nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
[h=2]
[/h]JUMATANO, DESEMBA 11, 2013 05:15 NA MWANDISHI WETU
KAULI iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete kwenye maadhimisho ya miaka 52 ya Uhuru wa Tanganyika, yaliyofanyika juzi jijini Dar es Salaam, kwa kuwataka watu wanaotaka uongozi kutokuwa na visasi imezua maswali kwa baadhi ya wasomi na wanasiasa.
Hatua hiyo imekuja kutokana na hotuba yake aliyoitoa kwenye maadhimisho hayo, Rais Kikwete bila ya kumtaja mtu wala chama, aliwanyooshea kidole baadhi ya wanasiasa ambao wamekuwa wakitajwa kutaka kuwania urais kwenye uchaguzi mkuu ujao.
Hivi karibuni Rais Kikwete alisema kuna watu wanataka kuingia madarakani kwa kulipa kisasi, jambo ambalo ni hatari na kwamba aliyekuwa Rais wa kwanza mweusi wa Afrika Kusini, Hayati Nelson Mandela hakufikiria kufanya hivyo alipoingia madarakani baada ya kuachiwa kutoka gerezani.
Mzee Mandela hana wa kumlinganisha naye, ni kiongozi wa aina yake ametufundisha mengi katika uongozi wake, lakini kubwa zaidi ni kusamehe hata kwa mtu aliyekosea, wengi wetu tuliopo hapa tunajiandaa kulipa kisasi pindi tutakaposhika nafasi za juu za uongozi.
Nawasihi tuache kuwazia mambo ya visasi, wengi tulioko hapa tunamawazo ya nikipata watanikoma, kwa mzee huyu ni tofauti, alipopata madaraka aliwashirikisha makaburu hao hao waliomtesa akiwa na lengo moja tu la kuleta umoja na maendeleo ya nchi,alisema Rais Kikwete.
Akizungumza na RAI Jumatano Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Parofesa Mwesiga Baregu ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) alisema Rais Kikwete anatakiwa kugeuka na kuwa mfano kwa kuwaomba radhi Watanzania kutokana na hila na visasi vilivyofanyika katika kipindi cha uteuzi wake katika nafasi ya urais.
Tunatakiwa kurudi nyuma na kukumbusha hila alizofanyiwa Dk. Salim Ahmed Salim, kiujumla haya ni mambo ambayo yalikuwa ni sawa na kulipiza visasi.
Rais Kikwete anatakiwa kuomba radhi kwa hilo ili kuwa mfano na kuwafanya watanzania wamwelewe kwa kauli yake,alisema.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa CUF bara, Julius Mtatiro, alisema kiujumla kauli ya Rais Kikwete ni ya kinafki kwa sababu mambo ya kulipiza visasi yanafanyika ndani ya serikali yake.
Watanzania wanalipiziwa visasi kwa nguvu kwa kuuawa na wanajeshi kama kule Mtwara na ndani ya migodi, aanze kwanza na serikali yake.
Mandela alijitahidi kufuta kabisa mambo kama hayo ndani ya uongozi wake, lakini kwa upande wetu hali ni tofauti sasa inashangaza anachokikemea Rais Kikwete ni kipi,alisema.
Mhadhiri wa kitivo cha siasa kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk. Benson Bana alisema kauli ya Rais Kikwete imewafumbua macho wananchi kwamba kukiwapo na kiongozi mwenye mrengo wa kulipiza kisasi hatapata kamwe kura za Watanzania.
Alisema kauli ya Rais imekuja wakati muafaka ambao kumeonekana dhahiri kuwapo kwa viongozi wenye nia ya kulipiza kisasi.
Rais ametukumbusha kwamba kama mtu ukishafanikiwa kupata lengo lako hutakiwi kulipiza kisasi. Hii ni njia ambayo hata Mandela ametukumbusha na amewakumbusha pia Watanzania.
Mandela aliifundisha dunia, na sisi tunapaswa kujifunza kutoka kwake, alisema.
Kwa upande wake Bashiru Ali kutoka UDSM, alisema pamoja na Rais Kikwete kuwatahadharisha viongozi wa chama chake, anatakiwa kuwaumbua kwa kuwataja ili waweze kufahamika vyema kwa wananchi.
Aidha alisema pamoja na sifa nyingi alizomwagiwa hayati Mandela, watu wanatakiwa kufahamu kuwa hakuwa malaika, kwani yapo mambo ambayo alishindwa kuyatimiza kwa wananchi.
Tunatakiwa kutafsiri kwanini wazungu na waafrika wamempenda, hii ina maana kwamba alipotoka gerezani hakumaliza tatizo, aliliendeleza kwa sababu wazungu wameendelea kumiliki migodi na rasilimali nyingi za waafrika, ndio maana wanamfurahia kwa kuwaachia yote hayo.
Tunaona Afrika kusini kila siku wanauana kutokana na ukandamizaji unaoendelezwa na wazungu, lakini yote hatuyaona tunabaki kumsifia pekee, ila suala la visasi kiujumla hiyo ni hulka ya mtu na wananchi wanatakiwa kupima kwa sababu naamini kila mtu amezaliwa kulingana na tabia zake, alisema Ali.