Kampuni ya StarTimes yaleta matumaini kwa waandaaji wa filamu Kenya

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,003
1,024
1645060898262.png

Kampuni ya Arise (AR) inayotayarisha filamu na yenye makao yake mjini Mombasa Kenya, imepata fursa ya kipekee ya kusaini mkataba wa kuandaa filamu inayoitwa NIA, ambayo inarushwa kupitia kituo cha runinga cha Rembo, kinachomilikiwa na kampuni ya StarTimes.

Akizungumza na CRI Kiswahili, Derrick Melvin, ambaye ni afisa mawasiliano wa kampuni ya AR anasema, kufanya kazi na StarTimes ni fursa ya kipekee ambayo imewapa jukwaa la kutangamana na watu wengi.

“Tumepewa mkataba wa miaka miwili na StarTimes kuandaa filamu ya NIA ambayo inapeperushwa kwenye Rembo TV. Ni fursa ambayo imetutangaza sisi kwa wateja wapya wa StarTimes na tayari tunahisi kuwa soko letu limepanuka”, alisema Melvin.

Kama njia moja ya kukuza vipaji vya Kenya, kampuni ya StarTimes ya China imetangaza kutenga shilingi milioni 200 (dola milioni 1.76) katika utayarishaji wa vipindi vya runinga vya asili ya Kenya.

Taarifa kutoka ofisi ya StarTimes iliyotolewa wiki iliyopita, inasema kuwa mtaji huu unatokana na ufanisi wa kituo cha televisheni cha Rembo, ambacho kinamilikiwa na StarTimes, na kurusha vipindi ambavyo hutayarishwa na kuigizwa na Wakenya.

Kwa mujibu wa Terry Liu, Mkurugenzu msaidizi wa mauzo ya StarTimes, kampuni hiyo imewekeza fedha nyingi katika utafiti, uigizaji na ubora wa uzalishaji ili kuja na vipindi vyenye ubora wa hali ya juu.

"Wiki hii tulianza kupeperusha kipindi kipya kwa jina NIA. Ni kipindi cha kwanza mwaka huu ambacho StarTimes imewekeza fedha ili kiwe chenye mvuto kwa wateja wetu. Hii inaonyesha jinsi gani StarTime imejotolea kuwapa wateja wake burudani isiyo na mfano,’ alisema Liu.

Ameeleza matumaini yake kwamba, kipindi hiki kipya cha NIA kitawavutia watazamaji wa Kenya, huku kampuni ya StarTimes ikiendeleza juhudi za kukita mizizi pembe zote za Kenya.

"Ili kupendwa na wateja wetu wa Kenya, lazima tuwekeze katika ubora wa vipindi tunavyopeperusha kwenye kituo chetu cha running cha Rembo. Tunataka kuwa na vipindi vya kipekee, na vyenye gharama nafuu kwa wateja wetu wote,’ alisema Liu.

Akizungumza na CRI Kiswahili, meneja uhusiano wa StarTimes Alex Mwaura amesema, shilingi milioni 200 zilizotengwa na StarTimes zitawafaa wengi wanaojihusisha na uzalisha wa vipindi vya runinga ya Rembo.

‘Wakati wa kutengeneza filamu au kipindi cha kupeperushwa kwenye runinga, kuna watu wengi wanaohusishwa. Fedha hizi zitawafaa wapishi, madereva, waigizaji wenyewe, walinzi, miongoni mwa wengine,’ alisema Mwaura.

Aidha, Mwaura alieleza kuwa kampuni ya StarTimes ina lengo la kubadilisha taswira ya sekta ya sanaa ya uigizaji nchini Kenya.

‘Tumetoa jukwaa kwa waigizaji wa hapa Kenya kujitangaza na kufikia ndoto zao. Kando na hili, tunataka kuhakikisha kuwa yeyote anayejihusisha katika uzalishaji wa filamu na vipindi vinavyorushwa na Rembo TV, analipwa vizuri,’ aliongeza Mwaura.

Hii si mara ya kwanza kwa StarTimes kutenga fedha za kuipiga jeki sekta ya uigizaji wa ndani ya Kenya. Mwaura anasisitiza kuwa miaka ijayo, kiwango hiki kitaongezeka, na wateja watarajie vipindi bora zaidi..

‘Mwaka huu tumewekeza shilingi milioni 200. Hii ina maana ya kuwa miaka miwili au mitatu ijayo, kiwango hiki kitakuwa mara dufu au mara tatu ya hiki. Tuko hapa kukuza vipaji,’ alisisitiza Mwaura.

Myke Mwai, mkurugenzi wa vipindi StarTimes, alisema kampuni hiyo itaanzisha ushirikiano na kampuni za uzalishaji vipindi nchini Kenya, ili kutayarisha vipindi vya kuvutia watazamaji, kwa kuzingatia tamaduni mbalimbali za Kenya. Kulingana na Mwai, ushirikiano huu utaimarisha ubora wa vipindi ili kuwawezesha watazamaji kujihusisha navyo.

Kwa mfano, kipindi kipya cha NIA kimetayarishwa na kampuni ya uzalishaji filamu ya AR yenye makao yake kule Mombasa. NIA ilionyeshwa kwa mara ya kwanza kwenye Rembo TV usiku wa Februari 14 na baadaye kupeperusha kila siku Jumatatu hadi Ijumaa kuanzia saa nane mchana
 
Back
Top Bottom