Kumbukizi ya maisha ya Maalim Seif imeandikwa na Profesa Ibrahim Haroun Lipumba

Kasomi

JF-Expert Member
Sep 3, 2014
11,037
20,333
Kumbukizi Ya Maisha Ya Maalim Seif imeandikwa na Profesa Ibrahim Haroun Lipumba.

SEHEMU YA KWANZA

BURIANI KAKA YANGU MAALIM SEIF SHARIF HAMAD

SEHEMU YA KWANZA: NILIVYOKUTANA NA MAALIM SEIF

Profesa Ibrahim Haruna Lipumba, 19 Februari 2021.

Nimepokea kwa masikitiko, simanzi na huzuni kubwa sana taarifa ya kifo cha Maalim Seif Shariff Hamad, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, na Mwenyekiti wa ACT-WAZALENDO; Kilichotokea Jumatano Februari 17, 2021.

Mara ya kwanza nilikutana na Maalim Seif Sharif Hamad mwezi Julai au Agosti 1973, msikitini, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Tulipokutana mimi nilikuwa mwaka wa kwanza Idara ya Uchumi, Kitivo cha Sanaa na Sayansi ya Jamii. Maalim Seif yeye alikuwa mwanafunzi wa mwaka wa pili, Idara ya Sayansi ya Siasa, Utawala na Mahusiano ya Kimataifa.

Wakati huo idadi ya wanafunzi Waislam tuliokuwa tunasali msikitini kila siku ilikuwa ndogo sana. Watu sita au saba. Tulikuwa hatujazi safu moja.

Kila nikienda kusali msikitini nilimkuta Maalim Seif. Baada ya sala aliendelea na dua na kuvuta nyiradi.

Tulizoeana kwa kukutana mara nyingi msikitini. Mara nyingi tukizungumza kwa muda mrefu mara baada ya sala ya usiku.

Nilijifunza historia ya siasa za Zanzibar - inayoelezeka na isiyoelezeka toka kwake.

Mwaka 1974, wanafunzi wa Kiislam tulimchagua Maalim Seif kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Wanafunzi wa Kiislam wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam-MSAUD. Marehemu Sitna Mohamed alichaguliwa kuwa Katibu wetu na mimi nilichaguliwa kuwa Muweka Hazina - japo kwa kweli hatukuwa na hazina yeyote ya kutunza.

Shughuli yetu kubwa ilikuwa kuhakikisha kuwa Mwezi wa Ramadhani tuna futari nzuri na daku pia. Aidha tuliwakaribisha wahadhiri wa Kiislam kutoka maeneo mbalimbali kutoa mihadhara.

Baadhi ya Wahadhiri ninao wakumbuka ni pamoja na marehemu Sheikh Mohammed Nassor, Dr Malik - aliyekuwa anafundisha Sekondari ya Tambaza, na Dr Ahmad Totonji, Mkurdi mzaliwa wa Iraq, lakini alikuwa raia wa Saudi Arabia.

Nakumbuka pia kuwa wakati wa uongozi wetu, viongozi wa MSAUD tulifanya ziara kutembelea Chuo cha Kiislam kilichoko Chan’gombe, jijini Dar es Salaam, ili kuielewa mipango yake na kuchangia fikra zetu jinsi ya kukiendeleza na kukiimarisha.

Maalim Seif alimaliza kidato cha sita mwaka 1963. Baada ya Mapinduzi ya 1964 hakupewa fursa ya kuendelea na masomo ya Chuo Kikuu. Badala yake alipangiwa kazi ya ualimu na kwa miaka kadhaa alikuwa Mwalimu wa shule za sekondari. Hicho ndiyo chanzo cha yeye kufahamika kwa jina la Maalim.

Tanzania Bara tunatumia msamiati wa 'Maalim' kwa Walimu wa madrassa na viongozi wa dini ya Kiislam. Tofauti na bara, Zanzibar walimu wa skuli au shule za kisekula ndiyo wanaitwa 'Maalim'.

Wanafunzi kutoka Zanzibar walianza kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1972. Maalim alikuwa miongoni mwa wanafunzi hao na alikuwa kiongozi wao.

Baadhi ya wanafunzi hawa ni pamoja na Juma Duni Haji, Omari Ramadhani Mapuri, Marehemu Abubakar Khamis Bakari, na wengine.

Karibu wanafunzi wote alioingia nao Chuo Kikuu mwaka 1972 alikuwa amewafundisha Skuli za Sekondari Zanzibar.

Mwaka 1975 nilichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa TANU Youth League, Wilaya ya Mlimani.

Wakati wanafunzi Wazanzibari wakisheherekea sikukuu ya Mapinduzi pale Chuoni kwenye ukumbi wa Baraza la Chuo (Council Chamber), Maalim alinialika kushiriki na kutoa salamu za vijana wa TANU.

Maalim Seif alipofika mwaka wa tatu karibu na kufanya mitihani ya mwisho, aliugua na kulazwa katika zahanati ya Chuo Kikuu.

Kila jioni nilienda kumjulia hali na kumpa pole. Mitihani ya mwisho ya mwaka wa tatu ilibidi aifanyie kwenye chumba alikolazwa.

Pamoja na kuwa alikuwa mgonjwa wakati anafanya mitihani ya mwaka wa mwisho, alifaulu vizuri sana na kuongoza katika Idara ya Sayansi ya Siasa. Katika mazingira hayo magumu Maalim Seif alipata shahada yake ya B.A daraja la juu (B.A. Hon First Class).

Walimu wake wa Chuo Kikuu na hasa Prof. Goran Hyden (raia wa Sweden) na Marehemu Nathan Shamuyarila (Mzimbabwe aliyekuja kuwa Waziri wa Mambo ya Nje baada ya Uhuru wa Zimbabwe 1980) walijaribu sana kumshawishi Maalim abakie Chuo Kikuu kama Mkufunzi Msaidizi na hatimaye kuendelea na masomo ya juu, lakini alichagua kuitikia wito wa kurudi Zanzibar na kwenda kuwa Msaidizi wa Rais wa Zanzibar, Marehemu Aboud Jumbe.

Mimi nilimaliza shahada ya kwanza 1976 na nikaajiriwa kama Mkufunzi Msaidizi, Idara ya Uchumi, Chuo Kikiku cha Dar es Salaam. Baadaye kidogo nilipata fursa ya kwenda kusoma Chuo Kikuu cha Stanford, nchini Marekani.

Niliporejea nchini mwaka 1983, hali ya uchumi ilikuwa ngumu. Kila bidhaa ilikuwa adimu isipokuwa majani ya chai.

Kuanzia mwaka 1984, Idara ya Uchumi ya Chuo Kikuu ilikuwa inafanya makongamano ya sera za uchumi za kupambana na hali ngumu ya maisha.

Akiwa Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya Rais Ali Hassan Mwinyi, Maalim Seif alisimamia sera ya kulegeza masharti ya kufanya biashara na kuimarisha upatikani wa bidhaa Zanzibar.

Sera za kurekebisha uchumi hasa katika biashara zilianza kutekelezwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kabla ya Serikali ya Muungano kwa sababu ya ushawishi wa Maalim Seif Sharif Hamad.

Miaka ya 1970 na 1980, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kilikuwa na utamaduni wa kufanya mkutano kila mwaka kuhusu harakati za Ukombozi Kusini ya Afrika.

Toka akiwa Chuo Kikuu, Maalim Seif alikuwa mtafiti na mfuatiliaji wa ukombozi wa Bara la Afrika. Mwaka 1986 akiwa Waziri Kiongozi, alikuwa Mgeni Rasmi kufungua Mkutano wa Ukombozi wa Kusini mwa Afrika jijini Arusha.

Wakati huo Makaburu walikuwa wanatawala na kuendeleza siasa za ubaguzi wa rangi Afrika ya Kusini na Namibia. Nakumbuka Maalim alitoa hotuba nzuri na kusisitiza kuwa nchi za Kiafrika hazitakuwa huru mpaka Makaburu wan’golewe Namibia na Afrika ya Kusini.

Alihimiza kwamba ilikuwa ni wajibu wa nchi zote za Afrika kuunga mkono juhudi za ukombozi.

Baada ya ufunguzi wa mkutano huo, mimi na Profesa Mwesiga Baregu tuliwakilisha washiriki kwenye Chakula cha mchana na Maalim Seif kwenye hoteli ya Mount Meru, Arusha alipofikia.

Tulipoingia katika mfumo wa Vyama Vingi, Profesa Baregu amekuwa akipenda kunikumbusha juu ya lunch yetu na Maalim Seif Mount Meru Hotel.

Maalim Seif aliachishwa kuwa Waziri Kiongozi na kufukuzwa uanachama wa CCM na hatimaye kuwekwa ndani mwaka 1988.

Nikiwa Chuo Kikuu mwaka 1989 niliishawishi Jumuiya ya Walimu (UDASA) kutoa Tamko la kuitaka serikali kumuachia huru Maalim Seif Sharif Hamad.

Nakumbuka aliyeandika rasimu ya mwanzo ya Tamko hilo ni Profesa Hamza Njozi, wakati huo akiwa Mhadhiri Idara ya Kiingereza, na ambaye baadaye alikuwa Makamo wa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislam, Morogoro.

Sikupata fursa ya kukutana na Maalim Seif mwanzoni mwa miaka ya 1990. Mwaka 1991 niliteuliwa rasmi kuwa Mshauri wa Rais Mwinyi kuhusu masuala ya Uchumi.

Mwaka 1993 nikapewa fursa ya kuwa Fulbright Visiting Professor of Economics, Williams College, Massachussets, Marekani. Niliporudi toka Marekani Julai, 1995 wakati tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu ndipo uhusiano wa kisiasa na Maalim Seif ulipoanza rasmi, kama nitakavyoeleza katika sehemu ya pili.

===
Zaidi soma>>>
Sehemu ya tatu

Sehemu ya nne

Sehemu ya tano
 

Similar Discussions

9 Reactions
Reply
Back
Top Bottom