Red Giant
JF-Expert Member
- Mar 9, 2012
- 15,658
- 20,889
KISIWA CHENYE HAZINA
Mtunzi: Robert Louis Stevenson,1883.
Mtafsiri: F johnson na Edwin W Brenn, 1928.
Marekebisho: Pictuss, 2021.
Pictuspublishers@gmail.com
Kinapatikana ndani ya maktaba app by pictuss.
SURA YA KWANZA: MZEE KAPTENI
Kuna mabwana wameniomba niandike habari zote za kisiwa chenye hazina tokea mwanzo mpaka mwisho, nisifiche hata neno moja ila pale mahali palipo kisiwa chenyewe tu, kwa sababu hazina nyingine zipo mpaka leo na bado hazijafukuliwa. Basi katika mwaka huu wa kumi na saba, naanza kushika kalamu yangu na kujaribu kukumbuka zamani, wakati baba yangu alipokuwa na nyumba ya wageni. Siku moja mzee mmoja baharia alikuja kupanga kwetu. Mzee huyu alikua na kovu la pigo la upanga usoni, na hata sasa naweza kuukumbuka uso wake ulivyokuwa.
Nakumbuka sana, kwani naona kama ni jana tu, alipofika alikuwa na sanduku lake kubwa likimfuata nyuma katika gari. Alikuwa mrefu, mwenye nguvu, tena mnene, na rangi yake nyeusi kidogo; nguo zake zilikua kuukuu zilizochafukachafuka. Kucha zake zilikua zimepasukapasuka, na hilo kovu alilokuwa nalo usoni lilikua liking’aa kuliko uso wake. Tena nakumbuka sana jinsi alivyokua akitazama huku na huku alipokua akiimba wimbo mmoja ambao alipenda kuuimba mara kwa mara katika siku za baadaye:
‘Watu kumi na tano Yoh-ho-ho-ho.
Juu ya sanduku la mfu Yoh-ho-ho-ho.
Na chupa ya mvinyo Yoh-ho-ho-ho.'
Basi akaja akabisha mlangoni kwa fimbo yake, na baba yangu alipofungua mlango, akaagiza kikombe cha mvinyo, akainywa kwa kusukutua kinywa kwanza apate kuona utamu wake vizuri, kisha akasema, “Mahali hapa ni pazuri na nyumba nayo ni nzuri. Je, Rafiki, watu wengi huja hapa kupanga?”
Baba yangu akajibu, “Watu wanaokuja si wengi.”
Basi yule mzee baharia akasema “Vema basi,mahali hapa patanifaa sana.” Akamwita yule mwenye gari akamwambia alete sanduku lake, tena amsaidie kulichukua na kuliweka nyumbani. Halafu akasema, “Mimi sina makuu, kama nikipata chakula changu na mvinyo na mahali pa kutazama meli zinazopita, basi sina haja ya kitu tena.
Na mimi ninaitwa ‘Kapteni’.”Basi akampa yule mwenye gari ujira wake.
Yule mwenye gari alituambia kuwa yule mzee baharia alifika kwenye gari lililofika mjini asubuhi, akauliza habari ya nyumba za wageni, ndipo akaambiwa kuwa nyumba yetu ndiyo bora, basi akamwambia amletee sanduku lake katika gari. Basi hatukuweza kupata habari Zaidi ila hii tu.
Yule mzee Baharia yaani Kapteni alikua mtu mkimya kabisa, na mchana kutwa alishinda pwani akitazama baharini huku na huku kwa darubini yake, na kila jioni alikaa katika chumba cha kunywea mvinyo. Mara nyingi alikua akiulizwa neno alikuwa hajibu na baada ya siku chache tulimzoea na kufahamu alikua hataki kujishughulisha na watu, ndipo tukamuacha kukaa kimya. Kila jioni aliporudi kutoka kutembea aliuliza mabaharia wengine wamepita na kwanza tulifikiri ya kuwa anamtaraji rafiki mwenziwe baharia, lakini badaye tulifahamu ya kuwa alitaka kuepukana nao. Mabaharia wengine walipokuja kupanga pale nyumbani kama walivyokua wakifanya mara kwa mara, yeye huja kuchungulia dirishani kwanza ili apate kuwaona kabla hajaingia humo ndani. Tena katika siku wanazokuwapo mabaharia wengine yeye huwa kimya kupita desturi ya siku zote. Mimi nilijua habari zote, kwa sababu siku moja aliniita faraghani na kuniahidi kunipa fedha kila mwezi kuwa ujira wangu ili siku zote niwe nikiangalia sana na kumwambia mara tu nikimwona baharia mwenye mguu mmoja.
Pengine mwisho wa mwezi nilipokuwa nikienda kudai ujira wangu, alikua akinitazama tu lakini kabla ya kupita juma nzima alikua akiniita na kunipa, akaniambia nizidi kupeleleza
Kwa kufikiri kwangu mara nyingi nilikuwa nikiota ndoto; hata siku moja nikaota kumwona baharia mwenye mguu mmoja tu, niliota mguu wake mmoja umekatikia penye goti, au penye paja. Kwa kweli ndoto hizo zilinitisha mno nikaona kuwa nastahili kupewa fedha zile. Na ingawa niliogopa kuja kumwona baharia mwenye mguu mmoja, yule mzee Baharia, Kapteni nilimwogopa zaidi ya watu wote wengine. Pengine ni sababu alikunywa mvinyo kupita kiasi, na hivyo ndipo tulipopata kumsikia akiimba wimbo wake kwa sauti kubwa: ‘na chupa ya mvinyo, yo-ho-ho-ho.’ Na alipokuwa amelewa alikuwa anakuwa mtu wa kutisha kweli kweli tena hushurutisha kila mtu kuimba pamoja naye, wala hakumruhusu hata mtu mmoja atoke nje ya nyumba mpaka aishe kulewa na kushikwa na usingizi.
Hasa yaliyowatisha watu yalikuwa ni hadithi alizozisimulia, hadithi za kutisha zilizohusu kunyonga watu, kuwatosa baharini, na matendo maovu mengine katika nchi za mbali. Kwa kujigamba kwake mwenyewe alisema kwamba alikua akiishi miongoni mwa watu walio waovu kabisa kuliko wote waliojaliwa na Mungu kusafiri baharini; na maneno aliyoyatumia yalishtusha watu kwa namna yalivyokuwa ya matusi. Mara nyingi baba yangu alikua akisema kwamba sifa ya nyumba yake itaharibika kabisa, na watu wengi watakataa kuja kupanga kwake tena kwa sababu ya tabia ya mtu huyo.
Mara moja tu ndipo nilipomwona kukasirika kabisa. Ilikua siku moja bwana daktari kaja kumtazama baba yangu ambae alikuwa mgonjwa, naye huyu kapteni alilewa sana siku hiyo akaanza kuimba kwa sauti kuu:
‘Watu kumi na tano Yoh-ho-ho-ho.
Juu ya sanduku la mfu Yoh-ho-ho-ho.
Na chupa ya mvinyo Yoh-ho-ho-ho.’
Mara ya kwanza niliposikia maneno yake, ‘Sanduku la mfu’ nilifikiri kama ni sanduku lile kubwa alilokuja nalo, na mara nyingi niliota katika ndoto zile za baharia mwenye mguu mmoja. Bwana daktari ndiyo kwanza asikie wimbo ule, nae akawa hataki kelele. Alafu yule kapteni akapiga meza kwa kishindo kikubwa, na sisi tuliokuwa tumemzoea, tukajua kuwa hii ndiyo ishara ya mzee kapteni kushurutisha watu wanyamaze, ila Bwana Daktari hakuwa na habari akaendelea katika maongezi yake. Mara kapteni akageuka kumtazama na kupiga meza mara ya pili na kumtukana, akimwamuru anyamaze.
Bwana Daktari akageuka kumuuliza, "Je,wasema na mimi?” Na alipomwambia ndiyo, akasema, "Basi mimi ninayo maneno machache nitakayokwambia. Ndiyo haya: Kama wewe utaendelea kunywa namna unavokunywa sasa, dunia itafarakana na mtu mwovu na mchafu.”
Lo! Hasira zilioje! Mzee kapteni aliruka gafla na kuvuta kisu chake kutaka kumpiga Bwana Daktari. Lakini yeye hakustuka hata kidogo ila alimwambia kwa upole, "kama usipoweka mara moja hicho kisu chako katika ala yake, nakwambia kuwa utahukumiwa na kunyongwa bila shaka.”
Basi baada ya kutazamana kidogo Mzee Kapteni akaweka kisu chake katika ala na akakaa na kununa kama mbwa aliyepigwa. Bwana Daktari akaendelea kusema, “Na sasa, maadam najua kuwa wewe wakaa mtaa huu, lazima nikuangalie sana. Mimi ni kadhi wa serikali, na nikipata habari ya matata yako kidogo tu, basi nitafanya niwezavyo upate kufukuzwa katika nchi hii." Basi Akaondoka akaenda zake. Na Mzee Kapteni akakaa kimya kabisa kwa mda wa siku nyingi.
SURA YA PILI: KUTOKEA NA KUTOWEKA KWA MBWA MWEUSI
Baada ya siku chache, nakumbuka kuwa siku moja baba yangu alikuwa hajiwezi sana hata ikamlazimu mama yangu kukaa pamoja naye kumuangalia, mimi nilikuwa nikitandika meza tayari kumwandalia Mzee Kapteni, maana yeye kama ilivyokuwa desturi yake alikwenda pwani kutembea basi mara mlango ukafunguliwa na mtu akaingia ndani; mtu huyo alikua mrefu na mkono wake mmoja ulikatika vidole viwili, tena ijapokuwa alikua na upanga kiunoni, nafikiri hakuwa shujaa.
Nikamuuliza haja yake, nae akaniambia nimletee kikombe cha mvinyo; basi nilipokuwa nikienda, akaniita, "Njoo, njoo hapa karibu.” Hata nilipomkaribia akaniuliza, “Je, unamtandikia meza rafiki yangu?” Nikajibu, “Simjui rafiki yako.” Akasema, “Vema, lakini jina la rafiki yangu ni Kapteni. Ana kovu la pigo la upanga usoni. Basi sasa niambie kama rafiki yangu yumo humu.”
Nikamwambia, “Rafiki yako amekwenda kutembea pwani.”
Basi akakaa mlangoni kumngojea, na kuitazama njia niliyomwonesha. Mara kitambo kidogo tukamwona Mzee Kapteni anakuja. Yule mgeni akasema, “Haya sasa na tuingie ndani tujifiche nyuma ya mlango, ili Mzee akifika tupate kumshtusha.”
Tukaingia ndani tukajificha nyuma ya mlango, lakini nilijua kuwa huyu mgeni ni mwoga sana. Kwani upanga wake katika ala ulilegea, na mara kwa mara alikua akimeza mate kwa hofu aliyokuwa nayo.
Basi Mzee Kapiteni akaja akafungua mlango kwa kishindo akaingia ndani, wala hakugeuka kutazama mkono wa kulia au kushoto, ila akaendelea tu mpaka mezani nilipoweka chakula chake. Mara yule mgeni akamwita akasema “Mzee” na Mzee Kapteni akageuka kwa upesi kabisa, hata uso ukampauka kwa kugutuka, akawa kama mtu alieona zimwi. Yule mgeni akasema, “Je! Mzee umenisahau? Humkumbuki rafiki wa zamani?”
Mzee Kapteni akashikwa na bumbuwazi kama mwenye kigugumizi. Kisha naye akamwita, “Mbwa mweusi!” Yule mgeni akajibu, “Mimi ndiye mbwa mweusi nimekuja kukutazama rafiki yangu wa zamani. Ah Mzee! Ama mimi na wewe tumeona mambo mengi tangu vidole vyangu vilipokatika.”
Mzee Kapteni akajibu, “Kweli! Na sasa umeniona ndiyo wataka nini? Sema, wataka nini?”
Basi wakaniamuru niwaletee mvinyo, kisha wakaniambia nitoke chumbani niwaache peke yao wasemezane wala mimi nisiwepo karibu kusikiliza. Basi nikawaacha. Na kwa muda sikusikia sauti ila ngurumo tu, lakini mara nikasikia sauti ikisema, “Hapana! Hapana! Hapana kabisa! Kama ni kunyongwa vema tunyongwe sote pamoja.”
Mara tena nikasikia kelele za ghasia nyingi na matusi na vishindo vya meza na viti kutupwatupwa, na milio ya panga zikipambana. Punde nikasikia kama mtu alieumizwa sana akiugua na nikamuona yule mgeni aliyeitwa mbwa mweusi akitoka mbio na huku akifukuzwa na yule Mzee Kapteni, na damu ikimtoka yule mgeni kama maji. Mara nikamwona mzee akimtupia tena upanga kwa nguvu zake na kama ungalimpata ungalimpasua pande mbili, lakini kwa bahati haukumpata, akazidi kukimbia, ijapokuwa alikwisha umizwa sana. Mzee Kapteni akasimama kiasi kidogo kama mtu mwenye wazimu kwa hamaki, alafu akaingia ndani ya nyumba, na mara akapepesuka kutaka kuanguka. Nikamuuliza kama umeumizwa, nikatoka kwenda kumletea mvinyo ili apate kujiburudisha, lakini mara nilipotoka chumbani nikasikia mkoromo mkubwa mno, nikarudi mbio, nikamkuta amelala chini. Basi na mama yangu akawa amesikia zile kelele akatoka na kunituma kumwita Bwana Daktari.
Alipokuja Bwana Daktari tukamuuliza ameumia wapi. Bwana Daktari akajibu, “Kuumia! Hakuumia hata kidogo! Mtu huyu ameshikwa na kiharusi kama nilivyomwonya juzi.” Basi akatwaa bakuli na kisu chake kumtoa damu, na baadaye kidogo Mzee akainuka tena, na mara alipomwona Bwana Daktari akakunja uso, lakini aliponiona mimi akawa hana neno. Badaye akauliza, “Je, Mbwa mweusi yupo wapi?”
Bwana Daktari alikuwa hana habari ya mambo yaliyopita, akajibu, “Hayupo mbwa mweusi hapa ila yule wa Maungoni mwako tu. Wewe umezidi kunywa mvinyo hata umepatwa na kiharusi kama nilivyokuonya juzi, nami nimekuponya, nusura ufe.”
Basi tukamsaidia kumwinua, tukamweka kitandani na Bwana Daktari akamwambia,
“Sasa tulia usilewe, kama ukinywa hata tone moja la mvinyo fahamu ndiyo mauti yako.” Basi tukatoka chumbani na Bwana Daktari akaniambia kuwa sasa yu salama, lakini kama akishikwa na kiharusi tena atakufa.
Mtunzi: Robert Louis Stevenson,1883.
Mtafsiri: F johnson na Edwin W Brenn, 1928.
Marekebisho: Pictuss, 2021.
Pictuspublishers@gmail.com
Kinapatikana ndani ya maktaba app by pictuss.
SURA YA KWANZA: MZEE KAPTENI
Kuna mabwana wameniomba niandike habari zote za kisiwa chenye hazina tokea mwanzo mpaka mwisho, nisifiche hata neno moja ila pale mahali palipo kisiwa chenyewe tu, kwa sababu hazina nyingine zipo mpaka leo na bado hazijafukuliwa. Basi katika mwaka huu wa kumi na saba, naanza kushika kalamu yangu na kujaribu kukumbuka zamani, wakati baba yangu alipokuwa na nyumba ya wageni. Siku moja mzee mmoja baharia alikuja kupanga kwetu. Mzee huyu alikua na kovu la pigo la upanga usoni, na hata sasa naweza kuukumbuka uso wake ulivyokuwa.
Nakumbuka sana, kwani naona kama ni jana tu, alipofika alikuwa na sanduku lake kubwa likimfuata nyuma katika gari. Alikuwa mrefu, mwenye nguvu, tena mnene, na rangi yake nyeusi kidogo; nguo zake zilikua kuukuu zilizochafukachafuka. Kucha zake zilikua zimepasukapasuka, na hilo kovu alilokuwa nalo usoni lilikua liking’aa kuliko uso wake. Tena nakumbuka sana jinsi alivyokua akitazama huku na huku alipokua akiimba wimbo mmoja ambao alipenda kuuimba mara kwa mara katika siku za baadaye:
‘Watu kumi na tano Yoh-ho-ho-ho.
Juu ya sanduku la mfu Yoh-ho-ho-ho.
Na chupa ya mvinyo Yoh-ho-ho-ho.'
Basi akaja akabisha mlangoni kwa fimbo yake, na baba yangu alipofungua mlango, akaagiza kikombe cha mvinyo, akainywa kwa kusukutua kinywa kwanza apate kuona utamu wake vizuri, kisha akasema, “Mahali hapa ni pazuri na nyumba nayo ni nzuri. Je, Rafiki, watu wengi huja hapa kupanga?”
Baba yangu akajibu, “Watu wanaokuja si wengi.”
Basi yule mzee baharia akasema “Vema basi,mahali hapa patanifaa sana.” Akamwita yule mwenye gari akamwambia alete sanduku lake, tena amsaidie kulichukua na kuliweka nyumbani. Halafu akasema, “Mimi sina makuu, kama nikipata chakula changu na mvinyo na mahali pa kutazama meli zinazopita, basi sina haja ya kitu tena.
Na mimi ninaitwa ‘Kapteni’.”Basi akampa yule mwenye gari ujira wake.
Yule mwenye gari alituambia kuwa yule mzee baharia alifika kwenye gari lililofika mjini asubuhi, akauliza habari ya nyumba za wageni, ndipo akaambiwa kuwa nyumba yetu ndiyo bora, basi akamwambia amletee sanduku lake katika gari. Basi hatukuweza kupata habari Zaidi ila hii tu.
Yule mzee Baharia yaani Kapteni alikua mtu mkimya kabisa, na mchana kutwa alishinda pwani akitazama baharini huku na huku kwa darubini yake, na kila jioni alikaa katika chumba cha kunywea mvinyo. Mara nyingi alikua akiulizwa neno alikuwa hajibu na baada ya siku chache tulimzoea na kufahamu alikua hataki kujishughulisha na watu, ndipo tukamuacha kukaa kimya. Kila jioni aliporudi kutoka kutembea aliuliza mabaharia wengine wamepita na kwanza tulifikiri ya kuwa anamtaraji rafiki mwenziwe baharia, lakini badaye tulifahamu ya kuwa alitaka kuepukana nao. Mabaharia wengine walipokuja kupanga pale nyumbani kama walivyokua wakifanya mara kwa mara, yeye huja kuchungulia dirishani kwanza ili apate kuwaona kabla hajaingia humo ndani. Tena katika siku wanazokuwapo mabaharia wengine yeye huwa kimya kupita desturi ya siku zote. Mimi nilijua habari zote, kwa sababu siku moja aliniita faraghani na kuniahidi kunipa fedha kila mwezi kuwa ujira wangu ili siku zote niwe nikiangalia sana na kumwambia mara tu nikimwona baharia mwenye mguu mmoja.
Pengine mwisho wa mwezi nilipokuwa nikienda kudai ujira wangu, alikua akinitazama tu lakini kabla ya kupita juma nzima alikua akiniita na kunipa, akaniambia nizidi kupeleleza
Kwa kufikiri kwangu mara nyingi nilikuwa nikiota ndoto; hata siku moja nikaota kumwona baharia mwenye mguu mmoja tu, niliota mguu wake mmoja umekatikia penye goti, au penye paja. Kwa kweli ndoto hizo zilinitisha mno nikaona kuwa nastahili kupewa fedha zile. Na ingawa niliogopa kuja kumwona baharia mwenye mguu mmoja, yule mzee Baharia, Kapteni nilimwogopa zaidi ya watu wote wengine. Pengine ni sababu alikunywa mvinyo kupita kiasi, na hivyo ndipo tulipopata kumsikia akiimba wimbo wake kwa sauti kubwa: ‘na chupa ya mvinyo, yo-ho-ho-ho.’ Na alipokuwa amelewa alikuwa anakuwa mtu wa kutisha kweli kweli tena hushurutisha kila mtu kuimba pamoja naye, wala hakumruhusu hata mtu mmoja atoke nje ya nyumba mpaka aishe kulewa na kushikwa na usingizi.
Hasa yaliyowatisha watu yalikuwa ni hadithi alizozisimulia, hadithi za kutisha zilizohusu kunyonga watu, kuwatosa baharini, na matendo maovu mengine katika nchi za mbali. Kwa kujigamba kwake mwenyewe alisema kwamba alikua akiishi miongoni mwa watu walio waovu kabisa kuliko wote waliojaliwa na Mungu kusafiri baharini; na maneno aliyoyatumia yalishtusha watu kwa namna yalivyokuwa ya matusi. Mara nyingi baba yangu alikua akisema kwamba sifa ya nyumba yake itaharibika kabisa, na watu wengi watakataa kuja kupanga kwake tena kwa sababu ya tabia ya mtu huyo.
Mara moja tu ndipo nilipomwona kukasirika kabisa. Ilikua siku moja bwana daktari kaja kumtazama baba yangu ambae alikuwa mgonjwa, naye huyu kapteni alilewa sana siku hiyo akaanza kuimba kwa sauti kuu:
‘Watu kumi na tano Yoh-ho-ho-ho.
Juu ya sanduku la mfu Yoh-ho-ho-ho.
Na chupa ya mvinyo Yoh-ho-ho-ho.’
Mara ya kwanza niliposikia maneno yake, ‘Sanduku la mfu’ nilifikiri kama ni sanduku lile kubwa alilokuja nalo, na mara nyingi niliota katika ndoto zile za baharia mwenye mguu mmoja. Bwana daktari ndiyo kwanza asikie wimbo ule, nae akawa hataki kelele. Alafu yule kapteni akapiga meza kwa kishindo kikubwa, na sisi tuliokuwa tumemzoea, tukajua kuwa hii ndiyo ishara ya mzee kapteni kushurutisha watu wanyamaze, ila Bwana Daktari hakuwa na habari akaendelea katika maongezi yake. Mara kapteni akageuka kumtazama na kupiga meza mara ya pili na kumtukana, akimwamuru anyamaze.
Bwana Daktari akageuka kumuuliza, "Je,wasema na mimi?” Na alipomwambia ndiyo, akasema, "Basi mimi ninayo maneno machache nitakayokwambia. Ndiyo haya: Kama wewe utaendelea kunywa namna unavokunywa sasa, dunia itafarakana na mtu mwovu na mchafu.”
Lo! Hasira zilioje! Mzee kapteni aliruka gafla na kuvuta kisu chake kutaka kumpiga Bwana Daktari. Lakini yeye hakustuka hata kidogo ila alimwambia kwa upole, "kama usipoweka mara moja hicho kisu chako katika ala yake, nakwambia kuwa utahukumiwa na kunyongwa bila shaka.”
Basi baada ya kutazamana kidogo Mzee Kapteni akaweka kisu chake katika ala na akakaa na kununa kama mbwa aliyepigwa. Bwana Daktari akaendelea kusema, “Na sasa, maadam najua kuwa wewe wakaa mtaa huu, lazima nikuangalie sana. Mimi ni kadhi wa serikali, na nikipata habari ya matata yako kidogo tu, basi nitafanya niwezavyo upate kufukuzwa katika nchi hii." Basi Akaondoka akaenda zake. Na Mzee Kapteni akakaa kimya kabisa kwa mda wa siku nyingi.
SURA YA PILI: KUTOKEA NA KUTOWEKA KWA MBWA MWEUSI
Baada ya siku chache, nakumbuka kuwa siku moja baba yangu alikuwa hajiwezi sana hata ikamlazimu mama yangu kukaa pamoja naye kumuangalia, mimi nilikuwa nikitandika meza tayari kumwandalia Mzee Kapteni, maana yeye kama ilivyokuwa desturi yake alikwenda pwani kutembea basi mara mlango ukafunguliwa na mtu akaingia ndani; mtu huyo alikua mrefu na mkono wake mmoja ulikatika vidole viwili, tena ijapokuwa alikua na upanga kiunoni, nafikiri hakuwa shujaa.
Nikamuuliza haja yake, nae akaniambia nimletee kikombe cha mvinyo; basi nilipokuwa nikienda, akaniita, "Njoo, njoo hapa karibu.” Hata nilipomkaribia akaniuliza, “Je, unamtandikia meza rafiki yangu?” Nikajibu, “Simjui rafiki yako.” Akasema, “Vema, lakini jina la rafiki yangu ni Kapteni. Ana kovu la pigo la upanga usoni. Basi sasa niambie kama rafiki yangu yumo humu.”
Nikamwambia, “Rafiki yako amekwenda kutembea pwani.”
Basi akakaa mlangoni kumngojea, na kuitazama njia niliyomwonesha. Mara kitambo kidogo tukamwona Mzee Kapteni anakuja. Yule mgeni akasema, “Haya sasa na tuingie ndani tujifiche nyuma ya mlango, ili Mzee akifika tupate kumshtusha.”
Tukaingia ndani tukajificha nyuma ya mlango, lakini nilijua kuwa huyu mgeni ni mwoga sana. Kwani upanga wake katika ala ulilegea, na mara kwa mara alikua akimeza mate kwa hofu aliyokuwa nayo.
Basi Mzee Kapiteni akaja akafungua mlango kwa kishindo akaingia ndani, wala hakugeuka kutazama mkono wa kulia au kushoto, ila akaendelea tu mpaka mezani nilipoweka chakula chake. Mara yule mgeni akamwita akasema “Mzee” na Mzee Kapteni akageuka kwa upesi kabisa, hata uso ukampauka kwa kugutuka, akawa kama mtu alieona zimwi. Yule mgeni akasema, “Je! Mzee umenisahau? Humkumbuki rafiki wa zamani?”
Mzee Kapteni akashikwa na bumbuwazi kama mwenye kigugumizi. Kisha naye akamwita, “Mbwa mweusi!” Yule mgeni akajibu, “Mimi ndiye mbwa mweusi nimekuja kukutazama rafiki yangu wa zamani. Ah Mzee! Ama mimi na wewe tumeona mambo mengi tangu vidole vyangu vilipokatika.”
Mzee Kapteni akajibu, “Kweli! Na sasa umeniona ndiyo wataka nini? Sema, wataka nini?”
Basi wakaniamuru niwaletee mvinyo, kisha wakaniambia nitoke chumbani niwaache peke yao wasemezane wala mimi nisiwepo karibu kusikiliza. Basi nikawaacha. Na kwa muda sikusikia sauti ila ngurumo tu, lakini mara nikasikia sauti ikisema, “Hapana! Hapana! Hapana kabisa! Kama ni kunyongwa vema tunyongwe sote pamoja.”
Mara tena nikasikia kelele za ghasia nyingi na matusi na vishindo vya meza na viti kutupwatupwa, na milio ya panga zikipambana. Punde nikasikia kama mtu alieumizwa sana akiugua na nikamuona yule mgeni aliyeitwa mbwa mweusi akitoka mbio na huku akifukuzwa na yule Mzee Kapteni, na damu ikimtoka yule mgeni kama maji. Mara nikamwona mzee akimtupia tena upanga kwa nguvu zake na kama ungalimpata ungalimpasua pande mbili, lakini kwa bahati haukumpata, akazidi kukimbia, ijapokuwa alikwisha umizwa sana. Mzee Kapteni akasimama kiasi kidogo kama mtu mwenye wazimu kwa hamaki, alafu akaingia ndani ya nyumba, na mara akapepesuka kutaka kuanguka. Nikamuuliza kama umeumizwa, nikatoka kwenda kumletea mvinyo ili apate kujiburudisha, lakini mara nilipotoka chumbani nikasikia mkoromo mkubwa mno, nikarudi mbio, nikamkuta amelala chini. Basi na mama yangu akawa amesikia zile kelele akatoka na kunituma kumwita Bwana Daktari.
Alipokuja Bwana Daktari tukamuuliza ameumia wapi. Bwana Daktari akajibu, “Kuumia! Hakuumia hata kidogo! Mtu huyu ameshikwa na kiharusi kama nilivyomwonya juzi.” Basi akatwaa bakuli na kisu chake kumtoa damu, na baadaye kidogo Mzee akainuka tena, na mara alipomwona Bwana Daktari akakunja uso, lakini aliponiona mimi akawa hana neno. Badaye akauliza, “Je, Mbwa mweusi yupo wapi?”
Bwana Daktari alikuwa hana habari ya mambo yaliyopita, akajibu, “Hayupo mbwa mweusi hapa ila yule wa Maungoni mwako tu. Wewe umezidi kunywa mvinyo hata umepatwa na kiharusi kama nilivyokuonya juzi, nami nimekuponya, nusura ufe.”
Basi tukamsaidia kumwinua, tukamweka kitandani na Bwana Daktari akamwambia,
“Sasa tulia usilewe, kama ukinywa hata tone moja la mvinyo fahamu ndiyo mauti yako.” Basi tukatoka chumbani na Bwana Daktari akaniambia kuwa sasa yu salama, lakini kama akishikwa na kiharusi tena atakufa.