TANZIA Kanali Fabian Massawe, aliyekuwa RC Kagera afariki dunia

Informer

JF-Expert Member
Jul 29, 2006
1,582
6,627
A0D14FB1-6D69-46EF-845D-2761293619AA.jpeg
F098D43B-284A-4251-BA51-FF55A86841E7.jpeg

Kanali Massawe aliwahi kuwa DC wa Kinondoni pia.

Alikuwa Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Jitegemee kuanzia mwaka 1986 hadi 2002.

Pia, alikuwa Mkuu wa Chuo cha NDC Kunduchi kisha Arusha.

Kanali Mstaafu Fabian Ignas Massawe amefariki leo tarehe 10 Machi, 2021 mchana katika hospitali ya Seifee karibu na St. Peters jijini Dar.

Kanali Mstaafu Fabian Massawe alikuwa Mwenyekiti wa Kigango cha Mt. Yohana Mbatizaji na Makamu Mwenyekiti wa Parokia ya Mwenyeheri Isdori Bakanja Boko.

Hadi anafikwa na umauti, alikuwa Lt. Gen wa JWTZ.

Apumzike kwa amani.

==========

Fabian Ignas Maswe ni mtoto wa kwanza wa mzee Ignas au Inyasi Mark Massawe na alizaliwa katika kijiji cha Kifuni kata ya Kibosho Magharibi. Elimu ya msingi alisoma Umbwe na Sekondari alisoma Umbwe Sec.

Kanali Mstaafu Fabian Ignas Massawe kabla ya kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera alifanya kazi mbalimbali na mahali pengi akiwa na uzoefu mkubwa wa uendeshaji na usimamiaji wa shughuli za umma. Kabla ya kuwa mwanasiasa alikuwa ni Afisa wa Jeshi la Wananchi Tanzania, Mtaaluma na Mwanamichezo.

Alijiunga na Jeshi la Wananchi Tanzania mwaka 1979 katika cheo cha Luteni Usu na aliendelea kupandishwa vyeo mpaka cheo cha Kanali alichotunukiwa Januari 2002. Akiwa Jeshini alihudhuria mafunzo lukuki hadi yale ya High Commander Defence Styles.

Kitaaluma, Massawe alikuwa Mwalimu na Mtaalamu wa Maendeleo (Development Studies). Aliteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Julai 2006, akiwa mtumishi wa umma mwenye uzoefu mkubwa hasa katika elimu ambapo alikuwa Mkuu wa shule maarufu ya Jitegemee ya Jijini Dar es Salaam kwa muda wa miaka 17.

Kwa upande wa michezo, Kanali Massawe alikuwa hazina kubwa ya uendeshaji na usimamizi wa michezo, aidha aliwahi kuwa Mkurugenzi wa Michezo katika Jeshi la Kujenga Taifa, Katibu Mkuu Tanzania Boxing Association, Makamu Mwenyekiti Kamati ya OlImpiki Kanda ya Tano na Mjumbe wa Balaza la Michezo Tanzania.

Medali alizowahi Kutunzwa

Massawe aliwahi kutunzwa medali 8 (nane) za utambuzi kutokana na mchango wake uliotukuka katika utumishi wa umma. Kwanza, Oktoba 1995 Wizara ya Elimu ilimtunuku cheti cha kuwa Mkuu wa Shule bora. Pili, Oktoba 1998 alitunukiwa cheti maalum cha utambuzi wa mchango wake uliotukuka (Excellent contribution) katika kukuza Uskauti nchini kutoka Skauti Tanzania.

Medali ya tatu, Januari 2002 alipewa hati ya kuutambua mchango wake katika kukuza mchezo wa handball Afrika Mashariki na Kati. Nne, Januari 2005 alipewa hati na Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (East African Cooperation) katika kutambua mchango wake mahiri akiwa kiongozi wa timu ya Jeshi la Wananchi Tanzania katika mashindano ya kwanza ya Michezo na Utamaduni ya Majeshi ya Ulinzi ya Afrika Mashariki mjini Kampala, Uganda.

Julai 2011 Kanali Massawe alipata cheti kutoka Bodi ya Kahawa Tanzania kwa mchango wake mkubwa katika kudhibiti magendo ya kahawa katika Wilaya ya Karagwe. Sita, Machi 2011 Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe ilimtunuku cheti maalum kwa kuongoza mafanikio makubwa ya mapambano dhidi ya mimba kwa wananfunzi na Oktoba 2011 alipata zawadi kutoka Chuo Kikuu cha Johns Hopkins cha nchini Marekani kwa kumlinda mtoto wa kike.

Utumishi wa Umma Kama Mkuu wa Mkoa

Chini ya uongozi wake kama Mkuu wa Mkoa wa Kagera, mkoa uliendelea kuwa katika hali ya amani na utulivu na aliuacha mkoa ukiwa wenye amani uhakika wa chakula. Pato la mwananchi lilikuwa shilingi 409,822/- mwaka 2011 aidha aliacha pato hilo likiwa shilingi 716,209/- mwaka 2014.

Katika kipindi chake, alisimamia mkoa katika usafi na kutunza mazingira ambapo wananchi wa Manispaa ya Bukoba waliipa siku ya Alhamisi kuwa "Massawe Day".

Katika Sekretarieti ya Mkoa Mhe. Massawe alihimiza mambo makuu muhimu yafuatayo:

Amani na na Maendeleo katika Mkoa, alikuwa mstari wa mbele katika kupigana vita dhidi ya maadui 14 ambao ni Malumbano ya kisiasa, Uhamiaji haramu, Wizi wa kutumia silaha, Mauaji ya albino na vikongwe, Uchukuaji wa sheria mkononi, Unyanyasaji wa kijinsia, Migogoro ya Ardhi na Wizi wa Mifugo.

Maadui wengine aliopambana nao Massawe ni pamoja na Biashara ya magendo ya kahawa, Upachikaji wa mimba kwa watoto wa shule, Ushirikina na upigaji wa ramli za kichonganishi, Uharibifu wa mazingira na uchomaji moto ovyo, Uzururaji ovyo na ukaaji vijiwni na kunywa kahawa muda wote wa kazi na unywaji wa pombe saa za kazi.

Kanali Massawe alihimiza wananchi kufanya kazi na alijenga Serikali ya Mkoa yenye kushirikiana na wananchi, Asasi za Kiraia, madhehebu ya dini pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo katika mkoa na nje ya mkoa wa Kagera.

Aidha, aliwahimiza wananchi kupendana na kufanya kazi na kuondokana na Kamunobele, Olwango, Kitandugaho, Eitima, Obunafu na Eilangira. Hiyo yote ilikuwa ni kuchochea maendeleo na ustawi wa mkoa wa Kagera ambao upo katika kitovu cha nchi za Afrika Mashariki.

Akiwa Kagera, alisimamia na kuongoza matukio matukio makubwa ya kitaifa mkoani Kagera. Kwanza, mwaka 2011 Maadhimisho ya Kitaifa ya wiki ya Nenda kwa Usalaama barabarani, Miaka 50 ya uhuru Tanzania Bara. Mwaka 2012 Maandalizi ya sensa na makazi ya watu.

Mwaka 2013 alisimamia Maadhimisho ya Siku ya Mashujaa Kitaifa mkoani Kagera, Mchakato wa wananchi kutoa maoni ya Katiba Mpya, Maadhimisho ya kitaifa ya Fimbo Nyeupe, Uendeshaji wa Operesheni Kimbunga. Mwaka 2014 - Uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa kwa rekodi kubwa ya maandalizi.
 
Mungu hapangiwi, ukifa roho na mwili vinatengna na hakuna maombi ya kumpangia Mungu
Sijampangia Mungu, atavuna alicho panda. Nimeomba kwa Mungu wa imani yangu amlaze mahali pema peponi.

Siwezi muombea mabaya maana sijui kesho yangu wala sio utu. Ingawa ninajua fika kuwa kila mtu at chukuwa mzigo wake mwenyewe.
 
Back
Top Bottom