Kipeperushi changu cha dawa za kulevya kimfikie Rais Magufuli

Dr. Wansegamila

JF-Expert Member
Feb 3, 2012
2,845
7,794
KIPEPERUSHI CHANGU CHA DAWA ZA KULEVYA KIMFIKIE RAIS MAGUFULI

Rais wangu mpendwa, Dk John Magufuli. Nimevutwa kuzungumza nawe kuhusu dawa za kulevya, hii ni vita ambayo umeitolea mkazo kuwa kila anayehusika akamatwe, ikiwezekana hata mkeo, mama yetu mpendwa, Janet Magufuli.

Kweli kabisa hata mwandani wako akamatwe kama anahusika? Mama wa watoto wako unaowapenda? Hakika Rais wangu unachukia sana dawa za kulevya. Hii imekuwa alama yako kuwa wewe ni mtu wa maneno yako.

Kipeperushi changu hiki nakileta kwako kuonesha hisia zangu jinsi ninavyokuunga mkono. Nina sababu za kiwango cha mwisho kabisa cha namba za kukuunga mkono katika vita hii. Sababu zote nilizonazo zinatafsiriwa na maneno manne tu; nachukia dawa za kulevya.

Binafsi naamini taifa kwa jumla linaunga mkono vita hii. Hata wale ambao wanakosoa utaratibu unaotumika wa sasa ulioanzishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, nao wanaunga mkono.

Shida iliyopo ni kuwa njia zinazotumika hazioneshi matarajio ya kufanikiwa vita yenyewe. Watu wanakosoa kwa sababu wanatamani kuona Tanzania inapata ushindi wa vita hii ili kuokoa nguvu kazi ya vijana wetu.

Wanakosoa kwa sababu wanataka kuona hatua mahsusi zinachukuliwa. Hatua ambazo zinafanana na ukubwa wa tatizo. Hatua ambazo zinatambua kuwa vita hii ni kubwa na yenye kuhitaji mapambano ya sayansi ya kiwango cha juu.

JE, VITA HII TUNAIJUA?

Kwanza nikupongeze kwa msimamo wako kisha nikuombee kwa Mungu ufanikiwe. Ufuatiliaji wangu wa vita dhidi ya dawa za kulevya ndiyo hunifanya nisisimke kila kiongozi anapotangaza vita dhidi ya dawa za kulevya, maana ugumu na uzito wake naufahamu.

Je, Rais Magufuli vita hii inafahamika vizuri? Rais wangu mapambano dhidi ya dawa ya kulevya hayatakiwi kuendeshwa kwa miluzi mingi. Ni vita yenye kuhitaji utulivu. Ni vita inayohitaji kuwa na dira makini.

Mapambano dhidi ya dawa za kulevya ni vita inayohitaji ushindi bila kushangilia. Unajua kumkimbiza mwizi kimyakimya? Basi wauza unga ndiyo huhitaji kufuatiliwa kwa mwendo huo. Ukiwapigia kelele huwapati.

Rais wangu Magufuli, uliwahi kumsema mtu mmoja kuwa alikuwa akiibia Serikali Sh7 milioni kwa saa. Kwa taarifa tu hizo ni fedha ndogo kwa biashara ya unga, maana dawa za kulevya zina mitandao ya watu wenye kuingiza mabilioni ya shilingi kwa saa. Umoja wa Mataifa (UN) wanasema, mzunguko wa fedha za unga kwa mwaka ni zaidi ya Sh972 trilioni.

Dawa za kulevya zina watu wenye jeuri zao. Kuna watu wamekamatwa lakini wanaishi ndani ya jela kama wapo kweny nyumba na ofisi zao. Wapo jela lakini wanaendesha magenge ya unga. Wakiamua wanatoka kwenda kufanya harakati zao kisha wanarudi ndani.

Magenge ya dawa za kulevya yana watu wenye utiifu kwa mabosi wao kuliko askari wengi wa nchi. Hiyo ni sababu wimbi la askari kutumiwa na magenge ya wauza unga ni kubwa.

LABDA HATUIJUI VITA

Rais Magufuli, je, unafahamu kuwa sasa hivi magenge ya wauza unga hutengenezesha magari maalum ya kusafirishia unga? Unaweza kulisimamisha na kulikagua kila mahali na usione unga.

Mfano wewe unaona gari ni Toyota Rav4. Watu wanajua Rav4 zilivyo. Wewe unakagua ndani kisha huoni kitu. Wenye gari lao wakifika mahali panapohusika, bodi la nyuma linavutwa, Rav4 inakuwa na mwonekano wa Pickup. Katikati kunakuwa eneo lenye kubeba hata Kg 300 za cocaine.

Tukokotoe sasa. Gram moja ya cocaine katika soko la dunia kwa bei ya kutupa ni dola 200, yaani Sh447,000. Kwa msingi huo, kg moja ya cocaine ni dola 200,000, Sh447 milioni. Kg 300, maana yake ni Sh134 bilioni.

Rais wangu Magufuli, vita hii ya dawa za kulevya isiendeshwe kwa jazba, inataka akili, maarifa mengi na ujanja. Ukiwa na dhamira bila kuijua vita yenyewe kiundani, unaweza kila siku ukawa unapambana vita batili na watu batili, matokeo yake haitakwisha.

Mtu ambaye anatengeneza Sh134 bilioni kwa mkupuo mmoja, anapoingiza magari 10 hatari yake ni kiasi gani? Magari hayo hupita mipakani na mengine hupokelewa bandarini na kulipiwa kodi na ushuru. Wakaguzi hawawezi kujua magari yamebeba nini. Wakiangalia dani yapo tupu.

Magari mengine yanatengenezwa kwa aina yake. Yale maeneo yenye power windows na chini ya viti yanafunguliwa kwa batons (vitufe). Sehemu moja ya power window inaweza kuwekwa mpaka kg 20 za cocaine.

Askari akiangalia, akivuta power window hazifunguki na kila eneo lipo sahihi, ila wenye magari yao wanabonyeza vitufe panaachia kisha mzigo unatolewa.

Wauza unga wanamiliki viwanda bubu na vingine halali. Unakuta makontena ya kondomu yanasafirishwa kwa sababu za kibiashara au misaada. Kagua kondomu imefungwa vizuri kwenye pakti yake. Kumbe ndani kondomu zimejazwa heroin.

Unga unasafirishwa kwa vinywaji vya kopo. Utakuta kinywaji na utafungua unywe kuhakikisha. Kumbe lile kopo limegawanywa katikati, juu kinywaji, chini unga. Hiyo ni kazi ambayo inafanyika kiwandani. Wahandisi wenye utaalamu wa hali ya juu huifanya hiyo kazi.

Watu wabaya hutumia mpaka magari ya jeshi kwenye baadhi ya Serikali. Gari linakuwa na matenki hewa ya mafuta yenye kutumika kuhifadhi unga. Maboti, meli na kadhalika, pia hutengenezwa kwa muundo maalum wenye kuwezesha usafirishaji wa unga.

Brian O'Dea, raia wa Uingereza, alikuwa bilionea wa unga kabla hajaacha. Katika kitabu chake kinachoitwa ‘HIGH: Confessions of a Pot Smuggler’, kilichotoka Aprili 11, 2006, anaeleza kuwa alifanikiwa kuifanya biashara hiyo kwa mafanikio kwa sababu haikuwa rahisi kumkamata.

O’Dea ambaye aliwahi kufungwa Marekani miaka 10, anaandika kuwa wakati fulani baada ya kutoka jela hakuwa na fedha, hivyo alikwenda Colombia na kujitambulisha kwenye genge la Sinaloa, linaloongozwa na ‘mtu mbaya’, Joaquin Guzman ‘El Chapo’ kuwa naye ni memba ila alikuwa jela.

Huko alipewa gram 50 tu za cocaine ambazo alipita nazo sehemu zote za ukaguzi lakini wakaguzi hawakugundua alibeba unga kwa sababu walimuona ameshika pakti ya sigara. Naye kuwapoteza aliifungua kabisa na kutoa sigara moja na kuvuta.

Kwamba unaona pakti la sigara, unafungua unakuta sigara zenyewe lakini ndani watu wabaya wamefunga mzigo kati ya gram 50 mpaka 100. O’Dea anasema baada ya kuuza gram hizo 50 Marekani, aliendelea kuzungusha cocaine ambazo ndani ya miezi miwili zilimfanya atengeneze dola 1 milioni, Sh2.23 bilioni kwa sarafu ya sasa.

Rais wangu, mtu anatoka jela kisha anaanzia mtaji wa gram 50 halafu kwa haraka ndani ya miezi miwili anafikisha utajiri wa Sh2.23 bilioni, je, biashara hiyo nguvu yake ni kubwa kiasi gani?

Sasa basi, kwa haraka O’Dea ndani ya miaka michache aliweza kufikisha dola 200 milioni, Sh447 bilioni. Akaweka makazi yake Marekani, akanunua meli ya uvuvi ambayo aliitumia kusafiri na kuuza unga ndani ya bahari ya Pacific. Wakaguzi walipoiona walikagua na kukuta samaki, lakini ndani kulikuwa na cocaine.

Anasema samaki hao walipakiwa kwenye malori na kupita barabarani wakiwa wamewekewa barafu kama vile wanaenda kuuzwa, lakini walipofika sehemu husika walitoa unga ndani ya samaki kisha biashara kubwa ilifanyika.

O’Dea anasema pia kuwa nguvu yake iliingia mpaka ndani ya kikosi cha ujasusi cha kupambana na dawa za kulevya Marekani (DEA), akawa na watu wake ambao walimpa taarifa za ndani, vilevile aliwatumia kwa mipango yake mingi, ikiwemo kuwakamatisha wauza unga wenzake kisha yeye kuvuna faida kubwa.

NAKUSIHI RAIS MAGUFULI

Nakubali dhamira yako na nakuamini sana, lakini ni vizuri kufahamu kuwa biashara ya dawa za kulevya si vita ya kelele. Tunahitaji Serikali ioneshe dhamira kama sasa hivi, ila ni vizuri kusikiliza ushauri, maana ushindi wa vita hii utalifaa taifa lote kwa jumla.

Bajeti ya DEA ni dola 2 bilioni, Sh4.47 trilioni kwa mwaka. Bajeti ya jumla ambayo hupewa Ofis ya Taifa ya Udhibiti wa Dawa za Kulevya Marekani (ONDCP), ni dola 25 bilioni, Sh55.9 trilioni. Bajeti nzima ya vita ya dawa za kulevya kwa mwaka 2016 Marekani ilifikia dola 30 bilioni, Sh670 trilioni.

Intelijensia ya Marekani ni kali sana na uwekezaji wao kifedha ni mkubwa lakini hali inazidi kuwa mbaya mno. Vita ya dawa za kulevya ina msisimko mkubwa kishetani. Kadiri unavyoipiga vita ndivyo inavyoshamiri.

Kuanzia wakati wa mdororo mkubwa kiuchumi (Great Depression) mwaka 1930 mpaka mwaka 1960, Marekani ilikuwa na kiwango cha wafungwa gerezani chini ya 150,000. Mwaka 1970, baada ya Rais wa 37 wa Marekani, Richard Nixon kutangaza kuwa adui namba wa nchi hiyo ni dawa za kulevya, hapohapo kasi ya wafungwa ikawa kubwa mpaka kufikia watu 250,000.

Watu zaidi ya 2.2 milioni wamefungwa Marekani, kati ya hao, asilimia 40 wanatokana na vita ya dawa za kulevya. Takwimu zinaonesha kuwa asilimia 5 ya watu wote duniani ni raia wa Marekani, takwimu pia zinabainisha kwamba asilimia 25 ya wafungwa wote duniani wapo Marekani.

Takwimu zinaeleza kuwa asilimia 50 ya Wamarekani wote kwa namna moja au nyingine hutumia dawa haramu za kulevya kwa sababu mbalimbali.

Hiyo ndiyo laana ya unga, jinsi mapambano yalivyo makali, ndivyo na kuenea kwake kunakua kwa kasi kubwa. Rais wa 41 wa Marekani, George Bush (Bush baba), alipoingia madarakani aliwekeza fedha nyingi mno, akiwa ni Rais wa kwanza wa Marekani kufanya hivyo, lakini matokeo yake biashara ilishamiri.

Tafakari; Bush aliyekuwa wa kwanza kuwekeza mpaka dola 11 bilioni, Sh25 trilioni, akaishia kutawala kipindi kimoja tu. Nixon aliyetangaza dawa za kulevya kuwa adui namba moja Marekani kisha akaianzisha DEA, aliondolewa madarakani kwa kashfa ya utawala wake kuhusika na uhalifu kwenye Skendo ya Watergate.

Haya sasa Rais wangu Magufuli tuulizane; sisi tumewekeza shilingi ngapi? Huwezi kupambana na biashara ya dawa za kulevya bila kuwa na fedha za kutosha. Hutaweza.

Je, tumejipanga? Maana Serikali inawatumia polisi na wauza unga wanawatumia polisi haohao.

Vipi upelelezi umeshafanyika na umekamilika? Wauza unga huwa hawakamatwi kwa kelele. Wahenga walishatueleza kuwa miluzi mingi humpoteza mbwa.

POKEA NENO RAIS MAGUFULI

Naunga mkono mapambano kama ambavyo wewe unamuunga mkono RC Makonda. Hata hivyo, naomba nikupe neno langu mapema kuwa jinsi mapambano haya yalivyoanza, ni rahisi kubashiri kuwa hayatafanikiwa.

Naunga mkono kukamatwa kwa mtu yeyote ili kufuatilia nyendo za wauzaji wadogo, wa kati na wakubwa. Swali; ilishindikana nini kuwakamata kimyakimya ili waweze kubanwa na kutaja? Kuna maslahi gani kwenye ukamataji wenye matangazo mengi? Narudia tena, miluzi mingi humpoteza mbwa!

Marekani wanahangaika sana. Maofisa wa DEA hutumia pia mbinu ya kukamata watuhumiwa wa dawa za kulevya na kuwashikilia kwa muda kwa mahojiano. Hayo mahojiano ni kumzungusha mtuhumiwa, kwani kipindi wakimhoji, wakati huohuo DEA kwa kutumia wataalamu wao wa magari, huingiza kifaa maalum kwenye gari la mtuhumiwa.

Kifaa hicho hufanya kazi mbili, kwanza ni simu, ambayo makao makuu ya DEA husikia kila anachozungumza akiwa kwenye gari, vilevile ni kitambusho cha eneo (GPS Locater), hivyo popote anapokwenda hufahamika kwa mashushushu wa DEA.

Mtuhumiwa anapongia kwenye gari lake huwa hajui kama amewekewa kitu, maana hukuta kila kitu kipo kama alivyoacha. Wakati mwingine DEA huwa hawakamati wahalifu, isipokuwa huyavizia magari ya wahalifu wa unga kwenye maeneo mazuri kisha kuingia ndani na kufunga simu zao pamoja na GPS Locater, hivyo kuwa rahisi kuwafuatilia na kuwakamata wakiwa na ushahidi.

Pamoja na nguvu zote hizo bado Marekani inateseka na inapambana kwa maarifa mengi kuliko kelele kwa sababu ya kufahamu nguvu za wauza unga. Ni kwa nini imeonekana Tanzania tunaweza kupambana kwa kelele?

Mataifa mengi yaliyoendelea yanatumia mfumo unaoitwa Snitch (Usaliti) kwa lugha za wauza unga, polisi huita Wanyetishaji Wahalifu (Criminal Informants), kwamba anakamatwa mhalifu mdogo na ushahidi, anaahidiwa akubali kuwa Snitch kwa kwenda kushirikiana na wenzake halafu anatoa taarifa polisi za kusaidia kukamata wale vigogo wa unga.

Ipo njia ya askari kanzu (undercover cops), wanaingia kwenye biashara ya unga kama wahusika kweli, mwisho wanasaidia taarifa za kuwakamata wahalifu. Hii ni njia ambayo huhatarisha maisha ya askari wengi lakini imesaidia wauza unga wengi kukamatwa.

Askari wa Uingereza, Donnie Brasco, Novemba mwaka jana, alitangazwa shujaa wa taifa, baada ya kujigeuza mhalifu wa unga kwa miaka mitatu, akilichunguza genge hatari la biashara ya dawa za kulevya na silaha. Kazi yake ilifanikisha kukusanya ushahidi na hivi sasa watu 24 walioonekana hawagusiki (the untouchables) wapo jela.

Rais wangu Magufuli, hapo maana yake ni kuwa vita ya unga inahitaji subira. Hao watu wana fedha, na mtu mwenye fedha huwezi kumfunga kwa hisia za kutajwa, inatakiwa kuwe na ushahidi wa kutosha.

Ukimkamata bila ushahidi utamzungusha mwisho atatoka. Ukimpeleka mahakamani, jaji atamwachia huru kisha utasema jaji amekula rushwa.

Rick Ross ‘Freeway Rick’ (siyo yule wa Hip Hop), alikuwa bilionea wa unga na kila mtu alijua, undercover cops walimfuatilia na kufanikiwa kumkamata na ushahidi. Alihuhumiwa kifungo cha maisha jela, ila alipokata rufaa alishinda kwa sababu ushahidi uliokuwepo haukutosha kumtia hatiani.

Hata hivyo, alifanya makubaliano na polisi kwa kukiri kosa, hivyo alifungwa miaka 10 na mwaka 2009 aliachiwa huru.

Katika documentary ya How to Make Money Selling Drugs, iliyoandikwa na kusimuliwa na Mathew Cooke kisha kutengenezwa na Adrian Grenier, Freeway anasema kuwa enzi zake alikuwa anatengeneza mpaka dol 3 milioni, Sh6.7 bilioni kwa siku.

Freeway anasema ubosi wa unga ulimfanya awe don wa polisi na jamii. Alitoa misaada kwa watu na polisi waliokuwa naye, walikuwa na uhakika wa kupata mpaka dola 40,000, Sh89.4 milioni kwa siku.

Huo ni mfano wa Marekani, lakini ripoti ya Ofisi ya Dawa na Uhalifu ya Umoja wa Mataifa (UNODC), inaeleza kuwa mazingira ya magenge ya unga yanafanana duniani kote.

Kwa mantiki hiyo, Rais wangu Magufuli anapaswa kufahamu kuwa ukiona askari mdogo anatumika kama wakala wa wauza unga, ujue kuna wakubwa zake wapo kundini. Wakubwa ndiyo huwafanya wadogo nao wajiunge.

Askari mdogo anaona akimkamata muuza unga, bosi wake anamkemea. Askari mdogo anashuhudia bosi wake anavyoneemeka kwa fedha za wauza unga, naye anaona bora atafute njia awe anakula. Vita hii inahitaji sayansi ya intelijensia.

Sayansi yenyewe ya intelijensia inapaswa kuanzia ndani ya vyombo vya usalama. Wanaotakiwa kuifanya kazi yenyewe wanatakiwa wawe ni wale ambao hawahusiki kabisa na michezo yenyewe. Vinginevyo siri zote za Serikali zitaendelea kumilikiwa na ‘wadudu’ hao hatari.

FAHAMU KANUNI YA VITA

Rais wangu Magufuli, vita dhidi ya dawa za kulevya kanuni yake ni moja ambayo ni Trust No One, yaani Usimwani Mtu.

Ukitaka kuiweza vita ya dawa za kulevya na kwa vile wewe ndiye Amiri Jeshi Mkuu, hakikisha unamtilia shaka hata yule ambaye anajifanya anachukia sana biashara yenyewe. Hiyo ndiyo kanuni.

Watakuwepo watu wenye uchungu mkubwa. Watakuja mbele yako na msululu wa mbinu za mapambano, kumbe haohao ndiyo wahusika. Wauza unga ni wakali wa kukamatisha wasiohusika ili kulinda mitandao yao.

Yolanda Madden ni mama wa watoto wawili, Marekani, alifungwa miaka mitano jela kimakosa. Sababu ni taarifa za uongo zilizotolewa na wauza unga na polisi nao wakamkamata na akahukumiwa kifungo jela.

Barry Cooper, askari wa zamani wa kikosi cha Swat, aliye na rekodi ya kukamata watuhumiwa wa unga mpaka 100 kwa mwaka, wakiwa na ushahidi, baada ya kuacha kazi, aliamua kufundisha jamii jinsi vita ya dawa ya kulevya inavyotakiwa kuendeshwa.

Cooper ameshatoa mfululizo wa DVD zinazoitwa Never Get Busted Again, akieleza kuwa ugumu wa vita hiyo ni kwa sababu askari wengi wanaojua vita ya dawa za kulevya nao wanahusika, wasiohusika hawajui nyayo za wauza unga.

Kupitia DVD ya Never Get Busted Again toleo la kwanza, Cooper alieleza kuwa watu wengi wamekuwa wakituhumiwa na kufungwa jela bila makosa kwa sababu ya taarifa za uongo kutoka kwa wauza unga, lengo likiwa kuwapiga chenga polisi wasifikie magenge yao.

Mfano mmojawapo ambao Cooper aliueleza ni wa Yolanda Madden kuwa alifungwa kimakosa. Kufuatia maelezo hayo, uchunguzi ulifanyika na kufanikisha kumweka huru mwanamke huyo.

Mwanamke mwingine alitajwa na kuvamiwa nyumbani usiku akiwa na mwanaye mwenye umri wa miaka mitatu. Mwanamke huyo alihukumiwa kifungo jela, hivyo akafungwa na mtoto wake wa kike. Hata hivyo, baadaye alionekana alisingiziwa.

Jaji wa Mhakama Kuu Marekani, Jim Gray anasema ndani ya documentary ya How to Make Money Selling Drug kuwa watu wengi wanatengenezewa kesi na kuhukumiwa.

Alisema kuwa watuhumiwa wengi wa biashara ya dawa za kulevya wanakamatwa na kuachiwa kwa sababu ya kukosekana kwa ushahidi ama ni kwa makusudi au bahati mbaya.

Hivyo basi Rais wangu Magufuli, vita ya dawa za kulevya siyo ya kuamini mtu. Wapo ambao huwa ‘wanoko’ kwa wengine halafu wanawalinda wenzao. Huo ndiyo ugumu wa vita.

Wauza unga huingiza ushawishi kwenye mabaraza ya mawaziri, vilevile huingia ndani ya Ikulu mbalimbali na kuchangia siri za nchi na watawala. Ndiyo maana kama kweli vita hii ipo kwa moyo mmoja, basi Rais wangu Magufuli hutakiwi kuwamini mtu.

Ukigeuka kushoto, unayemwona jiulize: “Hawezi kuwa huyu?” Ukitazama kulia, jiulize: “Au ndiye yeye?” Hii ni kwa sababu biashara ya dawa za kulevya inamhusisha kila mtu mwenye tamaa.

Bobby Carlton ni muuza unga aliyekuwa anatengeneza dola 50,000, Sh112 milioni kwa siku. Anasema dawa za kulevya zina mtandao mpana na huwezi kuwajua kwa wingi wao mpaka na wewe uwemo kwenye mzunguko.

Hayo ni maneno ya wahusika wenyewe. Kwa maana hiyo ni vizuri uchunguzi uwe mpana. Ndiyo maana ushauri wangu ni kutaka upelelezi ufanyike katika misingi ya kimyakimya ili walengwa hasa wasishtuke na kukimbia au kupoteza ushahidi.

Sina tatizo na ukamataji, lakini kama tunahitaji mafanikio yenye tija kwa taifa, basi watu warudi chini. Vita ya dawa za kulevya inataka intelijensia, wauzaji mwendo wao ni wa kijasusi, inatakiwa Serikali ifanye ujasusi zaidi yao.

Rais wangu Magufuli, hupaswi kusahau hili. Vita ya dawa ya kulevya inahitaji kipimo cha mtindo wa kimaisha (lifestyle audit) kwa kila msaidizi wako ili kujua nani wa kumwamini na yupi anafaa kuifanya hiyo kazi. Usije kupigana vita batili nje wakati adui mkubwa yupo ndani.

Je, wasaidizi wako wote wanazungumza lugha moja kutoka moyoni? Isije ikawa wengine wanatumika kuuza timu. Je, maisha yao wote yanafanana na usafi? Lifestyle audit inahitajika kwa kila kiongozi serikalini na vyombo vyetu vyote vya usalama ili tupate mafanikio kwenye vita hii.

NIKUTAKIE KAZI NJEMA

Mwisho kabisa Rais wangu Magufuli nakutakia kazi njema. Nakushauri uifanye kazi ili ikaache alama. Siku zote katika uongozi wako, jitahidi sana kushughulikia kiini cha tatizo.

Dawa za kulevya kama mti, wauza unga wana tabia ya kuotesha matawi yao haraka sana kila yanapokatwa. UNODC wanasema kuwa magenge ya wauza unga hufanya kazi kwa haraka kutengeneza mitandao mipya ya uhalifu kila baada ya ule wa kwanza kubomolewa na Serikali yoyote duniani.

Naamini Rais wangu Magufuli umekuwa Rais wa Tanzania kwa sababu Mungu amependa, maana uongozi ni uteule. Hivyo basi, hakikisha unampendeza Mungu kwa kutenda sawasawa na tatizo.

Inawezekana kweli matawi yanaongeza uzito, hivyo yaanze kukatwa yenyewe. Hata hivyo, kuchelewa kidogo tu matawi mengine yataoteshwa. Wauza unga ni wepesi, wazoefu na wana elimu kubwa ya intelijensia.

Wakati mwingine ukamataji wa wadogo kwa sauti huwa na gharama kubwa. Wauzaji wengi wadogo wanapokamatwa na wale wakubwa kujua walikamatwa, huwaua ili kuharibu ushahidi.

Muuza unga hapendi kufuatiliwa. Muuzaji mdogo anapokamatwa hata akiachiwa, wale wauzaji wakubwa humtafsiri kuwa ni Snitch. Kwamba tayari alishakubaliana na polisi ili kuwachoma, kwa hiyo kufupisha mzunguko huwa wanamuua.

Rachel Hoffman alikuwa binti anayesoma Chuo Kikuu cha Florida, Marekani. Alikamatwa na polisi kwa kujihusisha na biashara ya unga mwaka 1980. Alipoachiwa tu, mabosi wake walimhisi tayari ni Snitch, kwa hiyo alipigwa risasi. Wauza unga huwa hawana mchezo.

Vita hii pia iendane na ulinzi wa askari waaminifu. Wanaweza kufanya kazi nzuri lakini kwa sababu uaminifu ni mdogo, vibaraka huvujisha siri za jeshi kisha wale waaminifu huingia kwenye matatizo ikiwemo kuuawa.

Askari mstaafu wa kikosi cha dawa za kulevya Marekani, Neill Franklin anasema kuwa ukitaka uione dunia chungu basi wauza unga wakugundue wewe ni polisi na ulikuwa unawachunguza.

“Wakipata picha yako na familia yako ujue umekwisha, watakupigia simu uchague mawili, ama ujisalimishe kwao ili wakutumie kuwapa siri za polisi na uwasafirishie dawa au ukatae kisha waje wakuue na familia yako,” anasema Franklin na kukumbuka kifo cha bosi wake, Edward Toatley, aliyeuawa kwa kupigwa risasi baada ya wauza unga kumgundua.

Haya sasa Rais Magufuli nakuomba hii vita tukaipigane vizuri. Kipeperushi hiki nimekupa ili uyaone mazingira ya vita ili tushinde. Nilimwandikia pia SMS yake Makonda, naamini ukijumlisha na kile nilichomwambia Makonda na hiki kipeperushi ninachokuletea, utajua jinsi ya kuanza na kupigana mpaka mwisho.

Hata hivyo, nakukumbusha kuwa kuna vigogo wa dawa za kulevya, mabilionea kabisa kama Shkuba, Chonji, Mama Leila na wengine wengi. Hawa walikamatwa na aliyekuwa mkuu wa kitengo cha kupambana na dawa za kulevya nchini, Godfrey Nzowa.

Tafadhali Rais wangu Magufuli, ukubwa dawa, kama kweli tunataka ushindi mwite huyu mzee mzungumze mawili matatu, anaweza kukupa mengi ambayo huyajui kuhusu biashara ya dawa za kulevya nchini.

Mungu akubariki Rais wetu, Mungu ibariki Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Credit: www.luqmanmaloto.com
 
Mkuu mimi naamini Kwa nchi kama marekani hii vita ni kubwa Ila Kwa nchi kama tanzania haina ugumu Sana ni suala la maamuzi magumu tu. Waliopo nyuma ya hii biashara wapo wengi Ila wote Tukianza kuamua kuacha mambo ya busara kwenye hii vita basi lazima wakae. Serikali iamue Sasa magufuli pewa yale majina na kikwete Hawafiki hata 50 fanya kama ujitoe ufahamu kamata na uwaweke ndani Ulinzi mkali Sana Bila huruma Kwa mwezi mmoja tu tuone km madawa yataendelea kuingia.. Uamuzi pekee ndio huo . Atakayewatetea anahusika awe wa upinzani au serikali.. Fanya hio kitu magufuli Wewe ndio rais Ukisema ufuate sheria bado Sana
 
Pole sana mleta uzi hasa kwa muda na uchambuzi wako wote uliouleta humu.

Ila nasikitika sana mlengwa huwa hana uwezo wa kusoma paragraphs zaidi ya tano.
Na penyewe kwenye hizo tano aone umemtaja taja sana tena kwa kumsifia tu.

Kichwa alichonacho fyuzi ziliishaungua kwenye "maganda ya korosho", kwa uliyoyaandika na uzito wake, anaweza kusoma mpaka paragraph ya 3 akasahau ya kwanza ilikuwa inasemaje.
 
Trust no one, kweli mkuu umeandika Maneno kuntu sana maana inahitajika juhudi,uzalendo na uwajibikaji wa vitengo vinavyohusika
 
Kichwa alichonacho fyuzi ziliishaungua kwenye "maganda ya korosho",

Kwq maneno hayo hapo juu mkuu bilashaka utakuwa mchochezi wa namna ilivyopatikana PhD ya mkuu laki saba unayo?
 
Tatizo wanadhani wauza madawa ya kulevya ni watu wa hovyo wasiojielewa. My friend, these dudes are smart pengine kuliko hata hao polisi na vyombo vya usalama kiujumla. Hebu patia picha tuu, mtu anafanya biashara kwa wasiwasi huku akiwa anajifichaficha, but stil biashara inaenda na faida anapata.
 
Mimi nikushukuru kwenye aina na namna ambavyo imejaribu kulielezea hili suala vizuri kimsingi suala LA madawa ya kulevya silikubali hata kidogo kwani Athari zake ni mbaya sana na kwamba tahadhali ulioitoa inaweza ikaleta kitu cha maana
 
Lugman Maloto ameelezea vizuri sana. Bila shaka alifanya research kupata maelezo ya kina kuhusu biashara ya dawa za kulevya.

Magufuli naasikie haya. Kusema hii vita nurahisi Tz nikujidanganya tu. Hii biashara inafaida kubwa drug lords kamwe hawata give up kizembe. Sasa hivi watakuwa wanabuni mbinu mpya.

Alivyofanya Makonda kutangaza watuhumiwa hadharani wakati ndiyo kwanza vita inaanza lilikuwa kosa kimkakati. Alifanya hivyo pengine kwakutojua au kupata sifa tu.

Pia Maloto amegusia fedha zakutosha zitengwe kupambana na hii vita. Naunga mkono hoja. Isipofanyika hivi......polisi wataishia kuhongwa tu tena life inavyokaba...... watakuzuga tu.
 
Daaaah nianze na pongezi za dhati kwa mtiririko bora wa mawazo na hoja, hii inshu ni ngumu sana huwezi kutangaza eti waje mahakaman wenyewe ina maana walikuwa wajinga kiasi hicho eti waache data nyumbani.....
 
Story ni ndefu lakini inamashiko, hope wasaidizi wa Rais wameiona watamfikishia ujumbe.
 
62 Reactions
Reply
Back
Top Bottom