Kila fani ina zana!

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,475
39,988
Kila fani ina zana, nyingine zaitwa nyenzo,
Iwe kazi ya kitwana, yenye malipo ya dezo,
Au kazi ya kibwana, yenye mapochi ujazo,
Jembe lisilo mpini, halifai kwa kilimo!!

Jembe lisilo mpini, halifai kwa kilimo,
Halikiti ardhini, halifai chimba shimo,
Bila mpini la nini, au kichwani hazimo?
Nyavu hizo zisonasa, za nini hizo botini!!

Nyavu hizo zisonasa, za nini hizo botini,
Wataka kuleta visa, samaki hatuwaoni,
Utaja pata mkasa, upigwe ngumi puani,
Msumari usonyoka, hauingii mbaoni!!

Msumari usonyoka, Hauingii mbaoni,
Usije kukupochoka, ukaijeruhi mboni,
Watu wakaja kucheka, utadhani limbukeni,
Chanuo lisilochana, halifai kwa ususi!!

Chanuo lisilochana, halifai kwa ususi,
Usikazane kuchana, utajeruhi utosi,
Tafuta chako kitana, situmie bisibisi,
Moyo ule usopenda, haufai kwa mapenzi!

Moyo ule usopenda, haufai kwa mapenzi,
Wajikuta umekonda, kumkosa wa azizi,
Pale wewe umependa, mpaka wakosa pumzi,
Moyo kama vile zana, isofaa iachie!!


Na. M. M. Mwanakijiji (Sauti ya Kijiji)
 
Muungwana naona umekamilika...sio kule kwenye Siasa tu naona hata huku kwenye sanaa/Lugha unatukonga nyoyo zetu...nimemtupia Mama Lihamba hili shairi lako,nae amedai limekamilika,lina Mizani iliyokamilika 16 katika kila beti 8/8 na vina vilivyobeba mawazo ya beti...Mtiririko wa Lugha ni Mzuri kwani shairi lako ni rahisi kughani na linaleta maana..Hongera Mkuu!!
 
Muungwana naona umekamilika...sio kule kwenye Siasa tu naona hata huku kwenye sanaa/Lugha unatukonga nyoyo zetu...nimemtupia Mama Lihamba hili shairi lako,nae amedai limekamilika,lina Mizani iliyokamilika 16 katika kila beti 8/8 na vina vilivyobeba mawazo ya beti...Mtiririko wa Lugha ni Mzuri kwani shairi lako ni rahisi kughani na linaleta maana..Hongera Mkuu!!

nafurahi kuleta na burudani maana tukiwaacha mafisadi watukunjishe ndita muda wote, tutakosa kicheko.
 
Back
Top Bottom