Kijarida cha CHECHE kilivyowasha moto hapa nchini...Hapakukalika pale UDSM!!!

eliesikia

JF-Expert Member
Oct 29, 2010
787
755
KATIKA hali iliyovuta hisia za wasomi na wanazuoni, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Sayansi ya Tiba Muhimbili (Muhas), Profesa Karim Hirji amesema hana imani na viongozi wote wa serikali akiwemo Rais Jakaya Kikwete.Profesa Hirji alitoa kauli hiyo jana katika Maadhimisho ya Sherehe za Uhuru wa Tanzania Bara zilizoandaliwa na Taasisi ya Kigoda cha Mwalimu Julius Nyerere cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kufanyika chuoni hapo.

Profesa Hirji ambaye alikuwa Mwasisi na Mhariri wa kwanza wa Jarida la Cheche lililochapishwa na Jumuiya ya Wanafunzi wa Mstari wa Mbele katika Ukombozi wa Afrika (Usaaf) ya UDSM ambalo alilifungwa na serikali ya awamu ya kwanza, alisema hana imani na rais, mawaziri na wabunge kwa kuwa mioyo yao imejaa ubinafsi, ubepari, ubeberu na ukoloni mamboleo.

Prof Hirji alikuwa Mhariri Mkuu wa Jarida la Cheche ambalo wajumbe wa bodi yake ya uhariri walikuwa Zakia Meghji, Henry Mapolu, George Hadjivyanis na Balozi Christopher Liundi.

Bodi hiyo ya uhariri iliyosambaratika baada ya jarida hilo kufungwa, imetunga kitabu kinachoitwa Cheche kilichocapishwa mwaka huu (2010) ambacho jana na Mwenyekiti wa Umoja wa Wahadhiri wa UDSM (Udasa) Dk Adolph Kibogoya.
Kitabu hicho chenye sura 12 na zaidi ya kurasa 200 ambacho dhana yake kuu ni kuendeleza mawazo ya gazeti la Cheche ya kuendeleza mapambano ya kweli ya ukomboi wa Afrika kimeandikwa na watu mbalimbali akiwemo Profesa Hirji, Rais Yoweri Museveni wa Uganda.
Wengine ni Prof Hajivayanis, Mapolu, Liundi na Zakia Meghji aliyeandika Sura ya Sita ya kitabu hicho kuhusu historia ya Zanzibar na fikra za kimapinduzi ambazo baadhi ya Wazanzibari walijengeka kwazo.

Akizungumza katika hafla hiyo Profesa Hirji alisema: “Leo kiongozi wa nchi (Kikwete) anasema eti ili aweze kuwapatia wananchi vyandarua lazima twende kuomba msaada Marekani. Mimi naona hilo ni jambo la aibu kubwa".

Aliongeza: “Baada ya kuangalia mambo haya kwa muda mrefu, mimi binafsi nimepoteza imani na viongozi wetu wote nchini na katika bara la Afrika. Nimepoteza imani na marais, mawaziri, wabunge na viongozi wengine wote wa kisiasa, kiuchumi na kijamii".

Ingawa Profesa Hirji hakumtaja kiongozi yeyote, mifano yake imeonyesha kuwa amekuwa akiilenga serikali ya Rais Jakaya Kikwete iliyokuwa madarakani tangu mwaka 2005.

Profesa Hirji ambaye amewahi kufundisha UDSM katika miaka ya 1960, baadaye aliwageukia wasomi wenzake akisema nao wametawaliwa na ubinafsi, ubepari, ubeberu na ukoloni mambo leo.

Alisema katika jamii yenye matatizo mengi kama Tanzania, kazi kubwa ya wasomi ni kutumia taaluma na ujuzi wao kuonyesha njia zinaoweza kuleta ukombozi na maendeleo lakini hali hiyo ni tofauti kwa Tanzania ambako wasomi wanajali zaidi maslahi binafsi.

“Sisi wasomi wa Tanzania kwa sababu tumetawaliwa na fikra na vitendo vya ubinafsi, ubepari na ukoloni mambo leo, tumeamua kukaa kimya,” alisema Profesa Hirji na kuongeza:

“Tunakimbilia marupurupu ya wahisani, kamwe hatuna moyo wa kujitolea na kujenga nchi. Hata ukiitisha mkutano wa wasomi bila ya kutoa posho na marupurupu au chakula, hakuna atakayehudhuria”.

Huku akishangiliwa na kupigiwa makofi na mamia ya watu waliohudhuria sherehe hiyo, Profesa Hirji aliendelea kusema: “Hata kama tunahudhuria mikutano katika hoteli za kifahari, matokeo yake hayana maana yoyote katika maendeleo ya jamii.”

Alisema maprofesa na wahadhiri wa vyuo vikuu, wanavaa suti na tai lakini mawazo yao kwa kiasi kikubwa, yamepitwa na wakati.

“Ndio maana mimi binafsi pia nimepoteza imani na wasomi wetu waliopata shahada za juu, maprofesa, wahadhiri na viongozi wa vyuo vikuu waliopo hapa na wasiopo. Nawaheshimu lakini sina imani na kazi, tafiti na uongozi wao," alisema Profesa Hirji

Katika mkutano huo uliohudhuriwa na maprofesa na wahadhiri kutoka vyuo mbalimbali nchini, Profesa Hirji alisisitiza kuwa hawezi kuwategemea kabisa kuelekeza nchi katika njia ya kujitegemea, kujenga usawa, kulinda haki za watu wa kawaida na kuleta maendeleo halisi na ya haraka.”

“Mawazo yetu (wasomi) yametawaliwa zaidi na njia za kujilimbikizia mali. Tafiti zetu ni za kijuujuu. Tunafundisha mambo ya kuigaiga na hata kazi ndogo kama hizi wengi tunakwepa kuzifanya swasawa," Prof Hirji alisema na kuongeza:

“Sioni msomi anayeuliza maswali magumu, anayekosoa mfumo wa ubepari na ukoloni mamboleo, anayesema wazi kuwa ujamaa ndio njia pekee ya kuleta amani, haki na maisha ya Watanzania, kama wapo ni mmoja au wawili.”

Profesa huyo alisema mambo hayo yanahitaji kufikiriwa kwa undani, kufanyiwa utafiti na uchunguzi wa dhati wa kitaaluma na kwamba kama wasomi hawatakuwa mstari wa mbele katika jukumu hili, hakuna atakayelifanya.

Hata hivyo, Profesa Hirji alisema hajapoteza imani na kundi kubwa la vijana nchini akiamini kuwa wana mioyo na mwelekeo safi ambao haujachafuliwa na fikra na vitendo vichafu vya ubepari na ukoloni mamboleo.

“Ndio maana naona ni jukumu lao kuungana, kujielimisha kwa nguvu zao zote, kuanzisha vikundi vya kujisomea na kuanzisha magazeti yatakayochambua ukweli wa mambo, kuuliza maswali magumu na kufafanua mbinu za kujikomboa kwa wananchi,” alisema.

Awali profesa Hirji alitaja misingi ya Gazeti la Cheche kuwa ni pamoja na ukombozi halisi wa Afrika hauwezi kupatikana bila ya siasa ya vitendo ya ujamaa. “Tanu chini ya Nyerere ilikuwa na maneno matamu lakini ilikuwa na mapungufu mengi katika vitendo. Cheche ya leo pia inasema hayohayo.”

Msingi wa pili alisema ulikuwa ni ukombozi halisi wa Afrika utapatikana kwa jasho na juhudi Waafrika wenyewe na sio mabepari.

“Hatuwezi kutegemea mabepari na mabeberu katika hili. Siku hizi wanaitwa wawekezaji na wahisani, huo ni udanganyifu, hao wote wanataka kuendelea kuiba rasilimali zetu. Lazima tuungane na kuwaondoa mabeberu wanaoiba mali zetu,”alisema.

Alifafanua kuwa, msingi mwingine wa Cheche ya zamani ni kuheshimu ukweli na kusema ukweli bila kumwogopa au kumhofia kiongozi au mtu yeyote kwa maslahi ya maendeleo ya taifa.

“Msingi wa nne wa Cheche ya zamani ulikuwa ni kujitegemea na msingi wa tano ulikuwa ni umuhimu wa kujielimisha katika masuala na fikra za kisayansi na ukombozi,” alisema Hirji.

Kwa upande wake aliyekuwa Mhariri wa Jarida hilo Zakia Meghji alimpongeza Profesa Hirji kwa hotuba yake hiyo na kusema ameonyesha kutobadili msimamo aliokua nao tangu alipoanzisha jarida hilo.

“Hongera profesa Hirji Wewe ni yule yule wa miaka 1960,” alisema Meghji.

Mshiriki wa sherehe hiyo Dk Salim Msoma aliyepewa nafasi ya kufanya mapitio ya kitabu hicho alipinga baadhi ya mambo katika kitabu hicho akisema yanapotosha vijana.

Alisema katika sura ya kwanza ya kitabu hicho cha Cheche, mwandishi ambaye ni Prof Hirji amezungumzia dunia ya ujamaa huku akizigusa nchi za Urusi na China.

“Katika hili mimi napinga kabisa. Hakuna kitu dunia ya ujamaa hivi kuna mjadala mkali katika hili. Wasomi wameandika vitabu vingi kuhusu jambo hili kwa hiyo mambo kama haya yanaweza kupotosha na kudanganya vijana wetu,” alisema Dk Msoma.
 
Hii Ndio Aina ya wanafunzi wa Elimu ya Juu tunaitarajia na wote Kikwete ,,..Sitta..Warioba ...etc ..Siasa Zao Za chuo hazikuwa ...zikifungamana na system ..
Ukimaliza chuo utaiva ...na unaweza kujiunga na system ......Sasa kama msomi ..unanunuliwa ...mwanaume mzima ...kilichobaki ni nini ??? Tumekumbwa na nini???? Tunapenda dezoooo ...au ...
wasomi hawataki hoja Za kufikirushaaaa...wasomi hawahoji yanayotokea...

INABIDI PUNCH ARUDI VYUONI ILI KUWAFUNZA WAPENDA DEZO ...HUKATAZWI KUWA CCM AU CHADEMA AU CUF...BALI USIWE MTUMWA WA FIKRA ...USIWE MCHUMIA TUMBO .....HAPA MJINI UKIPENDA SANA BURE NI TABU ....
 
Uzi unaoishi...pamoja na kwamba watu hawasemi neno kwa zaidi ya miaka 4!! Ukweli mtupu
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom