hewa ya kikao cha madiwani anaweza kuchukuliwa hatua za kutolewa nje ya kikao lakini si yeye. Alimwambia kwamba hata akileta polisi kumtoa ndani ya ukumbi habanduki labda awe amekufa.

Shelembi ameaga dunia kabla ya kuona mabadiliko ya nchi yake aliyoyapigania kwa miaka mingi. Lakini ameondoka na kuacha nyuma nyayo ambazo hazitafutika hata kama historia ya nchi hii iandikwe upya leo ama kesho. Si ajabu kwamba ukombozi halisi wa Watanzania ambao Shelembi na chama chake wameupigania kwa miaka mingi utakuja karibuni.

Utakapopatikana na historia ya nchi hii kubadilishwa, jina la Shelembi litakumbukwa si na wana Shinyanga tu bali pia na wana CHADEMA wote na si wana CHADEMA tu bali na Watanzania wote. Na huu ndio ujumbe murua kwa kila mpiganaji anayepigania mabadiliko ya nchi hii si mwana CHADEMA tu bali pia mwana harakati kupitia uandishi wa habari, mashirika yasiyo ya serikali, wananchi wa kawaida, wanafunzi, wafanyakazi, wakulima, wafanyabiashara, makundi maalumu ya jamii kama walemavu na kadhalika.

Ujumbe ni kwamba unapopigania uhuru wa kweli wa nchi yako usijifikirie kwamba utapata uwaziri wa nini, ukuu wa mkoa gani ama wilaya gani, ubarozi wa nchi gani, ukuu wa taasisi gani ya serikali, wala usifikirie biashara zako zitafaidikaje na chama chako kuingia madarakani. Mawazo hayo ni ya mafisadi na sisi tukiwaza hivyo hatutakuwa tofauti na mafisadi na tutahukumiwa pengine hukumu mbaya zaidi kuliko mafisadi wa kale na kale.

Harakati zetu ziongozwe na kauli ambayo Mwenyekiti wa Taifa wa CHADEMA, Freeman Mbowe, alipata kusema kwamba, “Napigania ukombozi wa nchi yangu si kwa manufaa yangu binafsi. Naweza kutoweka duniani leo ama kesho, lakini nitaiacha Tanzania nzuri kwa ajili ya vizazi vijavyo ambao ni watoto wetu, wajukuu wetu, na vizazi vyao.”
Kalamu hii yaweza kuzimika leo na ikashindwa kuendelea kuandika kwa sababu mshika kalamu hiyo katoweka ghafla duniani kama alivyotoweka Shelembi.

Lakini harakati za Kalamu ya Mwigamba zitadumu miaka mingi ijayo ndani ya Watanzania waliopata kusoma maandishi ya kalamu hii na kutiwa moyo kufanya mapambano ya dhati ya kuikomboa nchi hii.

Zipo kalamu nyingi ziliwahi kuandika historia ya nchi hii kama vile kalamu zile zilizokuwa sehemu ya wanamtandao ambao hatimaye walikwapua mabilioni ya watanzania kwa ajili ya kumsimika JK kwenye utawala wa nchi hii.

Kalamu hizo ambazo nyingi zilikuwa za waandishi mashuhuri waliobobea kwenye taaluma hii leo zinakumbukwa kwa kuleta ombwe la uongozi nchini kwa miaka inayokwenda kumi sasa. Ombi langu ni kwamba kalamu hii ikumbukwe kama sehemu ya wanaharakati walioliletea taifa hili ukombozi wa kweli, uhuru wa kweli!

Mzee wetu Philip Magadula Shelembi ametoweka ghafla na ni dhahiri kwamba ameacha pengo kubwa hasa kwa chama chake. Lakini hebu makamanda waliobaki wasimame kama wanajeshi na hivyo mahali alipotoka Shelembi mara moja asimame kamanda mwingine na kuendeleza mapambano mstari wa mbele.

Kama Mwenyekiti wa CHADEMA Mkoa wa Arusha natoa pole za dhati kwa niaba ya wanachama wote wa CHADEMA Mkoa wa Arusha kwa Mwenyekiti wetu wa Taifa Freeman Aikael Mbowe (MB), Katibu Mkuu wa taifa, Dk. Willibrod Peter Slaa, viongozi wote wa kitaifa na Mkoa wa Shinyanga na wanachama wote wa Mkoa wa Shinyanga kwa kuondokewa na kamanda shupavu wa mstari wa mbele katika mapambano mapya ya mabadiliko ya kweli uhuru wa kweli!

Bwana ametoa na Bwana ametwaa, jina lake libarikiwe!

Source: Tanzania Daima
 
Yaan umeandika kwa ufasaha sana ndugu mwandishi, hata tuliokua hatumfahamu kamanda shelembi sasa tunaanza kupata picha ya harakati za ukombozi.
MUNGU aiweke mahala pema peponi roho ya mwanaharakati na mpiganaji Mzee wetu Shelembi. AMINA
 
wamemuua kwa kujua fika kwamba kesi yake anashinda, hao ndio CCM lakini tunaoma kesi hii iendelee kuendeshwa kama ni sawa kisheria mpaka tujue mwisho wake, tuje kumpelekea ushindi wake akiwa kaburini na naamini kabisa kama ilivyokua Tarime, uchaguzi ukirudiwa CHADEMA wataibuka na ushindi wa kishindo tu
 
R.I.P kamanda philip Shilembi your deeds will always be in our mind and your thoughts will live forever. ''Bwana alitoa na Bwana ametwaa jina la Bwana lihimidiwe.''
 
RIP comrade Shilembi. waTZ tutakukumbuka daima. ingawa haupo nasi lakini fikra zako zinaishi bado
 
nimeshindwa kumalizia na sita soma tena inaumaa sana kama ni mipango ya mungu tuko radhi vinginevyo tunamwachia mungu
 
apumzike kwa amani. raha ya milele uumpe ee bwana na mwanga wa milele umuangazie apumzike kwa amani. Amina. kwa jina la baba nala mwana na la roho mtakatifu amina.
 
wamemuua kwa kujua fika kwamba kesi yake anashinda, hao ndio CCM lakini tunaoma kesi hii iendelee kuendeshwa kama ni sawa kisheria mpaka tujue mwisho wake, tuje kumpelekea ushindi wake akiwa kaburini na naamini kabisa kama ilivyokua Tarime, uchaguzi ukirudiwa CHADEMA wataibuka na ushindi wa kishindo tu

Acha ushambenga na uchochezi!! Mwili wa marehemu ulifanyiwa uchunguzi mbele ya viongozi wa Chadema na ndugu zake na matokeo yalitangazwa RFA na vyombo vingine, sasa nani amumua. Kwani ulitaka afe nani? basi ungekufa wewe kama unaona wamemua. @#$%$@@#^&&
 
Tutakukumbuka daima,na kamwe hautaweza sahaulika kwa wana shinyanga,wana CDM,pamoja na wananchi wote kwa umakini wako,ujasiri,nk.
 
Ulale kwa amani Comrade...umefanya mengi kwa wakati wako na tazama safari yako imemalizika...daima tutauenzi mshikamano na hatutakubali kugawanywa km mafungu ya nyanya! Pole kwa ndugu zako,Familia,marafiki na wapenda maendeleo wote hata wale mliotofautiana kimtazamo!
 
R.I.P. Camarade Shelembi.

Hakika CHADEMA ilikuwa na hazina kubwa hapo Shinyanga. Mimi naomba kama kuna mwenye picha yake aiweke hapa ukumbini. Itakuwa jambo zuri.

Poleni sana wana-CDM.Tulimpenda Kamanda wetu lakini Mungu amempennda zaidi. Bwana ametoa na Bwana ametwaa,Jina la Bwana Yesu libarikiwe.
 
wamemuua kwa kujua fika kwamba kesi yake anashinda, hao ndio CCM lakini tunaoma kesi hii iendelee kuendeshwa kama ni sawa kisheria mpaka tujue mwisho wake, tuje kumpelekea ushindi wake akiwa kaburini na naamini kabisa kama ilivyokua Tarime, uchaguzi ukirudiwa CHADEMA wataibuka na ushindi wa kishindo tu

Mawazo finyu na ya kipuuzi kabisa, ww nawe utajiita great thinker ?
 
Back
Top Bottom