Kura ya kumng’oa rais yahitajika

abdulahsaf

JF-Expert Member
Aug 31, 2010
858
130
Na Sitta Tumma

NIMEWAHI kuandika makala ya kuwashauri wabunge watumie Ibara ya 46A(1), na sheria ya mwaka 1992 namba 20 ibara ya 8, na sheria ya mwaka 1995, kupiga kura ya kutokuwa na imani na Rais Jakaya Kikwete.

Niliwaomba wabunge wampigie kura Amiri Jeshi Mkuu huyu baada ya kuona mambo hayaendi sawa sawa na yeye akizidi kukaa kimya kana kwamba nchi ni shwari.

Katika hoja yangu, Rais Kikwete anaonekana kushindwa kuilinda na kuisimamia sheria ya maadili ya viongozi wa umma. Hii ni kwa ajili ya kifungu cha 2 (a), cha Katiba ya Jamhuri.

Sikuishia hapo. Niliwaomba pia wabunge wawe wazalendo kwa kumwajibisha na kumpigia kura ya kumkataa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Kwa mujibu wa Ibara ya 53 (1), cha Katiba ya nchi, Waziri Mkuu Pinda ndiye mwenye madaraka juu ya udhibiti, usimamiaji, utekelezaji wa siku hata siku wa kazi na shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano.

Kwa hali inavyoonekana sasa, Pinda ameshindwa kabisa kutekeleza wajibu wake. Ndiyo maana nikashauri Bunge litumie sheria ya mwaka 1992 na 1995 namba 12, na Ibara ya 53A (1), cha Katiba limfukuze kazi 'mtoto' huyu wa mkulima, ili arudi kwao kulima.

Kimsingi yote haya wabunge wetu waliyapuuza. Maana hawakudhubutu kufanya hivyo, hadi hapo juzi mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe alipoamua kufuata ushauri wangu huo.

Licha ya Zitto kufuata ushauri wangu huu. Bado kuna rundo la wabunge ambao waligoma. Lakini wabunge wengine walilazimika kukata kufumba macho bila kujali anatoka chama gani, wakasaini mapendekezo ya kumkataa Pinda.

Mapendekezo haya hayakufua dafu. Hoja haikuwasilishwa rasmi bungeni kwa Spika. Kwa maana nyingine haikufanikiwa kumng'oa waziri mkuu.

Kwa hali ya kawaida, kushindwa kwa wabunge kumwondoa madarakani Waziri Mkuu, Pinda mwenyewe anapaswa aanze kujitafakari.

Mambo muhimu ya kujiuliza ni haya. Mosi, kwa nini Serikali na viongozi waliopo chini yake wanazidi kutuhumiwa kwa ufisadi?

Pili, akiwa kama waziri mkuu na msomi mzuri wa sheria ameshindwaje kumshauri ‘bosi' wake Rais Kikwete awawajibishe kwa kuwafukuza kazi viongozi hawa wakiwemo baadhi ya Mawaziri wanaotuhumiwa kwa kukiuka maadili ya viongozi wa umma?.

Tatu, kama amemshauri Rais akakataa kusikiliza ushauri wake, ameshindwaje kuchukua maamuzi na kupaza sauti ya kujiuzulu kama alivyofanya mtangulizi wake, Edward Lowassa?

Nne, na kama anaona kujiuzulu kwake haiwezekani kwa kuhofia kukosa maulaji ya mahela kutokana na nafasi yake hiyo, safari za nje, heshima tukufu ya kuitwa waziri mkuu, anadhani anamfurahisha nani?

Swali la tano, haoni kwamba kuendelea kwake kung'ang'ania cheo ambacho bila Lowassa kujiuzulu pengine asingekipata katika 'maisha yake' wananchi kupitia kwa wabunge wao hawamtaki?.

Sita, hivi kama siku moja Bunge likakamilisha taratibu zote na kupitisha rasmi azimio la kumkataa, atang'ang'ania? Au ataficha wapi aibu hiyo?

Kimsingi, Pinda na Serikali yake ya Rais Kikwete wameshindwa kutuongoza Watanzania kwa misingi na taratibu zinavyotakiwa.

Namuomba waziri mkuu atafakari kwa kina hoja hii ya kuondoka madarakani kabla hajafukuzwa na wabunge kama ambavyo jaribio hilo lililofanyika Bunge lililomalizika Jumatatu wiki hii.

Nakushauri waziri wangu mkuu, tafakari, pima na uchukue hatua madhubuti kwa kuiachia nafasi uliyonayo kwa masilahi ya taifa na wananchi wake.

Ni heshima kubwa mno kwa mtu kama wewe ukiondoka bila shuruti ya wabunge au wananchi wenyewe!.

Nimkumbushe tu waziri wetu mkuu. Sheria ya kulinda mali ya umma ya mwaka 1984 namba 15 na Ibara ya 27 (1), inamtaka kila mtu kulinda maliasili ya Jamhuri pamoja na mali ya mamlaka ya nchi inayomilikiwa na wananchi wenyewe.

Ibara hiyo hiyo, kifungu kidogo cha pili, kinawataka watu wote akiwemo na Pinda na mawaziri wake, wanatakiwa na sheria za nchi kupiga vita aina zote za ubadhirifu.

Si hilo tu. Watu wote tunatakiwa kupambana na uharibifu wa mali za nchi pamoja na kuendesha uchumi wa taifa kwa umakini mkubwa kama watu ambao ndiyo waamuzi wa hali ya baadaye ya taifa lao.

Katika hili, siendi mbali kumkosoa waziwazi Pinda, Rais Kikwete, mawaziri wanaotuhumiwa kwa ufisadi pamoja na viongozi wasiowaadilifu.

Kwa hali ya kawaida, wakubali wasikubali Pinda, Rais Kikwete na Serikali yao wameshindwa kusimamia nchi. Wanaonekana kuacha mali za nchi zitafunwe ovyo kwa maslahi ya wachache.

Kwa hali hiyo basi. Lazima viongozi hawa wafikirie kwa umakini namna ambavyo walivyotufikisha hapa tulipo. Wajihoji wenyewe kwamba kwa nini kila kukicha ubadhilifu haupungui?.

Wajiulize maswali magumu wenyewe kwamba, kama viongozi waliopo chini yao wanatajwa tena kwa ushahidi kula mali ya nchi, wanatuhumiwa kwa kushindwa kutekeleza wajibu wao kwa maslahi ya taifa, wameshindwaje kuwatoa kwenye nafasi zao?.

Hapa kwa kweli Serikali hii ya CCM haitutendei haki Watanzania sisi masikini. Kinachoonekana pengine tayari serikali hii ya kina Pinda imeamua ijipinde kunyonya uchumi wa taifa hili.

Bila shaka, kwa hali ilivyo sasa pengine mtu anaweza kuanza kufikiria na kujihoji mwenyewe kwamba, kule Libya, Tunisia na Misri ilikuwaje baada ya serikali husika kupuuza sauti za watu wake?

Sipendi kabisa tufikie mawazo hayo. Hapa napenda sana tufikirie namna ya kudumisha amani, upendo na utulivu!.

Lakini wakati tunatafakari kuenzi amani tuliyoachiwa na Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, je viongozi wetu wana mawazo yapi katika hili?

Wanapenda kweli amani? Wanalipenda kweli taifa lao? Je, kama wanalipenda iweje baadhi ya viongozi wanaosakamwa kwa tuhuma za ubadhilifu wa mali, pamoja na kushindwa kutekeleza wajibu wao hawachukuliwi hatua?

Si siri, ninavyoona wakuu wetu wa nchi ndiyo wanaoweza kujipandikizia chuki kubwa dhidi yao na wananchi.

Chuki ni kitu kibaya sana. Kila mtu hapendi kuona mwenzake amemchukia....lakini kwa viongozi wetu inawezekana kuchukiwa kwao na wananchi wanaowaongoza ni baraka.

Kama kuna kiongozi mwenye mawazo na fikra kama hizi za kipumbavu, hafai kabisa kuitwa kiongozi.

Tanzania tunahitaji kuwa taifa makini, lenye heshima ya kipekee duniani pamoja na udhibiti halisi wa mali za nchi. Mambo ya yasiyofaa hayatakiwi kabisa.

Sina nia mbaya katika haya yote. Ila nahitaji kuona serikali inawajibika kwa wananchi wake kama ambavyo nchi nyinginezo duniani zinavyofanya.

Kwa hali ya kawaida, kushindwa kwa waziri mkuu kujiuzulu kutokana na shinikizo la baadhi ya wabunge bungeni, imeonesha wazi kabisa uwajibikaji wa kiongozi huyu kwa wananchi ni mdogo mithili ya tundu la sindano!

Nilitegemea kwa asilimia 1000 kumuona Pinda anatangaza kuachia ngazi bungeni hata kabla Rais Kikwete hajamruhusu kufanya hivyo. Lakini mmh.

Nilijipa moyo na matumaini makubwa kwamba, Pinda hawezi kuhitimisha hotuba yake ya kuahirisha Bunge bila kutangaza kung'atuka.

Lakini wapi, niliona anaendelea 'kujipinda' kutoa hotuba bila kutoa neno ama yeye kuondoka serikalini au mawaziri wake waliotakiwa kujiuzulu. Nilishangaa, na hadi leo hii bado namshangaa sana huyu waziri wetu mkuu.

Kwa ukimya huu wa Pinda, nimetafakari sana, nimewaza sana na hatimaye nimeelekeza matumaini yangu kwa Rais Kikwete kuwakonga nyoyo Watanzania kwa yale yote tuliyoyashuhudia katika Bunge lililomalizika wiki hii.

Lakini pamoja na matumaini yangu haya yote. Moyo wangu umeanza kujawa na shaka kubwa pengine rais na yeye akaamua kunyamaza kimyaa kama alivyofanya waziri mkuu.

Nafikiria haya yote yanaweza kutokea. Na kama Rais Kikwete atawafumbia macho kama ailivyowahi kuripotiwa kwenye baadhi ya vyombo vya habari hapo majuzi, nitamshangaa pia.

Lakini, nawaomba Watanzania wenzangu tusishangae Rais Kikwete atakaposhindwa kuwatimua kazini Mawaziri wake!. Hii ndiyo Tanzania yetu, na viongozi wetu walioachiwa nchi na Baba wa Taifa, Nyerere.

Kwa mantiki hiyo, Rais Kikwete, waziri mkuu wajibikeni kwa wananchi wenu waliowafikisha hapo. Vinginevyo ipo siku mnaweza kushitakiwa ICC.



0784 785294
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom