Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,447
- 39,857
UPDATE:
Kuna watu wanaulizia jinsi ya kupata nakala ya kitabu cha "Nyuma ya Pazia" cha Balozi Dkt. Wilbrod Slaa. Sasa kinaweza kupatikana baadhi ya mikoa:
Mbeya Piga Simu: 0759829015
Arusha Piga Simu: 0716505921
Dodoma Piga Simu: 0769663431
Mikoa mingine tukipata wakala tutawapatia: Bei ni shilingi 20,000/- tu kwa bei ya reja reja na ukitaka kwa jumla au zaidi ya kimoja unaweza kupata punguzo nono la bei.
Na. M. M. Mwanakijiji
Umpende au umchukie, umkatae au umkubali, umpinge au umuunge mkono Dkt. Wilbrod Slaa Dr Willibrod Slaa anabakia kuwa miongoni mwa wanasiasa wachache Tanzania ambao alama zao katika zama na nyakati za kisiasa ni vigumu kufutika. Unaweza kumuita majina mengi na ya rangi mbalimbali ya kejeli lakini ni vigumu kupuuzia, kudharau au kutupilia mbali mchango wake katika siasa za Tanzania kwa karibu miaka ishirini na mitano. Mchango wake katika kuimarisha siasa za Tanzania akiwa miongoni mwa wabunge wa kwanza kabisa wa upinzani umeacha historia kubwa kuanzia Karatu hadi Dar, toka Tunduru hadi Tarime.
Hata hivyo, matukio ya kisiasa ya mwaka 2015 yanabakia katika historia yetu kama mafundisho makubwa kabisa ya siasa zinavyoweza kuwafanya ndugu wawe maadui, marafiki wake mahasimu, na kutengeneza kile ambacho wenzetu Wamarekani wanasema ni “strange bed fellows” yaani kuwaona watu usiowadhania wamelala kitanda kimoja. Matukio haya yalitokea taifa likiwa katika mwamko mkubwa wa uchaguzi mkuu wa Rais na Wabunge.
Dkt. Slaa akiwa Katibu Mkuu wa chama Kikuu cha upinzani cha CHADEMA, alitarajiwa na alipitishwa na chama chake kuwa mgombea wa Urais huku mtifuano mkubwa ukitarajiwa na hatimaye ulitokea ndani ya Chama cha Mapinduzi. Kwa baadhi ya wachunguzi wa siasa mtifuano au mnyukano uliokuwa unatokea CCM ulifanya kazi ya mgombea wa upinzani uliounganika kuwa ya afueni zaidi.
Hata hivyo, kinyume na matarajio ya watu wengi na kinyume na mantiki zilizozoeleka za kisiasa Edward Lowassa aliyekatwa jina lake ndani ya CCM ambako alikuwa anaongoza kwa mashabiki na kura za maoni alikimbilia CHADEMA na kusababisha chama hicho cha upinzani kulala kitanda kimoja na mtu ambaye walitumia muda mwingi kumhusisha na ufisadi nchini. Ilisemwa “yeyote” isipokuwa CCM. Dkt. Slaa akafyekelewa mbali na chama chake na kusababisha mpasuko wa aina yake ndani ya CCM na CHADEMA.
Dkt. Slaa akaamua kuachana na siasa za vyama na yeye na familia yake wakahamia Canada. Miezi michache baadaye Rais John Magufuli alimteua Dkt. Slaa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Sweden kitu ambacho kilitafsiriwa na baadhi ya watu kwa namna mbalimbali.
Katika kitabu cha NYUMA YA PAZIA Dkt. Slaa anaelezea kwa kina matukio mbalimbali ambayo yalitokea hadi kufikia Lowassa kukaribishwa CHADEMA na kwa nini hakuwa tayari kusimama jukwaani kumnadi Lowassa na akabakia na utimamu wa kimaadili na akili. Hata hivyo, kitabu hiki kinaenda zaidi ya nyuma ya pazia la siasa za 2015. Inatufunulia kumuelewa Dkt. Slaa kwani kwa kiasi chake kitabu hiki pia ni bibliografia (historia ya maisha) ya mwanasiasa huyu nguli, mcheshi, na msomi.
Ndani ya kitabu hiki tunaweza kukutana na mtu ambaye anatufundisha mambo mbalimbali kuhusiana na uongozi. Mojawapo ya mambo ambayo msomaji atayafurahia atakapokutana nayo ni jinsi gani Dkt. Slaa ni mtunzaji mzuri sana wa kumbukumbu. Siyo tu katika akili lakini katika nyaraka na vielelezo mbalimbali. Anataja tarehe, mahali na siku kama shahidi katika kesi nzito. Bila utata anataja pia majina mbalimbali ya wahusika mbalimbali katika ujasiri ambao utawakumbusha watu wengi ile hotuba yake ya “Orodha ya Mafisadi” ya pale Mwembe Yanga.
Kitabu hakigusi siasa tu za 2015 lakini pia kinatudokeza safari ya Dkt. Slaa kutoka upadre hadi kuwa mwanasiasa mbobezi. Wengi watashtushwa, kushangazwa na kuburudishwa na masimulizi yake ya mikutano yake na Baba wa Taifa Mwl. Nyerere wakati huo Dkt. Slaa akiwa Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu. Pia watakutana na jinsi gani Dkt. Slaa alisimamia kupinga ufisadi ndani ya Kanisa Katoliki kiasi cha kumgonganisha yeye na mmojawapo wa maaskofu waandamizi wa wakati huo. Msomaji pia ataburudishwa na masimulizi yake ya kujaribu kuinua hali na maisha ya watu wa Karatu katika kile ambacho kilimsababishia kuwa mbunge mpendwa sana wa wana Karatu na kuthubutu kufanya kitu ambacho hakikuwahi kufanywa Tanzania – Karatu kuwa Halmashauri ya kwanza ya mji kuongozwa na upinzani.
Kubwa hata hivyo, ni sakata zima la siasa za 2015 na matokeo yake katika upinzani na siasa za Tanzania. Kitabu hiki kinatoa maonyo, mwongozo, na elimu kwa wanasiasa wanaofuatia katika upinzani na chama tawala na wapinzani watarajiwa na watawala watarajia. Mwanasiasa yeyote ni lazima apate nakala ya kitabu hiki, mwanahistoria yeyote ni lazima anunue nakala yake wakati wanafunzi wa shule na vyuo watapata elimu muhimu juu ya uongozi kutoka katika kitabu hiki kilichoandikwa kwa lugha ya Kiswahili.
Nyuma ya pazia ni kitabu kinachomfunua mbele yetu na kutujulisha kwa undani juu ya mtu, maisha, zama na nyakati za Dkt. Wilbrod Slaa, Balozi, Baba, Mume na miongoni mwa viongozi maridadi ambao Tanzania imepata nafasi ya kuwa nao na wameacha alama zisizofutika. Umpende au umchukie, umkatae au umkubali, umpinge au umuunge mkono Dkt. Wilbrod Slaa ametupatia hazina ya maarifa ambayo wenye hekima watawahi kuipata katika nakala chache ambazo zimeshaingia nchini.
UNAWEZA KUPATA NAKALA YAKO WAPI?
Unaweza kupata nakala yako kwa bei ya jumla au rejareja. Bei ya reja reja ni shilingi 20,000/- TU na kwa bei ya jumla unaweza kupata punguzo kubwa kufuatana na mahitaji yako.
Maeneo ya posta, mkabala na Jengo la Benjamin Mkapa karibu na Mahali yanapoegeshwa magari yaendayo Sinza yenye michoro ya Rangi Nyekundu.
Mhudumu Genoveva - 0753 059 144
Au wasiliana na Erasto Tumbo kuweza kuagiza nakala zako:
0713 474707/0688 211683