Katibu wa kikwete aomba ubunge kupitia ikulu;adai kuaidiwa u-pinda ni prosper mbena

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,720
21,779
Katibu wa Kikwete aibuliwa jambo zito

Mwandishi Wetu Aprili 28, 2010


Adaiwa kuanza kampeni za ubunge kwa jina la Ikulu

Akanusha kudai kuandaliwa Uwaziri Mkuu


WAKATI mjadala wa Sheria ya Gharama za Uchaguzi ukiwa unapamba moto, Katibu wa Rais Jakaya Kikwete, Prosper Mbena, ameingia katika mgogoro akitajwa kuanza kampeni za kuwania ubunge kwa njia zenye utata.

Mbena ambaye ni msaidizi wa karibu wa Rais Kikwete na Ofisa Mwandamizi wa zamani wa Wizara ya Fedha na Uchumi, anadaiwa kuingia katika utata huo akihusishwa na mchakato wa kuhakikisha anachaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini, ambalo kwa sasa linashikiliwa ni Hamza Mwenegoha.

Mbali ya kutajwa kuitisha vikao vya viongozi na baadhi ya wakazi wa jimbo hilo ambavyo vinadaiwa vimekuwa vikiendeshwa Dar es Salaam na Morogoro, Mbena amekanusha kujinadi kwa kutumia jina la Rais Kikwete, madai ambayo yanakwenda mbali zaidi kwamba amekuwa akiwaambia wapiga kura wake kwamba anaandaliwa nafasi ya Uwaziri Mkuu, madai ambayo amekiri kuyasikia.

Raia Mwema imezungumza na Mbena kuhusu masuala hayo lakini akishindwa kukataa au kuthibitisha kutaka kuwania ubunge na wakati huo huo, akikiri kusikia kuhusishwa na tuhuma hizo ambazo alidai ni za uongo akisema zinatokana na mivutano ya kisiasa inayoendelea mkoani Morogoro na kwamba madai kuwa anatumia vibaya nafasi yake hayana ukweli.

Taarifa zinasema hata hivyo ya kuwa mwanzoni mwa mwezi huu, Mbena aliwasafirisha wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutoka eneo la Matombo, Jimbo la Mogororo Kusini, mkoani Morogoro hadi jijini Dar es Salaam kwa lengo la kuwashawishi wampigie kampeni na hatimaye kura ili awe mbunge.

Wajumbe hao wanadaiwa kwamba waliahidiwa kuingizwa katika mkutano wa Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM uliofanyika Aprili 8, mwaka huu, pamoja na mkutano mwingine kuzindua uchangiaji wa chama hicho uliofanyika Aprili 9, mwaka huu. Mikutano yote ilifanyika ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam. Kati ya wageni hao waliosafirishwa yupo diwani wa kata mojawapo jimboni humo.

Tuhuma hizo ambazo zimewasilishwa katika ngazi mbalimbali serikalini na CCM, zinaeleza kwamba mwana CCM mmojawapo aliyeshirikishwa katika vikao hivyo ana makazi yake jijini Dar es Salaam na hakuwa akiishi katika hoteli iliyoandaliwa ‘wageni’ wenzake, iliyopo Sinza (jina tunalihifadhi kwa sasa). Wajumbe hao mbali na kugharimiwa hoteli, walikuwa wakilipwa posho ya Sh 10,000 kwa siku.

Raia Mwema limethibitisha kuwapo kwa wageni hao ambao ilielezwa na wahusika wa hoteli hiyo kwamba wamelipiwa gharama na “mkubwa mmoja” wa Ikulu na kwamba hata vikao vyote vilifanyika waziwazi katika eneo la hoteli hiyo maarufu eneo la Sinza.

Hata hivyo, uchunguzi wa Raia Mwema ambao pia umethibitishwa na baadhi ya ‘wageni’ hao umebaini kuwa mpango wa kuwaingiza kwenye mikutano ya CCM haukufanikiwa kama walivyoahidiwa kutokana na sababu mbili kubwa. Kwanza, ni ‘wageni’ hao kutokuwa na mwaliko rasmi; pili, taratibu za ulinzi wa mikutano hiyo kuwa ngumu.

Taarifa zilizopo zinazidi kubainisha kuwa Aprili 10, mwaka huu, Katibu huyo wa Rais Kikwete alifanya kikao katika hoteli hiyo ambako ndiko walikokuwa wakilala ‘wageni’ wake na ndiye aliyeongoza kikao hicho, eneo jirani na kaunta ya ukumbi hotelini hapo, upande wa kushoto lango la kuingia. Katika kikao hicho wajumbe sita walihudhuria (majina yanahifadhiwa kwa sasa).

Miongoni mwa maazimio ya kikao hicho kilichoanza saa mbili usiku ni pamoja na kuwapatia wajumbe fedha za kuanzia kampeni; za tahadhari na za kukodi pikipiki tatu za kutembelea jimboni wakati wa shughuli husika.

Mmoja wa wajumbe waliohudhuria vikao hivyo ameliambia Raia Mwema kwamba Katibu huyo wa Rais amewaambia wana CCM kwamba hakuwa na nia ya kugombea ubunge kwa kuwa angeweza kuteliwa kutokana na kuwa kwake karibu na uongozi wa juu lakini sasa analazimika kugombea ili kukidhi matakwa ya kikatiba ya nafasi inayoandaliwa kwa ajili yake ya uwaziri mkuu.

Taarifa hizo za uwaziri mkuu kuhusishwa na Mbena, habari zinasema, zilimfikia Mwenegoha ambaye amekaririwa akilalamika kuwa mwenzake huyo anaandaliwa mazingira ya ushindi na viongozi wakubwa nchini.

Akizungumza na Raia Mwema wiki hii kuhusu taarifa hizo Mwenegoha alisema: “Nimesikia lakini sijui…inawezekana ametumwa na kuahidiwa huo uwaziri mkuu au pia hakutumwa wala kuahidiwa huo uwaziri mkuu.”

Wakati wa mazungumzo hayo na Raia Mwema, Mwenegoha alikuwa katika mipango ya safari kutoka Dodoma alikokuwa akishiriki mkutano wa 19 wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, uliofungwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Aprili 23, mwaka huu.

Kwa upande wake, Mbena alizungumzia masuala hayo akisema; “Kwanza kuhusu suala la kugombea ubunge wakati wa kutangaza kwa upande wangu haujawadia, lakini wakati ukifika naweza nikatangaza, kuhusu hili la kumhusisha Rais, mimi pia nimesikia kama unavyonieleza lakini huo ni uvumi si kweli kabisa.”

Hayo yakiendelea taarifa zinasema katika moja ya vikao hivyo vya hotelini Sinza, mgombea mwingine mtarajiwa katika jimbo hilo (jina linahifadhiwa kwa sasa) alifika eneo la kikao na moja kwa moja alikwenda kuwasilimia wajumbe waliokuwa wakishiriki kikao cha Mbena na kuzua taharuki.

Katika taharuki hiyo, mjumbe mmoja aliwatuhumu wenzake kuwa walivujisha taarifa za kikao kwa mgombea huyo mtarajiwa.

Habari kutoka Mororgoro zinasema kwamba nyendo hizo zimewavuta wachunguzi na kwamba wiki kiasi cha mbili zilizopita, Aprili 16, maofisa waliojitambulisha kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) waliodai kutumwa kazi maalumu na Ikulu walifika katika Kanisa Katoliki la Mtombozi, jimboni humo na kumhoji Paroko wa kanisa hilo, Lazaro Gumbo pamoja na kiongozi wa kwaya kanisani hapo, Agata Felix.

Raia Mwema haikuweza kumpata moja kwa moja Paroko Gumbo lakini kiongozi wa kwaya, Agata, alithibitisha kufika kwa watu wawili waliojitambulisha kuwa maofisa TAKUKURU ambao waliwahoji kuhusiana na tuhuma za kuhusishwa na rushwa ya uchaguzi.

Mawasiliano hayo ya simu kati ya mwandishi wetu aliyepo makao makuu ya gazeti hili, Dar es Salaam na Parokia ya Mtombozi yalikuwa hivi, baada ya utambulisho;

Mwandishi: Tunazo taarifa za uhakika kwamba Aprili 16, mwaka huu, wasichana wawili walifika kijijini kwenu na kukuhoji, wakijitambulisha wametoka Makao Makuu ya TAKUKURU Dar es Salaam lakini wakiwa wametumwa kazi maalumu na Ikulu. Je, ulikutana na watu hao?

Agata: Umesema uko Dar es Salaam, mimi niko huku kijijini…kwanza namba yangu ya simu umeipata wapi wewe?

Mwandishi: Nimepata kutoka kwa watu wanaokufahamu, usihofu. Je, ulihojiwa na hao maofisa wawili na je, walimhoji Paroko?

Agata: Ni kweli walifika, walituhoji na kuondoka. Walijitambulisha wametoka Makao Makuu ya TAKUKURU kwa sababu tumechukua rushwa.

Mwandishi: Rushwa ya fedha taslimu au vifaa? Na mmechukua hiyo wanayodai ni rushwa kutoka kwa nani?

Agata: Ni sare za kwaya ambazo ni fulana kutoka kwa kijana (anataja jina), wanasema huyu (jina) naye anataka kugombea ubunge sasa sisi hata hatujui hilo la kugombea ubunge.

Mwandishi: Mliwahi kumuomba msaada au amejitolea tu wakati huu wa mwaka wa uchaguzi?

Agata: Tulimuomba tangu Novemba 2009 na si yeye tu tunayemuomba misaada ya kwaya wapo wengi tu. Na katika maombi yetu hayana uhusiano wowote na masuala ya uchaguzi.

Mwandishi: Nini kilitokea baada ya wewe kuhojiwa?

Agata: Walikwenda kumhoji Baba Paroko kuhusu suala hilo na baada ya hapo walisema wanarudi makao makuu. Basi, hatujui kingine zaidi ya hapo.

Imebainika kwamba mahusiano ya Mbena na Paroko yanahusishwa na masuala ya kiroho yakihusisha watu wawili ambao wote wanafanya kazi Dar es Salaam.

Baadhi ya wana CCM wa Morogoro wamesema kitendo cha Takukuru kwenda kumhoji Paroko kinaweza kuiathiri CCM na mmoja wa wana CCM hao alisema: “Hili limetushtua sana …la mtafaruku na kanisa…huyu mtumishi wa serikali anakuja na hili la kumpelekea paroko vyombo vya kumtuhumu kwa kula rushwa. Kama yeye ndiye amefanya hivyo hili linatugombanisha kanisa na CCM na Serikali yake.”

Uteuzi wa wagombea rasmi wa ubunge wa CCM unatarajiwa kuanza mwishoni mwa Julai mwaka huu, ukitanguliwa na uchukuaji fomu za kuwania nafasi hizo. Mchakato huo utaanza mara baada ya Bunge la sasa kuvunjwa.

Kwa mara ya kwanza, Uchaguzi Mkuu nchini unatarajiwa kufanyika chini ya udhibiti wa Sheria mpya ya Gharama za Uchaguzi iliyotungwa kulenga kudhibiti matumizi ya fedha.
 
Oyeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeee

rais ashakwambia ruksaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaa wanataka ninihao takukuru rushwa watupu
 
Back
Top Bottom