Kuna faida kubwa kwenye mfumo wa tiketi mtandao kwa ukataji tiketi kuliko hasara zake

Elisha Sarikiel

JF-Expert Member
Aug 29, 2020
889
1,515
Ndugu Wasomaji,
Mwanadamu siku zote ana tabia ya kuwa mzito kupokea mabadiliko hata yale yenye faida kwake, kwakuwa tu hajazoea mabadiliko hayo. Hofu inamtawala zaidi kuhusu madhara ya mfumo kuliko faida zake. Lakini pia mfumo wowote mpya ili utekelezwe lazima watu fulani waumie ama ni kwa sababu hawataki kubadilika ama ni kwa sababu mfumo unawaondoa kwenye utaratibu waliouzoea.

Mfumo mpya huwa una tabia ya kuwaathiri vibaya hasa wale waliokuwa wanafaidika na mfumo mbovu uliokuwepo kuliko waliokuwa hawafaidiki nao. Na hawa watafanya kila njia kujaribu kukwamisha mfumo mpya kwa sababu unakwenda kinyume na maslahi yao binafsi. Hata hivyo, mfumo unapokuwa na faida kwa wengi wachache hawana budi kuachana na kutetea maslahi yao na kuunga mkono maslahi ya wengi.

Mfumo pia unapaswa kuwa rafiki, wenye gharama nafuu na unaowezekana kukubalika sana na watumiaji (end users) kutokana na faida zake. Ndivyo ambavyo mfumo wa ukataji tiketi wa kieletroniki ulivyo. Ni mfumo ambao, ukitekelezwa vizuri, utakuwa na faida kwa wengi kuliko hasara.

Mifano ya Vitu Vilivyowahi Kutuletea Hofu
Hofu tumekuwa nazo kwenye vitu vingi vipya kuanzia tochi za kisasa za kupima mwendo, VTS, Utozaji faini kwa njia ya PoS, na hata TRA walipotulazimisha tuuziwe bidhaa kwa risiti za EFD mioyo ilikuwa mizito sana. Baadhi ya wafanyabishara walitoa sababu nyingi sana za kutoukubali mfumo hdi kugoma. Lakini leo hii EFD zinafanya kazi hadi vijijini, vituo vyote vya mafuta vinatoa risiti, serikali inajipatia mapato yake na sote tunaona faida zake. Hata kama mfumo huu wa EFD umeumiza waliokuwa wachapishaji risiti, nk.

Kwa hiyo niseme tu kwamba, tunakokwenda teknolojia haikwepeki inaweza kuahirishwa tu. Je, leo hii nani alijua kuwa itawezekana kulipia huduma au bidhaa kwa simu bila kuwa na hela keshi? Leo hii nani alijua itawezekana kutosafiri na furushi la fedha kutoka Mtwara au Iringa kuja kufunga mzigo Dar? Leo hii hatupangi tena foleni ndefu benki kwenda kulipia kodi na bili mbalimbali. Leo hii hatupangi foleni ndefu kwenda kununua LUKU kwenye vituo vya LUKU vilivyokuwa kwenye vituo vya mafuta (au mmesahau?). Leo hii vocha za kukwangua zimeshakuwa adimu sana unanunua tu kwenye simu, kwa nini isiwezekane kununua tiketi ya bus?

Nini Maana ya Ukataji Tiketi Kielektroniki(E-ticketing)?
Ukataji tiketi kielektroniki au tiketi mtandao kama wengine wanavyosema ni mfumo usiohusisha uhifadhi wa siti (booking) na ukataji tiketi kwa kuandika kwa mkono tiketi. Ni mfumo wa kidigitali unaohusisha chochote kati ya vifuatavyo:
(a) Mashine ya POS (kama zile za traffic au EFD za TRA)
Hii inatumika kwenye ofisi za Booking mteja akifika ofisini, kwenye stendi, na ndani ya basi kwa abiria wa njiani.

(b) Tovuti (website).
Mteja anaingia kwenye tovuti ya basi husika au tovuti maalumu iliyoandaliwa kwa kazi hiyo kisha anachagua siku ya kusafiri, siti kisha anaihifadhi au kulipa kabisa.

(c) Applications (Apps).
Mteja anapakua App maalumu kwenye simu yake kutoka kwenye “Play store au App store yake” na kisha kuitumia kufanya booking na hatimaye kulipa.

(d) Kwa simu ya kawaida kama anavyoweza kununua umeme au kulipia DSTV
Hapa Mteja/ abiria anatumia menyu(menu) ya kwenye simu yake kununua tiketi.

Je, Mfumo wa Ukataji Tiketi Kieletroniki ni mpya kabisa?
Kimsingi mfumo huu sio mpya, mbali ya kuwa mifumo hii inatumika sehemu nyingi duniani, mfumo huu umekuwa ukitumika hata kwa baadhi ya mabasi hapa Tanzania. Cha tofauti tu ni kwamba kila kampuni ilikuwa na mfumo wake tofauti usiounganishwa na mifumo mingine kama vile TRA, LATRA, na NIDC. Na mifumo hiyo ilikuwa haipatikani kwenye kapu moja. Mfumo wa sasa ni “integrated” yaani umeunganishwa na vitu vingi sana na taasisi nyingi sana. Baadae tutaangalia faida za mfumo wa tiketi mtandao na hasara zake.

Tunachofahamu, mamlaka kama mamlaka imefanya semina nyingi na wamiliki kuhusu mfumo huu mpya wa ukataji tiketi. Tusichokuwa na uhakika ni kwa kiasi gani Mamlaka imefanya mikutano na Mawakala au vyama vyao, madereva au vyama vyao. Hata hivyo, uelimishaji na uhamasishaji umma unapaswa kuwa endelevu zaidi katika hili.

Faida za Mfumo
Mfumo Ukitekelezwa vizuri una faida sio tu kwa mmiliki bali pia kwa abiria na hata wafanyakazi wa bus.
1. KWA MMILIKI
Kwa mmiliki mfumo una faida kubwa zifuatazo:
(a) Unampunguzia upotevu wa mapato sababu nauli yake yake anaipata ikiwa kamili. Kama ni 35,000 anaipata yote tofauti na sasa ambapo inaweza kumfikia 20,000 tu.
(b) Unampa kumbukumbu ya mapato ya bishara yake. Takwimu zinazoweza kumsaidia kuthathimni na kupanga bishara yake.
(c) Unampunguzia gharama za uchapishaji makaratasi
(d) Unampunguzia udanganyifu
(e) Unampunguzia kesi abiria wake kutapeliwa na baadae yeye abebe lawama.
(f) Ni rahisi kwa mmiliki kuwajua abiria wake watiifu (loyal passengers) na kuwapa bonus
(g) Unapunguza gharama za uendeshaji, mfano kuwalipa wapiga debe na mawakala.

2. KWA KONDAKTA NA DEREVA
(a) Unampunguzia ugomvi wa kugonganisha siti
(b) Unampunguzia muda wa kupiga hesabu kujua kiasi kilichopatikana
(c) Unamfanya dereva kujua kiasi kilichopatikana kwani rekodi zote zipo
(d) Madereva wanaweza kutumia mfumo huu kama msingi wa hoja ya kudai kuongezeka kwa maslahi yao sababu wanaweza kujua kwa uhakika ni kwa kiasi gani biashara ina tija kwa mmiliki tofauti na sasa.
(e) Unapunguza muda wa kupanda kwenye gari

3. KWA ABIRIA
Huyu anafaidika zaidi na mfumo huu
(a) Unamwepusha kuibiwa. (Kupewa tiketi ya basi ambalo halipo)
(b) Unampunguzia usumbufu wa kuzongwa zongwa wakati wa kwenda kukata tiketi
(c) Unamwondolea usumbufu wa kugonganishwa siti
(d) Unamwondolea adha ya kulanguliwa tiketi kwa kulipa nauli sahihi
(e) Anaweza kununua tiketi toka alipo na kufanya malipo kwa Pesa taslimu, mifumo ya simu (M-PESA, T-PESA, Tigo-Pesa, airtel money, nk), benki, au kulipa kwa kadi
(f) Kumwondolea gharama za kusafiri kwenda kukata tiketi. Mfano kutoka Tegeta kwenda Ubungo kukata tiketi kwa ajili ya kusafiri kesho yake.
(g) Uhuru wa kuchagua basi alitakalo

Hasara za Mfumo Zinazosababisha hofu
1. Mfumo ukifeli tiketi zinaweza zisipatikane mtandaoni isipokuwa kwenye mashine ya PoS pekee.

2. Namna gani abiria asiye na smartphone anaweza kukata tiketi hususani vijijini

3. Mamlaka ya Mapato (TRA) kujua mapato halisi ya kampuni na hivyo kuweza kukadiria kodi sahihi kampuni inayofanya biashara ya usafirishaji. [Kumbuka awali mmiliki alikuwa na uwezo wa kusema tu kwa ruti ya Dar Mwanza kwa siku naingiza 1,500,000 tu kabla ya matumizi. Lakini sasa TRA atakuwa anaona moja kwa moja kinachoingizwa na mmiliki.

4. Nyingi tunazoziona sasa kuwa ni kampuni za Mabasi, kimsingi sio kampuni ni ubia tu wa wamiliki hata 5 wanaotumia jina moja mfano KIJANI EXPRESS. Kwan je anaonekana Juma Sadi kama Mmiliki lakini ndani yake kuna John, Ally, Siraj, Kenge na kila mmoja ana bus moja lenye jina Kijani Express. Kuja kwa tiketi mtandao kunafanya hawa watu wajulikane jambo ambalo wao hawataki. Lakini pia kutafanya hela zote ziingie kwenye akaunti moja ya Juma Sadi yeye ndio baadae awagawie wenzake tofauti na sasa labda wanagawana cash.

5. Wapiga debe na mawakala wanahofia kukosa kazi. Lakini kimsingi wapiga debe ndio wataathirika zaidi kuliko mawakala. Maana mawakala rasmi/halisi bado watakuwa na mashine za PoS Mkononi.

6. Mfumo wa TIKETI MTANDAO kutokuwa na mabasi. Kila ukifungua unakutana na ujumbe “hakuna mabasi kwa sasa”.

7. Elimu ya kutosha bado haijatolewa kwa umma. LATRA wanapaswa kuendelea kutoa elimu kila siku ikiwemo kuingia ndani ya mabasi na kuwaelekeza abiria namna ya kupata tiketi na faida zake.

8. Hofu ya kupoteza e-mail au meseji yenye tiketi kwa kuifuta

9. Gharama za awali za kuweka mfumo (installation) na baadae kulipia huduma (service charge).

10. Hofu ya gharama za uendeshaji kuongezeka kwa wamiliki na kwa abiria, gharama za nauli kupanda.

USHAURI
Mfumo ungeanza kwa majaribio kwa baadhi ya njia chache tu mfano, Dar-Mbeya-Tunduma ambapo LATRA ingehakikisha wamiliki wote kwenye njia hiyo wameshajisajili kwenye mfumo na hivyo kuwezesha Mabasi yote kuonekana tofauti na sasa ambapo ukitafuta mabasi kwenye njia hiyo unapata mabasi ya kampuni 1 tu au 2.

Aidha, changamoto zilizopo zifanyiwe kazi ili kuleta ufanisi katika mfumo na kufanya umma uupokee mfumo kwa mikono miwili. Elimu izidi kutolewa ikiwemo upatikanaji wa vipeperushi vinavyoelezea kinaga ubaga mfumo unavyofanya kazi, na pia kuwepo na matangazo kwenye vyombo vya habari yanayoelezea(demonstrate) namna abiria anavyoweza kupata tiketi.


1610280648359.png

Nakala kutoka kwa RSA admin1 ROAD SAFETY AMBASSADORS -TANZANIA -Ukurasa wa Facebook
 
Haya maendeleo yamekuja haraka sana. Wananchi wengi hawana elimu ya mtandao hata kutumia barua Pepe. Kwakua serikali yote ni kijani, ofisi za chama kijijini au mtaani zianze kutoa elimu ya mtandao. Viongozi wapewe computer mpakato wafundishie wananchi wao.

Upinzani walituchelewesha sana katika kuleta maendeleo. Wao ni kupinga tu.
 
Haya maendeleo yamekuja haraka sana. Wananchi wengi hawana elimu ya mtandao hata kutumia barua Pepe. Kwakua serikali yote ni kijani, ofisi za chama kijijini au mtaani zianze kutoa elimu ya mtandao. Viongozi wapewe computer mpakato wafundishie wananchi wao.

Upinzani walituchelewesha sana katika kuleta maendeleo. Wao ni kupinga tu.
Kama wamejua kuomba na yakutolea hili ni jambo dogo sana wataelewa tu
 
MAELEZO KUTOKA LATRA: JINSI YA KUPATA TIKETI ZA MABASI YA MKOANI MTANDAONI KUPITIA VIDEO:


Meneja Mradi wa Tiketi Mtandao kutoka Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) Bw Tadei Z. Mwita anajibu maswali haya yafuatayo kupitia video hii kwa utaratibu huu:
Mwanzo
Majukumu ya mamlaka
Kuhusu utafiti wa usafirishaji
Kiini cha wazo la tiketi mtandao
Jinsi ya kupata tiketi mtandaoni
Cha kufanya kama huna simu janja
Faida za tiketi mtandao kwa wasafirishaji
Faida za tiketi mtandao kwa abiria
Faida za tiketi mtandao kwa serikali
Changamoto za mfumo
Njia zinazoanza kutumia tiketi mtandao
Utaratibu kwa abiria wanaopandia njiani
Utaratibu kwa abiria wa safari za dharura
 
Hio app mbona yapo ma bus machache na route nyingine hazina ma bus pia bei ya tiketi ni kubwa kuliko ukienda hapo ubungo
 
Mfumo bado uko hopeless, mabasi machache tu ndio yanayopatikana kwenye hiyo App. Kwanini mnafanya kazi kwa kukurupuka ninyi WEHU?
 
Iyo app iboreshwe bado Sana kwenye list kuna basi moja tu mengine yamegoma
Screenshot_20210113-210741.jpg
 
Mawakala wa M-pesa,Tigo,Ttcl nao watafaidika kwa wale watu wasioweza kununua tiketi wataenda kwa wakala wakatiwe tiketi.Ajira haitapotea bali itabadilishwa kutoka kwa mpiga Debe kwenda kwa wakala was e- money.Mfumo ni mzuri ila umecheleweshwa karibu miaka mitano sasa.Acha IT technician wapige pesa in muda wa wabunifu kuwa milionea.
 
Kama utaratibu huu Ni mzuri na wenye faida kede kede; MBONA WAMILIKI WA MABASI HAWAUPENDI???
Sawa sawa na kusema mwanamke Ni mzuri wakati hajaolewa Wala Hana mchumba.
 

Similar Discussions

7 Reactions
Reply
Back
Top Bottom