Elections 2010 Kikwete ni msahaulifu au mzembe?

rimbocho

Member
Jan 11, 2010
73
3
bul2.gif
Anakumbuka marafiki na kusahau ahadi


NAWEZA kudai kumfahamu Kikwete kuliko wengi wa mashabiki wake wanaohudhuria mikutano yake ya kampeni. Nimefanya naye kazi jeshini na serikalini kidogo, lakini nimefanya naye kazi sana kwenye Chama. Nimekuwa naye kwa karibu kama rafiki (siyo swahiba) kwa mambo ya kawaida. Anaweza kuandika hotuba nzuri ya kunisifia siku ya mazishi yangu. Haya yanatoka moyoni.
Mwaka 2005 yaliandikwa mengi ya kumsifia. Yakasemwa mengi ya kushadidia sifa zake – muungwana, mtu wa watu, mstaarabu, chaguo la Mungu, tumaini lililorejea, mkombozi wa Watanzania, Musa wa pili na chaguo la Watanzania.
Akazoa kura nyingi zikiwamo za wapinzani, maaskofu, vijana, wasomi, wafanyakazi, wakulima, wachimbaji wadogo, wahamiaji haramu, wanajeshi, na wanafunzi. Naam, hata mama ntilie au kwa jina la utani Mama Lishe! Matumaini yalikuwa makubwa.
Tuseme ukweli, walioonya wazi juu ya hatari ya huko mbele walikuwa wachache sana, na waliodiriki kufanya hivyo kwa uwazi, ilibidi usiku wawe wanahama vyumba vya kulala!
Wapo wachache, hata nikidai mimi ni mmojawapo sitaaminiwa kwa maana hakuna ushahidi wa waliokataa ghiliba hii ndani ya chama chetu. Miaka mitano imekuwa ya mateso makubwa kwetu.
Tumesutwa, tumetukanwa na wanaojifunza kutukana. Tumeitwa majina na tumefikia kuhudhuria vikao vya chama na kuandikwa kuwa hatukuhudhuria kwa sababu ya ukimya wetu.
Kwenye vikao vya kahawa, tumetumiwa wajumbe wa kutuambia hatuwezi kumfufua aliyekwishakufa (Nyerere), hatuwezi kurudisha nyuma saa iliyokwishakwenda mbele, wakati umepita, tukae kimya. Nani atabishia simulizi yangu hii? Waliokuwa wachambuzi na wasemaji wa kuwatia moyo Watanzania wako wapi? Wote hao wamekwenda, zimebaki sifa zao!
Nirudi kwenye hoja yangu ya leo. Hivi Rais Kikwete ni msahaulifu au mzembe? Mbona anakumbuka marafiki wake wa zamani na wa karibuni lakini anasahau ahadi zake na kauli zake?
Walio karibu naye katika kampeni watakubaliana nami kuwa Kikwete ana kumbukumbu kali juu ya watu aliowahi kuwa nao zamani. Kila sehemu anayofika kwa mkutano atakuambia nani anazaliwa pale, atauliza yuko wapi siku hizi, ataagiza mwambie amtafute wazungumze au ataagiza apatiwe hiki au kile kama ameambiwa kuna shida.
Akiambiwa alikwishakufa, atabadili ratiba akahani msiba au aitiwe mzazi au mjane ampe ubani. Atakumbuka hata dondoo ndogo sana za urafiki wake na mtu huyo.
Hii inavutia wengi na waandishi wetu wameagizwa na kuamriwa kuhakikisha matukio kama hayo yanakuwa katika picha na kurasa za mbele za magazeti.
Wakati huo huo, Kikwete ni msahaulifu wa ahadi zake kwa watu binafsi na hata kwa umma. Wapo wanaodai hili si tatizo lake, ni tatizo la watendaji wake ambao wanapaswa ama kuchukua kumbukumbu na kutekeleza au kumkumbusha. Mimi nadhani ni tatizo lake – nitaeleza sasa.
Uaminifu wa kutekeleza ahadi huanza na kauli. Kikwete ni msahaulifu wa aliyoyasema. Ama hatunzi kumbukumbu za aliyosema, au hafikirii madhara ya kauli zake, au yote mawili kwa wakati mmoja.
Alipoingia madarakani alisema “urais wake hauna ubia”. Alilenga kuwajibu waliokuwa wanamsakama kuwa ametekwa na marafiki. Juzi juzi wakati anachukua fomu ndani ya chama, pale Dodoma, akakausha macho na kusema; “Urais ni suala la kifamilia”.
Alilenga kuwajibu waliokuwa wanahoji kitendo cha mtoto wake Ridhiwani kuzungusha fomu ya kutafuta wadhamini. Mpaka hapa inaonyesha Kikwete amesahau alisema nini 2006 au sehemu zote mbili hakufikiri kabla ya kusema. Urais ni taasisi. Urais ni utumishi wa umma. Rais ni mbia wa urais na wananchi wa Tanzania. Ndiyo maana mtu haamki asubuhi na kujitangaza kuwa yeye ni Rais. Anakwenda kuwaomba wananchi wamchague awe rais. Akishakuwa rais, haina maana urais ni mali yake na familia yake.
Ni kituko kikubwa kwa rais kusema alivyosema Kikwete katika hafla hiyo ya Dodoma. Katika nchi zenye mifumo makini, serikali ingechukua hatua, au chama husika kingechukua hatua na kama vyote viwili vingeshindwa, basi, wananchi wangechukua hatua kupitia sanduku la kura.
Siyo siri kuwa hivi sasa familia ya Rais Kikwete imeingia kwa nguvu za ajabu katika uendeshaji wa nchi na hakuna mtu ndani ya Chama wala serikali anayeweza kuthubutu kulikemea jambo hili. Uliokuwa ubia wa urais kati ya Kikwete na marafiki zake, sasa umegeuka ubia wa Kikwete na familia.
Siku hizi si jambo la ajabu kumwona Mama Salma anaingia ndani ya vikao vya Kamati Kuu. Kamati ya maadili wananung’unikia kwenye korido, Kamati Kuu wanaongelea chini chini, wajumbe wa NEC hao ndiyo basi!
Mama Salma sasa anafanya majukumu ya kichama bila kibali cha kikao chochote, na mbaya zaidi anaagiza, anakemea, anatishia, ananyang’anya na kugawa madaraka. Viongozi wa serikali mikoani na wilayani wako hoi. Hawajui wafanye nini na mama huyu.
Mmoja wa wakuu wa mikoa ameniambia, safari hii, hata kwa risasi, hatakubali kuteuliwa kuendelea na ukuu wa mkoa kama mambo yanakuwa hivi. Anadai wiki hii unampokea Baba na madai yake, wiki inayofuata anakuja mtoto naye anataka uende uwanjani kumpokea, hujakaa sawa anakuja mama, unaambiwa uhame nyumba kumpisha, siku inayofuata anakuja yule mdogo wa chipukizi, unaambiwa umsindikize mpaka aondoke mkoani kwako.
Mkuu huyo wa mkoa anakang’aka: “Tumeteuliwa kutumikia familia”? Polisi wanapiga saluti kwa mama, mtoto Ridhiwani anadai ripoti kutoka kwa Mkuu wa Mkoa? Kamati za siasa na kamati za ulinzi wanachanganyikiwa hawajui wafanye nini?
Mpaka hapa mtu unajiuliza: Kikwete aliposema hana ubia na mtu alimaanisha nini ikiwa watoto wake wawili na mkewe wanafanya kazi za Chama na serikali kwa gharama za serikali?
Matokeo ya ubia huu wa Kikwete na familia yake ni kusitasita kwa Kikwete kuchukua hatua muhimu za kurekebisha hali ya nchi.
Watu wamelia, vyombo vya habari vimelalamika na ripoti kadhaa zimeandikwa lakini hakuna hatua iliyochukuliwa dhidi ya mafisadi, wala rushwa, wazembe serikalini, wakwepaji kodi wakubwa, wezi wa nyara za taifa, wauza madawa ya kulevya na majambazi.
Kusitasita kwake kunatokana na hujuma iliyo ndani ya familia yake. Maadui wa ndani ya taifa letu ambao ni mafisadi ni wajanja.
Walipoona kelele za watu zinaanza kumwingia Kikwete na kumnyima usingizi, wakamzunguka kupitia familia yake na wanajimu. Wanajua fika hapo hawezi kunasuka. Sasa baadhi yao wamezama katika ufisadi wa kutisha. Ni Mungu tu ajuaye hatima yao.
Kabla ya kufika mwisho wa “fitina” zangu hizi (ndivyo JK anavyoziita makala hizi), nikumbushe na kusisitiza jambo la msingi. Pamoja na wema wake na misimamo yake tata isiyompa nafasi ya kuwa mtendaji mzuri serikalini na kwenye chama, hivi sasa Kikwete ajue yafuatayo yako ukutani.
Nitataja bila kufafanua. Kwanza, pamoja na kusita kuwachukulia hatua mafisadi, hata wao hawamtaki na hawampendi kwa sababu wanamwona ni mdhaifu asiyeweza kuwahakikishia ulinzi mbele ya wanaolalamikia ufisadi.
Wameniambia kuwa Kikwete ni mzigo kwao na kwa taifa. Pili, Kikwete hana risasi za kuwaua Watanzania wote wanaolalamika na kuteketea kwa umaskini mbele ya utajiri wa taifa letu. Hukumu yao kuna siku itatolewa, kama si mwaka huu, basi wakati mfupi ujao.
Na wakati huo hata kama atakuwa hayupo duniani (sote twaenda huko), hata kutemea mate picha yake, kutampa mtu usingizi wa siku moja.
Tatu, uongozi usio na maadili huzaa mamluki wengi. Hivi sasa siri nyingi za Ikulu zimezagaa mitaani kwa sababu tu Kikwete ameruhusu Ikulu pawe pango la mafisadi, wanajimu, wafanyabiashara na matapeli. Watu wasio na maadili hawawezi kutunza siri za nchi, ndo maana hata mikataba ya siri inavuja.
Hawa siku moja watasimama kizimbani, si kama washtakiwa, bali kama mashahidi dhidi ya uongozi wa Kikwete uliokosa mwelekeo na kushindwa

Msomaji Raia​

Source: Septemba 15, 2010
 
Na wengine wamwambie, huu ndio ukweli kuhusu uongozi wa huyu msanii asiyejua anakowapeleka watanzania. Naapa, tena naapa. sina hamu ya kufanya kazi na serikali na system ya msanii kwa nafasi yoyote. Bora niendelee kutumia elimu yangu kulima mahindi na karanga tena kwa jembe la mkono. Am tired.
 
Kwa kweli mkuu umenena, natamani kila mtanzania including wale wanaomshabikia kikwete wangesoma habari hii.
 
Kweli huyu ndio 'Msomaji Raia' wa ukweli. Mimi nimependa hapa maana panatekelezeka, "Na wakati huo hata kama [KJ] atakuwa hayupo duniani (sote twaenda huko), hata kutemea mate picha yake, kutampa mtu usingizi wa siku moja".
 
Makala nzuri na imejaa kila aina ya ukweli lakini bado ina ile tabia maarufu ya kitanzania: Woga na Unafiki. Kwanini? Katika uma wa viongozi wenzake wa CCM (pamoja na mwandishi wa hii makala) hajapatikani hata mmoja mwenye ujasiri wa kumwambia ukweli? Mbona wananung'unikia uvunguni tu?
 
Siasa za Afrika zina vituko vingi sana. Kwa sababu ya ulimbukeni, tunapopewa madaraka mara nyingi tunasahau kuwa ni dhamana. Tunaanza kuyageuza kama vile nayo ni sehemu ya miradi yetu binafsi.
Namsifu mwandishi kwa kusema ukweli wa yaliyopo na yale tunayotarajia yatatokea. Kuna mambo ukishayafanya bwana huwezi kubaki salama. Hilo sio siri maana ndio universal principles zilivyo.
 
Makala nzuri na imejaa kila aina ya ukweli lakini bado ina ile tabia maarufu ya kitanzania: Woga na Unafiki. Kwanini? Katika uma wa viongozi wenzake wa CCM (pamoja na mwandishi wa hii makala) hajapatikani hata mmoja mwenye ujasiri wa kumwambia ukweli? Mbona wananung'unikia uvunguni tu?[/QUOTE]

Ungesema "MBONA TUNANUNG'UNIKA UVUNGUNI TU" we are aall responsible for this; we have to be serious!!
 
Nimemkumbuka Mkuu wa mkoa wa Iringa Enzi zile Mzee Luhanga alikataaga kupigia kampeni JK alipoombwa na Lowasa bse anamjua fika JK na alikuwa nae Jeshini.
JK alipoingia madarakani tuu akampiga chini Luhanga.
Ni kwa nini watu wanaomfahamu hawana imani nae?
 
Tuongee hoja na sio matusi na chuki binafsi bila kupima. matusi na maneno ya kashifa sio utamaduni wa Kitanzania.
 
Tuongee hoja na sio matusi na chuki binafsi bila kupima. matusi na maneno ya kashifa sio utamaduni wa Kitanzania.
Sasa hapo matusi ni yapi mzee
kweli ukweli unauma!
Big up Msomaji Raia
 
Mmmh, hapa ndo unawakuta watu kama akina Tandaleone na MS wanamfagilia huyu Mkwere. Na hilo ndo tatizo la maelfu ya watanzania. Wanaamua tu kumfagilia na kumshabikia kwa kuwa wamepata buku mbili au kwa vile wanatafuta cheo fulani kutoka kwa JK. Hii ni hatari sana kwa nchi.
 
Nimefurahi baada ya kusoma hii thread nimepata ile hasira niliyokuwa naitafuta
 
Makala imetulia sana,ila ungemalizia na hizo ulizomezea ingetulia zaidi.Ila ningependa tu kukukumbusha kuwa wanaposema ni chaguo la Mungu hawakukosea.Mungu huwa anaruhusu viongozi mbalimbali watokee ili kuwafundisha watu mambo fulani.NaaminiTanzania tutaendelea kupata viongozi wabovu mpaka tutakapoanza kujifunza kujali.watu hawapigi kura hata wanapoona viongozi wanaochaguliwa hawafai.watu wanaeneza siasa za chuki kwa sababu wengine wako upinzani,wanasahau kama wenzao nao ni raia na wana haki kama wao,lakini ukiwa upinzani unaonekana ni Adui,kumbe wakati mwingine ni kutokana na utofauti wa mitizamo.Lakini pia ukipewa madaraka kwa muda mrefu wakati mwingine unaanza ku personalize hata yale ya jamii na kujiona wewe ndiye unastahili kuliko wengine.Chama chetu kimejisahau sana mpaka inafikia hatua ya kutumia mbinu zote kujihakikishia ushindi.lakini hali hii huwa hufikia ukingoni kwa sababu kiukweli ni kwamba tunakua tunabomoa chama badala ya kukijenga."performing in diminishing rate" Inabidi kujitahidi kuweka viongozi watakaoshindana kwa ubora na sio kwa kuuzwa kama utumbo wa ng'ombe barabarani."Chema chajiuza kibaya chajitembeza" Watanzania wengi wazuri na wenye uwezo wa kuongoza wapo,lakini hawataki kujihusisha na siasa,lakini wanasahau ya kuwa siasa inaathiri maisha yetu sote kwa kiasi kikubwa sana"sasa unabaki na kujiuliza tunaelekea wapi?watu wameacha wakati ndio uamue hatma yetu.hali inazidi kuwa mbaya, uongozi umefikia hatua ya kuwa na kambi.Uko kambi yetu unapata kazi,hauko, unaondolewa na wala sio ubora tena.sasa zimebaki kuwa siasa za makundi,tunaacha kuangalia maisha ya watu tunabaki kushindana,kambi ipi ishike "Utamu"(hatamu). matokeo yake ni kuacha kuangalia maendeleo yetu sote kwa ujumla, na kubaki kushindana kambi hii na ile.Rwanda pamoja vita yote ile wanatuacha,zanzibar nao wanaonekana kutaka kutuacha.Kitakachotokea Mungu ndie anajua. Tubadilike jamani tuwahamasishe na wengine washiriki kuchagua viongozi.Hata kama hatupendi kufanya hivyo,tutakua tumelisaidia taifa letuhili.Tusisukumie kizazi kijacho kuja kutatua haya matatizo wakati rasilimali tulizoachiwa tutakua tumezimaliza.Tuwaachie jukumu la kuja kuendesha maisha yao wakati huo.

Ndugu Mwananchi.
 
Back
Top Bottom