Kiwanda cha akina Kenyatta chakaidi amri ya serikali Tanzania

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,007
Date::12/20/2008
Kiwanda cha akina Kenyatta chakaidi amri ya serikali Tanzania
*Ni kiwanda cha maziwa ya Brookside Arusha

Exuper Kachenje na Musa Juma
Mwananchi

WAKATI kiwanda cha maziwa ya Brookside, kinachomilikiwa na familia ya Jomo Kenyatta mjini Arusha kimezuiwa na serikali ya Tanzania, chenyewe kimeendelea kufanya shughuli zake kinyemela bila kufuata utaratibu.

Kufuatia hali hiyo, Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Mary Nagu amesema kinachofanyika ni kinyume cha utaratibu na serikali haiwezi kuruhusu hali hiyo.

Hali hiyo imekuja siku chache baada ya serikali kukifungia kiwanda hicho kufanya kazi zake kutokana na kukiuka taratibu za uwekezaji za kukusanya maziwa nchini na ya kupeleka nchini Kenya kuyasindika na baadaye kuyarejesha nchini kutafuta soko.

Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Diodorus Kamala aliamrisha kiwanda hicho kufungwa baada ya kubani kuwa kimeshindwa kutumika kwa uzalishaji badala yake kikawa kinanunua maziwa ya kuyapeleka kwenye kiwanda chake kingine kiitwacho Ruiru nchini Kenya.

Kiwanda hicho kinadai kuwa kimeshindwa kuendelea kuzalisha maziwa kwa kutumia kiwanda walichonunua hapa nchini kutokana na gharama kubwa za uzalishaji, ikilinganishwa na Kenya.

Uchunguzi wa Mwananchi Jumapili, umebaini kuwa kiwanda hicho kimeanza tena kukusanya maziwa tangu wiki iliyopita kwa madai kuwa kimepewa kibali na serikali, ingawa Waziri Nagu amesema hajui lolote.

Akizungumza Mwananchi Jumapili, Meneja Mkuu wa Brookside, Emmanuel Kanagisa alisema kampuni yake hiyo ilipewa kibali cha miaka miwili kuyapeleka maziwa hayo Kenya kusindikwa na iliiomba serikali kufanya hivyo.

"Tulipewa kibali kwa mwaka 2006 hadi 2008 na serikali, kununua maziwa na kuyapeleka Kenya kwa usindikaji, kisha kuyarejesha Tanzania kwa mauzo. Lengo lilikuwa kuongeza soko la maziwa kwa wakulima na kuishauri serikali kuandaa taratibu za udhibiti na kuondoa hofu ya udanganyifu,"alisema Kanagisa.

Alieleza kuwa hatua hiyo ilitokana na maziwa yanayokusanywa eneo hilo kutofikia kiwango kinachohitajika ili kuwezesha kufungwa kwa mashine za usindikaji wa muda mrefu ambazo zinagharimu kati ya Sh2 bilioni hadi tatu.

Hata hivyo, alisema kuwa serikali ilisitisha utaratibu huo Novemba 14 mwaka huu kwa madai kuwa Brookside ilikiuka masharti ya leseni hali iliyowalazimu kuandika barua kwa Kamishna wa Ushuru wa Forodha kulalamika.

Katika barua hiyo yenye kumbukumbu namba BRK/TZ/CU/1/08 nakala yake ilimbazwa kwa viongozi mbalimbali serikalini akiwemo Waziri Mkuu Mizengo Pinda, Wizara ya Viwanda na Biashara pamoja na kwa Mwenyekiti wa Kampuni ya Brookside, Muhoho Kenyatta.

Hatua hiyo, iliyoeleza malalamiko yao, jinsi hatua hiyo ilivyowakosesha mapato wao na wananchi wafugaji na kuharibu zaidi ya lita 8,000 za maziwa, hatua ambayo iliwezesha kampuni hiyo kupewa kibali kuendelea na shughuli hizo kwa mwaka mmoja ujao.

Hata hivyo, akizungumza na Mwananchi Jumapili Waziri Nagu alisema kimsingi masharti ya uwekezaji hayaruhusu kiwanda kama Brookside kupeleka bidhaa ghafi nje ya nchi kusindikwa.

"Kimsingi masharti ya uwekezaji hayaruhusu kiwanda hicho kupeleka bidhaa ghafi nje ya nchi ikasindikwe, lengo la kukibinafsisha ni kukiwezesha kusindika maziwa hapa nchini na kufaidisha taifa na watu wake," alisema Nagu

Aliongeza kuwa kiwanda hicho kilibinafsishwa ili mwekezaji aweze kukusanya na kusindika maziwa hapo na kutoa mazao yake ili kuwafaidisha Watanzania tofauti na ilivyo sasa.

Hata hivyo, alisema analifuatilia suala kwa msajili wa makampuni kujua ukweli wa mambo na namna leseni hiyo iliyotolewa kuweza kutoa msimamo wake.

Katika hatua nyingine baadhi ya mawakala wanaiouzia maziwa kampuni hiyo wamelalamikia kutolipwa pesa zao na kampuni hiyo ya mjini Arusha.

Mawakala hao binafsi na ushirika wa wauza maziwa walisema wamekuwa wakiiuzia maziwa kampuni hiyo lakini hawajalipwa fedha zao tangu Novemba 19, hivyo kuwasababishia kuongezeka kwa ugumu wa maisha.

Akizungumzia suala hilo Meneja Mkuu wa Brookside, Emmanuel Kanagashi alisema kuwa kampuni yake ilikuwa na utaratibu wa kulipa mawakala wake kila baada ya siku 14 na kwamba iwapo kuna mawakala wanaodai watalipwa kwani fedha yao ipo.

"Sisi tuna utaratibu wa kuwalipa mawakala wetu kila baada ya siku 14. Kama wapo wanaodai, fedha yao ipo watalipwa bila shaka," alisema kanagashi na kuongeza kuwa kama lilitokea tatizo hilo huenda lilisababishwa na kusimamishwa kwa shughuli zao.
 
Hivi wanasheria wanaomaliza vyuo wanakwenda wapi? Maana naona kuna kesi nyingi sana za kujijasiriamalisha...moja wapo ni hii. Au wanasubiri wale wa serikali watoe tongotongo huko waliko? Tanzania tuamke tuchangamkie kazi, kesi nzuri ni za uchokonozi kama hizi...wauza maziwa wamelipwa? wafanyakazi wana bima ya afya? Ukiona kuko sawa unaangalia kama wanatunza mazingira n.k n.k
 
Back
Top Bottom