Kuelekea sikukuu; Je ni Mgeni uliyewasili au uliyefika? Nimeumia Sana

Robert Heriel Mtibeli

JF-Expert Member
Mar 24, 2018
21,339
51,864
KUELEKEA SIKUKUU; JE MGENI UMEWASILI AU UMEFIKA. NIMEUMIA SANA.

Na, Robert Heriel.

Leo nataka kujua maana ya maneno haya; "Kuwasili, kufika, kuketi na Kukaa" maana huku nimekerwaaa Sana.

Sikukuu huku imeshaanza, mamia Kwa maelfu yameenda nyumbani Kula sikukuu. Nami ni mmoja wa watu nilirudi nyumbani kusherekea sikukuu na ndugu, jamaa na marafiki. Mambo ni Moto huku.

Jana kulikuwa na Kasherehe mshenzi Kama unavyojua huku Moshi, msimu huu kuna vitafrija vya hapa na pale vya watoto kubarikiwa n.k.

Kwa jinsi Ukumbi ulivyokuwa umeandaliwa na muziki mzuri uliokuwa ukipigwa kila mmoja wetu alijazwa na furaha.

Sasa tatizo likajitokeza kwenye utambulisho; roho yangu iliingiwa na simanzi Kama jinamizi. Kihoro kilinikaba Kama kamba shingoni.

Yule MC sikumuelewa alipokuwa akikaribisha na kutambulisha watu. Naomba ninukuu;

" Aaanh! Naona wageni kutoka Mbauda, Arumeru, ndio wamefika, makofi kwao jamani" MC anasema watu tunapiga makofi. Kisha anaendelea.

"Anyway! Nawaona wageni kutoka Uyole, Mbalizi, Kabwe, na Tukuyu wakiwa wamekaa nyuma kabisa" MC akasema kisha wageni wanasimama na kupunga Mkono kisha wanaamrishwa Kwa ukali waketi kwani muda mi mchache.

" Aaanh! Waliowasili ni wageni kutoka Dar es salaam. Wazee wa mujini, njia panda ya Ulaya, watu wa laki sio pesa. Jamani wamependeza hawajapendeza?( Watu tunaitikia Kwa nguvu wamependeza) haya tunaomba Siti hizo za mbele waketi, ninyi ambao hamtoki Dar kakaeni Viti vile Kule" MC akasema Kwa uchangamfu mkubwa Sana nadhani mnaelewa nikisema uchangamfu mkubwa.

" Tulieni tafadhali! Anayewasili ni mkurugenzi wa wizara nyeti hapa nchini, makofi kwake, DJ weka muziki Mkurugenzi ajisikie'" Muziki unapigwa wa heshima, namuona Mkurugenzi alipunga Mkono USO wake akiwa kaufungua vyema Kabisa.

" Tunashukuru Sana mkurugenzi, tukipata nafasi tutakupa Kipaza sauti useme neno. Haya wamefika wageni kutoka Makanya, Hedaru, Gonja, mombo na Handeni. Karibuni Sana. Mkae siti zile. Haya FANYENI haraka hatuna muda wa kutosha" Sisi wageni kutoka Makanya tunaharakisha Kama tilivyoamriwa na MC karibu tukanyagane.
Yaani hapakuwa na shangwe yoyote, wala hatukupewa heshima yoyote


" Anayewasili ni mke WA Waziri akiongozana na Mke wa Katibu, mke wa Mkurugenzi wa usalama wa taifa, mke wa Naibu waziri na wake wa wabunge. Jamani tuwashangilie Kwa nguvu na vigelele, wamependeza jamani, Wapi DJ" muziki mzuri unaachiwa wanaingia Kwa kucheza Kwa kufuata mdundo wa muziki. Ukumbi unalipuka Kwa shangwe, Sisi tuliotoka Uyole, mbalizi, Misungwi, na katoro tunabaki tumeachama mdomo isijulikane tunacheka au tunalia.

" Wanaofika sasa ni Wakulima wa Mbaazi, mahindi na mpunga kutokea Kilosa, itakata na turiani, nyuma Yao wafuatiwe na wakulima wa Mawese kutoka kasulu, Wakulima wa Karanga na warina Asali wa Nzega. Haya changamkeni muingie mkakae kwenye nafasi zenu" Masikini ya Mungu nawaona Wakulima wakiiingia Ukumbi hata hauna habari nao. Wala hakupigiwa muziki. Zaidi ya kuharakishwa kwani muda mi mchache.

"Warembo wanaowasili ni wasomi kutoka Udsm hao, piga kelele, wameongozana na warembo kutoka Muhimbili, SUA na Mzumbe. Hawa ndio vichwa tunavyovitegemea kwenye nchi hii. DJ mbona sikuoni" Muziki mkubwa unaachiwa, nawaona warembo hao wakicheza Kwa madoido na viatu vyao virefu vilivyowafanya watembee Kwa maringo. Ukumbi wote ulihamanika na kuburudika.

" Waliofika sasa hivi ni ndugu zetu wanaosomea vyuo vyetu hivi, siwezi vitaja vyote Ila mnavijua. Haya harakisheni mkakae tuendelee na Ratiba yetu" Masikini nikawaona wasomi hao kutoka vyuo ambavyo MC hajavitaja wakitembea Kama walikata tamaa. Watu ambao hawajaheshimiwa. Nikajisikia Vibaya.

" Nafahamu Bodaboda, Mamantilie, wauza mitumba, madalali, wachimba makaburi, nmefika. Ingieni haraka mkakae Kule nyuma" MC anasema alafu waliotajwa nawaona wakiingia nyuso zikiwa zimekata Kauli. Loooh?

" Gari iliyowasili ambayo ni V8 na BMW X6 ni zamaboss wetu, wakubwa wetu, Kaka zetu, Kwa kweli wakishuka kila mmoja wetu asimame na kushangilia. DJ utatupa Raha" kweli wanashuka wanaume wanne katika Yale magari ya kifahari wakiwa wametanua mikono Yao Kama ishara ya kujiamini,matumbo Yao makubwa kiasi yaliyoshibishwa vyema yakiwatangulia. Ukumbi unalipuka Kwa shangwe na muziki mzuri unawapokea. Wanaume Wale wanaenda Kwa DJ wanaanza kumtupia pesa, kisha MC anamwaga sifa ili kuwavutia kwake, MC anafanikiwa kuwavuta watu Wale, wanamfuta na kuanza kumpiga na notinoti usoni mwake. Loooh!

Wanaombwa waketi katika viti maalumu. Wanaketi.


Shida yangu ni Kwa nini Sisi makabwela tulitambulishwa na kukaribishwa Kwa namna Ile.

Ati watu wafupi tulifika alafu warefu waliwasili.
Warembo na wenye maumbo matata waliwasili na Wale vimbaumbau na wasiowarembo walifika wakakalishwa badala ya kuketishwa.

Tusio na nyumba wala magari tulifika wakati wenye navyo wakiwa wamewasili.

Baadaye sherehe ilipoisha nilimfuata MC aniambie maana ya mambo yote Yale.

MC akanijibu;
Mtu aliyefika ni Yule anayeenda sehemu ambayo hata asipoenda shughuli itafanikiwa. Mtu asiyeenda na zawadi, mtu ambaye hataifanikisha sherehe au shughuli hiyo.

Nikamuuliza, Kwa hiyo Sisi watu wa Makanya hatuna Mchango mwema kwenye shughuli. Akacheka kisha akanijibu Kwa matani yenye ukweli dhahiri; Aah! Nyie ni wafikaji tuu. Yaani haya msingekuja msingetupunguzia chochote.

Akasema, WALIOWASILI
Ni watu muhimu wanaofika kufanikisha sherehe au shughuli Fulani.
Kuifanikisha kiuchumi na kuburudani.
Wenye pesa, wenye vyeo vikubwa, wenye mishahara minono,
Wadada wazuri wenye maumbo ya kutamanisha hawa kazi Yao ni kuifanya shughuli iwe na mvuto hasa wakipita pita kwenda huku na Huku.

Wakaka mahandsome boy, kuifanya sherehe iwe na MVUTO.

Akaongeza kuwa, sherehe za mjini zile kubwa lazima kamati iwabalansi waliofika na waliowasili.
Kamati za shughuli zipo Radhi ziwakodishe warembo na pisi Kali zifike kwenye shughuli Yao ili tuu sherehe ifane.

Ninyi wenzangu na miye tutasameheana katika shughuli Kama hizi.

Niliona nimkimbie MC Kwa maneno yake maana alizidi kuniumiza. Hapa nilipo hata hiyo Christmas haiwezi nikutia hapa, narudi kwetu Makanya.

Ulikuwa nami Mfikaji;

Robert Heriel
Taikon wa Fasihi
Kwa sasa Kibosho Road, Moshi.
 
1640143144792.jpg
 
Yani uongo mwingine hauna akili kabisa.....


Hata katoto ka chekechea huwezi kukadanganya kirahisi hivi...
 
Yani uongo mwingine hauna akili kabisa.....


Hata katoto ka chekechea huwezi kukadanganya kirahisi hivi...
Mkuu wa kazi sijui hata kama ulilisoma andiko lote na kama ulilisoma lote, umezingatia context badala ya contents. Kama huwa unamsoma soma mwanafasihi huyu isingekupa tabu kuelewa anapeleka ujumbe gani kwa hadhira yake
 
Na mimi ndio nimefika kwenye uzi huu...ngoja niake huku nyuma nione kinachoendelea.
 
Umetuandikia insha ndefu yenye kuchosha ikiwa mantiki yake ni ndogo inaweza kuelezeka kwa maneno 10.
 
Nimechekaaa 🤣🤣🤣🤣
Haya mambo ni ukweli kabisa ukiwa huna pesa kwenye shughuli ya familia utaosha vyombo,watoto,kupika wale wenye pesa wanakaaa na kuchat tu
 
Back
Top Bottom