Mama Amon
JF-Expert Member
- Mar 30, 2018
- 2,021
- 2,478
Ndege ya Precision ikiwa imezama majini ndani ya Ziwa Viktoria
MANUSURA 19 katika ajali ya ndege ya Precision Air iliyotokea Novemba 6, mwaka jana – nje kidogo ya Uwanja wa Ndege wa Bukoba -- wataambulia malipo ya fidia ya Sh. milioni 70.2, Pambazuko linaweza kueleza.
Taarifa za awali ambazo Pambazuko limedokezwa wakati likienda mitamboni jana usiku, ni kwamba fedha hizo zitakatwa kiasi cha Sh. milioni 11.7 ambazo kila mmoja aliyenusurika katika ajali hiyo alilipwa wiki iliyopita, ikielezwa kuwa ni malipo ya awali kusaidia mahitaji ya tiba na kujikimu.
Endapo kiasi hicho kitakatwa kutoka kwa waguswa hao, kila mmoja atabaki na Sh. milioni 58.5.
Kutokana na mchanganuo ambao Pambazuko limeuona kwa haraka ni kwamba kampuni zilizopewa kandarasi ya kulipa fidia hizo, zitatoa takribani Sh. bilioni 1.34, ikiwa gharama ya kubadili fedha itakuwa dola moja ya Marekani kwa Sh. 2,340.
Hata hivyo, haikufahamika mara moja endapo haya sasa ndiyo malipo ya mwisho au vinginevyo na haikujulikana lini wataanza kulipwa fedha hizo za fidia.
Pambazuko limefuatilia kwa uongozi wa juu wa Precision Air ambao watendaji wote walikataa kuzungumza kuhusu malipo haya.
Hata hivyo, mmoja wa wakurugenzi wa bodi alizungumza kwa masharti ya kutoandikwa gazeti alikiri kufikiwa kwa hatua za mwisho-mwisho ili “kumalizana na manusura hao.”
“Labda nikudokeze tu kwamba mchakato wa kuwalipa unafanyika kwa umakini mkubwa na kwamba watalipwa haraka, ingawa sijui kiasi watakacholipwa kwa awamu inayofuata.”
Mwenyekiti wa Chama cha Kampuni za Bima Tanzania, Khamis Suleiman amesema kuwa inapotokea ajali ya ndege bima inatakiwa kumlipa aliyekumbwa na ajali hiyo kiasi cha fedha kisichopungua Sh. milioni 300.
Mkurugenzi wa kampuni hiyo ya ndege iliyopata ajali, Patrick Mwanri amekuwa akisisitiza kuwa malipo ya manusura hayo yatafanyika kwa usiri mkubwa.
Kamishna wa Bima nchini Tanzania, Dkt. Baghayo Saqware amesema kampuni ya Precision Air itafidiwa zaidi ya Sh. bilioni 116 kwa hasara ya kupoteza ndege yake huku akieleza manusura na wale waliopoteza maisha kufidiwa kiasi kinachoweza kufikia Sh. milioni 396.
Ndege sampuli ya ATR 42-500 hutengenezwa na kampuni ya ATR Aircraft ya Ufaransa. Sampuli hii imekuwa ikitengenezwa kati ya mwaka 1944 hadi mwaka 2012. Inahitaji marubani wawili na inaweza kubeba abiria 42.
Huweza kuruka hadi futi 25,000 kwenda juu angani na kasi yake hufikia maili 345 kwa saa. Bei yake ni wastani Sh. bilioni 28.34.
Manusura hao 19 ni miongoni mwa abiria 43 walioelezwa kuwamo ndani ya ndege aina ya ATR42-500 mali ya Shirika la Precision iliyolazimika kutua Ziwa Victoria, mita 150 kutoka Uwanja wa Ndege wa Bukoba.
Ndege hiyo yenye usajili 5H-PWF namba PW 494 iliyoanza safari yake kuelekea Bukoba alfajiri ya Jumapili, Novemba 6, mwaka huu, iliingia anga la mji huo pembezoni mwa Ziwa Victoria, lakini rubani wake, Buruani Rubaga alishindwa kutua uwanjani kutokana na hali ya hewa kuwa mbaya.
Chanzo: Gazeti la Pambazuko, Toleo Na. 027.