Kibanda: Kinana ni Kimbunga

Molemo

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
14,534
13,225
Mhariri Mkuu wa gazeti la Tanzania Daima Absalom Kibanda baada ya wiki iliyopita kuibuka na Makala isemayo NAMUOGOPA KINANA iliyokuwa ikimwagia kila aina ya Sifa, leo hii ameibuka na makala nyingine ya kumsifu Katibu mkuu huyo wa CCM huku akiponda mashabiki na wanachama wa CHADEMA kwamba ni walevi wa Fikra na anatabiri Kimbunga cha Kinana kwa CHADEMA kitakuwa 2015....Endelea.........


YAKO mambo ya msingi katika maisha ya kitaaluma katika fani zote za kielimu ambayo mtu yeyote anayetambua na kujali vyema wajibu wake anapaswa kuyasimamia na kuyalinda hata kama atafanya hivyo kwa gharama ya kupoteza maisha, kuchukiwa, kudharauliwa au kupuuzwa.

Moja ya mambo ya namna hiyo ni miiko ya kitaaluma ambayo aghalab huongoza na kujenga misingi ya uwepo na kustawi kwa kila fani iwe ni sheria, elimu, uaskari, uhandisi na hata ukachero.

Uandishi wa habari ni moja ya taaluma ambazo zina miiko na maadili yake. Zaidi ya hayo uandishi wa habari na waandishi wa habari wanaishi kwa kufuata na kuzingatia miongozo yao ya kikazi na kitaaluma.

‘Ukweli' ni moja ya misingi mikuu ya uandishi wa habari. Huu unaweza ukawa msingi mama katika taaluma hii adhimu. Ni kwa kuzingatia hilo ndiyo maana uandishi wa habari unatajwa na magwiji wa taaluma hii kuwa ni ‘noble profession'.

Naandika maneno haya huku nikitambua kwa dhati kwamba, mara kadhaa wanahabari wa hapa nchini na kwingineko duniani tumekuwa mstari wa mbele katika kukiuka msingi na muongozo huo muhimu kitaaluma kwa kujua au kutojua, kwa kukusudia ama kwa bahati mbaya.

Pamoja na mapungufu hayo ya kibinadamu katika taaluma hii ambayo siku zote nitabakia kuwa mwanafunzi wake, uandishi wa habari unaendelea na utaendelea kubakia kuwa mhimili wa nne wa dola baada ya serikali, Bunge na Mahakama.

Iwapo hivyo ndivyo, uandishi wa habari ni taaluma ambayo inao wajibu wa kusimama juu ya taaluma zote nyingine ambazo aghalab kwa nafasi zao hakuna hata moja ambayo imepata kuchukua taswira ya mhimili kama ilivyo kwa uandishi wa habari.

Kwa sababu hiyo basi, kama ilivyo kwa mihimili mingine ya dola, taaluma hii inao wajibu wa kukubali changamoto zinazoelekezwa kwake na wakati mwingine kuchukua maamuzi ambayo yanaipa mamlaka na taswira halisi ya kuonekana kuwa ni mhimili unaojitegemea kifikra, kimatendo na hata kimaadili.

Nimelazimika kuyasema yote haya katika utangulizi wa makala yangu ya leo kutokana na kile ambacho kilitokea wiki iliyopita baada ya safu hii kuwa na makala iliyokuwa na kichwa cha habari kisemacho: "Namuogopa Abdulrahman Kinana".

Makala ile ilibeba ujumbe rahisi kabisa. Kwanza mbali ya kueleza kwa sehemu tu kuhusu wasifu wa Kinana kwa mtazamo wa mwandishi wa safu hii ambaye ni mimi mwenyewe, ilieleza kwa muhtasari tu sababu ambazo zilimfanya Rais Jakaya Kikwete hatimaye akubali yaishe kwa kumfanya mwanasiasa huyo abebeshwe jukumu la kuwa Mtendaji Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Kama hiyo haitoshi, makala ile ilieleza kwa maneno yaliyo wazi kabisa kwamba, CCM ilikuwa ikichungulia kaburi na kimsingi mwenendo wa mambo katika kipindi cha miaka michache tu iliyopita hadi sasa ilikuwa ikichukua mwelekeo wa wazi wa kupoteza madaraka ya dola.

Ni kwa bahati mbaya sana kwamba, mashabiki wa vyama vya upinzani ambao siku zote wamekuwa hodari kushangilia hoja zetu za kuikosoa serikali au kuisuta CCM na viongozi wake kwa kuwaangusha Watanzania katika maeneo kadha wa kadha walipatwa na hasira kali waliposoma makala ile na kuona ikiwa na harufu ya kumsifu au kueleza uwezo wa kimikakati, kiutawala, kisiasa na kiintelijensia aliokuwa nao Kinana na pengine safu ya uongozi mpya wa chama hicho tawala iliyoundwa wiki mbili zilizopita.

Kwa sababu tu ya kulemewa kwao na ulevi wa chuki walizoijengea CCM na viongozi wake pasipo hata kuangalia muktadha wa makala ile, wadakuzi hao wa mambo kupitia katika mitandao ya intaneti, majukwaa ya jamii, ujumbe wa maandishi na kwenye simu yangu ya kiganjani na hata kwa njia ya ana kwa ana wakanisuta na kunitukana kila aina ya matusi ili kukidhi matakwa yao.

Lile kosa la wanasiasa na wapambe wao kukosa ustahimilivu ambalo tumekuwa tukiwahusisha nalo watawala, likachukua sura na mwelekeo tofauti.

Siri zikafichuka kwamba ndani ya mioyo ya baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani, wafuasi na mashabiki wao kulikuwa na hulka za hatari za udikteta ambazo ama zinalingana na zile walizonazo baadhi ya wana CCM na viongozi kadha wa kadha wa kiserikali.

Niseme wazi na kwa kujiamini kabisa kwamba, sikutishwa wala kubabaishwa na matukio hayo ambayo kwangu hayakuwa mageni hata kidogo kwani yalifanya kile ambacho nimekuwa nikikabiliana nacho tangu mwaka 1993 wakati nilipoanza kushiriki kikamilifu kuandika makala katika magazeti mbalimbali nchini na wakati mwingine kutoa maoni na mawazo yangu kwa viongozi mbalimbali wa kisiasa.

Haraka haraka hoja za kishabiki zilizokosa weledi ambazo zilikuwa zikivurumishwa na manazi hao wa kisiasa zilinikumbusha ujasiri niliokuwa nao mwaka 1995 wakati niliposimama imara kupinga mhemko wa kitaifa wa "Homa ya Augustine Mrema" ambayo ililitikisa taifa kwa kiwango cha kumchanganya akili Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Nilikuwa na ujasiri aliokuwa nao Jenerali Ulimwengu wa kumpinga Mrema katika maandishi na hata katika majukwaa ya mijadala.

Bado nakumbuka vyema namna nilivyosafiri kwa daladala kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam nilikokuwa nikisoma hadi Kariakoo zilizokuwa ofisi za NCCR Mageuzi na nikapata fursa ya kuwafikia Mabere Marando na Ndimara Tegambwage nikiwaomba watafakari upya uamuzi wao wa kumpa Mrema dhamana ya kuongoza harakati ghali za mageuzi katika taifa hili.

Makala nilizoandika katika magazeti ya Rai, Mtanzania, Wakati Ni Huu, Nipashe na kwingineko katika kipindi hicho cha 1995 na 1996 ambazo aghalab zilikuwa zikiwaasa Watanzania kupima mambo kwa kina badala ya kutukuza na kuendekeza ushabiki wa kisiasa ni ushahidi wa wazi wa kile ambacho nilikuwa nikikisimamia na nimeendelea kukisimamia siku zote.

Haikupita hata miaka miwili kabla ukweli wa kile nilichokuwa nikikizungumza na kukitetea kwa njia ya maandishi kuthibitika.

Mrema alifanya kile nilichokiona mapema, akawaangusha aliowaongoza na kuwaporomosha wale waliofikia hatua ya kumuabudu kwa kiwango cha kumuona mkombozi wao wa kisiasa.

Kama ilivyokuwa kwa Mrema mwaka huo huo wa 1995, nilikuwa miongoni mwa wanahabari ambao tulimpinga kwa hoja Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere katika harakati zake za kulazimisha aliyekuwa mgombea wake, Benjamin Mkapa, ateuliwe na kuwa mgombea wa urais wa CCM.

Katika hili, sikukubaliana na kile ambacho Jenerali Ulimwengu na wenzake walikitetea. Ingawa nilikuwa mpinzani mkubwa wa Mrema, sikufurahishwa hata kidogo na uamuzi wa Baba wa Taifa kupandikiza hulka za kidikteta katika kuchakachua mchakato wa urais kupitia katika tanuri la chama hicho tawala.

Kilichotokea miaka 10 baada ya Mkapa kustaafu urais mwaka 2005 ni ushahidi wa wazi wa kile ambacho baadhi yetu, japo hatuna majina makubwa tulikiona mapema.Rais huyo pamoja na kuonekana kwamba alikijengea heshima kiti cha urais na kuinunua harufu ya maendeleo ya kiuchumi, alifisha hata ndoto za ‘mentor' wake Mwalimu Nyerere. Hili linahitaji mjadala unaojitegemea.

Sikuishia hapo, mwaka 2005 wakati taifa na fani nzima ya habari ikiimba wimbo wa Kikwete, Kikwete Kikwete katika misingi ya ushabiki unaofanana na ule unaotokea leo, nilikuwa miongoni mwa waandishi wachache ambao tulikataa kuimba wimbo huo huku tukitoa tahadhari za waziwazi kuhusu hatari ambayo ilikuwa ikilinyemelea taifa.

Ingawa wakati huo nilikuwa Mhariri wa gazeti la Mwananchi Jumapili ambalo mmoja wa wakurugenzi wake alikuwa Rostam Aziz aliyekuwa katikati ya kitovu cha kampeni za Kikwete, nilikataa kuwa bendera fuata upepo na nikaandika mada kadha wa kadha kuhoji kuhusu uwezo wa mwanasiasa huyo kupewa dhamana ya kuongoza nchi.

Ushahidi wa kile nilichoandika kuhusu hilo uko wazi kabisa. Nilitenda na kutoa msimamo tofauti kabisa na ule waliokuwa nao baadhi ya wahariri na waandishi wa habari wa zama hizo kuhusu nafasi ya Kikwete katika kuliongoza taifa hili.

Hata yeye mwenyewe alipotangaza uamuzi wa kugombea urais kule Chalinze nilikuwa miongoni mwa wahariri na wanahabari ambao tulikwenda na kumuuliza maswali magumu kuhusu kugombea kwake.

Alipoteuliwa na chama chake kuwa mgombea kama ilivyotarajiwa na wengi, nilitafuta fursa na nikafanya naye mahojiano nyumbani kwake Dodoma nikiwa nimeongozana na mwanahabari mwenzangu, Nyaronyo Kicheere, aliyekuwa Mhariri wa Habari wa gazeti dada la The Citizen on Sunday.

Niliendelea na msimamo ule juu ya Kikwete kabla na baada ya kuteuliwa kwake kuwa mgombea urais. Waandishi na wahariri waliokuwa pale ni mashahidi wazuri kwamba, msimamo wangu huo ulipata kusababisha Rostam afikie hatua ya kueleza waziwazi kukerwa nao.

Mara kadhaa aliniita nyumbani kwake akijaribu kunishawishi na kuniaminisha kwamba Kikwete alikuwa ni mwanasiasa hodari na anayeweza kuliongoza taifa hili pengine kuliko mwingine yeyote.

Kilichotokea baada ya hapo kila mtu anakijua, Kikwete alishinda kwa kishindo na baadhi yetu ambao tulionekana kuwa vimbelembele kuhoji uwezo wake tukasutwa kweli kweli kwa kiwango cha baadhi ya wanahabari wenzetu kutuona wendawazimu.

Kwa sababu ya kuendekeza hulka za kishabiki, wanahabari tulishindwa kumuandaa Kikwete kuwa rais bora, tulimnyima fursa ya kujipanga kifikra na kifalsafa na tukaiacha ajenda ya urais iandaliwe kimkakati na kiintelijensia zaidi. Hiki tunachokiona leo ni matokeo ya kuendekeza ushabiki wa namna hiyo.

Ni jambo la bahati mbaya kwamba kile kilichotokea mwaka 1995 na baadaye mwaka 2005 bado kinaonekana kutofundisha Watanzania. Hulka za kinazi na kishabiki katika masuala ya msingi bado zinaendelea kutafuna vichwa vyetu.

Taifa zima linaimba wimbo mmoja tu, Slaa, Slaa, Slaa. Halitaki kusikia lolote. Ukimgusa Dk. Slaa tena kwa hoja za kumtahadharisha, kumuonya au hata kwa minajiri ya kumfanya ajiandae kukabiliana na kimbunga kama hiki cha Kinana, mashabiki wake wanalipuka kwa jazba na kwa hamaki kubwa.

Ukithubutu kuikosoa CHADEMA au kumgusa yeyote miongoni mwa viongozi wake kama nilivyofanya miaka mitatu au minne iliyopita wakati nilipopinga uamuzi wa Zitto Kabwe kugombea uenyekiti wa taifa wa chama hicho kwa sababu muda wake ulikuwa bado, idadi ya matusi utakayovurumishiwa kama ni mtu ambaye una moyo mwepesi unaweza ukaacha kuandika.

Hivi ndivyo ilivyokuwa wiki iliyopita wakati nilipowaonya wapinzani kukaa chonjo na Kinana kwani kimbunga ambacho alikuwa akielekeza kukipuliza kuelekea upande wa kambi ya upinzani kinaweza kusababisha upepo unaovuma sasa kubadili njia.

Sitaki kujifanya mimi ni nabii wa siasa za Tanzania. Hata hivyo bado naendelea kuamini na kusisitiza kwamba, Kanali Mstaafu Abdulrahman Kinana si mtu mwepesi, si mwanasiasa wa kumbeza wala kumpuuza.

Kama CHADEMA na mashabiki wanataka kupima kina cha maji kwa sababu tu ya ulevi wa fikra, basi wanao uhuru wa kufanya hivyo. Tusubiri fainali 2015. Huko ndiko tuendako.
 
Hayo ni maoni na mtazamo wake.

Ana haki ya kusema/kuandika kile anachokiamini. Lakini angetuelimisha zaidi kama angejadili 'mfumo' wa chama anachokiongoza Kinana pamoja na serikali yake na hatima ya nchi badala ya kujadili mtu in his personal capacity.

Tunasubiri makala nyingine ya mwelekeo wa siasa za tz na hatima ya Tanzania.
 
"Siri zikafichuka kwamba ndani ya mioyo ya baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani, wafuasi na mashabiki wao kulikuwa na hulka za hatari za udikteta ambazo ama zinalingana na zile walizonazo baadhi ya wana CCM na viongozi kadha wa kadha wa kiserikali".

Sasa naamini Kibanda ana matatizo, anaweza kutoa mfano wa huo udikteta? Haya maneno ya reja reja anayatoa wapi huyu!
 
Walikuwepo wengi wa hivyo wakapita, huyu naye atapita; Na mbwembwe zake zitapita, na uandishi wake Utapita.

Lakini kitu kimoja tu ambacho hakitapita ni UKWELI

Kweli ya Mungu Itabakia na hakuna Changanya changanya
 
anaomba msamaha,anaponda humohumo,anasifia humo humo..kesi inayomkabili imemfanya anunulike kirahisi sana,mwoga wa jela huyu.,anachonikera zaidi ni kujifanya genius kuliko wote sababu alisoma HGL.
amenunuliwa kwa bei nafuu sana,!!kibanda usiogope kwenda jela kwa kesi inayokukabili kama alivyofanya yule wa mwananchi na tume ya mwangosi..kwenye msafara wa mamba na kenge kama kibanda wamo
 
ccm ilikofikia imebakiwa na mbinu moja tu ya kuwabakisha madarakani, ambayo ni kutumia vyombo vya dola, Polisi, usalama wa Taifa na JWTZ. Kama ni kimbunga basi kimbunga pekee kinachoweza kuwakumba na kuwasomba wanamageuzi na wapinzani kwa ujumla ni hivyo vyombo vya dola na si vinginevyo.

Hizi ndoto za Kibanda kwamba kinana ni kimbunga wacha aendelee kuota mwenyewe sisi huko tulishaondoka siku nyingi. Huwezi kumfananisha hata kidogo Augustine Mrema na Dr. Slaa, hawa ni watu wawili walio mbali sana kiuwezo na kwa muono. Yeye aendelee tu kula matunda ya kumsafisha Lowasa na sasa kumjenga Kinana kwakuwa si haba anajipatia ujira wake na kuweza kusukuma mbele gurudumu la maisha na familia yake, lakini atambue kitu kimoja kwamba ccm ilipofikia hakuna mganga yeyote anayeweza kuinusuru na anguko kuu mwaka 2015, si kinana wala vinana!!
 
Last edited by a moderator:
Kila mtu na mawzo yake, kumsifia kinana au kumwogopa kwa kuwa tu anashinda kwa kura za wizi na kuwaza kuwaletea viongozi uchwara si maendeleo ni wazo pia la kuogopa. Tunahitaji kujipanga ndiyo (CHADEMA) ILA CCM HAITUFAI
 
Tanzania ni nchi ya kidemokrasia ambayo inaruhusu kila mtu kutoa mawazo yake ili mradi havunji sheria,mawazo ya Kibanda yamefikia na kuishia hapo,ndio utashi wake ulipo,tunaweza kumlaumu sana kuhusu makala yake ambayo kwa mtazamo wa wengi haijakaa vizuri.
 
''Niliendelea na msimamo ule juu ya Kikwete kabla na baada ya kuteuliwa kwake kuwa mgombea urais. Waandishi na wahariri waliokuwa pale ni mashahidi wazuri kwamba, msimamo wangu huo ulipata kusababisha Rostam afikie hatua ya kueleza waziwazi kukerwa nao.

Mara kadhaa aliniita nyumbani kwake akijaribu kunishawishi na kuniaminisha kwamba Kikwete alikuwa ni mwanasiasa hodari na anayeweza kuliongoza taifa hili pengine kuliko mwingine yeyote''

Kwa kipimo hicho hicho, je Mhe Mbowe Freeman (mmiliki wa TD) ameshakuita kama alivyofanya Rostam Aziz?
 
Acheni kumpa huyu kanjanja umaarufu asio stahili; please ignore him with all the contempt he desreves. anapalilia ukuu wa wilaya; but he is in for a rude shock.

Karibuni tutaona makala zake nyingi zenye titles kama: Kinana dume la mbegu au Kinana mwanaume wa shoka! au Kinana muarobaini wa wapinzani!

Kwa wenye akili wameshaelewa hamasa na motisha Kibanda kuandika makala hizo unatokana na nini! Huyo ni mchumia tumbo mwingine huyo in the making.
 
ccm ilikofikia imebakiwa na mbinu moja tu ya kuwabakisha madarakani, ambayo ni kutumia vyombo vya dola, Polisi, usalama wa Taifa na JWTZ. Kama ni kimbunga basi kimbunga pekee kinachoweza kuwakumba na kuwasomba wanamageuzi na wapinzani kwa ujumla ni hivyo vyombo vya dola na si vinginevyo.



Hizi ndoto za Kibanda kwamba kinana ni kimbunga wacha aendelee kuota mwenyewe sisi huko tulishaondoka siku nyingi. Huwezi kumfananisha hata kidogo Augustine Mrema na Dr. Slaa, hawa ni watu wawili walio mbali sana kiuwezo na kwa muono. Yeye aendelee tu kula matunda ya kumsafisha Lowasa na sasa kumjenga Kinana kwakuwa si haba anajipatia ujira wake na kuweza kusukuma mbele gurudumu la maisha na familia yake, lakini atambue kitu kimoja kwamba ccm ilipofikia hakuna mganga yeyote anayeweza kuinusuru na anguko kuu mwaka 2015, si kinana wala vinana!!
haya ndo yale anayayaongelea kibanda kwani viongozi na pro CDM mnakera sana pale ukweli ukisemwa juu yenu kwanini kama kweli mnajiamini mnapenda kusifiwa kila siku? kukosolewa na kuambiwa uwezo wa adui yako ni njia moja wapo ya kuweza kujipanga kwaajili ya mapambano,au ndo yale mkishapigwa chini 2015 mrudi na kutuambia wamechakachua? jua uwezo wa adui yako.So mlitaka aandike Kinana ni kilaza then mfurahi na kusherekea kutumia ruzuku hiyo ni challenge mnatakiwa mlifanyie kazi.

kwa hili Big up Kibanda.
 
Ndugu Kibanda bila shaka unafahamu vizuri sana ugomvi wa CCM na Watanzania , ni DHULUMA , kwa maana ya rushwa , wizi ,ufisadi ,upendeleo ( ajira nzuri kwa watoto wa vigogo ,rejea ya BOT ) nk , huyu Kinana wako anazo tuhuma ambazo hata wewe unazijua ! Sasa unamsifia kwa lipi ?

ikiwa yeye ni mtuhumiwa unadhani ataweza kusafisha uozo ndani ya CCM ? Bila kuondoa DHULUMA ccm haiwezi kupona na Kinana hawezi , wala hakuwahi kuweza , na wala hatakuja weza !

Sifa zinatoka wapi ? Kibanda najua unajiamini sana na ni vizuri , lakini wewe ni binadamu, kuna mengine huyaoni wengine wanayaona , unajua kwa nini Kikwete alimteua Mukama ? Na ni kwa nini kamng'oa ? Hebu umiza kichwa kidogo , ni kweli CDM hawatakiwi kubweteka lakini pia CDM hawana sababu yoyote kumhofia Kinana , hana jipya wala hakuwahi kuwa nalo ! Kama unampenda mtu kwa sababu ya sura yake basi nenda kanywe naye chai - JK NYERERE .
 
Back
Top Bottom