Elections 2010 Kuna kiwango cha kuvumilia uchakachuaji lakini siyo hiki cha mwaka huu

Gosbertgoodluck

JF-Expert Member
Mar 3, 2008
2,855
401
Kwenu Watanzania wenzangu mnaoitakia mema nchi yetu,

Kuna maneno ya ushawishi yameanza kuenezwa kupitia kwenye mtandao kwamba Dr. Slaa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo watumie uungwana kwa kukubali matokeo ya uchaguzi ili kuepusha vurugu zinazoweza kusababisha umwagaji wa damu. Maneno hayo yamekuwa yakielekezwa kwa namna ya kujificha sana lakini mwelekeo wake ndiyo huo kwamba Dr. Slaa eti atapata umaarufu sana na kuheshimika sana ndani na nje ya nchi kwa kuamua kukubali matokeo. Nimeongea na jamaa zangu kadhaa maeneo mengi nchini, inaonekana nao kwa kiasi fulani wameanza kushawishika kwa maelezo kuwa Dr. Slaa aanze kukusanya nguvu tayari kwa kuiondoka ccm mwaka 2015.

Awali ya yote niweke wazi hapa kwamba kuna kiwango cha uonevu kinachoweza kuvumiliwa lakini siyo hiki kilichofanywa kwenye uchaguzi wa mwaka huu. Ukweli siku zote hujitenga. Kwa maneno mengine UKWELI na UWONGO havikai na kamwe havitakuja vikae pamoja. Watanzania tumeonewa, tumedhurumiwa na kuteswa kiasi cha kutosha. Wanaosema tusubiri mwaka 2015 hawasomi alama za nyakati. Kama ni ukombozi huu ndiyo mwaka wenyewe. Dr. Slaa na Chadema wakikubali mambo yaishe kienyeji kienyeji bila sheria kuchukua mkondo wake watakuwa wameua vuguvugu kubwa lililosambaa nchini la wananchi kutaka mabadiliko. Ebu ndugu fikiri japo kidogo, pamoja na uzandiki, wizi na ujambazi wa chama hiki ambacho ni kokolo la mafisadi wote nchini, na propaganda zao za eti Chadema ni chama cha wachaga, bado Chadema imeongeza viti vya majimbo kutoka 5 hadi zaidi ya 20. Kwa upande wa madiwani ndiyo usiseme kabisa. Madiwani wameongezeka wengi zaidi. Isitoshe, takriban majimbo yote ukiondoa mikoa yenye "uswahili swahili" yaliyochukuliwa na ccm, wagombea wanaofuata ni wa Chadema. Ninachotaka kueleza hapa ni kwamba wimbi la mabadiliko ni kubwa sana. Wakati wa kampeni wananchi wengi walitamani uandikishaji wapiga kura uanze upya ili wajiandikishe wengi na kukiadabisha chama kinacholea mafisadi kwa gharama za wananchi wanyonge.

Wito wangu kwa Drt. Slaa, viongozi wa Chadema na wanaharakati wote tutumie fursa zote za kisheria zilizopo kupinga matokeo ya uchaguzi huu bila kusababisha damu kumwagika. Ikiwezekana maandamano ya amani yafanyike mara moja ili kuonyesha hisia zetu na jamii ya kimataifa ifahamu waziwazi. Hata kama ushindi hatimaye utaenda ccm tutakuwa tumewapunguzia uchungu wananchi wengi nchini walioumia kwa kuibiwa kura kwa kiongozi wao mpendwa Dr. Wilbroad Slaa. Viongozi na wanaharakati wote mikoani nao wanaweza kuandamana kuunga mkono jambo hili ili kuonesha hisia tu kwamba katika miaka mitano ijayo, kikwete atakuwa anawaongoza wana ccm wenzake tu na siyo watanzania kwa ujumla wao.

Viongozi wa dini zote ninawasihi sana kwa imani zao waendelee kuiombea nchi yetu inayopita katika kipindi kigumu cha ukombozi. Mungu tunayemwamini bila shaka anaona kila kinachoendelea na kama alivyosema Baba wa Taifa letu Hayati Mwl. J. K. Nyerere, makosa mengine ya mwanadamu hayasubiri hukumu, bali adhabu yake hutolewa hapa hapa duniani. Adhabu ya kuiba kura za wananchi adhabu yake haitasubiri hukumu ya mwisho. Itatolewa hapa hapa duniani.

Mungu ibariki Tanzania,
Mungu ibariki Afrika.
 
Back
Top Bottom