Stephano Mgendanyi
JF-Expert Member
- May 16, 2020
- 1,890
- 939
TAARIFA KWA UMMA
KATIBU MKUU WA CCM ATOA MAELEKEZO MATATU MAHUSUSI KWA VIONGOZI NA WATENDAJI WA SERIKALI NCHINI
KATIBU MKUU WA CCM ATOA MAELEKEZO MATATU MAHUSUSI KWA VIONGOZI NA WATENDAJI WA SERIKALI NCHINI
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi Ndugu Daniel Godfrey Chongolo, akiambatana na Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, akiwa katika ziara ya kukagua miradi na shughuli za maendeleo mkoani Dar Es Salaam, ametoa maagizo matatu mahsusi kwa serikali, akihimiza utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya 2020-2025 kwa ajili ya kuwaharikishia huduma wananchi na fursa za kujitafutia maendeleo.
Ukaguzi wa miradi hiyo, umefanyika tarehe 11 Agosti, 2021 katika mradi mkubwa wa Daraja la Tanzanite, hapo awali likifahamika kwa jina la Daraja la Salenda na mradi wa ujenzi wa soko la kisasa la Tandale.
Baada ya kupokea taarifa ya ujenzi huo wa Daraja la Tanzanite kutoka kwa Mtendaji Mkuu wa TANROAD Mhandisi Rogatus Mativila, unaotarajiwa kukamilika mwezi Desemba mwaka huu kwa kugharimu kiasi cha Sh. 243.7 Bilioni na ukiwa umefikia asilimia 91.1 zaidi ya malengo waliojiwekea ya kuwa asilimia 89 mpaka mwezi huu wa Agosti.
Katibu Mkuu ameipongeza TANROAD kwa usimamizi mzuri wa mradi huo ikiwa ni pamoja na kujumuisha wakandarasi wengi wazawa huku akitoa maelekezo kuwa ni muda mwafaka sasa iwepo programu maalum ya kukuza na kuwajengea uwezo wakandarasi wazawa ili fursa na kandarasi zinazoendelea za ujenzi hapa nchini baadae ziweze kufanywa na wazawa kwa kiasi kikubwa.
"Hapa nchini hatuna programu mahsusi ya kukuza uwezo wa wakandarasi wetu wa ndani, hakuna programu maalum kwa ajili hii na ikapimwa na kufuatwa kwa viwango maalum, ingawa kuna sheria ambayo inataka kila mkandarasi wa nje anapopewa kazi lazima kuwepo na mkandarasi mdogo wa ndani, lakini pamoja na yote ni lazima tuwe na programu mahususi ya kuwawezesha wakandarasi wetu wa ndani kuwa sehemu ya ujenzi wa mindombinu yetu ya nchi,” Katibu Mkuu.
Wakati huo huo, akiwa katika mradi wa ujenzi wa daraja hilo, pia ametumia fursa hiyo kutoa maelekezo mahsusi kwa Serikali, hususan kupitia Halmashauri, katika robo hii ya mwaka kuhakikisha inatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya madarasa ya shule kwa mwezi Januari mwaka 2022 ili kuepuka kufanya kazi kwa mtindo wa zimamoto kila inapofika mwezi Disemba kwa ajili ya kupokea wanafunzi wa darasa la kwanza na Kidato cha Kwanza.
"Kama nchi tumekuwa na changamoto kubwa sana ya kufanya baadhi ya mambo kwa zimamoto, kila mwaka tumekuwa tukisubiria mwezi Desemba, kuhangaika kukimbizana na madarasa kama vile ni jambo la dharura, hatujui maoteo kwa kipindi cha mwaka mzima, na hatujui bajeti nzima. Hili jambo halina afya kwa maendeleo ya elimu, serikali chini ya Rais Samia inatenga fedha kwenye kila mwanzo wa mwezi wa mwaka wa fedha, Julai mosi, kuanza kutumika kwa ajili ya miradi mbalimbali ya maendeleo na madarasa yanakuwa ni sehemu hiyo,” Ndg. Chongolo.
Aidha, akitoa maelekezo kuhusu suala hilo Katibu Mkuu amesema, "Sasa mwaka huu lazima robo hii ya mwaka wa fedha itumike kutenga fedha zote ambazo zipo kwenye bajeti kuzielekeza kutumika kwenye miradi ya miundombinu ya madarasa ya shule zetu ili ikifika Januari, 2022 watoto wetu wote wapokelewe kwenye shule zetu bila usumbufu wala kufanya mambo kwa dharura, lazima tusimamie haya mambo ili tutafsiri matokeo ya tija ya elimu bila malipo.”
Katika hatua nyingine Katibu Mkuu ametembelea ujenzi wa mradi wa Soko la Tandale ambapo hakuridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa mradi huo wa kisasa, kutokana na kusua sua kwa utolewaji wa fedha za malipo kwa wakati, hivyo amesema;
"Kumekuwa na kadesturi kabaya sana, ka watu wanaohusika na masuala ya fedha, kufanya makusudi kuchelewesha malipo ya fedha kwenye miradi kwa ajili ya maslahi yao binafsi, mtu anayehusika fedha zikimfikia, kuidhinisha tu zile fedha kwenda kwenye miradi inakuwa kama vile ni anasa ama zawadi au sandakalawe,” Katibu Mkuu amefafanua.
Akitoa maelekezo Katibu Mkuu amesema, "Sasa soko kama hili la Tandale wananchi wote wametolewa wapo barabarani na watu wanacheleweshewa huduma, anayetakiwa kuidhinisha fedha ambazo zimeshatengwa, mpaka apigiwe goti. Hili jambo kwenye serikali hii inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi likome, kwa sababu serikali inaingia gharama kubwa kulipa fedha za ziada ambazo zingefanya kazi nyingine."
Ziara hii imejumuisha Wajumbe wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa akiwemo Naibu Katibu Mkuu (Bara) Ndugu Christina Mndeme, Naibu Katibu Mkuu Zanzibar Dkt. Abdullah J Saddala, Makatibu wa NEC, Oganaizesheni Ndugu Mauldine Castico, Itikadi na Uenezi Ndugu Shaka Hamdu Shaka, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa Ndugu Ngemela Lubinga na Makatibu Wakuu wa Jumuiya za CCM, Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana Ndugu Kennan Kihongosi, Katibu Mkuu wa Wanawake Dkt. Philis Nyimbi na Katibu Mkuu wa Wazazi Ndugu Gilbert Kalima pamoja na viongozi na watendaji wa serikali wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Ndg. Amos Makala.
Imetolewa na;
Said Said Nguya
Afisa Habari
Ofisi ya Katibu Mkuu
CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM)h