Kuhusu tuhuma zilizotolewa dhidi ya Mkurugenzi Mkuu wa bodi ya kahawa Tanzania

Pius B. Ngeze

New Member
May 30, 2011
2
3
30/5/2011


TANZANIA COFFEE BOARD


P. O. BOX 732, MOSHI, TANZANIA




KUHUSU TUHUMA ZILIZOTOLEWA DHIDI YA MKURUGENZI MKUU WA BODI YA KAHAWA TANZANIA


Mnamo tarehe 1 Machi, 2011 nilisoma kwenye Jamii Forum tuhuma zilizodaiwa kuandikwa na “Wafanyakazi” wa Bodi ya Kahawa Tanzania dhidi ya Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo.

Nimefanya utafiti wa kina kuhusu tuhuma hizo na napenda kuwashirikisha wasomaji wa Jamii Forum matokeo ya utafiti huo kama ifuatavyo:

Mara baada ya habari hiyo kutoka, Kamati ya Uongozi wa Chama cha Wafanyakazi (TPAWU), Tawi la Bodi ya Kahawa Tanzania, ilikutana kujadili barua hiyo inayodaiwa kuandikwa na Wafanyakazi wa Bodi. Katika kikao hicho, Wajumbe wa Kikao hicho waliikana pamoja na yaliyomo na kuazimia kumwandikia Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika kukanusha “Wafanyakazi wa Bodi” kuandika au kuhusika na kuandika tuhuma hizo. Walifanya hivyo kwa barua yao Kumb. Na. TCB/TPAWU/01/2011 ya tarehe 7 Machi, 2011.

UCHUNGUZI WA TUHUMA HIZO
Kwa upande wangu, kama Mwenyekiti wa Bodi hiyo, niliamua kufanya utafiti ili kubaini ukwweli wa tuhuma hizo. Katika kufanya kazi hivyo, nilikutana kwanza na Wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya TPAWU (katika kikao chao rasmi), baadhi ya Wakuu wa Idara na Vitengo vya Bodi (mmojammoja), baadhi ya Makatibu Muhtasi ikiwa ni pamoja na wa mtuhumiwa, mfanayakazi anayeaminiwa/ anayedhaniwa kuwa ndiye mwandishi wa tuhuma hizo na mwishoni mtuhumiwa mwenyewe.

Kutokana na mazungumzo yangu na hawa wafanyakazi (mmojammoja), karibu wote (zaidi ya asilimia tisini (90%) walimtaja mwenzao mmoja. Wanasema yaliyomo katika barua hiyo yanafanana na aliyokuwa akiyasema kwa baadhi ya wafanyakazi. Hata siku habari hiyo ilipotokeza kwenye Jamii Forum ilionekana kuionyesha baadhi ya wafanyakazi kwa bashasha.

Kwa kujua historia yake katika utumishi wa Bodi, hata mimi sikushangaa!. Hulka yake ni ya ajabuajabu.

MAELEZO YA TUHUMA MOJAMOJA
Baada ya kueleza hayo, naomba sasa kutoa matokeo ya utafiti wangu kama ifuatavyo:

Tuhuma Na. 1: Kuendesha Shirika la Umma kama Shirika binafsi ili kutekeleza ajenda zenye manufaa binafsi

Jibu: Si kweli. Bodi ya Kahawa inaendeshwa kwa kuzingatia Sheria ya Kahawa Na. 32 ya 2001 na Kanuni zake za 2003. Pia, kwa kuzingatia Kanuni za Idara ya Utumishi wa Umma na Kanuni za Utumishi za Bodi ya Kahawa kama Staff Service Regulations, Financial Regulations na Bajeti ya kila mwaka. Aidha, Menejimenti inazingatia maazimio na maelekezo ya Bodi ya Wakurugenzi. Ni vigumu sana kwa Mkurugenzi Mkuu kupata fursa ya kutenda matakwa yake binafsi.

Tuhuma Na. 2: Kufumua muundo wa Bodi na kuunda mpya na kuanza kuutumia kabla haujaidhinishwa na serikali

Jibu: (a) Ndugu A. Kumburu alipokabidhiwa Ofisi ya Mkurugenzi Mkuu, tarehe 2/10/2008 na Mkurugenzi Mkuu aliyestaafu, moja ya mambo aliyokabidhiwa ni pamoja na Muundo mpya wa Bodi ambao ulikuwa na changamoto ya kuchelewa kuutekeleza kadiri ya maagizo ya serikali (Msajili wa Hazina) yaliyotokana na maagizo ya Waraka wa Serikali wa Machi 2006 katika kurazinisha majukumu ya Bodi za Mazao nchini.

Vyeo vipya vilitajwa katika muundo aliokabidhiwa ambao uliandaliwa mwaka 2004 na hata katika barua ya Mkurugenzi Mkuu ya makabidhiano, vyeo hivyo vimetajwa. Hata hivyo, alishauriwa kuufanyia mapitio (review) kabla ya kuanza kuutekeleza, kazi ambayo pia aliambiwa haikukamilishwa ili kuuweka sambamba na majukumu mapya ya Bodi katika Waraka wa Serikali wa 2006.

Muundo huo ulipitishwa kwenye kikao cha Bodi cha 59 na 60 na kupekekwa Hazina kupata idhini. Hazina ilituma wataalamu wake Bodi ya Kahawa kushauri juu ya kada mbalimbali katika muundo huo ambao walifanya kazi kwa siku tatu mapema 2009.

Ili kuisaidia Bodi kuanza kuajiri watumishi, kikao cha wataalamu wa Hazina kilishauri ajira zianze kutekelezwa kwa kuzingatia rasimu ya muundo uliopitishwa na Bodi na kuwekewa maoni ya wataalamu wa Hazina. Hiyo ndiyo nguzo iliyotumiwa na Idara Kuu ya Utumishi kukubali kutoa kibali cha vyeo vipya katika ajira za mwaka 2010 na zilizoombwa 2011. Hilo pia liliwezesha Hazina kurekebisha mishahara ya watumishi wote wa Bodi mwaka 2010/11.
Kipaumbele cha ajira kilitolewa kwa Wakuu wa Idara kwa sababu kwa kipindi kirefu Idara ziliongozwa na Makaimu.

(b) Uhamisho wa watumishi ulitokana na maamuzi ya Bodi ya Wakurugenzi ya kupanua huduma za Bodi kwenda maeneo ya uzalishaji ili kuwa karibu na wakulima. Badala ya kusubiri ajira mpya, Menejimenti ilichukua hatua ya kuwahamishia watumishi wenye ujuzi wa kahawa kwenye Ofisi za Kanda ambazo zilikuwepo hapo awali badala ya kujazana Makao Makuu, Moshi.

(c) Walioadhibiwa utaratibu ulifuatwa na walikuwa na haki ya kupinga adhabu iwapo hawakuridhika nayo.

Tuhuma Na. 3: Ubia na Asasi isiyo ya Serikali (NGO) kuomba pesa za maendeleo ya kahawa na pesa kutolewa kwa NGO kwa manufaa binafsi.

Jibu: Hoja hii inahitaji ushahidi wa NGO iliyopata fedha kwa andiko la Bodi ya Kahawa na chanzo cha ufadhili huo, na ni kiasi gani. Makao Makuu ya Bodi hayana kumbukumbu ya NGO, hata moja, iliyopata fedha za namna hiyo.

Tuhuma Na. 4: Bodi ya Kahawa kuingizwa kwenye malumbano na viongozi wa mikoa ya Kigoma na Wilaya ya Tarime

Jibu: Uongozi wa Bodi ya Kahawa (Bodi ya Wakurugenzi au Menejimenti) haujawahi kukaa kikao na viongozi wa Mkoa wa Kigoma kujadili au kulumbana juu ya maagizo ya Bodi katika mkoa huo. Kama malumbano hayo yapo, mkoa huo haujayaleta Bodi ya Kahawa.

Kwa upande mwingine, Bodi ya Kahawa (Mwenyekiti na Mkurugenzi Mkuu) tumewahi kufanya mkutano na Mkuu wa Mkoa wa Mara pamoja na Wakuu wa Wilaya za Musoma, Serengeti, Rorya na Tarime. Katika kikao hicho cha tarehe 8/10/2010 tulitoa ufafanuzi juu ya kusimamishwa Makampuni binafsi ya ununuzi wa kahawa Wilayani Tarime ambayo yalikiuka kanuni kwa kuchanganya Arabika laini (Mild Arabica)na Arabika ngumu (Hard Arabica) kwenye soko. Kikao kiliisha vizuri na tarehe 9/10/2010 kwa pamoja tukafanya Mkutano wa Wadau wa Kanda ya Mara uliofanyika Mjini Tarime ukiwashirikisha pia viongozi wakuu wa Serikali wa Mikoa ya Mara na Mwanza. Katika kikao hicho Bodi ya Kahawa ilitoa ufafanuzi wa muafaka huo.
Tuhuma Na. 5: Kufuta leseni ya kununua kahawa mbivu ili kulinda Kilicafe

Jibu: Leseni ya kununua kahawa mbivu (cherry) haijafutwa na inaendelea kutolewa kwa waombaji wenye sifa zinazotakiwa.

Tuhuma Na. 6: Kamati ya Nidhamu

Jibu: Kadiri ya Kanuni za Utumishi za Bodi ya Kahawa, Mwenyekiti wa kikao cha Kamati ya Nidhamu ni Mkurugenzi Mkuu. Ushirikishwaji wa Chama cha Wafanyakazi unategemea ngazi ya mfanyakazi mtuhumiwa. Sheria inampatia mfanyakazi fursa ya kumchagua mfanyakazi mwenzie au mwakilishi wa Chama cha Wafanyakazi wakati wa kusikilizwa utetezi wa tuhuma zake. Haki za msingi za mfanyakazi asipozipata, upo utaratibu wa kanuni wa kuzidai kupitia chama cha wafanyakazi.

Tuhuma Na. 7: Kujilimbikizia mali

Jibu: (a) Mkurugenzi Mkuu aliingia Bodi ya Kahawa 2008 akitokea Technoserve, Arusha, ambako alikuwa akiishi kwenye nyumba yake binafsi. Alihamia Arusha kutokea Mbinga ambako tayari alikuwa na nyumba zake mbili binafsi, moja ikiwa ya biashara na moja ya kuishi. Alikuwa na kiwanja Mjini Songea ambacho kilijengwa banda lililoezekwa tu.

Aliingia Bodi ya Kahawa akiwa na magari mawili, Toyota Prado ya kutembelea na Toyota Hiace iliyokuwa inafanya biashara Mjini Dar es Salaam. Leo hii Mkurugenzi Mkuu ana magari binafsi mawili ya familia bila kufanya biashara, yaliyonunuliwa baada ya kuuza hayo yaliyotajwa hapo juu.

Ni vema utafiti au ushahidi ukalotewa juu ya malimbikizo ya utajiri unaodaiwa, upo katika mali gani au akaunti binafsi zilizopo Exim Bank na CRDB Bank.

(b) Posho za vikao na safari zina kanuni na bajeti zake. Kama kuna malipo yaliyofanyika kinyume na kanuni yatolewe ushahidi.

HITIMISHO
Ndugu A. Kumburu alipoteuliwa kuongoza Bodi hii aliikuta ikiwa na mapungufu kadhaa, ikiwa ni pamoja na malalamiko ya wafanyakazi dhidi ya mishahara midogo na maslahi duni n.k. Katika kipindi cha miaka miwili iliyopita hali hiyo imebadilika sana.

Ndugu Kumburu anajua kuitumia Bodi ya Wakurugenzi na ameitumia. Kwa sababu hii, mambo mengi aliyoyafanya ni baada ya kupata kibali cha Bodi ya Wakurugenzi.

Amefanya mengi na wafanyakazi wengi wanakiri kuwa ni mchapakazi na mtetezi wao. Hata Jumamosi na Jumapili (baada ya kutoka kanisani) hurudi ofisini kuchapa kazi.

Kwa upande mwingine, ni kweli kuwa kutokana na Ofisi Kuu ya TCB kuwa mbali na Dar es Salaam, safari za kwenda Dar es Salaam ni nyingi. Hana njia ya kuzikwepa.

Sisi kama Bodi ya Wakurugenzi hatujawahi kulalamikia utendajikazi wake na tunamshkuru sana kwa bidii yake ya kusimamia majukumu ya Bodi (TCB) kwa mujibu wa Sheria na Kanuni, kuwajali wafanyakazi na chama chao, kutetea wakulima wa Kahawa nchini ili waweze kupata bei nzuri, kurejesha taswira (image) ya TCB kwa Umma wa Tanzania na Kimataifa na kwa msimamo wake usioyumba katika masuala ya msingi katika utekelezaji wa sheria ya Kahawa, Na. 23 ya 2001 na Kanuni zake za 2003, Taratibu za Serikali na Maagizo ya Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika.

Kwa upande mwingine, sitarajii kati ya wafanyakazi 58 wa Bodi wote (100%) wafurahie kazi yake! Haitawezekana hata siku moja!!.

Kutokana na uamuzi wa Kamati ya Uongozi ya TPAWU kukana kuhusika na kuandika tuhuma hizo na kutokubaliana na yaliyomo, na kutokana na maelezo yangu kuhusu tuhuma hizo, ni dhahiri kuwa tuhuma hizo si za kweli na ni za mtu binafsi mwenye sababu zake binafsi.


Pius B. Ngeze
MWENYEKITI WA BODI,
BODI YA KAHAWA TANZANIA
Baruapepe: ngezep@yahoo.co.uk
tepultd@yahoo.com

simu: 0784 – 690277
0768 – 023019
 
Ahksante Mzee...

Hii ni dalili nzuri inayoonyesha mwelekeo mzuri na uwajibikaji - At least you went one more mile ahead...
 
wewe CHADEMA TU. UNAANGAMIZA CCM YETU KWA UFISADI WENU. JIVUE GAMBA NA UTWACHIE CCM YETU SAFI

Malaria sugu u mgonjwa, yaani wewe unajiona ni CCM halisi kiasi cha kumwona Mzee Ngeze ni Fisadi? Wewe ID yako umeificha, Mzee Ngeze kaja waziwazi na ID yake kwa kuwa anaamini anachokisema na kukitetea; wewe kwa uzuzu wako unampiga madongo Mzee Ngeze na kujiona wewe u CCM safi! Tueleze basi waziwazi, wewe u nani? Jitokeze hadaharani na ID yako kama Wana-CCM wenazko wanavyofanya humu ndani, vinginevyo u manafiki wewe na wewe na wanafiki wenzako ndo mmekifikicha CCM hadi kuwa Chama Cha Mafisadi, Chama cha Majambazi, Chama cha Magamba, Chama cha Mitandao, Chama cha Makulaji, nk, nk.

Ama kweli ufalme wenu unaparanganyika!
 
Asante mwenyekiti at least umeonyesha mfano kwa kufanyia kazi tuhumu zilizoelekezwa kwako. Lakini ndenda mbali zaidi kwa kuhakikisha unatenda haki ili mambo kama haya yasijitokeze tena
 
Hongera saana mwenyekiti wa Bodi.

Hii inaonyesha tunawafikia na mnatusikia. Ila katika andiko lako, sijaelewa, kulikuwa kuna maana gani ya kumtafuta mtuhumiwa badala ya kujibu tuhuma? Huyo mfanyakazi inawezekana akawa yeye au si yeye, manamuweka katika wakati gani? Kwani mngejibu tuhuma bila kuhangaika na mfanyakazi mnamuhisi mngepungukiwa nn? Au ni mbinu ya kuwafunga watu mdomo?
 
30/5/2011


TANZANIA COFFEE BOARD


P. O. BOX 732, MOSHI, TANZANIA




KUHUSU TUHUMA ZILIZOTOLEWA DHIDI YA MKURUGENZI MKUU WA BODI YA KAHAWA TANZANIA


Mnamo tarehe 1 Machi, 2011 nilisoma kwenye Jamii Forum tuhuma zilizodaiwa kuandikwa na "Wafanyakazi" wa Bodi ya Kahawa Tanzania dhidi ya Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo.

Nimefanya utafiti wa kina kuhusu tuhuma hizo na napenda kuwashirikisha wasomaji wa Jamii Forum matokeo ya utafiti huo kama ifuatavyo:.....................................................

Umeonyesha mfano mzuri wa uongozi. Kutoa response ya malamiko. Sijui kama majibu uliyotoa yanaelezea hali halisi on the ground but nakupongeza sana. Na nashawishika kukubaliana na hoja zako. Ten nimependa hujaiweka hii habari kwenye sisasa maana wengine kila kitu ni siasa tu

Wewe CHADEMA TU. UNAANGAMIZA CCM YETU KWA UFISADI WENU. JIVUE GAMBA NA UTUACHIE CCM YETU SAFI
Unasema awaachie CCM yenu. Awaaachie wewe na akina nani?
 
Mzee Pius Ngeze nakupongeza sana kwa ufuatiliaji wako makini...Huu ni mfano mzuri sana kwa Wazee wenzako na umeonyesha unakwenda teknolojia HONGERA SANA!!!
 
Hivi pamoja na kufuatilia haya yote, hao bodi ya kahawa wameweka mechanims gani kwa wafanyakazi kueleza yale wasiyoyakubali?
 
Mzee Ngezo si ungeanza na salaamu wa wenyeji kabla ya kujibu tuhuma? hata hivyo nakupongeza kwa kujali kuvinjari mitandao ya kijamii, maana wazee wa rika lako hawathubutu kuingia huku.

Ila kuna swali moja, ilikuwaje ukateuliwa Mweneyekiti wa Bodi ya Kahawa wakati huko Ngara mnalima 'mashaza' tu, si kahawa? Njua mwaka 2005 ulitamka wazi wazi na bila kumung'unya maneno, kuwa wewe ulikuwa mwanamtandao wa Kikwete; ni enzi hizo ukiwa mwenyekiti wa CCM wa mkoa Kagera, bila shaka sasa ndio hasa inalipa:A S-rose:
Hongera!:pound:
 
Mzee Ngeze kitendo cha kumtetea Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya kahawa ni cha kujidhalilisha kwani maelezo uliyoyatoa katika mtandao huu ni ya ujumla tena sio kweli.

Siyo kweli kwamba tunapewa leseni za kununua kahawa mbivu (Cherry). Hii inatufanya tuffikiri kwamba wewe ndiye unampa kiburi cha kuvuruga sekta ya kahawa kama alivyotaka kuvuruga kiwanda cha kukoboa kahawa cha Mbinga wakati akipambana na Bosi wake Bw. Kasongo.

Mzee Ngezi tunajua unavyopenda kutumia mabavu kama ulivyokuwa unapambana na Jeshi la Polisi likitekeleza sheria ya kuzuia baiskeli mkoani Kagera badala ya kupambana kubadilisha sheria kwanza. Tulisikia ulivyoshangilia pale kamanda Tosi (Mchapa kazi) alipoamishwa. Kutataka kutumia mabavu ndiko kulikufanya ukawa unapambana na Mfuru, Masilingi na Sebabili.

Ubabe huo sasa umeanza kuuleta katika sekta ya kahawa kwa kutegemea mahusihano yako. Je kulikuwa na sababu ya kutumia mabavu kutaka kumziba mdomo mjumbe toka Tarime katika Mkutano Mkuu uliofanyika Morogoro.

Mkurugenzi wa Bodi ya kahawa amegundua madhaifu yako anyatumia kutekeleza malengo yake na mwisho wa yote wewe ndiye unayejivunjia heshima kwani ukweli utathibitika.
 
Mzee Ngeze ni mtu ambaye anafanya kazi kwa hisia.Mzee Ngeze ameeandika baadhi ya vitabu kwa watu mnaojua na kufuatilia historia,hata nilipoona amejibu hoja hii yeye mwenyewe wala sikutaharuki.Ila ameteleza sana kwa sababu yeye kama Mwenyekiti wa bodi hakupaswa kumtetea mkurugezi waziwazi namna hii,hata kama hoja za wafanyakazi hazikuwa na ukweli kuna namna ya kuzijibu ili ulete suluhu kati ya Mkurugezi na wafanyakazi.Maelezo ya mzee Ngeze yamejaa ushabiki na wala sio ya kitafiti kwa sababu utafiti unataratibu zake.
Kaatika tuhuma zile moja ya tuhumu zilikuwa zinamuhusisha yeye mzee ngeze kwamba anafanya kazi za wataalamu wakati yeye sio mtaalamu,sasa utafiti wake amezungumzia nini kuhusu hilo?.Wazee wa namna hii ndio wanaotuvurugia nchi na kutufanya tuwe maskini zaidi kwa kufikiri kuwa maamuzi /mawazo yao ni sahihi kuliko maamuzi ya watu wenge.
Napata wasiwasi na madaraka uliyonayo na unavyoyatumia,Inakuwaje Uelezee hisia zako kwa kutumia jina la Bodi ya Kahawa.! Hii inanipa picha kuwa Bodi hii ni mali yako na Mkurugezi Mkuu A.Kumburu.
Pia umenisikitisha na kunishangaza kujibu hoja ya Kuendesha Bodi kama Shirika binafsi,Shirika la umma lina misingi na taratibu zinazoendana na utawala bora.Ila kitendo cha wewe kukurupuka na kuja kumtetea Mkurugezi huku kwenye mitandao ya kijamii inadhihirisha wazi shirika hilo mnaliendesha kama taasisi ya watu binafsi.

Tafakari sana hichi ulichoshauriwa na A. Kumburu kuja kuonyesha kuwa wewe ni wa kisasa.Heshima yako unaidhohofisha siku zinavyozidi kwenda .
 
Back
Top Bottom