Kuuawa kwa mwanae Ennis – Ulikuwa ni mwaka wa mikosi wa mwigizaji Bill Cosby

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,393
ennis-cosby.jpg

Ennis Cosby
bill-ennis-cosby.jpg



Ennis na baba yake Bill Cosby

tumblr_m2fwqtFvHW1rtz32io1_r1_500.jpg

Mikael Markhasev

1279743709997_6.jpg

Picha ya kuchora ya Mikail Markhasev iliyopelekea kutambulika na kukamatwa

Hadi kufikia Januari mosi 1996, Bill Cosby muigizaji maarufu wa vichekesho nchini Marekani alikuwa kwenye kilele cha mafanikio akiwa amejikusanyia mashabiki wengi nchini Marekani na Ulaya. Kwa ujumla alikuwa ni tajiri na mwenye mafanikio makubwa katika sanaa ya uigizaji wa vichekesho. Wiki mbili baadaye, muigizaji huyu aliyekuwa na umri wa miaka 59 wakati huo, mikosi ilianza kumuandama. Ni mikosi ambayo, yeye binafsi aliwahi kukiri kwamba, hatakuja kuisahau maishani mwake.

Kwanza ilikuwa ni Januari 14, 1996 wakati binti mmoja aliyekuwa na umri wa miaka 22 aitwae Autumn Jackson alipotuma ujumbe kwa mwanasheria wa Bill Cosby kumjulisha kwamba yeye ni mtoto wa nje ya ndoa wa Bill Cosby na alitaka alipwe dola za Marekani milioni 40 kama fidia ya kumsitiri Bill Cosby kwa miaka yote ile bila kutoa siri ile.

Pia alitishia kuuza ile siri kwenye magazeti ya udaku ya nchini humo kama fidia ile haitatekelezwa. Bill Cosby kwa kushirikiana na mwanasheria wake waliwajulisha FBI na binti yule akakamatwa pamoja na mfadhili wake aitwae Jose Medina aliyekuwa na umri wa miaka 51.

Baadae walifunguliwa mashitaka ya kula njama ya kukashifu kwa makusudi. Bill Cosby alikanusha hadharani kwamba Autumn Jackson ni binti yake, lakini alikiri kuwahi kumlipia ada yake ya shule kupitia mfuko wake aliouanzisha miaka ya 1970, wa kusaidia vijana wenye asili ya Afrika wanaotoka katika familia masikini nchini Marekani kwa kuwalipia gharama za kupata elimu.

Lakini huo ulikuwa ni mwanzo wa mikosi kumwandama Bill Cosby, kwani siku mbili baada ya kashfa ya mtoto wa nje ya ndoa kuibuka na wakati ikiwa inaendelea kuandikwa na vyombo vya habari vya nchini Marekani na hasa magazeti ya udaku, Bill Cosby akiwa kwenye chumba cha mazoezi ya kuigiza katika kituo cha Luninga cha Queens New York, aliitwa nje ili kupokea simu kutoka kwa meneja uhusiano wake aitwae David Brokaw.

David Brokaw akiongea kwa sauti ya kutetemeka alimwambia Bill Cosby….. “Ninayo taarifa mbaya sana ya kukueleza na ningependa kukupa pole……, mwanao pekee Ennis ameuawa kwa kupigwa risasi kichwani huko Los Angeles.”

Ennis Cosby mtoto pekee wa kiume wa Bill Cosby ambaye alikuwa na umri wa miaka 27, mwili wake ulikutwa ukiwa umelala kwenye dimbwi la damu majira ya saa 7:45 usiku pembeni ya gari lake aina ya Mercedes Benz huku taa za gari zikiwa zinawaka na gurudumu la gari hilo likiwa limefunguliwa.

Mazingira yalikuwa yanaonesha dhahiri kwamba, Ennis Cosby alikuwa anabadilisha tairi la gari lake lililopata pancha wakati anauawa. Msemaji wa Polisi wa Los Angeles, Willie Williams alisema anaamini mauaji yale yalikuwa ni ya uporaji. Baada ya kupata taarifa zile, Bill Cosby alipanda gari lake aina ya Range Rover na kurudi nyumbani kwake Manhattan Brownstone. Alipofika nyumbani kwake alikutana na kundi la waandishi wa habari nje ya nyumba yake ambapo aliwaeleza kwa kifupi, “Mwanangu Ennis alikuwa ni shujaa wangu, huu ni msiba mkubwa ambao sitousahau katika maisha yangu.”

Polisi waliamini kwamba mauaji yale ni ya kushtukiza na muuaji alikuwa ni mbahatishaji tu ambapo mara nyingi mauaji ya aina ile ni vigumu kupatiwa ufumbuzi. Hata hivyo kulikuwa na uwezekano wa mtuhumiwa kukamatwa kwani alikuwepo shahidi mmoja muhimu aliyekuwepo katika eneo la tukio wakati mauaji yanatokea.

Naye si mwingine bali ni mwandishi wa michezo ya kuigiza aitwaye Stephanie Crane, mama wa umri wa miaka 47. Inasemekana Ennis alikuwa anaenda kumtembelea mama Crane ndipo gari lake lilipopasuka tairi la nyuma wakati akiwa njiani. Alipopata tatizo hilo, alimpigia simu mama Crane akimuomba aende na gari lake ili amulike wakati anabadilisha tairi, kwani barabara ile taa zake zilikuwa na mwanga hafifu. Mama Crane alisema alifika katika eneo alilokwama Ennis saa 7:40 usiku, ikiwa ni dakika 15 tangu alipopigiwa simu. Alipofika aliegesha gari lake pembeni na kummulikia Ennis kwa taa za gari lake wakati akibadilisha tairi la gari lake lililopasuka.

Mara alimuona mtu mwenye muonekanano wa kihalifu akielekea alipo Ennis. Mama Crane alikiri kwamba alipata wasiwasi juu ya usalama wao hivyo akaondoka haraka kwenye eneo hilo na gari lake kwa mwendo wa kasi na kumuacha Ennis peke yake.

Baadae aliporudi aliukuta mwili wa Ennis ukiwa kwenye dimbwi la damu baada ya kupigwa risasi kichwani na kufariki hapo hapo. Mama Crane aliwapigia Polisi na kuwajulisha kuhusu tukio hilo ambapo haikuwachukuwa muda Polisi kufika. Akihojiwa na Polisi, mama Crane alisema kwamba, walfahamiana na Ennis wiki moja iliyopita baada ya kutambulishwa na rafiki yake wa karibu wakiwa kwenye sherehe.

Akielezea wajihi wa muuaji alisema, kijana huyo alikuwa na umri kama wa miaka 20 hivi na alikuwa na urefu wa kama futi tano na nusu. Baadaye Polisi walimchukuwa mama huyo na kumpeleka makao makuu ya Polisi kwenye kitengo cha wataalamu wa kuchora sura za watu ili awaelezee muonekanao wa huyo kijana kwa ajili ya kuchora picha yake ili isaidie katika upelelezi.

Polisi walikuwa na maswali mengi ya kujiuliza juu ya mauaji yale kwani mauaji yalitokea katika eneo ambalo lina usalama wa hali ya juu na uhalifu katika eneo hilo ulikuwa ni wa kiwango cha chini kabisa nchni Marekani.

Pia mwili wa Ennis ulikutwa ukiwa na pochi ambayo Polisi walieleza kwamba ilikuwa na kiasi kikubwa cha fedha, na hata tairi la gari lake lililopasuka lilikuwa na muonekano tofauti, kiasi cha kutilia shaka kwamba, kuna uwezekano wa tairi kupasuliwa baada ya mauaji yale.

Hata hivyo wapelelezi walikuwa na wakati mgumu katika kufuatilia nyendo za za Ennis kabla hajauawa. Ennis alikuwa anafanya kazi katika kituo kimoja cha michezo kilichopo Los Angeles. Na siku hiyo alifanya kazi kati ya saa kumi na mbili na nusu asubuhi na saa nne na nusu usiku, lakini wafanyakazi wenzie walisema hawakujua alielekea wapi baada ya kutoka kazini.

Polisi walitoa taarifa wakisema kwamba, hakukuwa na uwezekano kwa Ennis kuuawa na mtu anayemfahamu, kwani siku ya tukio alikuwa ndio amerejea Los Angeles akitokea New York, alikokwenda kwenye mafunzo mafupi, na hata hivyo kando ya watu wa karibu wa baba yake waishio Los Angeles hakuwa akifahamika sana katika jiji hilo.

Familia ya Bill Cosby haikuwa peke yake katika kuomboleza kifo cha mtoto wao, bali jamii nzima ya Wamarekani wenye asili ya Afrika waliungana na familia ya Bill Cosby katika kuomboleza msiba huo mzito.

Kwao, Ennis alikuwa ni mtu muhimu aliyesimamia maendeleo ya mtu mweusi. Akiwa ni kijana aliyepambana na tatizo la kutojua kusoma, linalofahamika kitaalamu kama Dyslexia, Ennis alimudu kujibadilisha na kufaulu katika masomo yake na kuendelea hadi chuo kikuu ambapo alipomaliza alijiunga na shule za kufundisha wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Mmoja wa wanafunzi wake aitwae Walter Stephen Douglas alisema, “nilipopata taarifa za kuuawa kwake nilichanganyikiwa, nililia mchana kutwa na nilikuwa nikiangalia picha yake mara kwa mara nisiamini kile kilichotokea.”

Douglas aliendelea kusema, “baba yake hakukosea aliposema Ennis alikuwa ni shujaa wake, ni kweli alikuwa ni shujaa wangu pia, nilitaka kuwa kama yeye, alivyopambana na matatizo ya kutojua kusoma na akafanikiwa.”

Hata hivyo, Douglas alisema kwamba, anataka kufanya yale Ennis aliyokuwa akitarajia kuyafanya katika uhai wake, mojawapo ikiwa ni kufungua shule kwa ajili ya watoto wenye mahitaji maalum kama yeye. Ukweli ni kwamba wapo watu wengi watakaomkumbuka Ennis na hasa wanafunzi aliosoma nao.

Wakati Polisi wakiendelea na uchunguzi wa kifo cha mwanaye, Bil Cosby alikuwa bado akiandamwa jinamizi la kuzaa mtoto nje ya ndoa. Mnamo January 27, 1998, Bill Cosby alikubali yaishe, kwani alipokuwa akifanyiwa mahojiano na kituo kimoja maarufu cha luninga nchini Marekani cha CBS, mwishoni mwa mahojiano, mtangazaji wa kipindi hicho, bwana Dan Rather alimuuliza Bill Cosby kama alipata kumjua mama wa mtoto Autumn Jackson aitwae Shawn Jackson, Bill Cosby akijibu swali hilo, alikiri kumfahamu mama huyo na kuendelea kusema, “kama unauliza iwapo niliwahi kufanya mapenzi na mama huyu, jibu lake ni ‘ndiyo.’ ”

Alipoulizwa kama yeye ndiye baba wa Autumn Jason, Bill Cosby alijibu kwa kifupi, “kuna uwezekano wa kuwa hivyo.”

Wamarekani wote walistushwa na taarifa ile ya Bill Cosby, na hiyo ilisababisha magazeti yote yaliyokuwa yakiandika makala mbalimbali juu ya kifo cha mwanaye kuacha na kumgeukia na kumshutumu kwa kuisaliti ndoa yake.

Jamii ya watu weusi nayo ilinyong’onyeshwa na taarifa ile, na wengi waliohojiwa walikiri kumuona Bill Cosby kama kioo cha jamii, lakini baada ya kukiri kwake kuzaa nje ya ndoa kuliwafanya wakose imani naye.

Mkewe alipoulizwa na waandishi wa habari kuhusiana na taarifa ile alisema, “sisi bado ni wanandoa na ndoa yetu bado ni imara, kilichotokea miaka 23 iliyopita siyo muhimu sana kwetu, kilicho muhimu kwetu ni kukamatwa kwa muuaji wa mtoto wetu.”

Mara baada ya Ennis Cosby kuuawa, jarida moja la nchini humo liitwalo The National Enquirer lilitangaza kutoa zawadi ya dola laki moja kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa zitakazosaidia kukamatwa kwa muuaji. Lakini pamoja na kutoa taarifa hiyo, gazeti hilo lilitoa habari inayomhusu Autumn Jackson na madai yake ya kuwa yeye ni mtoto wa Bill Cosby. Mke wa Bill Cosby alimpigia simu mhariri wa gazeti hilo, Steven Coz na kumuamuru aiondoe zawadi yake katika msako wa muuaji wa mwanaye, kwa madai kwamba hataki fedha za gazeti hilo zihusishwe na mwanaye.

Hata hivyo, pamoja na kuzuiwa kutoa zawadi ile, jarida hilo lilipata taarifa ambazo walizipeleka polisi na hivyo kupelekea kukamatwa kwa muuaji.

Mnamo Machi 12, 1996, msemaji wa Polisi wa Los Angeles, Willie Williams alitangaza rasmi kuhusu kukamtwa kwa kijana mmoja aliyekuwa na umri wa miaka 18, mhamiaji kutoka Ukraine, aitwae Mikail Markhasev akituhumiwa kwa mauaji ya Ennis Cosby. Lakini msemaji huyo wa Polisi hakulitaja gazeti la Enquirer kama ndilo lililofanikisha kukamatwa kwa muuaji.

Baada ya kutangaza kutoa zawadi kwa mtu yeyote atakayewapelekea taarifa zitakazosaidia kukamatwa kwa muuaji, walipokea simu nyingi sana ambazo miongoni mwa simu zilizopigwa zilikuwa ni za kupuuzia. Lakini ilipofika Januari 26, 1996, siku kumi baada ya mauaji ya Ennis Cosby, gazeti hilo lilipata simu kutoka kwa kijana mmoja ambaye jina lake linahifadhiwa ambaye alitoa taarifa za kumfahamu muuaji.

Gazeti hilo lilifanya mpango wa kukutana na mtoa taarifa, ambapo walipokutana, aliwaeleza jinsi ilivyotokea kumfahamu Mikail. Aliwaeleza kwamba wiki moja baada ya kutokea mauaji ya Ennis, alikuwa na ahadi na rafiki yake ambaye naye jina linahifadhiwa, ambaye alikuwa na ahadi ya kwenda kwa Mikail kuazima silaha. Rafiki yake huyo alimfahamu Mikail kama kijana mhalifu anayehusika na magenge ya watoto wahalifu wa mitaani.

Siku hiyo waliondoka na gari lake akiwa na huyo rafiki yake hadi eneo la magharibi mwa Hollywood ambapo walisimama kwenye eneo lenye vibanda vya simu na kisha rafiki yake akaenda kupiga simu.
Dakika kumi baadae kijana mmoja mrefu mwembamba alifika pale walipo na kutambulishwa na rafikiye kwamba, anaitwa Mikail. Mtoa taarifa huyo alisema kitu cha kwanza alichokiona kwa Mikail ni ‘ushapu.’ Alikuwa ni mwenye wasiwasi wakati wote na alikuwa anaongea sana. Mikail aliingia kwenye gari na kumwelekeza waelekee mitaa ya pembezoni mwa mto Los Angeles.

Walipofika walishuka akiwa na rafiki yake na kuelekea kwenye mto, sehemu ambayo kulikuwa na kijipori kidogo. Ambapo walikwenda kutafuta kitu alichokuja kugundua baadae kuwa ni silaha. Baadae walirejea na kusimama umbali wa kama mita tatu kutoka usawa wa mtoa taarifa alipoegesha gari, na kuanza kuzungumza.

Hapo ndipo mmtoa taarifa aliposikia mazungumzo yao ambapo Mikail alisikika akisema, “Nimeua ‘Niga’ mmoja, nashangaa habari zimesambaa kila mahali.”

Waliporejea ndani ya gari la mtoa taarifa, Mikail aliendelea kusema kwamba, ilikuwa inambidi arudi nyumbani haraka sana kwani alikuwa na mpango wa kuondoka pale Los Angeles na kupotelea kusiko julikana kwa kipindi kirefu kidogo.

Awali mtoa taarifa huyo hakumuelewa Mikail akajua ni kauli ambayo ni ya kawaida kwa watumiaji wa dawa za kulevya. Walipokuwa wakiondoka kutoka katika eneo lile, Mikail akasema wameikosa silaha waliyoifuata, akadai kuna uwezekano ikawa imesombwa na maji. Mtoa taarifa aliendesha gari mpaka nyumbani kwa kina Mikail, aliposhuka aliwaalika waingie ndani wakajiburudishe na bia za Kirusi, lakini walikataa kwa madai kwamba wana mambo mengi ya kufanya na kuondoka zao.

Walipokuwa njiani mtoa taarifa alimuuliza rafikiye kwamba inawezekana Mikail ni mhalifu hatari? Rafikiye akamjibu kwamba, Mikail ni mhalifu hatari na ndiye aliyemuua mtoto wa Bil Cosby.

Kwa mujibu wa maelezo ya rafikiye mtoa taarifa, Mikail alimtokea Ennis Cosby na kumuamuru atoe fedha. Ennis alichelewa kutoa fedha kama alivyoamriwa na Mikail, ndipo alipomuua na kutoweka bila kuchukuwa chochote kwa kuhofia kukutwa katika eneo la tukio.

Mtoa taarifa alisema kwamba hakuamini, kwamba Mikail ndiye aliyemuuwa Ennis Cosby mpaka alipoona picha ya kuchora iliyosambazwa na Polisi ikionesha sura ya mtu anayetuhumiwa kwa mauaji hayo. Ndipo alipomshauri rafikiye watoe taarifa, lakini rafikiye alikataa kuhusishwa katika mpango huo wa kutoa taarifa.

Mnamo Machi 7, 1996, jarida la The National Enquirer walikabidhi taarifa zote za mtoa taarifa pamoja na jina lake ikiwemo namba yake ya simu kwenye kituo kikuu cha Polisi cha Los Angeles.

Baadae Polisi waliwasiliana na mtoa taarifa na alipohojiwa alitoa maelezo yanayofanana na yale aliyoyatoa wakati anaongea na waandishi wa habari wa gazeti la The National Enquirer.

Polisi waliondoka na mtoa taarifa hadi kwenye eneo walilokwenda na Mikail kuchukua silaha ambayo hawakuipata, lakini Polisi hao walibahatika kuipata silaha hiyo, ambayo ilikuja kujulikana baadaye kuwa ndiyo iliyotumika kumuua Ennis Cosby. Polisi walimweka Mikail Markhasev chini ya uchunguzi kwa muda wa siku tano, bila yeye kujua, kabla ya kumkamata na kumfungulia mashitaka ya mauaji ya Ennis Cosby.

Mnamo Machi 1, 1996, Mikail Markhasev alifikishwa kwenye mahakama ya Los Angeles na kushitakiwa kwa kosa la kuuwa, ambapo kama akikutwa na hatia adhabu yake inaweza kuwa ni kuhukumiwa kunyongwa.

Kifo cha Ennis ndiyo kimetokea na hakuna awezaye kumrejesha duniani. Lakini yapo maswali ya kujiuliza. Inakuwaje mtu anapata pancha njiani, kisha anaamua kubadilisha tairi la gari lake, halafu anatokea mtu mwingine ambaye anaamua kumpiga risasi na kumuua……! Kwa sababu gani hasa….? Yaani fedha kidogo ambazo hata hivyo hakuweza kuzichukuwa ndiyo zitoe uhai wa mtu…..?

Kwa ujumla maisha ya watu hawa wawili, hayafanani hata kidogo. Ennis ni msomi ambaye ametokea kwenye familia ya mtu tajiri na maarufu nchini Marekani, na Mikail ni mtoto wa mhamiaji kutokea katika nchi iliyosambaratika ya Jumuiya ya Kisoviet, aliyeingia nchini humo mwaka 1989 wakati huo akiwa na miaka 10.

Historia yake inaonyesha kwamba, alikuwa na akili sana darasani hadi akaingizwa kwenye mpango maalum wa kuwaendeleza watoto wenye vipaji, lakini haikupita muda mrefu, tangu aingizwe kwenye mpango huo, akajiunga na magenge ya kihalifu ya Wamexico ambapo alishindwa kuendelea na masomo na kujikuta akiwa mtaani kwenye viunga vya watumiaji na wauzaji wa dawa za kulevya vya jijini Los Angeles huku akishirikia katika uhalifu mdogo mdogo.

1. Alikulia katika mazingira ya unyanyaswaji na kulazimika kuanza kutumia pombe aina ya Vodka akiwa na umri mdogo

2. Alizaliwa katika mazingira mazuri nchini Ukraine lakini kutokana na nchi hiyo kukumbwa na vita familia yake ililazimika kuhamia nchini Marekani na kuishi katika viunga masikini vya jiji la Los Angeles,

3. Wanafunzi wenzie walikuwa wakimdhihaki kutokana na lafudhi yake ya Kirashia na jinsi alivyokuwa akipumua kwa kukoroma kutokana na hali ya hewa kumuathiri

4.
Kila alipojaribu kujiunga na makundi ya vijana wenzie wa kizungu walikuwa wakimuepuka, kwa kifupi kila kundi alilojaribu kutaka kujiunga walimkataa yakiwemo makundi ya watu weusi, kwa sababu alikuwa ni Mrashia.

Hata hivyo yapo maswali mengi ambayo watu wengi nchini humo walikuwa wanajiuliza:

1. Je Ennis alikuwa anafanya nini usiku huo katika eneo hilo linalokaliwa na na watu weupe (wazungu).

2.
Je alikuwa anataka kununua madawa ya kulevya?


3.
Je alikuwa anawinda wasichana wa Kirashia?

4. Au alikuwa na miadi ya kukutana na baba yake mahali fulani?

Maswali yote hayo hayakupatiwa majibu.Kesi yake ilipoanza kusikilizwa rasmi, Mikail alikiri kumuua Ennis Cosby, ambapo alihukumiwa kifungo cha maisha jela bila uwezekano wa kufungwa kifungo cha nje (Parole).

Ingawa mwanasheria wake alimkatia rufaa lakini Mikail aliandika barua ya kuomba radhi kwa familia ya Ennis Cosby, na watu wote walioguswa na kifo chake, vilevile aliiomba mahakama iliyomhukumu kuondoa rufaa yake kwa madai kwamba, rufaa ile ni ya uongo, kwa sababu ni kweli alimuuwa Ennis Cosby na haoni kwamba ni busara kukata rufaa wakati anastahili hukumu aliyopewa.

Jaji wa mahakama ile na mwendesha mashitaka walionesha kushangazwana uamuzi alioufikia Mikail na kusema kwamba, hawajawahi kushuhudia jambo kama lile hapo kabla…………..
 
Naomba sana mniwie radhi wasomaji wapenzi wa JF, leo nimechelewa kuweka bandiko hili la kila Ijumaa kutokana na mikasa ya barabarani.

Leo hii tena niko nchini Marekani, bado nahangaika kutafuta kesi za hapa nchini, lakini nilizobahatika kuzipata ni za kawaida sana, na ndio maana nasita kuziweka hapa.

Kesi ya leo nisingependa kusema lolote kwa sababu kila kitu kinajieleza na nimejitahidi sana kuiandika yote kama nilivyoipata mtandaoni. lakini hata hivyo kuna kitu cha kujifunza katika kesi hii.

Nawatakia usomaji mwema.
 
Asante Mtambuzi

Yaani umenikumbusha mbali sana. huyu kijana jamani kifo chake kilisikitisha sana.

Eh mungu dunia hii, inwatu na viatu.
Wengine kuua kwao wala si isuue ona sasa kijana madhara aliyo ipatia familia Ennis na yeye mwenyewe kufia jera.
LAITI KAMA HAWA WATU WANGEKUWA WANAFIKILI KABLA YA KUTENDA NA KUANGALIA FAIDA NA HASARA ZAKE.
 
Last edited by a moderator:
Mimi ni mpenzi sana wa huyu commedian Billy, tangu nikiwa mdogo miaka ya 95 nilikuwa mpenzi wa series zake na ukizingatia wengi walimpenda Mr. Bean mimi nilimchukia kwaajili ya mapenzi yangu kwa Cosby. Kwa hii habari leo umenifurahisha sana, nimezikubali juhudi zako katika kutupanua uelewa wetu

Sent from my BlackBerry 9910 using JamiiForums
 
Kwa kawaida huwa sisomi articles ndefuuuuu kama hizi, ila kwa leo nimejikuta naaanza toka mwanzo na naisoma kikamilifu mpaka mwisho bila kuruka hata herufi moja. Umeiandika kimvutomvuto Bro
 
Kifo cha Ennis ndiyo kimetokea na hakuna awezaye kumrejesha duniani. Lakini yapo maswali ya kujiuliza. Inakuwaje mtu anapata pancha njiani, kisha anaamua kubadilisha tairi la gari lake, halafu anatokea mtu mwingine ambaye anaamua kumpiga risasi na kumuua……! Kwa sababu gani hasa….? Yaani fedha kidogo ambazo hata hivyo hakuweza kuzichukuwa ndiyo zitoe uhai wa mtu…..?
1. Kwa mujibu wa taarifa za kiuchunguzi, Bwana Mikail alikuwa akifanya kazi katika mgahawa uliokuwa karibu na maeneo ambayo mauaji yalifanyika. Katika dhana pana ya udhibiti wa kiuhalifu, ili tukio lolote la kihalifu litokee mambo matatu lazima yatokee:

1. Mazingira yanayoweza kusababisha uhalifu kutokea
2. Mhalifu pia lazima awepo kwa ajili ya kutekeleza uhalifu
3. Mtendewa uhalifu (victim)
2. Vilevile suala la namaa uhalifu unavyoweza kutokea liko ndani ya maamuzi ya mhalifu mwenyewe ingawa kuna wakati kuna baadhi ya matukio yanatokea bila ya ridhaa ya mhalifu mwenyewe. Kwa mfano mhalifu anaweza kuingia ndani ya nyumba kwa lengo la kupora mali/fedha lakini wakati wa purukushani, na hasa ukitokea upinzani wakati wa uhalifu anaweza kuua.

3. Suala la pesa kidoogo haliondoi nia ya mhalifu kutekeleza uhalifu wake. Mfano mdogo ni mtu na mkewe waliokwenda kilabuni na pesa kidogo kwa ajili ya kunywa pombe za kienyeji na nauli ya kurejea nyumbani kwao. Ulipofika usiku wa manane wakati wanarejea wakagundua hata pesa ya nauli wametumia. Walianza kutembea kwa miguu kurejea nyumbani ndipo kundi la wahalifu liliwavamia kwa nia ya kuwapora na hawakufanikiwa kupata chochote ndipo kwa hasira wakawajaza michanga vinywani mwao hadi wakazimia na asubuhi yake wakajikuta hospitalini. Mfano mwingine ni aina ya uhalifu wa kubahatisha unaofanywa na wahalifu wa Manispaa ya Mtwara - Mikindani. Wahalifu hawa maarufu kama tukale wapi mara nyingine huwavizia watu wanaorejea majumbani mwao kutoka katika starehe zao. Mara lango linapofunguliwa wao huingia pamoja na gari lakini si kuwa mara zote wanafanikiwa. Cha kujifunza hapa ni kuwa mara zote ni muhimu kuwa makini na mazingira ya aina zote ambayo kwa namna moja au nyingine waweza kufikiri uhalifu unaweza kutokea.

Tabia za kihalifu kwa Bwana Mikail ilijengeka toka utoto wake. Mazingira ya shule pia yalipalilia sana tabia zake za kiuhalifu. Hadi anaanza kufanya kazi alikwishakuwa mhalifu mzoefu. Wazazi wanapaswa kuwa makini sana na tabia za watoto wao ili kuepukana au kupunguza kundi la wahalifu ndani ya jamii yetu.

utaalamu wa kutambua watendaji wa uhalifu kwa kutumia vinasaba DNA ni njia rahisi sana ya kuwatambua wahalifu halisi badala ya kuwavictimise hata wasiokuwa wahalifu (wahalifu wa kusingiziwa ni tatizo kubwa katika nchi yetu). Bwana Mikail alichunguzwa pia kwa njia hii na iligundulika katika kofia/matambara aliyozungushia katika bastola aliyoitumia kufanyia mauaji ya ENNIS.

HATA UKIWA JAMBAZI SUGU KIASI GANI HALI YA UTU BADO IKO KATIKA KILA MOYO (WITH NO REGARD NI NDOGO KIASI GANI). BWANA MIKAIL ALIKIRI KWA MAKOSA ALOFANYA NA KWA KUTAMBUA KUWA ALIKUWA AMELIFANYA KOSA ALIAMUA KUONDOA NA RUFAA YAKE

Nashukuru sana Mtambuzi kwani nakumbuka sana visa na mikasa ya kiuhalifu niliyowahi kuisikia miaka ya nyuma. Twasubiri mikasa mingine mingi zaidi

The Listener - Ex - detective
 
Wenzetu wamepiga hatua yani picha inachorwa na kupelekea kupatikana kwa mtuhumiwa.Safiiiiiii sanaaa mtambuzi
 
Back
Top Bottom