Katiba: JK Anastahili Pongezi...

maggid

JF-Expert Member
Dec 3, 2006
1,084
1,246
Ndugu zangu,

Kupitia kwenye runinga nilimwona Rais wetu akiwa mwenye furaha. Ni siku ile ya kukabidhiwa Rasimu Ya Pili ya Katiba.

Nami kama raia nimeipitia rasimu hiyo. Nimejisikia ni mwenye furaha. Na Watanzania wengi waliosikia, japo kwa muhtasari, juu ya yaliyomo kwenye rasimu hiyo, nao wana furaha. Ni Rasimu itakayozaa Katiba itayofufua matumaini mapya kwa Watanzania wa sasa na vizazi vijavyo.

Hapa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, chini ya Jaji Warioba, nayo inastahili pongezi za kipekee. Rais wetu ni wa kupongezwa kwa vile, katika mfumo wa Kirais- Presidential System, yeye kama yeye, angeweza, kama asingekuwa na dhamira ya kutaka mabadiliko ya kimsingi, kuzuia, kwa namna moja au nyingine, mabadiliko hayo.

Ndio, ni furaha ya wengi. Tumeona hapa Iringa jana jioni, wakati Mbunge wa Iringa Mjini akihutubia pale Mwembetogwa, kuwa alitamka kumpongeza Kikwete kuhusiana na Katiba, na umati nao ukalipuka kwa furaha kumshangilia Kikwete. Na Kikwete huyu atashangiliwa zaidi atakapoondoka madarakani. Maana, ndipo hapo Watanzania wengi watakapotambua maana ya alichowafanyia.

Ilipotoka Rasimu ya kwanza ya Katiba niliandika yafuatayo kupitia jarida la Raia Mwema, na bado naamini katika nilichoandika;
"MABADILIKO makubwa yamefanyika katika nchi yetu kwa mujibu wa Rasimu ya Katiba Mpya iliyozinduliwa wiki hii.

Haya ni mabadiliko makubwa kuwahi kufanyika tangu mwaka 1977. Ni mwaka ambao Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania ilifanyiwa marekebisho makubwa. Mwaka huo wa 1977 yalifanyika mabadiliko makubwa pia kwenye uongozi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na hata ndani ya mfumo wa uongozi wa Serikali.

Naam, katika dunia hii, mabadiliko ya kijamii hupelekea mabadiliko ya kisiasa. Na Wanasholojia wanasema zipo sababu mbili zenye kupelekea mabadiliko hayo. Sababu za ndani ya jamii husika (endogenous) na sababu za nje ya jamii (exogenous).

Kwa upande wetu, tunaona kwamba sababu za ndani na za nje, kwa pamoja, zimesukuma kwenye kufikia hatua hii ya kufanyika mabadiliko haya makubwa ya Katiba.

Na kwa jamii yetu kwa upana wake, ina sababu za msingi za kuyafurahia mabadiliko haya, maana, ni sawa na mwanadamu aliyepewa kikombe chenye nusu ujazo wa maziwa.

Utafahamu kama amefurahia au amechukizwa kwa namna atakavyochagua kukielezea kikombe kile anayekiona ni ‘kikombe nusu cha maziwa’ anaonyesha kutoridhika, na anayekiona ni ‘kikombe kilichobaki nusu tu kujaa’ huyo amekifurahia na anaonyesha matumaini kuwa iko siku kitajaa. Inahusu kuwa na matarajio chanya (optimism) na kuwa na matarajio hasi (pessimism).

Binafsi, nichukue fursa hii kuwapongeza Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa kazi yao njema iliyotufikisha kwenye hatua hii ya kuwepo kwa Rasimu ya kwanza ya Katiba. Lakini, mwingine wa kupongezwa kwa ujasiri wake mkubwa wa kiuongozi, ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete.

Historia itamkumbuka Rais Kikwete kwa ujasiri wake wa kuachana na fikra za ukale na kuwa tayari, kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi hii, kukaa meza moja na makundi yote, wakiwemo wapinzani wa chama chake kujadili mustakabali wa nchi yetu.

Maana, hili la Katiba halihusu mustakabali wa chama cha siasa, bali mustakabali wa nchi yetu. Vyama vya siasa vinakuja na kuondoka, lakini nchi yetu itabaki pale pale. Leo unaweza kuwa kiongozi wa chama fulani, lakini, mtoto wako au mjukuu wako, akaja kuwa mwanachama au kiongozi wa chama tofauti na chako.

Kwa ujasiri wa kuongoza mchakato huu wa Katiba, na kimsingi mabadiliko makubwa kwa maslahi ya taifa, Rais Kikwete anatupitisha kwenye ‘Jakaya-stroika’ ya kwetu wenyewe, maana, kimsingi, mabadiliko mengi makubwa ya kimfumo, kiuchumi na kijamii, yanakuja kufuatia Katiba Mpya inayokuja.

Na katika dunia ya sasa, hakuna anayeweza kuyazuia mabadiliko yanayotokana na msukumo wa ndani ya jamii. Kwa mfano, Urusi ya zamani kule, Mikhael Gorbachev alipoanzisha mageuzi makubwa ya kisiasa, kiuchumi na kijamii katika Urusi, watu wake hawakuamini walichokiona.

Gorbachev aliuona wakati uliobadilika. Mabadiliko yale makubwa ya kimfumo kule Urusi yalipata majina mawili. Perestroika na Glasnot. Perestroika ina maana ya ujenzi mpya wakati Glasnot ni uwazi.

Kabla ya mageuzi yale makubwa, Urusi ilikuwa ikikabiliwa na tatizo la kuwepo na fikra za ukale na kukosekana kwa uwazi. Jamii ilijawa hofu, mambo mengi yalikuwa ya kufichaficha. Kulikuwa na usiri mkubwa!

Lakini, ndani ya kufichwa huko, kulikuwa na harufu ya uoza mkubwa. Gorbachev, daima atakumbukwa kwa kvunja ukimya na kuifanya Urusi kuwa nchi ya kisasa kama inavyoonekana sasa.

Na kwa hakika, ‘kuzaliwa’ kwa Katiba Mpya yetu, ni sawa na Taifa letu kujivua gamba. Maana, kujivua gamba huku kama taifa, kunapaswa kuendane na kuanza kubadili mifumo yetu ya kifikra. Tuanze sasa kufikiri juu ya malengo ya taifa, kwa maana ya ndoto za taifa letu badala ya kutanguliza sana malengo ya vyama vyetu au zaidi malengo binafsi ya vyeo na mamlaka.

Nchi yetu ni kama nyumba kongwe. Tuendelee kwa umoja wetu kuifanya kazi ya kuikarabati upya nyumba yetu. Ipate mwonekano mpya. Kuikarabati upya nyumba kongwe, huweza pia kupelekea kuibomoa nyumba yenyewe.

Kutakuwa na fito na vipande vya matofali vya kurudishia. Kutahitajika fito na matofali mapya pia. Ndiyo, fito na matofali mengine yatakuwa ni ya kutupa tu, na ni lazima yatupwe, basi. Na hapo utakuwa umeikarabati upya nyumba yako.

Maana, katika jamii, mabadiliko yanapaswa yaendane pia na fikra mpya. Na jamii huingiwa na mashaka na kukosa imani pale fikra mpya zinapotekelezwa na watu wale wale ambao hawataki kabisa kuwaruhusu wengine kushiriki uongozi wa nchi.

Watu ambao bado miongoni mwao wanaamini kwamba tofauti za kifikra ni jambo baya. Kwamba upinzani ni uadui, ni uhaini. Kwamba wapinzani ni wa kuwakatakata na kuwatupa. Sasa, katika hali ya sasa utawachinja wangapi ukawamaliza? Ni fikra za kiwendawazimu tu!

Nchi yetu inapita sasa katika kipindi kigumu tangu tupate Uhuru wetu. Ni kipindi kinachowataka viongozi, na hususan viongozi wa kisiasa, kutanguliza hekima na busara badala ya jazba, chuki na visasi. Hayo matatu ya mwisho ni mambo maovu yenye kuambukiza kwa haraka.

Kamwe tusiruhusu jazba, chuki na visasi vitawale siasa zetu. Hii ni nchi yetu. Ni nchi yetu sote. Hakuna mtu, kikundi au chama cha siasa chenye haki zaidi ya kuongoza nchi hii kuliko wengine wote.

Na kwa mwanadamu, lililo kubwa ni uwepo wa matumaini. Na imani ya wananchi kwa taifa na viongozi wao, ni shina la matumaini yao. Inakuwaje basi mwananchi anapokosa imani na taifa, na hata kwa kiongozi? Katiba yetu iwe chachu ya kurudisha mioyo ya uzalendo kwa taifa letu.

Mungu Ibariki Tanzania." ( Makala yangu, Raia Mwema)

Maggid Mjengwa,
Iringa.
MjengwaBlog :: Habari, Picha, Matangazo na Matukio
 
Maccm wenzake walikuwa na sura mkunjamano kama wamelishwa chloroquine kusikia habari ya serikali 3.
 
Jk atastahili pongezi mara tu ya kuueleza umma juu ya kisa na mkasa wa kukatisha maisha ya Dr Mvungi.
 
Maggid greetings and happy new year.

naamini pongezi Zako umezitoa mapema mno. No doubt so far he has done a nice job. But please hold your breath. Tunakoenda ni mbali kuliko tuliko toka. Anything can happen and JK has the key to the whole process. So tuvute subira.

wasalaam,

masanja
 
Ahsante sana Mkuu huyu jamaa amekurupuka bila kujua kwamba bado tuna safari ndefu sana hasa ukitilia maanani MACCM wengi wanataka kupindisha zoezi la kupatikana katiba mpya hivyo kuandika katiba waitakayo wao ili waendelee kuitawala Tanzania milele.

Maggid greetings and happy new year.

naamini pongezi Zako umezitoa mapema mno. No doubt so far he has done a nice job. But please hold your breath. Tunakoenda ni mbali kuliko tuliko toka. Anything can happen and JK has the key to the whole process. So tuvute subira.

wasalaam,

masanja
 
Kwahili kweli anastahili pongezi kwa sababu kawatosa hadi wahafidhina wa chama chake ccm,kamtosa hadi Ngombari mwiru, na wenye akili mgando wote.....
Wanamuona kama msaliti vile
 
Kwa Zanzibar bado tunaona Serikali ya Kikoloni ya Jamhuri ya Muungano bado imejilimbikizia madaraka ya Kikoloni. Hizo sifa bado sana kutolewa maana Nasikia harufu ya kuendelea na Katiba hii tulonayo
 
Back
Top Bottom