Pius B. Ngeze
New Member
- May 30, 2011
- 2
- 3
30/5/2011
TANZANIA COFFEE BOARD
P. O. BOX 732, MOSHI, TANZANIA
P. O. BOX 732, MOSHI, TANZANIA
KUHUSU TUHUMA ZILIZOTOLEWA DHIDI YA MKURUGENZI MKUU WA BODI YA KAHAWA TANZANIA
Mnamo tarehe 1 Machi, 2011 nilisoma kwenye Jamii Forum tuhuma zilizodaiwa kuandikwa na Wafanyakazi wa Bodi ya Kahawa Tanzania dhidi ya Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo.
Nimefanya utafiti wa kina kuhusu tuhuma hizo na napenda kuwashirikisha wasomaji wa Jamii Forum matokeo ya utafiti huo kama ifuatavyo:
Mara baada ya habari hiyo kutoka, Kamati ya Uongozi wa Chama cha Wafanyakazi (TPAWU), Tawi la Bodi ya Kahawa Tanzania, ilikutana kujadili barua hiyo inayodaiwa kuandikwa na Wafanyakazi wa Bodi. Katika kikao hicho, Wajumbe wa Kikao hicho waliikana pamoja na yaliyomo na kuazimia kumwandikia Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika kukanusha Wafanyakazi wa Bodi kuandika au kuhusika na kuandika tuhuma hizo. Walifanya hivyo kwa barua yao Kumb. Na. TCB/TPAWU/01/2011 ya tarehe 7 Machi, 2011.
UCHUNGUZI WA TUHUMA HIZO
Kwa upande wangu, kama Mwenyekiti wa Bodi hiyo, niliamua kufanya utafiti ili kubaini ukwweli wa tuhuma hizo. Katika kufanya kazi hivyo, nilikutana kwanza na Wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya TPAWU (katika kikao chao rasmi), baadhi ya Wakuu wa Idara na Vitengo vya Bodi (mmojammoja), baadhi ya Makatibu Muhtasi ikiwa ni pamoja na wa mtuhumiwa, mfanayakazi anayeaminiwa/ anayedhaniwa kuwa ndiye mwandishi wa tuhuma hizo na mwishoni mtuhumiwa mwenyewe.
Kutokana na mazungumzo yangu na hawa wafanyakazi (mmojammoja), karibu wote (zaidi ya asilimia tisini (90%) walimtaja mwenzao mmoja. Wanasema yaliyomo katika barua hiyo yanafanana na aliyokuwa akiyasema kwa baadhi ya wafanyakazi. Hata siku habari hiyo ilipotokeza kwenye Jamii Forum ilionekana kuionyesha baadhi ya wafanyakazi kwa bashasha.
Kwa kujua historia yake katika utumishi wa Bodi, hata mimi sikushangaa!. Hulka yake ni ya ajabuajabu.
MAELEZO YA TUHUMA MOJAMOJA
Baada ya kueleza hayo, naomba sasa kutoa matokeo ya utafiti wangu kama ifuatavyo:
Tuhuma Na. 1: Kuendesha Shirika la Umma kama Shirika binafsi ili kutekeleza ajenda zenye manufaa binafsi
Jibu: Si kweli. Bodi ya Kahawa inaendeshwa kwa kuzingatia Sheria ya Kahawa Na. 32 ya 2001 na Kanuni zake za 2003. Pia, kwa kuzingatia Kanuni za Idara ya Utumishi wa Umma na Kanuni za Utumishi za Bodi ya Kahawa kama Staff Service Regulations, Financial Regulations na Bajeti ya kila mwaka. Aidha, Menejimenti inazingatia maazimio na maelekezo ya Bodi ya Wakurugenzi. Ni vigumu sana kwa Mkurugenzi Mkuu kupata fursa ya kutenda matakwa yake binafsi.
Tuhuma Na. 2: Kufumua muundo wa Bodi na kuunda mpya na kuanza kuutumia kabla haujaidhinishwa na serikali
Jibu: (a) Ndugu A. Kumburu alipokabidhiwa Ofisi ya Mkurugenzi Mkuu, tarehe 2/10/2008 na Mkurugenzi Mkuu aliyestaafu, moja ya mambo aliyokabidhiwa ni pamoja na Muundo mpya wa Bodi ambao ulikuwa na changamoto ya kuchelewa kuutekeleza kadiri ya maagizo ya serikali (Msajili wa Hazina) yaliyotokana na maagizo ya Waraka wa Serikali wa Machi 2006 katika kurazinisha majukumu ya Bodi za Mazao nchini.
Vyeo vipya vilitajwa katika muundo aliokabidhiwa ambao uliandaliwa mwaka 2004 na hata katika barua ya Mkurugenzi Mkuu ya makabidhiano, vyeo hivyo vimetajwa. Hata hivyo, alishauriwa kuufanyia mapitio (review) kabla ya kuanza kuutekeleza, kazi ambayo pia aliambiwa haikukamilishwa ili kuuweka sambamba na majukumu mapya ya Bodi katika Waraka wa Serikali wa 2006.
Muundo huo ulipitishwa kwenye kikao cha Bodi cha 59 na 60 na kupekekwa Hazina kupata idhini. Hazina ilituma wataalamu wake Bodi ya Kahawa kushauri juu ya kada mbalimbali katika muundo huo ambao walifanya kazi kwa siku tatu mapema 2009.
Ili kuisaidia Bodi kuanza kuajiri watumishi, kikao cha wataalamu wa Hazina kilishauri ajira zianze kutekelezwa kwa kuzingatia rasimu ya muundo uliopitishwa na Bodi na kuwekewa maoni ya wataalamu wa Hazina. Hiyo ndiyo nguzo iliyotumiwa na Idara Kuu ya Utumishi kukubali kutoa kibali cha vyeo vipya katika ajira za mwaka 2010 na zilizoombwa 2011. Hilo pia liliwezesha Hazina kurekebisha mishahara ya watumishi wote wa Bodi mwaka 2010/11.
Kipaumbele cha ajira kilitolewa kwa Wakuu wa Idara kwa sababu kwa kipindi kirefu Idara ziliongozwa na Makaimu.
(b) Uhamisho wa watumishi ulitokana na maamuzi ya Bodi ya Wakurugenzi ya kupanua huduma za Bodi kwenda maeneo ya uzalishaji ili kuwa karibu na wakulima. Badala ya kusubiri ajira mpya, Menejimenti ilichukua hatua ya kuwahamishia watumishi wenye ujuzi wa kahawa kwenye Ofisi za Kanda ambazo zilikuwepo hapo awali badala ya kujazana Makao Makuu, Moshi.
(c) Walioadhibiwa utaratibu ulifuatwa na walikuwa na haki ya kupinga adhabu iwapo hawakuridhika nayo.
Tuhuma Na. 3: Ubia na Asasi isiyo ya Serikali (NGO) kuomba pesa za maendeleo ya kahawa na pesa kutolewa kwa NGO kwa manufaa binafsi.
Jibu: Hoja hii inahitaji ushahidi wa NGO iliyopata fedha kwa andiko la Bodi ya Kahawa na chanzo cha ufadhili huo, na ni kiasi gani. Makao Makuu ya Bodi hayana kumbukumbu ya NGO, hata moja, iliyopata fedha za namna hiyo.
Tuhuma Na. 4: Bodi ya Kahawa kuingizwa kwenye malumbano na viongozi wa mikoa ya Kigoma na Wilaya ya Tarime
Jibu: Uongozi wa Bodi ya Kahawa (Bodi ya Wakurugenzi au Menejimenti) haujawahi kukaa kikao na viongozi wa Mkoa wa Kigoma kujadili au kulumbana juu ya maagizo ya Bodi katika mkoa huo. Kama malumbano hayo yapo, mkoa huo haujayaleta Bodi ya Kahawa.
Kwa upande mwingine, Bodi ya Kahawa (Mwenyekiti na Mkurugenzi Mkuu) tumewahi kufanya mkutano na Mkuu wa Mkoa wa Mara pamoja na Wakuu wa Wilaya za Musoma, Serengeti, Rorya na Tarime. Katika kikao hicho cha tarehe 8/10/2010 tulitoa ufafanuzi juu ya kusimamishwa Makampuni binafsi ya ununuzi wa kahawa Wilayani Tarime ambayo yalikiuka kanuni kwa kuchanganya Arabika laini (Mild Arabica)na Arabika ngumu (Hard Arabica) kwenye soko. Kikao kiliisha vizuri na tarehe 9/10/2010 kwa pamoja tukafanya Mkutano wa Wadau wa Kanda ya Mara uliofanyika Mjini Tarime ukiwashirikisha pia viongozi wakuu wa Serikali wa Mikoa ya Mara na Mwanza. Katika kikao hicho Bodi ya Kahawa ilitoa ufafanuzi wa muafaka huo.
Tuhuma Na. 5: Kufuta leseni ya kununua kahawa mbivu ili kulinda Kilicafe
Jibu: Leseni ya kununua kahawa mbivu (cherry) haijafutwa na inaendelea kutolewa kwa waombaji wenye sifa zinazotakiwa.
Tuhuma Na. 6: Kamati ya Nidhamu
Jibu: Kadiri ya Kanuni za Utumishi za Bodi ya Kahawa, Mwenyekiti wa kikao cha Kamati ya Nidhamu ni Mkurugenzi Mkuu. Ushirikishwaji wa Chama cha Wafanyakazi unategemea ngazi ya mfanyakazi mtuhumiwa. Sheria inampatia mfanyakazi fursa ya kumchagua mfanyakazi mwenzie au mwakilishi wa Chama cha Wafanyakazi wakati wa kusikilizwa utetezi wa tuhuma zake. Haki za msingi za mfanyakazi asipozipata, upo utaratibu wa kanuni wa kuzidai kupitia chama cha wafanyakazi.
Tuhuma Na. 7: Kujilimbikizia mali
Jibu: (a) Mkurugenzi Mkuu aliingia Bodi ya Kahawa 2008 akitokea Technoserve, Arusha, ambako alikuwa akiishi kwenye nyumba yake binafsi. Alihamia Arusha kutokea Mbinga ambako tayari alikuwa na nyumba zake mbili binafsi, moja ikiwa ya biashara na moja ya kuishi. Alikuwa na kiwanja Mjini Songea ambacho kilijengwa banda lililoezekwa tu.
Aliingia Bodi ya Kahawa akiwa na magari mawili, Toyota Prado ya kutembelea na Toyota Hiace iliyokuwa inafanya biashara Mjini Dar es Salaam. Leo hii Mkurugenzi Mkuu ana magari binafsi mawili ya familia bila kufanya biashara, yaliyonunuliwa baada ya kuuza hayo yaliyotajwa hapo juu.
Ni vema utafiti au ushahidi ukalotewa juu ya malimbikizo ya utajiri unaodaiwa, upo katika mali gani au akaunti binafsi zilizopo Exim Bank na CRDB Bank.
(b) Posho za vikao na safari zina kanuni na bajeti zake. Kama kuna malipo yaliyofanyika kinyume na kanuni yatolewe ushahidi.
HITIMISHO
Ndugu A. Kumburu alipoteuliwa kuongoza Bodi hii aliikuta ikiwa na mapungufu kadhaa, ikiwa ni pamoja na malalamiko ya wafanyakazi dhidi ya mishahara midogo na maslahi duni n.k. Katika kipindi cha miaka miwili iliyopita hali hiyo imebadilika sana.
Ndugu Kumburu anajua kuitumia Bodi ya Wakurugenzi na ameitumia. Kwa sababu hii, mambo mengi aliyoyafanya ni baada ya kupata kibali cha Bodi ya Wakurugenzi.
Amefanya mengi na wafanyakazi wengi wanakiri kuwa ni mchapakazi na mtetezi wao. Hata Jumamosi na Jumapili (baada ya kutoka kanisani) hurudi ofisini kuchapa kazi.
Kwa upande mwingine, ni kweli kuwa kutokana na Ofisi Kuu ya TCB kuwa mbali na Dar es Salaam, safari za kwenda Dar es Salaam ni nyingi. Hana njia ya kuzikwepa.
Sisi kama Bodi ya Wakurugenzi hatujawahi kulalamikia utendajikazi wake na tunamshkuru sana kwa bidii yake ya kusimamia majukumu ya Bodi (TCB) kwa mujibu wa Sheria na Kanuni, kuwajali wafanyakazi na chama chao, kutetea wakulima wa Kahawa nchini ili waweze kupata bei nzuri, kurejesha taswira (image) ya TCB kwa Umma wa Tanzania na Kimataifa na kwa msimamo wake usioyumba katika masuala ya msingi katika utekelezaji wa sheria ya Kahawa, Na. 23 ya 2001 na Kanuni zake za 2003, Taratibu za Serikali na Maagizo ya Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika.
Kwa upande mwingine, sitarajii kati ya wafanyakazi 58 wa Bodi wote (100%) wafurahie kazi yake! Haitawezekana hata siku moja!!.
Kutokana na uamuzi wa Kamati ya Uongozi ya TPAWU kukana kuhusika na kuandika tuhuma hizo na kutokubaliana na yaliyomo, na kutokana na maelezo yangu kuhusu tuhuma hizo, ni dhahiri kuwa tuhuma hizo si za kweli na ni za mtu binafsi mwenye sababu zake binafsi.
Pius B. Ngeze
MWENYEKITI WA BODI,
BODI YA KAHAWA TANZANIA
Baruapepe: ngezep@yahoo.co.uk
tepultd@yahoo.com
simu: 0784 690277
0768 023019