Kumbe CHADEMA haina imani na Zitto!

Mtu wa Pwani

JF-Expert Member
Dec 26, 2006
4,184
671
Kumbe CHADEMA haina imani na Zitto!

WIKI iliyopita, nilizungumzia kwa kirefu sababu zangu ambazo mimi binafsi niliziona ni za msingi katika suala la kumtaka mzee Benjamin Mkapa asijitokeze kujibu tuhuma na mawaziri wanaotuhumiwa ufisadi.

Nilitoa mawazo yangu kwa njia njema nikiamini kwamba watakaobahatika kusoma wataziangalia hoja zangu na kuamua kuziunga mkono au kuzipinga, tena kwa hoja, nikiamini hii ni njia mojawapo nzuri ya kubadilishana mawazo na kuelimishana katika mambo yanayohusu taifa letu.

Nashukuru wengi waliosoma waliwasiliana na mimi, nilipata ujumbe mfupi kwa njia ya simu zaidi ya 120 na wengine walinipigia simu kutoa maoni na madukuduku yao. Wapo walioungana nami na wapo walionipinga, jambo ambalo lilinifurahisha kwa kuwa nililitegemea.

Lililonitia huzuni kidogo ni kuona kwamba hadi leo bado Kiswahili kimekuwa kigumu kwa wananchi walio wengi. Hapa napenda kumpongeza Makamu wa Rais, Dk. Ali Mohamed Shein kwa msisitizo alioutoa hivi karibuni wa kusisitiza Kiswahili kipewe nafasi zaidi katika shughuli za kitaifa ili kuwapa nafasi wananchi wengi kukielewa zaidi na pia kukikuza.

Nasema hivyo kwa jinsi nilivyoona baadhi ya waliosoma makala yangu kushindwa kuelewa jambo nililokuwa nazungumzia, wakachanganya na kufikiri nilikuwa natetea waliotuhumiwa.

Mimi ninaamini katika utawala wa sheria, sikuwa nimekusudia kumhukumu au kumtetea yeyote kwa kuwa sina mamlaka hayo, naomba wale ambao hawakunielewa, warudie tena kusoma ili waelewe halafu watoe hoja zao nami niweze kujifunza kutoka kwao.

Mbali ya baadhi ya wale waliokosa kunielewa kutumia lugha ambazo si za kiungwana, bado nasimama katika hoja zangu kwamba mzee Mkapa hana sababu ya kujibu akijibu majibu yake yataanzisha malumbano zaidi, hasa kwa kuzingatia unyeti wa nafasi alizokuwa nazo huko nyuma.

Kwa upande wa mawaziri, pia nasisitiza kwamba enzi za utawala wa chama kimoja tuhuma hazikuwa zinatolewa hovyo hovyo, tena na maadui wa serikali (wapinzani wa serikali au chama tawala), mawaziri wakijiuzulu kiholela, tena kwa kushutumiwa na wapinzani wao, kuna hatari ya serikali kuyumba jambo ambalo litaweza pia kuyumbisha uchumi wetu.

Hili nalo nililisema kwa nia njema baada ya kuona shutuma (mabomu) ndio silaha pekee iliyobaki ya wapinzani maana siku hizi kila baada ya muda kidogo wanakuja na bomu jipya, nasema hivyo si kwa kutetea, bali kwa kuzingatia jitihada zetu za kujikwamua kiuchumi ambazo nadhani zinaweza kuwa ngumu zaidi tukiyumbisha mamlaka kuu ya nchi yetu (serikali).

Njia nzuri ni kwa wale wanaotuhumu kwenda katika vyombo walivyoshiriki kuviunda pale bungeni kushughulikia mambo kama hayo halafu hujuma zikithibitishwa ndipo tusubiri kuona hatua zitakazochukuliwa, najua wapo wanaosema zamani shutuma zilitosha kumuondoa mtu au kumtaka ajiuzulu, lakini ieleweke zamani haikuwa rahisi kwa mwananchi wa kawaida kutoa shutuma dhidi ya serikali au kiongozi wake.

Nyakati zile shutuma zilizokuwa zinatolewa zilikuwa zinatoka katika taasisi ambazo zilikuwa zinamsaidia rais katika kufanikisha kazi zake kwa hiyo zilikuwa zikifanya uchunguzi wa kina kabla ya kupeleka kwa rais kwa hatua zake.

Leo mambo yamekuwa tofauti, uhuru wa kusema umeongezeka na wengine wanaweza kuutumia vibaya kwa faida zao binafsi ukiachilia uwepo wa vyama vingi vya siasa, kwa upande wangu leo nahitimisha mchango wangu katika hoja hii kwa kusema shutuma haziwi na maana hadi zitakapothibitishwa.

Aliyewahi kuwa mbunge wa chama cha Labour na mpingaji mkubwa wa vita vya Iraq, George Halloway aliwahi kushutumiwa kupata fedha kutoka kwa Sadam Hussein kwa sababu tu alionekana kutokubaliana na vita hivyo.

Wabaya wake ndani ya chama chake cha Labour, wakala njama na kumsimamisha kushiriki vikao vya Bunge, akashitakiwa na kutakiwa kwenda kujitetea katika Kamati ya Seneti ambako alikwenda na kutoa utetezi mzuri.

Njama dhidi yake ziliendelea ndani ya chama chake hadi mwaka 2003 akafukuzwa rasmi katika chama hicho. Katika uchaguzi uliofuata, akaamua kugombea kupitia chama kipya cha Respect (heshima) na kumbwaga mgombea wa Labour akiwa ndiyo mbunge pekee kutoka chama hicho.

Tuhuma zilizotolewa kwake kwa kuwa hazikuthibitishwa hazikummaliza kisiasa na anaendelea kukijenga chama chake kipya akisubiri uchaguzi ujao kwa hamu kubwa.

Ndiyo maana nasema mzee Mkapa akijibu au mawaziri wakijiuzulu, nitashangaa sana na huo utakuwa ushindi mkubwa kwa maadui wa CCM na wale binafsi wa mzee Mkapa.

Ni jambo la kufurahisha kuona Rais Kikwete amekuwa makini sana pale wapinzani wanaposhutumu, wananchi wanapotoa maoni na madukuduku yao au pale wengine wanapojaribu kuupotosha umma.

Ameendelea kuchukua hatua mbalimbali ambazo ni muhimu kwa taifa baada ya kufanya utafiti wa kina na kuliacha taifa likizidi kuimarika na kuelekea katika Tanzania tunayoikusudia ya maisha bora kwa kila Mtanzania. Amefanya hivyo huku akikataa kuburuzwa na wale walio nje ya taasisi ya urais. Si tu kwa kuzingatia kwamba urais hauna ubia bali kwa kuelewa kila hatua anayoichukua ni lazima iwe ya kujenga nchi na kuiimarisha na si vinginevyo.

Amefanya maamuzi mengi mazuri mengine yakiwa magumu kwa utulivu na ukimya na kwa mara ya kwanza alichukua muda mrefu kuelezea vizuri masuala yote ya kitaifa na mtazamo wake kuhusu taifa letu pale Chimwaga, mkoani Dodoma katika hotuba yake ya kihistoria ambapo aligusia pia suala la madini, ambalo aliahidi kuunda kamati ambayo itamsaidia yeye na taifa katika kuboresha muelekeo wetu kwenye uboreshaji wa uwekezaji katika sekta hiyo.

Baadhi yetu hawakuamini wakati alipozungumzia suala la kuunda kamati itakayoshirikisha wapinzani, na mara tu alipoiunda, mshangao wao ukaanza kwa kupinga kuwamo baadhi ya wajumbe bila kujua kuwemo kwao kutasaidia kuondoa wasiwasi kwa yatakayojiri katika kamati hiyo.

Tumpe nafasi rais na wale wote waliopewa dhamana ya kumsaidia katika kuboresha taifa letu. Si vibaya endapo kuna wenye ushahidi wa kuwepo mafisadi au wala rushwa wakampelekea ili naye kupitia vyombo vyake, atafute ukweli zaidi.

Lakini kama kila tuhuma zitakuwa zinafanywa kuwa ni za kweli kabla ya vyombo vyenye mamlaka ya kuthibitisha hivyo havijatimiza majukumu yake, nchi itajikuta imeacha kufuata utawala wa sheria na hapo ndipo misingi ya kusingiziana na kuoneana itakuwa imeanza kujengwa.

Nchi yetu iko katika mikono salama ya Rais Kikwete, tusubiri na tuone atakavyolifikisha taifa salama mwaka 2015 huku tukimpa msaada wa taarifa zitakazomsaidia badala ya kushambulia serikali yake bila sababu za msingi.

Ameahidi na anaendelea kuthibitisha umakini katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya 2005 bila kusahau kwamba amesema tuhuma zote au malalamiko yanayotolewa na wananchi yanafanyiwa kazi, haraka zetu na malumbano yatatusaidia nini?

Wakati nikiendelea kutafakari kuhusu makala yangu ya wiki iliyopita na wengine wakimpongeza rais kwa kuunda Kamati ya Madini inayojumuisha wapinzani, nilipata mshangao mkubwa kusikia kwamba baadhi ya wananchi na viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), tayari wameingia katika malumbano makali ya kumtaka mbunge wao wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto, asiingie katika kamati hiyo na kwamba suala hilo sasa limehitishiwa kikao maalum cha kukinusuru chama kilichosababisha hata Mwenyekiti wa CHADEMA kurejea nyumbani akitokea masomoni Uingereza, kuokoa chama chake.
Hili lilinishtua sana, lilinishtua kwa kuwa katika makala yangu ya Oktoba 17, mwaka huu, nilisema tatizo walilo nalo watu wa upinzani ni kujenga hisia mbaya kwamba kila mtu anayepata nafasi ya kutekeleza jambo kubwa au muhimu kwa taifa huwa ni fisadi.

Kwa mawazo hayo hayo hata Zitto kuingia katika kamati wanaona mwenzao kapata nafasi ya kwenda nje ya mstari. Sasa kama huu ndio utaratibu nani ataamini kwamba wanazungumza kwa niaba ya taifa na wala sio hisia mbovu na ubinafsi.

Kumuambia Zitto ambaye alikuwa analalamikia kwamba mikataba imekuwa ya siri kubwa na haionekani, asiende kule ambako sasa ataiona na kama analo la kusema aseme zaidi, ni mshangao mkubwa kwa sisi ambao awali hatukuelewa au kuamini yaliyokuwa yanasemwa.

Na ndiyo maana wengi tunajiuliza, CHADEMA hawamuamini Naibu Katibu Mkuu wao Zitto kushiriki katika kamati hiyo?Na kama CHADEMA wanatuambia Zitto akishiriki katika kamati hataweza kutimiza malengo ya chama chao kwa uadilifu, maana yake ni nini? Kwamba viongozi wa chama hicho si wa kweli na kwamba wakipata nafasi za kutumikia umma watajinufaisha binafsi?

Tuliyoyasikia ni mengi kutoka CHADEMA, lakini endapo Zitto atazuiwa na chama chake kushiriki katika nafasi aliyopewa na rais, hii itatusaidia kuelewa kumbe tatizo la CHADEMA na viongozi wake ni kukosa kuamini wengine.
Hawamuamini Karamagi, Zitto na yeyote atakayepewa jukumu kubwa la kitaifa, na hapo ndipo utakuwa mwisho wa wimbo wa ufisadi, itabaki hisia na kutoaminiana.

Tambwe Hiza aliwahi kuwa Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chama cha Wananchi (CUF), lakini kwa sasa ni kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Naibu Mkuu wa Kitengo cha Propaganda na Uenezi cha CCM.
 
Tambwe Hiza,
Ni matumaini yangu ndugu Hiza unapitia ktk kijiwe kama wanavyofanya wengine. Makala yako imebeba mtazamo wako na dhana ambazo umezijengea tuhuma bila wewe mwenyewe kuwa na Uthibitisho. Ni rahisi kunyooshea watu kidole na kudai ushahidi wakati hayo uyasemayo wewe hayana ushahidi isipokuwa habari za kuokoteza ktk magazeni na vijiwe.

Kiswahili ni lugha nyepesi sana na ikiwa utakuwa ukitafsiri vitu kwa mtazamo huo basi mjomba una kazi kubwa mbeleni na hasa ktk shughuli ulizojihusisha nazo.

Maelezo yako yamejijenga sehemu moja KUJIKOSHA ama kwa kiswahili cha kizamani tunasema KUJIPENDEKEZA kwani umeyaona mabaya sehemu moja tu bila kujali uzito wa tuhuma ama lawama hizo.

Lini umeona Tuhuma zikitanguliwa na uthibitisho?.... hata jambazi linapokamatwa huanza na tuhuma kisha ukafanyika Upelelezi wakafuatwa baadhi ya watuhumiwa na sio wananchi wote pasipo kuwepo ushahidi wa kutosha kuweza kumweka mtuhumiwa chini ya Ulinzi. Ni huo Upelelezi ndio utakuja vumbua ushahidi tosha wa Kulifikisha jambazi mahakamani, haiwezekani vinginevyo..

Hiyo misingi ya kusingiziana kama ulivyosema hutokea tu ikiwa serikali itapuuza tuhuma hizi kwa madai ya ushahidi jambo ambalo haliwezi tokea kwa aina yeyote ya kesi duniani. Waziri wa Fedha mama Meghji mwenyewe alipoingia Kisha kubali kuwepo kwa ubadhilifu wa fedha, sasa without suspects ataweza vipi kujenga hoja ya kuanzisha uchunguzi?.

Ulichoweza kukiona vizuri ni toka Upande wapili tu! Upande wa Chadema ambako kwa lugha yako mwenyewe umeonyesha kuzua tuhuma ambazo hazina uthibitisho kwani mgongano wa mawazo baina ya wanachama haina maana kabisa ni kukosekana kwa imani kati yao.

Unapomkataza mkeo kutoshiriki ktk vikao vya majungu haina maana huna imani na mkeo isipokuwa huna imani na aidha wahusika ama vikao hivyo.

Pili, Ukimkataza mwanao kutotembea na kundi fulani la watu haina maana huna imani naye isipokuwa huna imani na hao vijana wenziwe...na mabishano yoyote kati yako na mwanao hayana maana kuwa kuna kutokuelewana ndani ya nyumba.

maelezo yako yote ni CCM against the REST.. yaani hata maoni ya WANANCHI umeyaweka chini na kutanguliza maslahi ya chama CCM hata kukiweka kuwa kina maadui..CCM ina maadui hii lugha gani kwa mwanasiasa kuweza kuitumia hasa pale wananchi wanapodai haki yao. Leo unawaona Chadema kama Wapinzani, sintashangaa kesho ukianza kuwaita Chadema ni maadui wa CCM.

Pole mjomba, katika zizi la CCM bado kabisa hujapata barehe yani wapo wanaume wanaoweza kuonekana umaarufu na wala Umaarufu hautafutwi kwa njia hizi.
 
Tambwe Hiza,
Ni matumaini yangu ndugu Hiza unapitia ktk kijiwe kama wanavyofanya wengine. Makala yako imebeba mtazamo wako na dhana ambazo umezijengea tuhuma bila wewe mwenyewe kuwa na Uthibitisho. Ni rahisi kunyooshea watu kidole na kudai ushahidi wakati hayo uyasemayo wewe hayana ushahidi isipokuwa habari za kuokoteza ktk magazeni na vijiwe.
Kiswahili ni lugha nyepesi sana na ikiwa utakuwa ukitafsiri vitu kwa mtazamo huo basi mjomba una kazi kubwa mbeleni na hasa ktk shughuli ulizojihusisha nazo.
Maelezo yako yamejijenga sehemu moja KUJIKOSHA ama kwa kiswahili cha kizamani tunasema KUJIPENDEKEZA kwani umeyaona mabaya sehemu moja tu bila kujali uzito wa tuhuma ama lawama hizo.
Lini umeona Tuhuma zikitanguliwa na uthibitisho?.... hata jambazi linapokamatwa huanza na tuhuma kisha ukafanyika Upelelezi wakafuatwa baadhi ya watuhumiwa na sio wananchi wote pasipo kuwepo ushahidi wa kutosha kuweza kumweka mtuhumiwa chini ya Ulinzi. Ni huo Upelelezi ndio utakuja vumbua ushahidi tosha wa Kulifikisha jambazi mahakamani, haiwezekani vinginevyo..
Hiyo misingi ya kusingiziana kama ulivyosema hutokea tu ikiwa serikali itapuuza tuhuma hizi kwa madai ya ushahidi jambo ambalo haliwezi tokea kwa aina yeyote ya kesi duniani. Waziri wa Fedha mama Meghji mwenyewe alipoingia Kisha kubali kuwepo kwa ubadhilifu wa fedha, sasa without suspects ataweza vipi kujenga hoja ya kuanzisha uchunguzi?.
Ulichoweza kukiona vizuri ni toka Upande wapili tu! Upande wa Chadema ambako kwa lugha yako mwenyewe umeonyesha kuzua tuhuma ambazo hazina uthibitisho kwani mgongano wa mawazo baina ya wanachama haina maana kabisa ni kukosekana kwa imani kati yao.
Unapomkataza mkeo kutoshiriki ktk vikao vya majungu haina maana huna imani na mkeo isipokuwa huna imani na aidha wahusika ama vikao hivyo.
Pili, Ukimkataza mwanao kutotembea na kundi fulani la watu haina maana huna imani naye isipokuwa huna imani na hao vijana wenziwe...na mabishano yoyote kati yako na mwanao hayana maana kuwa kuna kutokuelewana ndani ya nyumba.
maelezo yako yote ni CCM against the REST.. yaani hata maoni ya WANANCHI umeyaweka chini na kutanguliza maslahi ya chama CCM hata kukiweka kuwa kina maadui..CCM ina maadui hii lugha gani kwa mwanasiasa kuweza kuitumia hasa pale wananchi wanapodai haki yao. Leo unawaona Chadema kama Wapinzani, sintashangaa kesho ukianza kuwaita Chadema ni maadui wa CCM.
Pole mjomba, katika zizi la CCM bado kabisa hujapata barehe yani wapo wanaume wanaoweza kuonekana umaarufu na wala Umaarufu hautafutwi kwa njia hizi.

Heshima yako mkuu wangu,

Bob unazidi kunifanya niamini kuna vipaji vingi tu Tanzania.Duh,maneno mazito hayo mkuu wangu
 
Ndugu Tambwe, Title yako ni Vague haiko specific in relation to the main body of your article" Umejaribu ku-widen the net katika harakati zako za propaganda dhidi ya vyama vya upinzani. Nimejaribu kuchambua hoja chache tu kati ya mengi uliyoeleza, watanzania wenzangu wataongezea au kupunguza katika niliyoyasema na pengine kuzi-dissect hoja zako ambazo mimi sikuzigusia.


"Mbali ya baadhi ya wale waliokosa kunielewa kutumia lugha ambazo si za kiungwana, bado nasimama katika hoja zangu kwamba mzee Mkapa hana sababu ya kujibu akijibu majibu yake yataanzisha malumbano zaidi, hasa kwa kuzingatia unyeti wa nafasi alizokuwa nazo huko nyuma"

Marais wa nchi nyingine huwekwa kitimoto hata kama wapo madarakani( refer to Clinton Vs Lewinsky saga). Sembuse ya huyu Mkapa kuhusishwa na matumizi mabaya ya madaraka akiwa madarakani, tena ambayo yanaendelea ku-cost Watz dearly.

Kwa upande wa mawaziri, pia nasisitiza kwamba enzi za utawala wa chama kimoja tuhuma hazikuwa zinatolewa hovyo hovyo, tena na maadui wa serikali (wapinzani wa serikali au chama tawala), mawaziri wakijiuzulu kiholela, tena kwa kushutumiwa na wapinzani wao, kuna hatari ya serikali kuyumba jambo ambalo litaweza pia kuyumbisha uchumi wetu.

"Enzi za chama kimoja, ilikuwa ni utawala msonge, habari nyingi zilikuwa zinafichwa, lakini katika Dunia hii ya utandawazi plus watu walioko kwenye system kuchoshwa na Muungwana na Team yake, ndiyo maana imekuwa rahisi zaidi kupata "Classified" information ambazo nyingi ni mikataba mibovu kabisa ambayo haijawahi kutokea. Marais wa nchi zenye kujua nini maana ya uwajibikaji hujiuzulu pindi wanapotuhumiwa sembuse mawaziri wa Danganyika. Haihitaji shule kubwa kujua kuwa uchumi wetu upo taabani, na labda wakijiuzulu hali itaboreka zaidi kuliko ilivyo sasa."

Hili nalo nililisema kwa nia njema baada ya kuona shutuma (mabomu) ndio silaha pekee iliyobaki ya wapinzani maana siku hizi kila baada ya muda kidogo wanakuja na bomu jipya, nasema hivyo si kwa kutetea, bali kwa kuzingatia jitihada zetu za kujikwamua kiuchumi ambazo nadhani zinaweza kuwa ngumu zaidi tukiyumbisha mamlaka kuu ya nchi yetu (serikali).

Mr. Tambwe, umeonyesha unazi wa waziwazi, Hivi kweli hizo "Classfied information" unaziita "Mabomu ya wapinzani" Je, Machunde amekanusha kuwa si mwajiriwa wa Karamagi? Kashfa ya RADA unaiita mabomu wakati inawagharimu watanzania maskini. Please be serious and fair. Vyama hivi vitakuja na kupita lakini Generation ya watanzania is there to stay. Usiandike tu ili upate mkate wa leo bila kujali your grandchildren. Jitihada za kujikwamua kiuchumi haziwezi kufanywa na kutekelezwa na watu selfish ambao kila kukicha wanafikiria kuanzisha "Multi-billions projects" kwa ajili ya kushibisha matumbo yao. Was it fair to privatize NBC kwa bei ya kununua peremende? Umeona wenzetu wanavyoona mbali baada ya kuinunua, wameiuza NBC kwa faida kubwa. Na haya kwako ni mabomu. Uchumi unakuzwa kwa sera bora, mikakati na nia ya dhati na ya kizalendo ya kuitekeleza mikakati hiyo na siyo kuiingiza nchi kwenye mikataba kama ya Richmonduli.

Njia nzuri ni kwa wale wanaotuhumu kwenda katika vyombo walivyoshiriki kuviunda pale bungeni kushughulikia mambo kama hayo halafu hujuma zikithibitishwa ndipo tusubiri kuona hatua zitakazochukuliwa, najua wapo wanaosema zamani shutuma zilitosha kumuondoa mtu au kumtaka ajiuzulu, lakini ieleweke zamani haikuwa rahisi kwa mwananchi wa kawaida kutoa shutuma dhidi ya serikali au kiongozi wake.

"Imani ya wananchi kwa Bunge imepungua sana, tatizo limebaki kwenye katiba. Tume ya uchaguzi wakati hu-play role kubwa sana kwenye maamuzi ya kura. Hivyo, hadi hapo tutakapokuwa na tume huru ya Uchaguzi,bunge letu litaendelea ku-rubber stamp mikakati ya serikali hata kama inaua nchi.Hivi mwananchi ni nani? Unajua hata Watu wanaovujisha siri toka sirikali(ni) ni wananchi, tena wazalendo. Hapa ndipo naifagilia JF kwa sababu inatoa nafasi kwa watu kama hao kuendelea kuianika Serikali wanapoona Walalahoi hawatendewi haki."


Ndiyo maana nasema mzee Mkapa akijibu au mawaziri wakijiuzulu, nitashangaa sana na huo utakuwa ushindi mkubwa kwa maadui wa CCM na wale binafsi wa mzee Mkapa.

Hapa suala si ushindi kwa nani, hoja ni accountability kwa watanzania waliompa dhamana. Kumbe wewe upo kwenye dunia ya nani mshindi hata kama ushindi huo una madhara kwa Taifa. Kweli tuna safari ndefu sana katika kufikia maisha bora.


Nchi yetu iko katika mikono salama ya Rais Kikwete, tusubiri na tuone atakavyolifikisha taifa salama mwaka 2015 huku tukimpa msaada wa taarifa zitakazomsaidia badala ya kushambulia serikali yake bila sababu za msingi.

"Usipotoshe umma wa Tanzania,nchi haiko kwenye mikono ya JK peke yake, imo mikononi mwa watanzania wote ila JK amepewa jukumu la kuwaongoza. Sasa hawezi kuachiwa peke yake 'ETI KWA KUAMINI NCHI IKO KWENYE MIKONO SALAMA'. JK ni binadamu kama tulivyo wengine, anaweza kukosea kama wanavyokosea wengine. Unless unataka tuamini kuwa ana uwezo usio wa kawaida ulio juu ya Watanzania wengine.Naona kweli umepania, unaanza hata kumpigia debe ili achaguliwe 2010?"
 
Huyu bwana alimwanika Tambwe uchi kabisa kiasi kwamba kama Tambwe angekuwa na akili ya binadamu wa kawaida asingerudia kuandika ujinga huu. Hebu soma hii makala hapa.
_____________________________________________________

Mkapa anapochuuzwa na kina Hiza


Nkuzi Kwanzi

KWA aliyesoma utumbo wa mtu anayetapatapa kwa kujifanya msemaji wa Rais mstaafu Benjamin Mkapa, aitwaye Tambwe Hiza, atakuwa amesikitika na kuwashangaa Mkapa na Hiza.

Licha ya utetezi wake kuwa mfu na usio na mashiko, ni tahadhari kwa Mkapa kuwa kama hatakuwa makini, waganga njaa watamtumia wakijionyesha wanampenda, kumtetea na kumjali ilhali ukweli ni kwamba wanapaza sauti ili awasikie na awatupie makombo.

Hakuna mtu aliyetapatapa kipindi hiki kama Hiza. Alianza na kuvizushia vyama vya upinzani huku akijirejesha kundini alikokuwa kwa kulamba matapishi yake.

Hakujua kuwa CCM waliishaistukia janja uchwara ya wachumia matumbo na matapeli wanaohama hama vyama kukidhi njaa zao.

Kutokana na usuhuba na Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba, Hiza na makapi wengine walifinyangiwa ofisi na idara ya uani ya propaganda!

Jaribio la kuuza machukizo ya kundi hili wakati wa kutapatapa kutetea bajeti mikoani, waliishia kuzomewa.

Hiza hakuchoka kuusaka mkate na kuridhisha wasitiri wake. Aligombea ujumbe wa NEC na kubwagwa kama taka. Ameona hii janja ya nyani kutofanikiwa, amedandia utetezi mfu wa Mkapa.


Kwa mtu mwenye akili timamu na hekima na anayemjua Mkapa vizuri na zigo la madhambi yake, hawezi kupoteza muda wake kutaka kufanya muujiza wa kumsafisha.

Hiza ni nani akilinganishwa na vigogo kama Daudi Mwakawago, Jaji Mark Bomani, Joseph Butiku na watu wengine wenye majina na waliomuonya Mkapa kuwa anachojaribu kufanya ni kujichimbia kaburi na hakistahili kufanywa na mtu wa nafasi yake?

Watetezi wa Mkapa wanamdhalilisha sawa na wapambe wa utawala wa sasa wanavyousukumizia motoni. Hakuna kitu kibaya kama kumdanganya mtu. Maana ni kumfanya mpumbavu.

Kibaya zaidi ni kudanganya nawe ukajidanganya. Adui yako kweli muombee njaa. Hiza anajifanya kama Mtanzania aliyekuwa ughaibuni wakati ukweli kuhusu Mkapa ukiwekwa njia panda ili kila mpita njia ajionee na kuhukumu.

Hiza ataleta jipya gani iwapo akina Kingunge, Makamba, Mwanri, Warioba wamechemsha? Hiza anajua nini zaidi ya kuendeshwa na mkuno wa njaa tumboni?

Bahati mbaya CCM nayo imekula hasara. Maana kama kuna fasheni inayotumika kuiibia na kuitapeli si nyingine ni watu kuhama vyama au taaluma zao tayari kupewa kazi ya kuzoa uchafu wake wasiuweze. Dawa ya yote haya ni kusafisha nyumba yako na kuwa msafi.

Hiza asiyejua hata kujenga hoja zaidi ya kulalamika na kusifia, ana msaada gani kwa Mkapa iwapo ameshindwa kujisaidia mwenyewe kiasi cha kusaidiwa kwa njia ya kudhalilishwa? We Hiza we, tafuta njia ya uhakika ya kuishi na siyo salata na urongo.

Hata bata bingwa wa kuchokoa taka huwa halali chooni wala kujisifia matendo yake. Yeye kama hayawani hana jinsi. Hayo ni majaliwa yake. Nepi siku zote ni nguo ya aibu si vizuri kujisifia unepi wala fisi mpenda mizoga hajisifii ufisi wake. Hiza ni mahuluku wa ajabu anayeonekana kuendeshwa na njaa kiasi cha kuvuka mipaka!

Na hili inabidi liwe somo kwa watawala wasio waadilifu. Ufisadi unamtoa mtu utu na heshima kiasi cha kutetewa na majambazi wa kisiasa. Tangu lini kuku akamtetea mwewe hata ahaidiwe kutoliwa vifaranga vyake? Visipoliwa vyake vya wenzake vitaliwa. Je, kuna usaliti mchafu kama huu?

Mkapa kwa kutetewa na vyangu wa kisiasa, anazidi kumomonyoka na kuonekana mhalifu japo hataki aeleweke hivyo. Hakanushi wala hata kuwakemea kimya kimya huko wanakokutana kama wanakutana.

Je, Mkapa anawatuma akina Hiza kufanya kazi chafu kwa ajili yake au wanajikomba na kujipendekeza ili lau waambue makombo? Kama ni mkakati, basi umeshindwa hata kabla ya kufanyiwa kazi.

Hivi nani anadhani Watanzania ni majuha na wendawizimu kumsikiliza au kumwamini kiumbe asiyejiamini wala kuamini anachosema? Nani mpuuzi amuamini mkaanga sumu na majungu.

Hiza anadhani kuwa alipokuwa Mbeya hivi karibuni alijivua nguo hadharani kwa kukiri kuwa alikuwa mpika majungu mkuu alipokuwa CUF? Je, ameokoka lini kuacha kilema hiki cha akili hadi tumwamini?

Mkapa, kwa viwango vyovyote ni msomi, hata kama elimu yake aliitumia vibaya. Tangu lini msomi akatetewa na mbumbumbu mzungu wa reli? Ni ajabu kipofu kumtetea mwenye macho au shehe kutetewa na mlevi! Hii inazidi kumfanya Mkapa aonekane si Mr Clean kama tulivyoaminishwa.

Wazungu husema ‘show me your friends I will tell you who you are’. Na Mkapa japo amekataa kujitetea, bado hajahukumiwa kiasi cha kutetewa na vibaka na wasaka mkate. Ni aibu na hatari kwake.

Watu wenye majina yao, japo walipotea njia kama akina Jaji Joseph Warioba walijaribu wakazomewa na kusutwa, sasa wamenywea itakuwa Hiza!

Aliponiacha hoi Hiza ni pale alipowasingizia marehemu. Anadai Oscar Kambona alikuwa mwanazuoni! Pia anadai alipomtuhumu mwalimu JK Nyerere eti Mwalimu alinyamaza! Uongo, tena unaonuka.

Kama Hiza kaishiwa hoja afunge mdomo. Kwani Nyerere alieleza bayana kuwa hana tatizo na madai ya Kambona bali anachoomba auleze umma na vyombo vyake zilipo na zikiwapo basi wazichukue.

iza anachokifanya ni kujenga mazingira mazuri ya kuweza kujuana na Mkapa (kama atakuwa naye ameishiwa kiasi hicho) kwa kujifanya ni mtetezi wake. Tumewaona wengi hata waliofanya utapeli kwa kusingizia walitekwa na CCM kumbe ilikuwa ni kuwachuuza wenzao.

Ila tunakokwenda mchezo huu ni hatari. Maana ni usaliti. Wanachofanya ni kujipaka mafuta halafu wanakwenda kupita kati kati ya moto.

Kwa mtu anayeunga mkono mambo ya Mkapa na biashara zake za Ikulu iwe ni kwa njaa zake au upenzi wake au kwa vile alinufaika chini ya utawala wake, ni adui wa umma.

Nafasi haitoshi. La muhimu ni wananchi kuanza kuongeza idadi ya maadui wao kama umma ambapo hili genge jipya linalotumiwa au kujipandikiza kutetea uoza na kuhujumu harakati zao inabidi liangaliwe kwa jicho baya.
 
Huyu bwana alimwanika Tambwe uchi kabisa kiasi kwamba kama Tambwe angekuwa na akili ya binadamu wa kawaida asingerudia kuandika ujinga huu. Hebu soma hii makala hapa.

Niliusoma uchambuzi huu kwa makini kabisa, nami nikajazi wa kwangu, nadhani kama Tambwe angekuwa na uelewa hata wa mtoto wa shule ya chekechekea basi asingethubutu kuendelea kuubeba msalaba ambao inaonekana unamwelemea.

Nimeona waganga njaa wengi lakini huyu bwana ni mwisho wa yote.
 
sikuona uhusiano wa Title na article....

Kweli, unajua nimeanza kusoma thread nikajua Zitto ndio kaandika. Nikakuta mwandishi kaweka bold vijisehemu vya Zitto. Katika paragraph 31, ni para 4 zimewekwa bold. Paragraph 4 zimeipa title thread.....mmh.
Naona Nkuzi Kwanzi na Mkandara wamefunika.
 
Nilifikiri huo ujumbe umeandikwa na Zitto, kumbe ni tapeli Hiza, halafu huyu mtu wa Pwani, naona hana kazi ya kufanya, yaani kutwa na usiku amekalia majungu tu, aone wapi wamezungumza mambo ya CHADEMA, ili alete kijiweni. Huyu jamaa wa wapi? Kaa ukijua kuwa kinachoendelea nchini, ni zaidi ya CHADEMA na CCM, watu wamechoka na viongozi wababaishaji.
 

Similar Discussions

1 Reactions
Reply
Back
Top Bottom