Kikwete na CCM Watikiswa na Vyama vya Msimu

Rugemeleza

JF-Expert Member
Oct 26, 2009
668
136
‘Vyama vya msimu’ vyatibua ushindi wa kishindo wa CCM


9c516874b7367b90471604f9fbda1a9b

Na Hilal K. Sued - Imechapwa 10 November 2010

MARA nyingi washindi huwa wanatamba; “Uwe halali, wa mizengwe au wa kupora ushindi ni ushindi.” Haya ni maneno ya kishabiki maarufu kwa mashabiki wa mpira ambao baada ya mechi watazungumzia kwenye vijiwe vyao namna ushindi ulivyopatikana.


Lakini katika chaguzi za siasa za kidemokrasia, ushindi wa aina nyingine yoyote mbali na ule wa halali na haki una athari zake kwa amani na utulivu wa nchi husika, hasa hali ikiwa inarudiwa rudiwa miaka nenda miaka rudi. Hakuna haja ya kutoa mifano, iko tele katika Bara la Afrika.


Kwa upande wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kilichotolewa kamasi na vyama vilivyodaiwa vya msimu – kukosekana katika uchaguzi huu kile ambacho huitwa “ushindi wa kishindo”—kumeibua, kwa mara ya kwanza, msukumo wa kuwepo kauli mpya kutoka kwenye uongozi wa juu wa chama hicho.


Akitoa hotuba baada ya kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi katika Ukumbi wa Karimjee siku ya Ijumaa, Jakaya Kikwete alionyesha kustushwa na ushindi mdogo alioupata mwaka huu (wa asilimia 61.10) ikilinganishwa na miaka mitano iliyopita (asilimia 80.2).


Alisema: “Kuna changamoto (matatizo) zilizojitokeza ambazo zitaifanya CCM kukaa chini na kutafakari ili kutafuta ufumbuzi wake… kutafuta nguvu mpya katika chaguzi zijazo...” Kauli hiyo aliirudia katika hotuba yake baada ya kuapishwa Jumamosi.


Pamoja na ujasiri aliounyesha katika kujaribu kusema ukweli kuhusu matokeo, alishindwa kukiri kinagaubaga kwamba “vyama vya msimu” navyo vina uwezo wa kutoa dhoruba kali kwa chama kilichoko madarakani kwa miaka 50.


Kikwete hana haja ya kuumiza kichwa kutaka kujua hatima ya chama chake katika miaka mitano ijayo kwani kasi na njia ya mporomoko tayari imeonekana. Miaka mitano iliyopita inatoa mwanga wa jibu la mwelekeo wa hatima ya chama hicho miaka mitano ijayo.


Wapambe na washauri wake walikuwa wanalijua hilo, kwamba mtu wao, baada ya miaka mitano, kapoteza mvuto mkubwa na hivyo kinachotakiwa ni kumnadi kwa nguvu zote.


Tumeona msisitizo mkubwa kwenye mabango ya bei kubwa, matangazo katika vyombo vya habari vya elektroniki (TV na redio) ukiachilia mbali matumizi ya nyenzo za serikali na utoaji ahadi lukuki zisizokuwa na mantiki.


Kwa mujibu wa katiba ya chama, yeye ndiye mwenye mamlaka kamili ya kuzuia mporomoko wake–kwa kufanya maamuzi yaliyo sahihi. Lakini kwa Kikwete hili limo katika nadharia tu, kihalisia hawezi – kwa sababu hana kitu kinachoitwa ujasiri wa kufanya maamuzi sahihi na ya makusudi.


Tayari mtikisiko mwingine umeanza Andrew Chenge – Mbunge mteule wa Bariadi Mashariki, na aliyewahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na baadaye Waziri wa Miundombinu amechukua fomu za kuwania uspika.


Huyu ni mtuhumiwa wa kashfa ya ufisadi wa ununuzi wa rada kwa bei kubwa na wapelelezi wa serikali ya Uingereza walishatoa ripoti kwamba wanao ushahidi wa kimaandishi na uliothibitika wa kuweza kumpandisha kizimbani.


Lakini ameruhusiwa na chama chake kugombea ubunge na sasa anawania uspika ili awe na udhibiti wa Bunge. Hii ni jeuri isiyoelezeka.


Ujasiri wake unatokana na imani yake kwamba suala hilo limeisha na hata kama lingekuwepo hakuna mtu au mamlaka inayoweza kumzuia kiurahisi – pamoja na mwenyekiti wa chama chake – Jakaya Kikwete.


Baada ya matokeo ya kura za ubunge yaliyoonyesha kuwa chama hicho kimepoteza majimbo muhimu na wagombea wake mashuhuri, wakiwemo mawaziri wa sasa na wa zamani, baadhi ya makada wa chama hicho wamejaribu kutoa sababu za kimbunga hicho.
Mawaziri wakuu wa zamani, Dk. Salim Ahmed Salim na Joseph Warioba walilaumu mipasuko ndani ya chama hicho iliyotokana na kura za maoni katika mchakato wa uteuzi wa wagombea.


Hii inaweza kuwa kweli kwa kura za wabunge katika baadhi ya majimbo, lakini siyo kweli kwa kura za urais. Ni vigumu kuhusisha minyukano ya makundi ndani ya chama hicho iliyotokana na uteuzi wa wagombea ubunge katika jimbo na kura za urais.


Na kama hili ni kweli limetokea, basi ni ishara nyingine inayoonyesha mporomoko katika chama hicho kuwa ni mkubwa na unatisha zaidi kuliko inavyodhaniwa.


Makada hao hawakutaka kulihusisha suala la kupungua kwa umaarufu wa Kikwete na ufisadi ambao wengi wanaona unakitafuna chama na serikali yake. Pia hawakutaka kuzungumzia Kikwete anavyoisimamia kansa hiyo.


Hawakutaka kusema wazi kwamba suala la ufisadi limemgharimu Kikwete katika uchaguzi huu. Iwapo kweli vyombo vya usalama wa taifa vingekuwa vinafanya kazi sawasawa – kujua wananchi wa kawaida wanasema nini kuhusu Kikwete anavyolishughulikia suala la ufisadi – wangemweleza ukweli kwamba wananchi wengi hawaridhiki na hilo.


Kwa mfano, kitendo chake cha kumwinua mkono na kumnadi mbele ya halaiki ya wapiga kura, mwenye kesi ya ufisadi mahakamani kuwa ni mtu safi, ni dharau kwa wapiga kura hao. Na kama ilivyotarajiwa, wapiga kura walitoa hukumu yao iliyo sahihi – kama ishara kwa Kikwete kwamba vita yake dhidi ya ufisadi ni geresha tu, na kwa mahakama kwamba nayo ijiangalie.


Kikwete kuonekana kwenda kinyume na matarajio ya wapigakura katika mapambano dhidi ya ufisadi ndiko kulikomwongezea dhoruba aliyoipata, siyo tu minyukano baina ya makundi majimboni.


Sababu nyingine iliyomgharimu Kikwete ni usimamizi wake mbovu kuhusu masuala ya udini. Alishindwa kuyasimamia kikamilifu, licha ya kukumbushwa mara kwa mara na lile tangazo la hotuba ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere katika ITV.
Aidha ikulu yake imehusishwa kuchochea udini kwa lengo la kukichafua chama kimoja cha upinzani.
Kwa mfano, wiki iliyopita, gazeti hili lilikuwa na habari chini ya kichwa cha habari “Ikulu yagharamia kuchafua upinzani” ambayo iliielezea jinsi ikulu, kupitia kitengo chake Kurugenzi ya Mawasiliano kilivyolipia tangazo la taarifa moja iliyochapishwa katika baadhi ya magazeti.


Taarifa hiyo iliyodaiwa kutoka kwa muumini mmoja wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG) jijini Dar es Salaam, pamoja na mambo mengine, ilieleza kuwa mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete ni chaguo la Mungu na kwamba wanaotaka kumng’oa madarakani wanashindana na alichokipanga Mungu.


Katika hotuba yake baada ya kuapishwa, na siku chache baada ya chapisho la habari hiyo, Kikwete, alivishutumu vyama vya siasa, vyombo vya habari na makundi mengine kwa kupandikiza chuki za kidini na ukabila wakati wa kampeni. Mtu hapa anapata kizunguzungu!


Chanzo: Mwanahalisi 10 Novemba 2010.
 
80.20% - 61.17 = ? Kama JK anataka akumbukwe baada ya 2015, kama afya yake itamruhusu kufika huko, ashughulikie suala la ufisadi!
 
80.20% - 61.17 = ? Kama JK anataka akumbukwe baada ya 2015, kama afya yake itamruhusu kufika huko, ashughulikie suala la ufisadi!

Labda hiyo hesabuu nig ngumua sana mkuu. Kwa jinsi ninavyowajua watu wengi sana wanaogopa hesabu kama ukoma, wanaweza wasihangaike kutafuta jibu la hizo namba na kwenda mbali zaidi ya namba. Na mbaya zaidi namba hizo ni feki. Hebu fikiria zingetoka namba halisi...nadhani sasa hivi tungekuwa tunashuhudia mtu mwingine akichukua mkondo kama ule wa Ariel Sharon.
 
80.20% - 61.17 = ? Kama JK anataka akumbukwe baada ya 2015, kama afya yake itamruhusu kufika huko, ashughulikie suala la ufisadi!
Kwa vyovyote vile JK ni lazima atakumbukwa, mapungufu yake hayawezi kusahaulika !
 
80.20% - 61.17 = ? Kama JK anataka akumbukwe baada ya 2015, kama afya yake itamruhusu kufika huko, ashughulikie suala la ufisadi!

Bill Buchanan....Atashughulikia vp???? watuhumiwa wote ni watu watu wake wa Karibu...hili swala litashughulikiwa na vyama mbadala.....Trust me ikitokea siku CCM chali utaona watu hasa wahindi watakavyokimbia nchi hii au kujiua ikibidi......
 
Back
Top Bottom