Yoyo Zhou
Member
- Jun 16, 2020
- 72
- 110
Mwezi zaidi ya mmoja umepita tangu maandamano ya kupinga kifo cha mmarekani mwenye asili ya Afrika George Floyd mikononi mwa polisi kuibuka nchini Marekani na kusambaa katika Ulaya, Australia na baadhi ya nchi za Afrika.
Dhamira ya awali ya maandamano hayo ilikuwa ni kupinga ubaguzi wa rangi, haswa dhidi ya polisi wazungu wanaotumia nguvu kupita kiasi dhidi ya watu weusi hata kama wakifanya makosa sawa na wazungu. Lakini sasa maandamano hayo yameanza kuonekana kubadilika kuwa “mapinduzi”, na kwamba waandamanaji nchini Marekani wanasemekana kuwa watalipua kwa mabomu Mlima Rushmore ambao ni mashuhuri kwa sababu umechongwa sanamu za marais wanne wa Marekani George Washington, Thomas Jefferson, Theodore Roosevelt na Abraham Lincoln, kwani wanaona Mlima huo ni alama ya ukosefu wa usawa.
Pia tumesikia jinsi alama za zamani za nchi hiyo zikianza kushambuliwa na kuvunjwa kutokana na kile kilichotajwa kuwa zinatonesha madonda ya historia ya utumwa na ubaguzi wa rangi. Katika kaunti ya Orange ya jimbo la California, jina la John Wyne limetolewa kwenye uwanja wa ndege wa kaunti hiyo kwa madai kuwa John Wyne aliwahi kuhojiwa na kuonyesha maoni ya kibaguzi. Hali kama hiyo, hivi karibuni kumekuwa na ombi kubwa la kufutwa kwa Chuo Kikuu cha Yale, kwa sababu jina Yale linatokana na mfanyabiashara wa watumwa, mkoloni Elihu Yale ambaye ni mfadhili wa chuo kikuu hicho. Na hata waandamanaji wenye msimamo mkali wamedai kuwa wahitimu wa vyuo vikuu vilivyofadhiliwa na watawala wanatakiwa kuchukuliwa hatua za kisheria akiwemo Bibi Hillary Clinton aliyehitimu kutoka Chuo Kikuu cha Yale.
Matukio kama hayo pia yamesikika barani Ulaya, na nchini Uingereza sanamu mbili zilizotengenezwa katika karne ya 17 zimevunjwa kwa madai kuwa zinawatukuza watu waliofanya vitendo vya ukatili dhidi ya watu wengine duniani wakati wa ukoloni. Nchini Uganda nako baadhi ya wabunge na wasomi wanataka majina ya mitaa, barabara na maziwa yabadilishwe ili kufuta majina ya kikoloni.
Jana tarehe 30, Juni, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo DRC iliadhimisha miaka 60 ya uhuru. Mfalme Philippe wa Ubelgiji alimwandikia barua rais wa DRC Félix Tshisekedi, akieleza kusikitishwa na jinsi watu wa nchi hiyo walivyotendewa kinyama chini ya utawala wa Ubelgiji, lakini hakuomba radhi kutokana na uhalifu uliofanywa na babu yake Leopold II hadi mwaka 1960. Haijulikani kama hii ni njia ya dhati kwa nchi hiyo kujikosoa kutokana na historia yake, au ni hofu ya shinikizo linaonekana sasa duniani kuchukia vitendo vya ukatili bila kujali vilitokea lini.
Hata hivyo Ubelgiji ni mfano mzuri, japo sio wa kuridhisha kwa asilimia 100. Lakini mfano ni mfano, inafaa kwa nchi nyingine zilizowahi kuzitawala nchi za Afrika na kuwatendea vibaya watu wa Afrika katika enzi za ukoloni kutafakari kwa makini na kujiandaa vya kutosha kutokana na historia hizi za kuhuzunisha ambazo zimehifadhiwa sio tu katika kumbukumbu hizi zikiwemo sanamu bali pia mioyoni mwa watu wa Afrika.