Kikwete 'jino kwa jino' na Lowassa

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,007
Kikwete ‘jino kwa jino' na Lowassa


picture-4.jpg

Na Saed Kubenea - Imechapwa 13 April 2011
Mwanahalisi


HATUA ya kukivua gamba Chama Cha Mapinduzi (CCM), imegeuka vita vya "jino kwa jino" kwa viongozi kukamiana.
Lakini kama Rais Jakaya Kikwete alilenga kuwafukuza watuhumiwa wa ufisadi kwenye chama, hakika ameshindwa.

Ameishia kuwaengua Rostam Aziz na Andrew Chenge kutoka Kamati Kuu (CC) lakini ameshindwa kuwang'oa kwenye Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC).

Pamoja na kwamba mjadala ulikuwa mkali kuanzia CC na hatimaye kwenye NEC ambako watuhumiwa hao wawili na Edward Lowassa walikamiwa kung'olewa, Kikwete "alipoteza mwelekeo" na kikao kumalizika bila maamuzi juu yao.

Vikao vya CC na NEC vilimalizika juzi Jumatatu usiku mjini Dodoma.
Uwezekano wa kung'olewa kwa vigogo hao ulionekana mapema katika hotuba za wajumbe wa CCM na kauli za hapa na pale za mwenyekiti, Rais Jakaya Kikwete tangu mwanzo wa vikao Ijumaa iliyopita.

Ndani ya CC, Kikwete amenukuliwa akisema, "Kanuni ya chama chetu inataka kila kiongozi anayeshiriki katika masuala yanayotilia mashaka uadilifu wake, haraka ajitoe katika uongozi, asipokubali, basi chama kimtose."

Alisema, "Sitaki kusikia tuhuma za ufisadi katika chama na (madai kuwa) uadilifu wa viongozi siyo tatizo. Hilo ni tatizo na lazima lipatiwe ufumbuzi."

Alitaka wajumbe wa CC kujadili hoja hiyo kwa kina na bila kile alichoita, "Kumung'unya maneno."
Akiwa mzungumzaji wa kwanza baada ya Kikwete kutema nyongo, alikuwa Yusuf Mohammed Yusuf (Mrefu).

Alinukuliwa akisema, "…Chama hiki kina utaratibu wa kulinda haki za wanachama. Tuhuma pekee hazitoshi. Kufanya hivyo (kuwatema watuhumiwa), tutakuwa tunakiuka haki za wanachama wetu."
Katika mjadala wa Jumamosi jioni, kila mjumbe aliyesimama kuchangia, ukiondoa Sophia Simba na wajumbe wengine wawili wa Zanzibar, wote waliunga mkono hoja ya Kikwete.

Hoja ambayo ilikuwa mbele ya wajumbe wa CC wakati huo, ilihusu tathimini ya uchaguzi na maadili ya viongozi wa chama hicho. Iliandaliwa na Profesa Eginald Mihanjo na kada wa muda mrefu, Wilson Mkama.
Miongoni mwa sababu ambazo zilitajwa na baadhi ya wachangiaji kuwa zilisababisha CCM kupata matokeo ambayo haikutarajia katika uchaguzi mkuu, ni migawanyiko iliyoletwa na utaratibu wa kura za maoni.
Sababu nyingine ni "kutoandikwa vizuri" na baadhi ya vyombo vya habari, kampeni kutoratibiwa vizuri na tuhuma za ufisadi dhidi ya baadhi ya viongozi.

Taarifa zinasema, mara baada ya hoja hiyo kuingizwa ndani ya mkutano wa CC, Yusuf akiongea kwa njia ya kutetea watuhumiwa wa ufisadi alisema, "Mwenyekiti tumetoka katika uchaguzi jana tu. Si vizuri kuanza kushughulikiana."

Akichangia hoja hiyo, Bernard Membe alisema, "Utawala wa Roma ulianguka kwa mambo hayahaya ya ufisadi. Tuhuma tu? Tusidanganyane. Tuchukue hatua."

Membe aliwataka wajumbe wenzake wa CC kuacha kupuuza tuhuma zinazokikabili chama chao, badala yake akasema, "Tusitumie kisingizio hicho cha kukosa ushahidi kulinda watu ambao si waadilifu."
Taarifa zinasema hadi hapo hakukuwa na mjumbe hata mmoja aliyekuwa ametaja jina la mtuhumiwa.

Lakini alikuwa Sophia Simba, mtetezi mkuu wa Chenge, aliyesema "Mwenyekiti, haya ni maneno ya magazeti. Kibaya zaidi, magazeti hayo ni yale ya wapinzani."

Akirejea kauli yake ya siku nyingi, kwamba Chenge ameshasafishwa na shirika la upelelezi la makosa ya jinai la Uingereza (SFO) kuhusiana na ufisadi wa rada ya kijeshi, Simba alisema, "Tuhuma zenyewe si za kweli. Ameshasafishwa na SFO."

Kauli ya Simba kwamba Chenge ameshasafishwa na SFO, iliibua mguno na minong'ono kwa wajumbe wa kikao.

Mguno wa wajumbe utakuwa ulitokana na taarifa zilizotangazwa kwa mapana na marefu zikisema Ubalozi wa Uingereza jijini Dar es Salaam, umekanusha na kukosoa kauli ya Simba kuhusu kazi ya SFO.

Mara baada ya Simba kumtaja Chenge, ndipo mtoa taarifa anasema, Kikwete alipata ujasiri wa aina yake na kutoa kauli yenye uthabiti.
"Mimi sitaki unafiki. Nataka tuseme hapa, nani hao mafisadi wanaosemwa. Hatuwezi kukaa hapa kwenye kikao, huku tukiwa tumepewa dhamana na wananchi na wanachama wetu, kisha tunataja watuhumiwa bila kutaja majina."

Akionekana mwenye hasira kali, Kikwete aliuliza, "Hivi tunamdanganya nani? Kwa nini watu wazima tunakuwa wanafiki?"
Kauli hiyo ilimwinua Pius Msekwa, makamu mwenyekiti wa chama hicho Tanzania Bara. Alitaja majina ya Lowassa, Rostam na Chenge.
"Nikiwa mwenyekiti wa Kamati ya udhibiti na nidhamu, majina ambayo yamekuwa yakitajwa na wana-CCM, ni Rostam Aziz, Edward Lowassa na Andrew Chenge."

MwanaHALISI limeelezwa mara baada ya Msekwa kutaja majina hayo matatu, ndipo Kikwete akasema, "Sasa tumeshapata majina na tuendelee. Tuache kumung'unya maneno."

Naye George Mkuchika, aliyekuwa naibu katiku mkuu hadi juzi Jumamosi, akichangia suala hilo, imeelezwa alikumbusha wajumbe sakata la kujiuzulu kwa Ali Hassan Mwinyi.

Mwinyi alijiuzulu uwaziri kutokana na mauaji ya wafungwa katika gereza la Kahama mkoani Shinyanga katika miaka ya 1970.
Mkuchika alisema wakati Mwinyi anajiuzulu alimwandikia Rais wa Jamhuri, Julius Nyerere "…akisema yeye hakushiriki katika mauaji ya wananchi wale. Hakushauriwa wala hakujua. Lakini aliombwa kujiuzulu kwa kuwa hayo yalitokea chini ya utawala wake."

Katika kile kinachoonekana kuwa "liwe na liwalo," Abdulrahaman Kinana, mmoja wa wajumbe wa CC wanaoheshimika, aliamka na kusema yale ambayo baadhi ya wajumbe wamekiri hawakutegemea kusikia yakitoka kinywani mwake.

"Mwenyekiti, vyama vyote makini vya siasa, vinajali na kuthamini uadilifu wa viongozi wake. Suala la viongozi kutoingia katika mambo yanayochafua uongozi wao, na kutilia mashaka, ni masuala muhimu sana. Yasipoangaliwa yatakiathiri chama, tena vibaya sana," amenukuliwa Kinana akisema.

Kinana alisema, "Ufisadi upo. Watuhumiwa wa ufisadi wanajulikana. Hivyo basi, wanapaswa kuwajibika."
Alisema, "Ili tusiendelee kubishana na kubabaishana, ni vema CC na sekretarieti yake vijiuzulu ili kumpisha mwenyekiti kuunda upya kamati kuu."

Pendekezo la Kinana liliungwa mkono na rais mstaafu Mwinyi aliyesema, "Kwanza, naunga mkono hoja ya Kinana ili kumpa fursa rais kupata wasaidizi wapya."

Pili, Mwinyi alinukuu msemo wa kiarabu unaosema, "Ukitembea na mlevi, nawe utaitwa mlevi." Akasema, "Kama kwenye CC kuna mafisadi, basi kuna hatari ya kuathiri hadhi na heshima ya CC."
Akihitimisha hoja hiyo iliyoonekana kupunguza, kwa kiwango kikubwa, kasi ya Lowassa ya kuwania urais, mwaka 2015, Kikwete alisema, "Kinana alisema, ‘Sitaki kuwadanganya.' Nami sitaki mtu anidanganye. Lazima tuimarishe tabia ya wana-CCM kusema ukweli, hasa sisi viongozi."

Alisema, "Ninaafiki uamuzi wa Kamati Kuu kujiuzulu na sekretarieti yake; na mimi mniachie nitaunda Kamati Kuu nyingine na nitaleta mapendekezo NEC kwa lengo la kuijenga upya CCM."
Kikwete alihoji "…nani kati yenu anaweza kwenda kwenye mkutano wa hadhara na kusema hakuna ufisadi na wananchi wakampigia makofi?"
Akiongea kwa sauti ya ukali, Kikwete alisema, "Wote watakaotuhumiwa kwa ufisadi, rushwa na ufujaji wa mali ya umma, nawaomba waanze kujiondoa wenyewe kwenye chama chetu. Iwapo hawatajitoa, chama kiwaondoe…"

Wakati wa mjadala katika Halmashauri Kuu, Jumatatu jioni, wajumbe wawili walioongea mwanzo walikubaliana na uamuzi wa kuvunja Kamati Kuu lakini walipendekeza makubwa zaidi. Walitaka watuhumiwa waachie nafasi za uongozi.

Profesa Mark Mwandosya alisema chama kimedhoofika kutokana na tuhuma za muda mrefu za ufisadi, hoja yake ikishindilia hoja za awali kwamba watuhumiwa wajiondoe kabisa katika uongozi.
Naye Makongoro Nyerere alisema watuhumiwa wakuu watatu "washuke kutoka kwenye jahazi kwa kuwa linazama;" akimaanisha Lowassa, Rostam na Chenge.

Makongoro amenukuliwa akisema, "Rostam ni kaka yangu. Kaka yangu Rostam; kaka yangu Lowassa; kaka yangu Chenge, ondokeni jahazi hili linazama kwa ajili yenu…Kikwete ni rafiki yenu…mtaendelea kuwa marafiki lakini katika hili tuachieni…"
Kushindwa kwa Rais Kikwete kutekeleza alichotamani, wameeleza wachunguzi wa mambo ya siasa, "kumewaponza walioongea kwa uaminifu na uadilifu kwa chama."
Gazeti toleo na. 237

MWANAHALISI
 
:teeth: Ukweli ni kwamba waliotajwa hapo juu hawakujua kwamba kujivua gamba kwa CCM kunge wadhoofisha kihivyo. Kujivua gamba ni kama kumewapa ushindi mkubwa kundi la Sitta na mwakyembe.

Sasa kwa taarifa hawa mabwana wamerudi kwenye drawing board kuangalia wachukue hatua gani kujinusuru. Ikumbukwe wakijiuzulu au wakivuliwa uongozi ndio watakuwa wamekufa kisiasa. Ni ukweli pia kwamba vita hii itakuwa ngumu zaidi kuliko vita dhidi ya Slaa.

Hapa CCM inapigana na adui wa ndani anayeyafahamu yote na hasa wanamfahamu sana JK. Wanajiandaa kufanya mambo mawili. Kwanza kutoa mabomu ili serikali na chama kichafuke ionekana mafisadi si wao tu na pia kwenda mahakamani kuzuia majina yao kuendelea kuchafuliwa.

Mambo yote mawili yatainyongonyesha sana CCM na kufa kabisa. Kwa mawazo yao, ni afadhali kuwasaidia wapinzani washinde kwa mkataba kwamba hawatawabughuti kuliko kumwachia mtu wa CCM ashinde. Tutaona mengi ila sioni CCM kama watatoka salama katika hili maana akina Lowassa wana ufuasi mkubwa mno ndani ya chama na huko kujivua gamba kunapingwa sana na wanachama walio wengi.


Chadema ni muda muafaka wa kuvuna zaidi ndani ya mgogoro huu. Hoja kubwa ya kuitumia ni kwamba hawa jamaa wameiibia serikali si CCM. Kama CCM wanakiri hawa ni mafisadi wawapeleke mahakamani bila hivyo bado CCM inawalinda mafisadi.

Onyesheni hasara serikali inapata kwa ufisadi na mambo ambayo yangeweza kufanywa na pesa hizo. Zungumzeni pia nyie mtafanya nini mkishinda hasa katika vita ya ufisadi. Ipigeni CCM pressure msiwape punzi. Wataendelea kuweweseka maana wanapigana vita katika front mbili.

Front ya ndani ambayo ni ngumu zaidi na front ya nje. Pia mjiandae ku attack sera zao hata kama wamejivua gamba bado sera zao ndio zinatutia umaskini. Fuatilieni ahadi zao na mpige kelele, mbona hazitekelezwi na kuonyesha hawa ni waongo.

Mkienda mikoani kwenye mikutano msizungumze sana, wapeni watu nafasi waulize maswali na kutoa maoni. Mkijua watanzania wanataka nini basi yatumieni maoni na maswali yao kupiga kele huko juu hasa bungeni ili waone nyie ndio watetezi wao. Mkipigana vizuri 2015 mtashinda kwa kishindo. :hug:
 
Lowassa na wafuasi wake kiama chao kimefika japo hawana macho ya kuona na bongo zao zatazama zaidi urais wa 2015.
mlio karibu nao waambieni kwani waazidi poteza nguvu na resourses bure kwa jambo litakaloshindwa.
 
Makongoro amenukuliwa akisema, "Rostam ni kaka yangu. Kaka yangu Rostam; kaka yangu Lowassa; kaka yangu Chenge, ondokeni jahazi hili linazama kwa ajili yenu…Kikwete ni rafiki yenu…mtaendelea kuwa marafiki lakini katika hili tuachieni…"

Ndio kusema kama jahazi lisingezama mngewaacha? Nyie hamjali masilahi ya Taifa mnajali kutawala tu?
Hamtudanganyi.
 
KAMA KWELI MANENO HAYA YALITAMKWA KWENYE KIKAO BASI KIKAO KILIKUWA CHA KISHKAJI SHKAJI TU. Hakukua na seriousness yoyote hapo.
 
hakuna mnafiki kama jk..............ni juzi tu mwezi wa kumi amepita kwenye majimbo ya hawa watu na kuwanyanyua mikono kuwa ni wasafi......leo anajifanya kusema hawa watu ni wabaya watupishe............kama kweli hawa jamaa watatoka ccm walahi huyu hamalizi mda wake uliobaki
 
hahaaa JK bwana sasa yeye mwenyewe mbona kashindwa kuwataja hao...hikli jamaa bwana sio kabisa
 
UUUUWIIIIII!!! km bado kuna mwenye akili timamu na anaendelea kushabikia chama cha magamba mie siiimo.
 
hakuna mnafiki kama jk..............ni juzi tu mwezi wa kumi amepita kwenye majimbo ya hawa watu na kuwanyanyua mikono kuwa ni wasafi......leo anajifanya kusema hawa watu ni wabaya watupishe............kama kweli hawa jamaa watatoka ccm walahi huyu hamalizi mda wake uliobaki


Kwakweli JK mnafiki sana, ila mimi binafsi napenda unafiki wake kwani unasaidia kwa namna moja kuimaliza ccm na kuinua ufahamu wa watanzania, wengi sasa wanataka kuona mafisadi wakikamatwa lakini kwa jinsi jamaa alivyo wataishia kupoteza nyadhifa zao tu na hapo ujue wadanganyika kuna watakalojifunza
 
ndio maana zitto alimwambia yule mwenyekiti wa cdm aliehamia ccm anahamia chama kinachokufa akina lowasa wakisimama kidete kwenye hili ccm mazishi yamekaribia wao kazi ni moja tu kumwaga mboga tu
 
Kwanza ni vigumu kwa hawa ambao napenda kuwaita " the three musketeers" kuweza kupambana uso kwa uso na CCM wakashinda hasa katika hili joto kali la suluba. Wakijaribu watafukuzwa kwenye chama na hivyo kupoteza ubunge. Wakijaribu kujiaunga na vyama vingine kwa wakati huu hakuna chama kitawataka maana ni mzigo (liability) maana hakuna chama kinaweza kuwabeba "mafisadi". Kitu ambacho wanaweza kufanya ni kusubiri hadi 2015 na kuleta fijo zao dhidi ya CCM maana hawatakuwa na kitu cha kupoteza. Nionavyo mimi ni rahisi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko EL kupata ugombea urais kwa tiketi ya CCM. He is damaged goods now.
 
sitaki kuamini haya..EL ana roho kama ya paka ...ni mgumu sana kushindwa mambo na ana ngozi ngumu sana kuhimili mikwaruzo
 
Kwanza ni vigumu kwa hawa ambao napenda kuwaita " the three musketeers" kuweza kupambana uso kwa uso na CCM wakashinda hasa katika hili joto kali la suluba. Wakijaribu watafukuzwa kwenye chama na hivyo kupoteza ubunge. Wakijaribu kujiaunga na vyama vingine kwa wakati huu hakuna chama kitawataka maana ni mzigo (liability) maana hakuna chama kinaweza kuwabeba "mafisadi". Kitu ambacho wanaweza kufanya ni kusubiri hadi 2015 na kuleta fijo zao dhidi ya CCM maana hawatakuwa na kitu cha kupoteza. Nionavyo mimi ni rahisi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko EL kupata ugombea urais kwa tiketi ya CCM. He is damaged goods now.

Kila mara tumekuwa tumekuwa tukiwatahadharisha viongzi waioko madarakani kuacha ushabiki wa Katiba mbovu. Laiti kama Katiba ya Tanzania ingekuwa inaruhusu mtu kuhama chama na akaendele na ubunge wake kama ilivyotokea Kenya wangekuwa na uwezo zaidi wa kupambana. Hii ni wake up call kwa wanasiaisa wote kutengeneza level playing field which might one day help you.
 
Back
Top Bottom