Kutokuwepo kwa ukabila kwamkuna balozi wa Ujerumani

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,316
33,125

Rehema Matowo, Hai.
BALOZI wa Ujerumani nchini, Guido Herz ameisifu Tanzania kwa kutokuwa na tatizo la ukabila akisema jambo hilo ni moja ya sababu kuu zinazoimarisha utulivu wa kisiasa.Balozi huyo alibainisha hayo jana wakati wa ufunguzi wa majengo matatu yaliyojengwa kwa ufadhili wa nchi hiyo. Majengo hayo ni ya Chuo cha Ufundi cha St Joseph kilicho wilayani Hai na kinachomilikiwa na Kanisa Katoliki.

Akizungumza baada ya ufunguzi wa chuo hicho, Herz aliisifu siasa ya utulivu nchini Tanzania na kusema ni nchi yenye makabila mengi, lakini imefanikiwa kuondoa tofauti hizo kutokana na mfumo mzuri wa uongozi.

Alisema kutokana na kuwepo kwa amani, rasilimali nyingi zilizopo zikitumiwa vizuri nchi inaweza kupata maendeleo.
“Tanzania ni nchi yenye rasilimali nyinyi kama vivutio mbalimbali vya utalii, madini pamoja na ushirikiano mzuri na mataifa ya nje. Rasilimali hizo zikisimamiwa kitaalamu zitaleta maendeleo ya nchi,” alisema.

Akizungumzia uchaguzi wa mwaka huu, balozi huyo aliwataka wanachi kujitokeza kuwachagua viongozi ambao watawaletea maendeleo, bila kuangalia kabila au dini kwa lengo la kuipa maendeleo nchi yao. Naye msimamizi wa chuo hicho, Padri Beatusi Urasa alisema kuwa ujenzi wa majengo hayo uligharimu Sh25,275,000 zilizotolewa na balozi huyo pamoja na Eberhad Leitz ambaye ni raia wa Ujerumani.

Alisema kuwa chuo hicho kinachukua wanafunzi kutoka mikoa yote nchini kuanzia vijana waliohitimu darasa la saba na kidato cha nne na kwamba wanapata mafunzo ya ufundi wa magari na ushonaji.

Mkuu wa wilaya ya Hai Dk Norman Sigala alisema kuanzishwa kwa vyuo vya ufundi kutasaidia kutatua tatizo la ajira kwa vijana.

“Ongezeko la watu ni kubwa husa ni vijana. Kuna vijana ambao wameshindwa kuendelea na masomo kutokana na sababu mbalimbali na kwa hiyo kuwepo kwa vyuo hivi kutasaidia kutatua tatizo la ajira," alisema Sigala.

Chanzo: Gazeti la Mwananchi
 
Back
Top Bottom