Kazi ya kuubomoa upinzani ndiyo imeanza ama inatekelezwa?

Mugishagwe

JF-Expert Member
Apr 28, 2006
300
58
Wapinzani waanza na uzushi Bungeni

2006-06-20 11:03:33
Na Nelson Goima, Dodoma


Katika muda usiozidi saa moja Bungeni jana, vigogo wawili wa kambi ya upinzani, walilazimika kufuta kauli za uongo, walizotoa wakati wakisoma maoni ya kambi yao juu ya Hotuba za Bajeti? ya Serikali na Hotuba ya Mipango na Uchumi.

Vigogo hao ni Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Bw. Hamad Rashid Mohamed, aliyetoa maoni juu ya Bajeti ya Serikali.

Bw. Hamad alilidanganya Bunge kwa kudai eti kuwa Rais Jakaya Kikwete anaiogopa ndege ya kisasa ya Rais, hatua iliyomfanya hivi karibuni kudandia lifti ya ndege hadi Dodoma.

Kigogo mwingine ni Msemaji katika Wizara ya Mipango, Bw. Kabwe Zitto, aliyedai kuwa watu serikalini ’’wamenona na wana majumba ya kifahari Pretoria, Afrika Kusini’’.

Zitto alisema watu hao ni waliotia saini mkataba wa kuendesha menejimenti ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na kampuni ya NetGroup Solution ya Afrika Kusini.

Alisema mkataba huo umetumbukiza nchi pabaya na kusababisha matatizo makubwa ya umeme, lakini walioingia mkataba huo ’’wamenona na wana majumba Pretoria’’. Pretoria ni mji mkuu wa Afrika Kusini.

Wa kwanza kutoa maoni alikuwa Zitto, ambaye alisoma maelezo mengi na baadaye akachomeka suala hilo la NetGroup Solution na TANESCO.
Alisema mkataba baina ya makampuni hayo haujainufaisha nchi na pia ingawa NetGroup inakaribia kuondoka, kuna watu wamenufaika.

Mara tu Zitto alipoanza kutoa madai hayo, Mnadhimu Mkuu wa Serikali Bungeni, Bw. Juma Akukweti, alisimama na kueleza kuwa utaratibu wa Bunge umekiukwa.

’’Kanuni za Bunge Kifungu cha 50 kinasema mbunge hatakiwi kusema jambo la uongo bungeni, hivyo Mheshimiwa Naibu Spika namuomba Mbunge afute kauli yake au atoe ushahidi wa madai yake kuwa watu walioingia mkataba huo, sasa wamenona na wana majumba Pretoria,’’ alisema Bw. Akukweti, ambaye pia ni Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Bunge.

Papo hapo, Naibu Spika Bi. Anne Makinda, alimtaka Zitto athibitishe kauli yake au alete ushahidi, ambapo alisema anaondoa hoja yake. Hivyo, akaruhusiwa kuendelea kutoa maoni yake.

Alipomaliza Zitto, alifuatia Bw. Hamad Rashid kutoa maoni ya wapinzani kuhusu Hotuba ya Bajeti.

Alisoma maelezo marefu, lakini kama ilivyokuwa kwa Zitto naye alichomekea suala la ndege la Rais.

Bw. Hamad alidai kuwa ndege hiyo ya Rais iliyonunuliwa kwa mabilioni ya fedha, hivi sasa imebaki ’’white elephant’’, kwani haitembei na wala haitumiwi na mwenyewe(Rais).

Alidai kuwa wao wapinzani walipinga kununuliwa kwa ndege hiyo ya kifahari pamoja na radar kubwa, iliyopo Dar es Salaam.

Alidai kuwa wakati ndege hiyo inanunuliwa walielezwa kuwa ingemwezesha Rais kusafiri raha mustarehe bila usumbufu, lakini hivi sasa Rais anadandia lifti na anaiacha ndege yake.

Baada ya kutoa kauli hiyo, Bw. Akukweti alisimama na kusema ’’Kifungu cha 50 kinaeleza kuwa maelezo anayotoa Mbunge ndani ya Bunge, lazima yawe sahihi na siyo ya kubahatisha.

Tungependa kufahamu kama Mheshimiwa Mbunge ana ushahidi kuwa ni kweli Rais anadandia lifti. Kama ana ushahidi atoe na kama hana afute kauli.’’

Ndipo Naibu Spika, Bi Anne Makinda, alimtaka Bw. Hamad afute kauli yake au atoe ushahidi, ambapo Bw. Hamad alisema ’’Mheshimiwa Naibu Spika sisi katika mazoea yetu ya kawaida, tunapomuona Rais ambaye ana ndege yake maalum anatumia usafiri mwingine, tunachukulia kuwa amepewa lifti.’’

Baada ya kutoa jibu hilo, Hamad alibanwa na Naibu Spika atoe ushahidi ni ndege gani iliyompa lifti Rais au afute kauli yake kama hana ushahidi, Bw. Hamad alisema ’’naondoa hoja yangu.’’

Baada ya hapo alipewa ruhusa ya kuendelea kutoa maoni yake.


SOURCE: Nipashe
 
Kwanza nianze kwa kutoa pongezi zangu kwa jj kwa kuniwezesha kuifahamu web site hii kwani nimekuta mnajadili mambo ya msingi sana kuhusu mustakabali wa taifa letu,
Pili nipende kutoa maoni yangu kuhusu kikao cha bunge la budget kilichofanyika ktk ya nchi yetu tukufu Dodoma.

Ni kweli kama ukiangalia kwa makini jinsi ambavyo vyombo vya habari vimeripoti michango ya wapinzani jana utagundua kabisa kuwa upinzani umeanza kushuhulikiwa kwa njia mpya na ya kipekee sana kwani mh. Zitto alizungumza mambo mengi sana na tena ya msingi kweli kweli ila alipokanusha tuu kauli yake ama kwa kuhofia kutoa ushahidi ama kwa sababu anazozijua yeye magazeti leo yakaifanya hiyo ndio habari ya kuwahabarisha watanzania wenzangu eti wapinzani hawana hoja.

Pia ukiangalia hotuba ya zitto utagundua ni miongoni mwa watanzania wachache tena wabunge ambao wana mapenzi mema na nchi yao tofauti na wengi wao ambao kuwa bungeni ni hatua ya kuponda mali za walala hoi wa nchi hii, ningewashauri wana habari kufanya mambo yafuatayo,

1. Kamwe wasikubali kutumiwa kwa maslahi ya watu fulani kwani kwa kufanya hivyo wanamnyima mtanzania maskini haki ya kuujua ukweli na kutafakari kwa kina kuhusu mustakabali wa taifa lake kwani kama wananchi wa kigoma waliomchagua zitto kwa jinsi habari ilivyowekwa watakuwa wanalishwa sumu wasiyoijua.

2. Na yale mazuri yaliyosemwa ambayo yanalenga kulisaidia taifa letu yawekwe hadharani ili watanzania wajue kwamba kuna baadhi ya wabunge wachache wenye uchungu na raslimali zao hata kama ni wa kambi ya upinzani kwani tunapaswa tuangalie zaidi mustakabali wa taifa letu kuliko mtu ama kikundi cha watu wachache.

3. Wapinzani wawe macho sana kwani inavyoelekea mkakati wa kuwamaliza kwa sasa unafanywa tena ndani ya bunge kwa kutumia waandishi wa habari wenye malengo yao wanayoyajua wao binafsi.

Swali la kujiuliza ni je? Kweli zitto hakuwa na ujumbe wowote mzuri ktk hotuba yake ama waandishi wameipotosha kwa makkusudi ama kwa kutokujua wanachofanya?

Niachie hapo kwa sasa ila nitatoa maoni yangu baadae kidogo ,kazi ya kumaliza upinzani ndio inatekelezwa kwa kasi na ari.
 
Mrema,

Asante.

Nakubaliana nawe kuwa kuna mkakati wa kubomoa upinzani ndio maana habari kuhusu upinzani zinachukuliwa negatives too!(waandishi wako stand by kuangalia upinzani umeteleza wapi kuliko hata ni mambo gani yana maslahi kwa taifa na jamii pana).

Lakini maoni yangu binafsi katika suala hili. Upinzani nao ulipaswa kuwa tayari kusimamia kauli walizozitoa. Hoja za Ndege ya Rais na TANESCO zina msingi mkubwa. Hata hivyo zinakuwa na msingi zaidi zikisimamiwa na regardless the cost! Hii ndio dhana ya ushajaa ambayo mara nyingine tunatofautiana na mkandara. Au niite ujasiri. But lets discuss this matter in a more positive way for our national interest.
NB: Mkandara na wengine mlioandika kwenye post nyingine-niko njiani kuelekea New York. Nikifika nitawajibu na kuchangia mjadala huu. Kwa sasa nawaomba udhuru.

Ila nimeona niweke "chakula kingine cha fikra' kuhusu mjadala huu.

Hii ni hotuba ya Zitto kujibu hotuba ya Ngasongwa(waziri husika) ambayo inapatikana katika tovuti ya bunge.

HOTUBA YA WAZIRI KIVULI WA MIPANGO, UCHUMI NA
UWEZESHAJI MHE. KABWE ZUBERI ZITTO (MB) KUHUSU HALI YA UCHUMI WA TAIFA NA MPENDEKEZO YA MPANGO WA MUDA WA KATI NA MFUMO WA MATUMIZI WA SERIKALI KATIKA KIPINDI CHA MWAKA 2006/2007 – 2008/2009.


Utangulizi

1. Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwa niaba ya kambi ya upinzani, napenda kutoa maoni ya kambi ya upinzani kuhusu hotuba ya bajeti kuhusu mipango, uchumi na uwezeshaji kwa mwaka wa fedha 2006/2007 kwa mujibu wa kanuni za Bunge kifungu cha 43(5)(b)(c) na 81(1) toleo la mwaka 2004.

2. Aidha nakupongeza wewe Mhe. Spika, Mhe. Ana Makinda Naibu wa Spika kwa kuchaguliwa kushika nyadhifa hizo.

Tuna imani kubwa na ninyi na tunaamini kuwa mtaitumia imani hiyo kujenga Bunge lililo imara na lenye uwezo wa kuisimamia serikali katika utendaji wa kazi za wananchi.

3. Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii pia kuwapongeza Mhe. Edward Lowassa na Mhe. Hamad Rashid Mohamed kwa kuchaguliwa kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania na Kiongozi wa Upinzani Bungeni sawia.

4. Mheshimiwa Spika, Vile vile ninatoa pongezi zangu za dhati kwa Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ushindi wake ni ishara ya imani waliyo nayo Watanzania kwake. Naamini hatawaangusha.

5. Mheshimiwa Spika, Kwa heshima na taadhima nawapongeza viongozi wetu wa vyama vya upinzani waliogombea Urais kwa kazi walioifanya japokuwa uwanja wa mashindano haukuwa sawa, nawapongeza kwa kazi walioifanya.

6. Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi hii, kwa mara nyingine, kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Kigoma Kaskazini kwa kunichagua kuwa Mbunge wao.

Nitahakikisha kuwa imani waliyonayo kwangu kwa kunichagua niirudisha kwao kwa kutimiza yale yote yaliyomo ndani ya uwezo wangu kuyafanya kwa dhati kwa maendeleo ya Jimbo langu.

7. Mheshimiwa Spika, Kwa namna ya pekee natoa shukrani zangu za dhati kwa shirika la Friedrich Ebert Stiftung kwa kunilea kiuongozi na kunipa elimu na maarifa kupitia mafunzo na baadae kazi. Mchango wao
kwangu nina uthamini.

8. Mheshimiwa Spika, naomba niwapongeze kwa dhati kabisa, Waziri wa Mipango, uchumi na Uwezeshaji Mhe. Juma Alfa Ngasongwa na Naibu Waziri Mhe. Salome Joseph Mbatia kwa kuteuliwa na Mhe. Rais kushika nyadhifa hizo. Fanyeni kazi ya umma kwa uadilifu, kwa viwango na kwa kasi na bila ubaguzi wa aina yeyote kwa Watanzania wote.

9. Mheshimiwa Spika, Napenda kumshukuru mwenyezi mungu kwa kutuwezesha kuwepo hapa na kutekeleza majukumu yetu ya kitaifa.

Namwomba Mwenyezi Mungu atujaalie afya njema na hekima ili tuwatumikie vema Watanzania.

Mungu atupe busara ili tuwatumikie Watanzania bila kujali rangi, kabila, dini, jinsia, hali ya maungo, hali ya afya na bila kujali itikadi za vyama vyetu vya siasa.

10. Mheshimiwa Spika, Ni jukumu letu kuhakikisha kuwa serikali inatekeleza mipango ya maendeleo kwa Watanzania bila kubagua.

Yasipotekelezwa, tutawaambia wananchi kuwa walikosea kuchagua. Hivyo, sisi ni changamoto kwa chama kinachounda serikali.

11. Mheshimiwa Spika, hatutokaa kimya tukiona serikali inakosea. Tutaisema humu Bungeni na kutoa mwelekeo mzuri kwa maslahi ya mtanzania. Tunawatahadharisha Mawaziri waliopewa dhamana na Rais kutekeleza majukumu yao kwa kasi na viwango ili tija iwe wazi kwa kila mtanzania.

12. Mheshimiwa Spika, Dira ya nchi ni moja kama tulivyokubaliana kutengeneza vision 2025, mkakati wa nchi kutekeleza Dira hiyo nao ni moja. Hata hivyo, kila chama kinaweza kuwa na mtazamo wa autekelezaji unaotofautiana.

Mitazamo hiyo isigawe Watanzania, wala kubaguana kwa vile yote ina lengo la kutajirisha na kufikia haraka malengo ya kitaifa.

13. Mheshimiwa Spika, Hivyo Bajeti ya Mpango ni utekelezaji wa dira ya Taifa, na inapaswa kuwa shirikishi na yenye kutuunganisha zaidi kuliko kutugawa.

14. Mheshimiwa Spika, Serikali inapaswa kutekeleza dira na mikakati ya Taifa ambayo imetungwa na Watanzania wote kufuatia mbinu shirikishi. Mfano halisi ni Dira ya maendeleo ya Taifa (VISION 2025) na Mpango wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini (MKUKUTA), ulitungwa na wananchi wote kupitia mashirika yasiyo ya kiserikali na warsha za kanda.

15. Mheshimiwa Spika, Vyama vya siasa vinapaswa kutoa miongozo ya namna bora ya kutekeleza hiyo mipango iliyopangwa na wananchi. Na vyama hivyo havitegemewi kutumia bajeti ya Serikali katika kutoa miongozo hiyo kwani hayo ni majukumu rasmi ya vyama hivyo.

16. Mheshimiwa Spika, Baada ya Utangulizi huo, naomba sasa nijadili hali ya uchumi wa nchi na kutoa mapendekezo ya namna bora ya kuboresha Mpango huo wa Taifa. Serikali iliyoko madarakani ni hiyo hiyo iliyopo madarakani toka tupate uhuru, tukiacha tofauti ya majina, maneno ya awamu ni lugha tu lakini wahusika wakuu ni wale wale. Mheshimiwa Spika, Hivyo, tunapopitia hali ya uchumi, tunapima utekelezaji wa serikali moja ya CCM kwa kipindi chote. Hivyo, chama cha Mapinduzi hakiwezi kukwepa mapungufu ya Serikali hiyo.

MAPITIO YA HALI YA UCHUMI KWA UJUMLA NA MAONI YA KAMBI YA UPINZANI

17. Mheshimiwa Spika, wakati akitoa hotuba ya hali ya uchumi mwaka 2004, mheshimiwa Waziri wa Mipango, Uchumi na Ubinafsishaji aliliambia Bunge lako tukufu tarehe 9 juni 2005, kwamba

  • Pato la Taifa litakua kwa asilimia 6.7 mwaka 2005, asilimia 7.2 mwaka 2006, asilimia 7.6 mwaka 2007 na asilimia 7.9 mwaka 2008
  • Kiwango cha kasi ya upandaji bei kisichozidi asilimia 4.0 kufikiwa ifikapo mwezi Juni mwaka 2006.
18. Mheshimiwa Spika, ukuaji wa uchumi ulifikia asilimia 6.8 tu na kasi ya upandaji wa bei mpaka mwezi June imefikia takriban asilimia 7. Hali ni mbaya zaidi kwa kasi ya upandaji bei ya vyakula ambayo imefikia asilimia 10.7 mwezi wa Machi 2006. Mheshimiwa Waziri amesema uchumi mwaka 2006 utakua kwa asilimia 5.9 tu tofauti na makisio ya mwaka jana. Hii inaonesha kwamba serikali imeshindwa kufikia malengo iliyojiwekea.

Mheshimiwa Spika, sababu za kwamba uchumi umeharibiwa na ukame na tatizo la umeme haitoshi.

Lengo la asilimia 7.2 kushuka mpaka asilimia 5.9 linahitaji maelezo zaidi ya ukame, umeme na mafuta.

19. Mheshimiwa Spika, ukame hutokea nchini kwa wastani wa kila baada ya miaka kumi. Ni kosa tu la kutumia takwimu za hali ya hewa vizuri, na kutokuwa na sera ya kuweka tahadhari ya wakati wa maafa kama hayo. Hata Afrika ya Kusini, na hata Ulaya hupata maafa kama haya lakini kwa sera nzuri huweza kujikimu ndani kwa ndani.

20. Mheshimiwa Spika, Tulikuwa wapi kuweka mipango bora na sera sahihi za kuzuia ukame kutuathiri?

Tulikuwa wapi kuweka sera bora za kuhakikisha umeme unakuwapo wa kutosha? Madhara tunayoyapata sasa ni makosa ya kisera na kimfumo yaliyofanyika miaka ya nyuma. Madhara tutakayoyapata kesho ni matokeo ya sera mbaya tunazoziweka leo.

21. Mheshimiwa Spika Kambi ya Upinzani inamwomba Mheshimiwa Waziri alieleze Bunge lako tukufu kuna mipango gani ya kuepuka madhara ya ukame mwakani ili malengo ya mwakani yafikiwe.

22. Mheshimiwa Spika, hali ya uchumi wetu sio nzuri kwa sasa. Tangu mwezi Januari mwaka huu mfumuko wa bei (kasi ya kupanda kwa bei) unaongezeka kwa wastani wa asilimia 0.2. Shirika la Nchi zenye viwanda (OECD) limekisia kuwa ukuaji wa uchumi wa Tanzania utashuka mwaka huu na kwamba uchumi unakadiriwa kukua kwa asilimia 5.8 tu na sio 5.9 kama alivyobashiri Mheshimiwa Waziri wa Mipango. Hii ni hatari kwani kwa ukuaji huu hatuwezi kufikia wastani wa kukua kwa uchumi kwa asilimia 8 kwa miaka mitatu mfululuzo ili tuweze kupunguza umasikini kwa nusu mwaka 2010.

23. Mheshimiwa Spika, Ukuaji wa uchumi wetu unachangiwa na sekta kadhaa, sekta ya kilimo ikiwa inaongoza. Mchango wa sekta ya kilimo mwaka jana ulikuwa asilimia 45.6 tofauti na mwaka 2004 ambao ulikuwa asilimia 46.3. Kwa uchumi wowote unaokua, mchango wa sekta ya kilimo katika uchumi unapaswa kupungua mwaka hadi mwaka kwani ukuaji wa sekta nyingine kutokana na kupanuka kwa uchumi hupunguza mchango wa sekta ya Kilimo. Hata hivyo, kwa Tanzania nadharia hii bado haifanyi kazi. Mchango wa sekta ya Kilimo katika pato la Taifa unashuka kutokana na ukame na kupungua kwa uzalishaji wa mazao ya Kilimo na Chakula. Hii inaonesha kuwa bado hatujafanya kazi sawa sawa katika kuleta mapinduzi ya Kilimo.

24. Mheshimiwa Spika, sekta ya madini ilikua kwa asilimia 15.7 mwaka 2005. Mwaka 2004 sekta hii ilikua kwa asilimia 15.4. Hata hivyo, ukuaji wa sekta ya madini hauendani na ukuaji wa ajira na kupungua kwa umasikini.

Taarifa ya hali ya umasikini nchini inaonesha kuwa, sekta ya madini inachangia ajira chini ya asilimia moja. Yaani katika kila ajira 100 zinazotengenezwa nchini katika mwaka, sekta ya madini inachangia chini ya mtu mmoja katika ajira.

25. Mheshimiwa Spika, Hii inasababishwa na sababu moja kubwa, kwamba migodi ya madini inamilikiwa na wageni wachache, serikali haijafanya juhudi kuimarisha wazawa walio katika sekta ya madini na Migodi haina mahusiano na sekta nyingine za uchumi (forward and backward linkages). Ndio maana leo hii ni jambo la kawaida kwa migodi ya madini kununua hata nyanya na vitunguu kutoka Afrika ya Kusini. Sera mbaya ya madini isiyomjali Mtanzania masikini ndio chanzo cha tatizo hili.

26. Mheshimiwa Spika, sekta ya Utalii vilevile nayo mchango wake katika uchumi wa nchi unakua lakini mchango wake katika ajira ni mdogo. Watalii wanakuja Tanzania, katika mbuga zetu, mlima wetu wa Kilimanjaro na fukwe zetu nzuri za Zanzibar wakiwa wamelipa kila kitu huko kwao (package tourism). Kuna ukwepaji kodi uliokithiri katika hoteli za kitalii . Sera mbaya za sekta ya Utalii ambazo hazimjali Mtanzaia masikini ndio chanzo cha tatizo hili.

27. Mheshimiwa Spika, Taarifa ya hali ya umasikini nchini, ambayo mheshimiwa Waziri hakuigusia katika hotuba yake imeeleza hali ya umasikini kwa kila Wilaya ya Tanzania. Taarifa imetaja Wilaya ya kwanza mpaka ya Mwisho kwa umasikini.

28. Mheshimiwa Spika, Kwa taarifa nitaje Wilaya tatu tajiri (wananchi wake wengi wana uwezo wa milo mitatu kwa siku – percentage of population below basic needs poverty line) na wilaya masikini zaidi mwaka 2005.
i. Wilaya tajiri ni Bukoba Mjini, Arusha Mjini na Mbeya Mjini. Kati ya wananchi 100 wa Bukoba Mjini, wananchi 11 tu ndio hawana uwezo wa mahitaji ya msingi. Arusha Mjini ni watu 12 na Mbeya Mjini watu 12.
ii. Wilaya masikini zaidi ni Geita, Musoma Vijijini na Bunda. Wananchi 62 kati ya 100 wa Geita hawana uwezo wa mahitaji ya msingi, 64 Musoma Vijijini na 68 Bunda.
29. Mheshimiwa Spika, Taarifa hii ni muhimu sana kutolewa katika Bunge ili tuweze kujipima kwa ngazi ya umasikini ya Wilaya zetu ili iwe changamoto katika kazi ya kuleta maendeleo. Taarifa ya hali ya umasikini
(Poverty and Human Development Report 2005) ni ya serikali na inastahili kuletwa Bungeni na Waziri wa Mipango na pia iwe sehemu ya hotuba ya hali ya uchumi.

30. Mheshimiwa Spika, ni lazima tujiulize maswali, ni kwa nini Wilaya ya Geita yenye utajiri wa dhahabu lukuki, Samaki wa Ziwa Viktoria, Pamba, Ng’ombe na watu wenye nguvu inakuwa wilaya masikini? Zaidi ya nusu ya wananchi wake hawana uwezo wa kula, kuvaa na kulala. Ni lazima tujiulize maswali magumu yenye majibu sahihi. Wilaya ya Geita ni mfano tosha wa jinsi Rasilimali za nchi zilivyo hazisaidii maendeleo ya watu.

31. Mheshimiwa Spika, ili kukua kwa uchumi kuwe na manufaa kwa Watanzania ni lazima serikali kwa makusudi kabisa iamue kuweka sera rafiki kwa masikini (pro-poor policy). Sera rafiki kwa watu masikini ni zile sera zinazoelekea kuweka rasilimali katika sekta zinazokua na zinayoajiri watu wengi zaidi. Kilimo ni sekta pekee inayoweza kuondoa umasikini nchini Tanzania. Hivyo, lazima maamuzi ya makusudi yafanywe ili kuwekeza
rasilimali katika kilimo.

32. Wataalamu wanasema kuwa iwapo tukiweza kufanya kilimo kikue kwa asilimia 10 kwa miaka mitatu mfululuzo, umasikini nchini utapungua kwa asilimia hamsini kabla ya muda wa mwisho wa malengo ya milenia.


USHIRIKIANO WA KIKANDA NA KIMATAIFA

33. Mheshimiwa Spika, Tanzania imeendelea kuwa mwanachama wa mashirika ya kikanda na ya kimataifa.

Tanzania ni mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya Maendeleo kusini mwa Afrika (SADC), Umoja wan chi huru za Afrika (AU), ushirikiano wa nchi za Afrika, Karibeani na Pasifiki na Jumuiya ya Ulaya (ACP), Tume ya Bahari ya Hindi (IOC) . Malengo mbalimbali yanatufanya tujiunge na mashirika haya ya kikanda na kimataifa ikiwemo biashara na masula ya usalama na misaada ya maendeleo.

34. Mheshimiwa Spika, Tanzania ilijitoa katika soko la pamoja kwa nchi za kusini mwa Afrika (COMESA) mwaka 2000. Inawezekana kabisa kuwa uamuzi huo ulikuwa mwafaka kwa wakati huo. Hata hivyo tafiti mbalimbali zilizofanywa na wataalamu wa biashara ya kimataifa na umoja wa wafanyabiashara kama Confederation of Tanzania Industries (CTI) zinaonesha kuwa Tanzania inapata hasara kwa kuwa nje ya COMESA. Tunatambua umuhimu wa SADC kihistoria.

Lakini tutaishi mpaka lini ndani ya mfuko wa historia? Dunia sasa inaendeshwa kwa masuala ya kiuchumi. Tulitarajia kuwa katika hotuba ya hali ya uchumi ya Tanzania, Waziri mwenye dhamana ya uchumi angeweza kusema kitu kuhusu COMESA na madhara tunayopata kwa kutokuwa mwanachama wa COMESA.

35. Mheshimiwa Spika, hivi sasa nchi zote za AKP ikiwemo Tanzania zimo katika mjadala, kupitia makundi yao, wa kitu kinachoitwa Economic Partnerships Agreements (EPA). EPA kwa lugha nyepesi ni umoja wa soko huria (ESH). EPA inadhamiria kuondoa vikwazo vya biashara kati ya nchi za AKP nchi za Umoja wa Ulaya (EU). Mahusiano ya biashara yaliyopo hivi sasa ni ya upendeleo (non- reciprocal) ambapo Tanzania inauza bidhaa zake zote isipokuwa silaha katika soko la EU bila kodi (Everything But Arms – EBA). Mahusiano haya ya biashara yanawezeshwa na msamaha (waiver) kutoka Shirika la Biashara la Kimataifa (SBK) au kwa kiingereza World Trade Organisation (WTO). Msamaha huu unaisha mwezi Disemba mwaka 2007. Kwa masikitiko makubwa, nimeshangazwa na hatua ya serikali ya kuongeza juhudi katika mwaka 2006/2007 kutumia fursa ya soko la EBA ambalo limebakiza mwaka mmoja tu.

Inasikitisha kuwa wakati tunaomba kuongeza muda huo, lakini hata AGOA tumeshindwa kutumia fursa zake kikamilifu.

36. Mheshimiwa Spika, Katika rasimu ya makubaliano iliyowasilishwa jijini Brussels makao makuu ya EU, Afrika ya Kusini sasa imeomba rasmi kuwa katika SADC – EPA na kuzitaka nchi nyingine zote za SADC- EPA kuwa wanachama wa SACU (Associate members). Hili Mheshimiwa Waziri hakuligusia kabisa. Bunge linapaswa kujua kuwa ndani ya mwaka mmoja na nusu ujao hatutakuwa na uhuru wa kupanga kodi zetu kwani Afrika ya Kusini itapanga kwa niaba yetu kupitia SACU.

37. Mheshimiwa Spika, Nchi za Kenya na Uganda zinajadili EPA kupitia kundi la ESA ambalo ni wanachama wa COMESA. Kitendo cha nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kujadili EPA katika makundi tofauti ni kitendo kitakachoua Ushuru wa forodha wa Jumuiya ya Afrika mashariki kwani kitaalamu, nchi moja haiwezi kuwa mwanachama wa Ushuru wa forodha mbili tofauti. EPA inapelekea makundi ya nchi kuwa na Ushuru wa forodha. Sisi kama nchi, tukijua kabisa madhara, tumeamua kujiweka katika ushuru wa forodha na Afrika ya Kusini badala ya ushuru wetu wa forodha na Kenya na Uganda.

MIPANGO MAALUMU YA KIUCHUMI NA KIJAMII

38. Mheshimiwa Spika, serikali imeendelea kutengeneza mikakati mbali mbali ya kuendeleza nchi. Tulikuwa na PRSP, sasa MKUKUTA, MKURABITA na neno jipya kabisa MKUMBITA. PRSP haikueleweka na wala matokeo yake hatujajulishwa, tukatengezea MKUKUTA. MKUKUTA ni mpango mzuri sana. Umeshirikisha jamii nzima, mashirika yasiyo ya serikali, vyama vya siasa, vyama vya wafanyakazi na wataalamu mbali mbali. Namshukuru Mungu pia hata mimi nilishiriki katika kutengeneza MKUKUTA kupitia Asasi ya vijana ya TYVA. Sasa MKUKUTA haujaeleweka, umekuja MKURABITA. Huu haujaeleweka kabisa kwani wenyewe haukuwa shirikishi, ni mambo ya De Soto haya. Juzi tumeletewa MKUMBITA. Hii misamiati hii haiwezi kuleta maendeleo. Tunachanganya tu wananchi wetu.

39. Mheshimiwa Spika, MKUKUTA ndio dira ya kutuongoza kukuza uchumi na hatimae kupunguza umasikini. Kazi iwe ni kuufanya MKUKUTA utekelezeke hata kwa mtu mmoja mmoja. Maeneo matatu ya MKUKUTA – Ukuaji wa Uchumi na upunguzaji wa umasikini wa kipato, uboreshaji wa maisha na ustawi wa jamii na utawala bora na uwajibikaji – yapaswa kujulikana kama azimio la Arusha lilivyojulikana na kuimbwa.

40. Mheshimiwa Spika, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii TASAF umefanya kazi nzuri sana. Napenda kutoa pongezi za dhati kwa Mkurugenzi Mkuu wa TASAF ndugu Likwelile kwa kazi nzuri inayofanywa na TASAF. Hata hivyo, kuna watu wanataka kuharibu kazi nzuri ya TASAF. Miradi ya TASAF sio ya kisiasa, ni miradi ya wananchi wote. Wanasiasa wanaopita pita huko vijijini kudanganya wananchi kuwa wajiunge makundi ili wapate mikopo kutokana na itikadi za vyama. Fedha za TASAF ni miradi ya kijamii. Ni marufuku kwa wanasiasa kupitia jumuiya zao kuwagawa wananchi kivyama. Ni jukumu la serikali ya Kijiji au Halmashauri ya Mtaa kuratibu upatikanaji wa miradi ya TASAF.

Mkutano Mkuu wa Kijiji au Mtaa ndio chombo cha
mwisho chenye jukumu la kupitisha miradi na wala sio kundi dogo la wanasiasa pale kijijini au sheha.

41. Mheshimiwa Spika, zoezi la ubinafsishaji wa mashirika ya umma limeleta lawama kubwa kutoka kwa wananchi. Baadhi ya lawama zimeanza kujidhihirisha.

Bunge litakumbuka kelele zilizopigwa kuhusu TANESCO na NetGroup Solution. Netgroup tunawafukuza lakini walioingia mkataba huu wamenona, wameshiba. Taifa linaangamia. Wizara ya fedha inatoa mabilioni kila mwezi kama ruzuku kwa TANESCO.

42. Mheshimiwa Spika, Lakini hebu tujiulize nani anatumia umeme? Kule Kalinzi, Nyarubanda, Kagunga, Nyamhoza, Kigalye na Chankabwimba hakuna umeme. Umeme unatumika na watu wa middle class. Mabilioni ya fedha yanatumika kwa matajiri tu. Watu masikini wangeweza kujengewa mashule, zahanati, barabara za vijijini n.k.

Lakini fedha zote zinaenda TANESCO. Ruzuku ya mwezi mmoja kwa TANESCO ni sawa na gharama za barabara moja ya Mwandiga – Manyovu. Hivyo rasilimali za nchi zinaenda kwa wenye nacho. Lakini walioingia mkataba wa NetGroup si Watanzania? Hatuwajui?

43. Mheshimiwa Spika, Tulibinafsisha Mashirika yetu ya ndege ATC na Benki ya Biashara (NBC LTD) na sasa linaitwa ATCL na NBC, 1997 LTD. Tulitarajia kuwa ubinafsishaji huu ungeweza kutuletea unafuu.

Tulitarajia kupata ndege zaidi lakini matokeo yake Makaburu wakachukua ndege kutoka kwao na kukodishwa kwa kampuni yetu na sio yao ya SAA. Njia za ndani zimekufa. Ndege za dash 8 zilikodishwa kutoka Afrika Kusini wakati tungeweza kukodisha kutoka ndege ya serikali F 28. Leo ATC haiendi Tabora, Dodoma, Shinyanga wala Kigoma. Mfumo mzima wa tiketi upo Afrika Kusini, code inayotumika 0183 ambayo ipo katika tiketi za ATC ni yao na si ile yetu ya 0197.

NBC nayo ina vituko vya ajabu. Hata ukitaka Bank Statement, Balance ni lazima kwanza ipatikane kutoka Afrika ya Kusini. Siku Mtandao hauko shughuli zote za Benki zinasimama. Hata kitabu cha Benki tu ni lazima kusubiri Wiki 2 kitoke Afrika ya Kusini. Hakuna duniani nchi ya aina hii. Tumepata hasara, hakuna hatua zinazochukuliwa. Wahusika ni matajiri sasa,
wengine wana majumba hata Pretoria. Mali ya umma, haina mwenyewe. Nchi inapukutika.

Tunalaumu wageni, wakati sisi ndio tunafuja nchi. Tunawajua. Historia inaandika, watoto wetu watatuhukumu.

44. Mheshimiwa Spika, tumekodisha uwanja wa KIA kwa dola 1000 kwa mwaka. Uwanja hauendelezwi. Mwekezaji kadanganya nchi. Mwekezaji KADCO amekuwa tajiri mno, kwani kila siku anapata dola 5000 kutoka KLM peke yake inaposhuka pale KIA. Kila unaponunua tiketi kwenda Arusha au Moshi kuna fedha unampa Mwekezaji huyu. Sasa ameanza kukodisha ardhi kwa Watanzania wanaolima pale, kwa heka shilingi 20,000. Tupo kimya, rasilimali zetu zinaliwa.

Wachache wanatajirika. Hatuyaoni haya.

Wabunge wameomba wauone mkataba wa KIA, serikali haitaki. Nini kinafichwa? Kambi ya Upinzani inaomba maelezo ya kina kuhusu kinachoendelea.

45. Mheshimiwa Spika, TIC bado ina changamoto kubwa.

Ni lazima tutumie pesa nyingi kujitangaza. Kuna
ushindani mkubwa katika kila nchi kujitangaza, wengine hata majimbo hujitangaza. Lazima tuchangamke sasa katika ulimwengu huu wa ushindani. Kama tunataka wawekezaji wa maana ni lazima tujitangaze.


MISINGI NA MALENGO YA MPANGO WA MUDA WA KATI NA BAJETI KWA MWAKA 2006/2007 – 2008/2009

46. Mheshimiwa Spika, kwa aya mbili napitia misingi ya malengo mapana kama yalivyowasilishwa na Waziri na pia mpango wenyewe na kisha ninatoa Mapendekezo ya Mpango wa muda wa Kati ili kukuza uchumi wetu, na kuondoa umasikini ambao umewafukarisha wananchi wetu wa Tanzania.

47. Mheshimiwa Spika, hali ya uchumi ya mwaka jana si sawa na ya mwaka huu. Wakati Waziri mwaka jana anasoma hali ya uchumi mwezi Juni, alikuwa anaongea katika mazingira tofauti ya kiuchumi. Hivyo misingi ya malengo mapana ya mpango na Bajeti pia yalikuwa tofauti. Haiwezi kuwa tofauti sana lakini haiwezi kuwa sawa kwa Kila kitu. Hata hivyo, Mheshimiwa Waziri mwaka huu amefanya kunakili misingi ile ile ya mwaka jana kana kwamba hali ni sawa. Ni lazima tuwe makini.

Moja ya misingi ambayo nilitarajia Mheshimiwa Waziri angeitaja ni pamoja na; Kutoendelea kupanda kwa bei za mafuta, Utabiri wa Hali ya hewa na kudhibitiwa kwa mfumuko wa bei ambao unatishia utengemaza wa uchumi mkuu (macro economic stability). Pia kutafsiriwa kwa MKUKUTA kivitendo katika kila Halmashauri ya Wilaya nchini.

48. Mhesimiwa Spika, katika malengo ya uchumi jumla, Waziri pia amerudia malengo yale yale aliyoyataja Waziri Kigoda bila kuzingatia hali ya sasa. Kwa mfano, Waziri mwaka jana alitarajia uchumi kukua kwa asilimia 7.3 mwaka 2007, na Mheshimiwa Waziri mwaka huu pia nae hivyo hivyo. Hata hivyo, hili ni jambo ambalo haliwezekani kwani mwaka huu uchumi utakua kwa asilimia 5.9 tofauti na alivyokadiria Kigoda mwaka jana kuwa uchumi ungekua kwa asilimia 7. Vile vile kwa upande wa kasi ya kupanda bei, matarajio ya Waziri sio sahihi kwani hayazingatii hali ya uchumi ya sasa. Ni vema sasa tuweke malengo yetu katika hali halisi na Mawaziri waepuke kunakili hotuba za miaka ya nyuma ili kuepuka makosa.

MAPENDEKEZO KUFIKIA MALENGO YA MKUKUTA

49. Mheshimiwa Spika, MKUKUTA umeweka mafungu (Clusters) matatu; kukua kwa uchumi na kupunguza umasikini wa kipato – hapa tokeo tarajiwa la jumla ni kukua kwa uchumi kwa mapana na usawa na ukuaji kuwa endelevu (broad based and equitable growth is achieved and sustained). Moja ya lengo hapa ni upatikanaji wa chakula cha kutosha na ongezeko la kipato kwa mwanamke na mwanaume wa Tanzania, mijini na vijijini. Fungu la Pili ni kuboresha hali ya maisha ikiwa na lengo la kupunguza gap la matajiri na masikini (reduce inequality). Fungu la tatu ni utawala bora na uwajibikaji ambapo lengo moja wapo ni kuwapo kwa amani na stahmala ya kisiasa nchini. Kambi ya upinzani inaamini kuwa uchumi ukikua na ukawa mpana na kuwafikia wananchi wengi, hali ya maisha ya mwananchi itaboreka na amani itadumu. Hivyo, tunapendekeza mikakati ifuatayo ili kufikia malengo ya MKUKUTA na wananchi kufaidi kukua kwa uchumi.

50. Mheshimiwa Spika, Kilimo ndio suluhisho la tatizo la umasikini nchini. Hakuna lolote linaloweza kufanyika na uchumi ukakua na kuwafaidisha wananchi kama hatutowekeza nguvu zetu katika kilimo. Ukuaji wa uchumi Vijijini (Rural growth) ni muhimu sana katika kupunguza umasikini nchini na ukuaji wa sekta ya Kilimo ni muhimu zaidi. Mkakati uwe ni kufikia ukuaji wa sekta ya kilimo kwa asilimia 10. Iwapo Ukuaji wa sekta ya Kilimo utafikia wastani wa asilimia 10 kwa miaka mitatu, wataalamu wa umasikini wanasema, umasikini utapungua kwa asilimia 50. Kwa kuwa sekta ya kilimo inachangia asilimia 45 ya pato la Taifa, hivyo ukuaji wa sekta ya kilimo utapelekea kukua kwa kasi kwa uchumi na mapana yake(broad based growth). Ili kilimo kikue kwa asilimia kumi na zaidi mambo yafuatayo yafanyike;

i. Kuongeza uzalishaji kwa mkulima mdogo. Mkulima mdogo aweze kuzalisha zaidi katika ekari alizonazo hata sasa. Kwa kuwa hatuna uwezo wa kupandisha bei, mkakati wetu uwe ni wingi wa mazao (volume) badala ya bei (prices). Kuongeza uzalishaji ipo chini ya uwezo wetu, kupanga bei ipo nje ya uwezo wetu. Kila Halmashauri ya Wilaya iweke mipango kutafsiri lengo hili la kuongeza uzalishaji.

ii. Kugawa nchi katika kanda za umwagiliaji.
Hatuwezi kumsaidia mkulima kama ataendelea kutegemea mvua. Maji ya ziwa Viktoria yasitumike kwa kunywa tu, bali yatumike kwa kilimo katika mikoa ya Shinyanga na hatimae yafike Singida. Maji ya Ziwa Tanganyika yafike Tabora na mito yote mikubwa itumike kwa umwagiliaji.

Dhana ya sasa ya umwagiliaji katika mabonde, ipanuke zaidi. Tufikishe mifereji ya maji vijijini ili uzalishaji uongezeke. Mpango wa kufikisha maji ya kumwagilia vijijini ni ghali sana. Lakini inawezekana kama inavyopendekezwa hapa chini.

iii. Kuongeza maafisa ugani vijijini kwa kuwasomesha wahitimu wa kidato cha nne katika kila kijiji ili wawe maafisa ugani wasaidizi kutokana na aina ya kilimo katika Wilaya husika. Halmashauri za Wilaya ziweke mipango hii.

iv. Kuifanya sekta ya madini kutumikia sekta ya kilimo. Sekta ya Madini ndio sekta inayokua sana lakini inachangia kidogo sana katika pato la Taifa.

Sekta ya madini haina mahusiano mazuri na sekta
nyingine (strong forward and backward linkages), hivyo faida ya sekta hii haiwezi kufikia wananchi kwani wamiliki wa madini ni wachache na mchakato wa madini ni wa mashine za kisasa, hivyo ajira zinazotengenezwa ni kidogo sana. Sera na sheria za madini zibadilike na kuifanya serikali ikusanye mapato mengi zaidi katika madini. Kwa mfano mrahaba kufikia japo asilimia 10 ya mauzo ya madini. Fedha za sekta ya madini ziendeleze sekta ya Kilimo. Taifa liamue kwa makusudi kabisa kuwa katika mrahaba asilimia 3 itengwe mahususi kwa ajili ya kuendeleza kilimo na asilimia iwe kuendeleza Sekta ya madini ikilinga zaidi wachimbaji wa kati na wadogo kwa lengo la kuwafanya Watanzania wafaidi rasilimali yao kimaendeleo.

v. Kuifanya sekta ya Utalii kutumikia sekta ndogo ya biashara ya nje na kuvutia wawekezaji. Sekta ya Utalii ni sekta nyingine inayokua kwa kasi lakini mchango wake katika pato la taifa ni mdogo. Mapato mengi yanapotea kupitia kitu kinachoitwa package tourism.

Serikali iwezeshe Watanzania kufungua makampuni ya utalii katika nchi zinazoleta watalii wengi zaidi ili kuzuia kupotea kwa mapato kutokana na package tourism.

Utalii utumike kutangaza fursa za uwekezaji katika nchi na hasa uwekezaji katika kuongeza thamani ya masoko ya kilimo

vi. Kuongeza ukuaji wa sekta ya viwanda na hasa viwanda vidogo vidogo katika maeneo ya vijijini. Sekta ya kilimo ikukua kwa kiwango cha asilimia 10, mazao ya kilimo yatakuwa mengi vijijini, katika hali ya miundombinu ya sasa kuna hatari ya mazao kuoza.

Serikali iweke sambamba njia za kukuza viwada vidogo vidogo vya kusindika mazao ya Kilimo bila kutumia nishati ghali na hivyo sekta ya viwanda kupanuka. Na nadharia za uchumi zinatuambia kuwa, sekta ya kilimo ikikua, inatoa mwanya kwa sekta nyingine kukua bila
kuhitaji juhudi za serikali moja kwa moja.

51. Mheshimiwa Spika, nchi yetu imeteuliwa kupata msaada kupitia shirika la Millenium Challenge Corporation (MCC) linaloendesha mradi wa Millenium Challenge Account. Nchi imepatiwa jumla ya Dola milioni kumi na moja ili kuimarisha juhudi za kupambana na rushwa kama sehemu ya kufikia vigezo vya kupata msaada huu. Hata hivyo,tumeshuhudia miradi mingi ya kimataifa kuishia maeneo yale yale ya nchi siku zote. Matokeo yake impact haionekani. Kwa kuwa tumechagua maeneo ya miundombinu, nishati na maji kama maeneo ya kuelekeza msaada wa MCC wa jumla ya Dola milioni 700 (shilingi Bilioni 840), basi msaada huu uelekezwe katika mikoa ya pembezoni mwa nchi ili kuifungua na kuifanya ishiriki katika kukuza uchumi wa nchi. Mikoa hii ni Kigoma, Tabora, Rukwa, Ruvuma, Pwani na Pemba (Kaskazini na Kusini). Tukifanya hivi tutaona dhahiri matokeo ya msaada huu kutoka Marekani.

Sekta zibaki hizo hizo yaani Barabara (Kigoma – Tabora - Itigi, Mwandiga – Manyovu – Bujumbura, Tunduma – Sumbawanga – Mpanda – Uvinza, Masasi – Mmbamba Bay, barabara za kuunganisha wilaya za Mkoa wa Pwani, na barabara zote za Pemba), nishati (Umeme wa Grid Kigoma na Ruvuma) na Maji safi na salama kwa Wilaya zote za mikoa hiyo.

52. Mheshimiwa Spika, Hivi sasa nchi yetu ina mkataba wa msaada na nchi za Jumuiya ya Ulaya wenye thamani ya Euro Milioni 355 (Shilingi Bilioni 532) kupitia Mfuko wa Maendeleo wa Ulaya (EDF 9th). Mkataba huu unaisha Disemba mwaka 2007. Kupitia msaada huu tumepata msaada wa miundombinu kama barabara ya Tinde – Isaka, Mandela Road, Morogoro – Dodoma na ukarabati wa Bandari ya Zanzibar. Hata hivyo, kwa sasa tupo katika mjadala wa mkataba mpya ambao tumepangiwa kupata jumla ya Euro milioni 444 (Shilingi Bilioni 666). Bado hatujaamua vipaumbele vyetu. Lakini barabara ya Nyakanazi – Kigoma iwekwe katika vipaumbele. Msaada huu pia utumike kuimarisha barabara za Vijijini katika mikoa iliyo pembezoni ili kuboresha usafirishaji wa mazao ya Kilimo pamoja na msaada wa kawaida wa Bajeti ya
serikali ili kuanza kuziba mapengo wa EPA ambayo tutasaini mwanzoni mwa 2008.

MAMBO YA JUMLA
53. Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia hotuba yangu, kambi ya upinzani inapendekeza mambo kadhaa ya jumla kama ifuatavyo:

54. Mheshimiwa Spika, Miradi ya Kilimo nchini iwekwe chini ya uratibu mmoja badala ya sasa ambapo Wizara ya Kilimo na Chakula haina uratibu wa miradi yote. Miradi ya Kilimo imezagaa Wizara nyingi. Hii haifai kwani msimamizi wa sera ya Kilimo ni Wizara ya Kilimo.

Uratibu wa sekta unasaidia sana kuhakikisha rasilimali za kilimo zinatumika vizuri.

55. Mheshimiwa Spika, bado kuna uvujaji mkubwa wa mapato ya serikali ama kwa serikali kupoteza mapato au kwa watumishi wa serikali kufuja fedha za umma. Tafiti zinaonesha kuwa ufujaji mkubwa unatokea katika serikali za mitaa na hasa kwa sekta za Elimu na Afya.

Utafiti wa REPOA unaonesha kuwa kuvuja kwa fedha kunasababishwa hasa na fedha kutopelekwa katika shughuli zinazotoa huduma kwa jamii na badala yake fedha nyingi kupelekwa katika shuguli kama za utawala, masurufu ya safari na warsha. Pia sehemu kubwa ya fedha za umma zinaenda kwa maafisa wa serikali na hata viongozi kama ‘allowances’. Waziri Kivuli wa Fedha atasoma mpango wa kupata mapato kutoka katika matumizi haya ya ‘allowances’ muda mfupi ujao.

56. Mheshimiwa Spika, Kambi ya upinzani inasema, Tanzania sasa ijiunge na COMESA ili wafanyabiashara wake wafaidike na unafuu wa kodi kwa bidhaa wanazouza nje katika nchi za COMESA. Hatuwezi kuendelea kuvumilia hasara tunayopata kwa kuwa nje ya COMESA.

57. Mheshimiwa Spika, Kambi ya upinzani inataka Tanzania sasa ijadili mashirikiano mapya ya biashara na nchi za Jumuiya ya Ulaya kupitia kundi la ESA ili kuimarisha Jumuiya ya Afrika Mashariki na pia kupata faida ya soko kubwa la nchi za ESA. Uamuzi huu pia utatuweka katika nafasi nzuri ya kushika masoko ya bidhaa zetu za Kilimo kwa nchi za Burundi, Rwanda na
mashariki mwa Kongo DRC.


MWISHO

58. Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaamini kabisa kwamba iwapo mipango hii tuliyoianisha itafanyiwa kazi na serikali, matokeo ya ukuaji wa uchumi yataonekana kwa mwananchi mmoja mmoja kijijini na mijini. Hili ndio lengo la MKUKUTA, hili ndio lengo letu sote, kumuinua kiuchumi Mtanzania.

59. Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.


KABWE ZUBERI ZITTO (MB)
WAZIRI KIVULI WIZARA YA MIPANGO, UCHUMI NA UWEZESHAJI
19.06.06


Tuzijadili hotuba zote mbili pamoja na habari husika.

JJ
 
J J Mnyika,

Nimeisoma hotuba ya Zitto,

Jamaa mkali, jasiri na nampongeza sana kwa sababu kila hatua aliyodai maradhi kasema pia dawa yake. Tatizo kubwa linakuja kwamba nchi yetu na hasa nchi maskini huwa tuna maradhi ya upungufu wa kumbukumbu -yaani wasahaulifu. Zitto ni jasiri bado kabisa kuwa shujaa. Ushindi wa hoja yake kwa manufaa ya wananchi bado, na ndicho muhimu kwa hiyo tunaomba aendelee kupigania haki hiyo hadi hapo wananchi watapata mwanga wa kuendelza mapigano yake hadi kufikia ushindi.

Nchi za kiafrika jamani, ajabu sana - Tutakuwa na njaa miaka kumi na hata kupoteza maelfu ya watu lakini tukija pata kidogo husahau kabisa njaa ile na kuanza kujirusha kabla hata ya kujenga misingi ambayo itahakikisha hali ile hairudi tena. Na kila siku tutakuwa na sababu ama mtu wa kumyooshea kidole.

Ajabu kubwa ktk hili bunge letu ni kwamba njaa nchini imekuwepo toka 1995 na kila mwaka hupata nafuu tu pale mvua inaponyesha, lakini serikali haikufanya kitu kwa miaka yote. Zoezi la umwagiliaji leo hii ndio kwanza linatazamwa kwa mapana ya kitaifa! sababu kubwa ya uzembe kama huu inatokana na mikakati mibovu na hasa huo wa KUPUNGUZA UMASKINI. Mkakati huu ni mbovu kwa tafsiri yake na mipango yake kwa sababu Tanzania nchi nzima ni MASKINI. Nasema hivi kwa sababu MIUNDOMBINU yetu bado kabisa haijafikia hata nusu ya hali halisi inayotakiwa kwa nchi inayoendelea. Miundombinu michache tuliyokuwa nayo haitoshelezi kabisa na leo hii ipo mikononi mwa wageni kama BIASHARA. Ni kosa kubwa kuchukua uti wa mgongo kuwa sehemu ya uzalishaji. Hata ktk viungo vya binadamu, Mungu sii mjinga kuupa uti wa mgongo nyaya zote za hafamu lakini viungo vya mwili ndivyo hufanya kazi kwa kutegemea huo uti wa mgongo.

Hakuweka mikono wala miguu mgongoni isipokuwa viunganisho vya mifupa kurahisisha ubebaji na matumizi ya uti huo wa mgongo. Unapotibu maradhi yaliyosambaa mwilini huwezi kutafuta kiungo dhaifu kinachoshindwa kufanya kazi bali unatafuta kiini cha maradhi yenyewe. Ikiwa ni virus basi itafutwe kinga kwa wananchi wote huku tiba ikiendelea.

Nchi yetu inahitaji mfumo wa kichumi wa kitaifa ambao utakuwa wa majimbo chini ya viongozi waliochaguliwa na wananchi. Trust me, hata hiyo hesabau ya miji ya Arusha na Bukoba ni hesabu ambayo imeongewa marashi. Watu wamehama sehemu hizo ktk miaka kumi hii ni zaidi ya robo kwa sababu maisha yamekuwa magumu sana sehemu hizo.

Kwa hiyo mikakati kama ya MKUKUTA ni mizuri sana kwa wananchi lakini yote hii haitakuwa na manufaa ikiwa kuna mikono ya watu ambao wanaitumia kama sehemu ya kujitangazia. Pia haiwezi kuwa na mwisho mzuri kwa sababu mikakati kama hii haikupangwa kitaifa chini ya uangalizi ambao utamnufaisha Mtanzania.

Kibaya kuliko yote ni kwamba haya yote aliyoyasema Zitto, yamekuja potea tu kwa sababu ya madai yake kuhusu ndege ya rais?...Navyowafahamu Watanzania hotuba nzima imeharibika na sasa hivi anaonekana mchawi tu. Madai halali na yenye kila uzito yatawekwa kapuni na kubakia report ktk makabrasha.

Je, kuna majibu yaliyootolewa kuhusiana na hoa zake toka kifungu cha 19 hadi mwisho tukiondoa hilo la ndege!.
 
Wanabodi,
Mtanisamehe kwa kuchanganya chuzi hapo juu. Nilikuwa nataka kuandika swala la IPTL na sio swala la ndege. Kumradhini...utu uzima tena.
 
Inamaana magazeti yote ni ya serikari siku hizi au serikari ishawanunua waandishi wote?
 
So good to have Mrema on board. Yeye ni mtanzania wa mwanzo kupinga wizi na ufisadi ndani ya serikali karibu Lyatonga. Tuna imani kuwa unaweza kutupa insight zaidi. Janja ya kuupaka matope upinzani this time haitakubalika na it is very unlikely that it will work.
Hapa JF mengi yanawezekana, watashangaa kama siku evidence ikiwekwa hapa ya umiliki wa hayo majumba. Kuprove the obvious sio kazi kubwa
 
Bongolander,
Mrema kisha ingia mitini longtime!...alinusa hapa wakati kuna ushirikiano wa Upinzani lakini mambo yao yalipovurugika basi hata JF pia hapakumfaa tena... why nadhani inabidi tummulize vizuri maanake kama kweli yeye ni mwakilishi wa wananchi iweje JF kuwa ktk fungu la wakosa!
 
Hakuna kitu ila ujumbe umefika kwa walengwa ambao ni wafuasi wa Sultani CCM.Inatosha kabisa unafikisha ujumbe halafu unafuta hoja ,wananchi tumewaelewa wabunge wa fungu la upinzani kamba hiyo hiyo ,ila tunahitaji KATIBA MPYA na NYETI ISO na VIRAKA. Aidha tunahitaji Tanganyika yetu na Zanzibar yetu ili tuwe na shiorikisho lisilo na Utata.... Viva Upinzani ,,,,Viva wabunge...Viva wawakilishi ..Aluta Continuer.
 
So good to have Mrema on board. Yeye ni mtanzania wa mwanzo kupinga wizi na ufisadi ndani ya serikali karibu Lyatonga. Tuna imani kuwa unaweza kutupa insight zaidi. Janja ya kuupaka matope upinzani this time haitakubalika na it is very unlikely that it will work.
Hapa JF mengi yanawezekana, watashangaa kama siku evidence ikiwekwa hapa ya umiliki wa hayo majumba. Kuprove the obvious sio kazi kubwa

Huyo sio Mrema unayemfikiria...fanya uchunguzi zaidi utagundua hilo.
 
Wa-Tanzania na Tanzania kuanzia Wan-Saiasa, Wasomi, Watu wa Kawaida hawawezi kujifunza alama za wakati na saa zote wapo katika kujidanganya kuwa ni nchi ya Amani, wanaendeleza fikra za Mwalimu, Tanzania ni mfano, Tanzania ni nchi yenye haiba ya kila kitu.

Mie nikiwa M-Zanzibari nasema kuwa Tanzania lazima wajifunze na wajiulize kuwa Somali, Liberia, Siera Leone na kwengineko ghasia na fujo na vita vilikuja hivihivi tu? Tanzania umasikini umetopea na kila kukicha maisha hayaridhishi nikusema kuwa kutafika wakati watu waseme potelea mbali kusihi na kutoishi kote ni sawa, hapo tena mabalaa yaje.

Chaguzi mbovu duniani hazipo kama Tanzania, lakini sijui kitu gani Wafadhili wameifanya Tanzania kama East Temor haina mashaka na kila walifanyalo ni sawa. Tanzania inaingia kwenye mabalaa inapofika uchaguzi, hususan Visiwani. Wizi wa kura na watu kupiga kura mara tele hilo ni la mwisho, balaa ni pale kwenye mtiririko mzima wa uandikishaji na Campaign hapo ndipo kwenye mashaka, watu mali zao zitapotea, watabakwa, watafungwa na mchochezi mkuu wa haya ni bara, kwani hutuma Majeshi Zanzibar kushadidia hayo.

Wapinzani niseme kama alivyosema Karl Marx "Kazi ya cahama cha upinzani nikuelekea Ikulu" sasa utasikia Politician wakisema kuwa verejee kila mtu akimbilie IKULU? Unajiuliza hawa watu wanaelewa Siasa au wanakimbilia mloo tu na ulio rahisi ni SIASA kuingia Bungeni. Wapinzani lazima watafute mbinu ya kutaka kuingia IKULU na wao wakisema hata lilokuwa sahihi huambiwa ni Waongo na wanaongoza hata wakisema Uwongo huwa ni kweli Mia fil Mia.


Nikionacho Tanzania inaelekea kubaya kwa kuwa hakuna wana siasa.

Panganyile
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom