Dilunga
JF-Expert Member
- Apr 8, 2009
- 679
- 49
Kwa hili Kikwete apongezwe na kuigwa...Rais Kikwete apima macho hospitali ya Muhimbili
Patricia Kimelemeta na Devotha John
RAIS Jakaya Kikwete jana alifanyiwa uchunguzi wa macho na kutibiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Mwananchi ilinasa habari hizo kwenye Hospitali ya Muhimbili na baadaye kuthibitishwa na afisa uhusiano wa hospitali hiyo, Aminiel Aligaisha kuwa Rais Kikwete alikwenda hapo kuchunguzwa macho.
Rais Kikwete alifika hospitalini hapo majira ya saa 5:30 asubuhi na kuingia vyumba namba 44 na 46 ambako alikutana na madaktari na kupatiwa huduma.
Kwenye chumba namba 44 ndiko mkuu huyo wa nchi alipimwa macho na baadaye kuingia chumba namba 46 ambako alipewa miwani na kupata ushauri.
Wakati Rais akiwa anahudumiwa, huduma kwa wagonjwa wengine wa macho katika vyumba hivyo, zilimama kwa muda.
Afisa habari wa Muhimbili, Aminiel Aligaisha alisema hiyo si mara ya kwanza kwa Rais Kikwete kupatiwa matibabu kwenye hospitali hiyo kubwa kuliko zote nchini.
Alisema mara kadhaa Rais Kikwete hufika hospitalini hapo kuchukua vipimo na kutibiwa na hivyo si jambo la ajabu kwa wale wanaofahamu utaratibu huo wa rais.
Baadhi ya wagonjwa waliozungumza na gazeti hili hospitalini hapo walieleza kufurahishwa na kitendo cha Rais Kikwete kutumia hospitali za hapa nchini kupata matibabu.
Walisema utaratibu wa baadhi ya viongozi kwenda kutibiwa nje ya nchi si mzuri hasa kwa nchi maskini kama Tanzania.
"Tunapomwona rais wetu anakuja kutibiwa kwenye hospitali ya hapa nchini, tuna imani kwamba anajali wananchi kwa sababu tunaamini kuwa viongozi wengi wanatumia hospitali za nje kupima afya na kupata matibabu," alisema Musa Abdalah.
Aliongeza kusema: "Hali hiyo imeonyesha uzalendo wa kweli ambao viongozi wengine wanapaswa kuiga kwa maendeleo ya nchi na watu wake."
Ujio wa rais kwenye hospitali hiyo jana ulikuwa wa kawaida ikilinganishwa na misafara yake mingine wakati anapokuwa anafanya ziara za kikazi.
http://mwananchi.co.tz/newsrids.asp?id=14209