Kampuni tatu za madini zadaiwa kodi ya mabilioni

JIS

Member
Dec 5, 2011
73
48
KAMPUNI tatu za madini zinazoendesha shughuli zake nchini, zimewekewa vikwazo na Serikali ikiwa ni kuzishinikiza kulipa mabilioni ya fedha za kodi inazodaiwa.
Habari zilizopatikana na kuthibitishwa na uongozi wa Wizara ya Nishati na Madini zimetaja kampuni hizo kuwa ni Tanzanite One, Mgodi wa Dhahabu wa Geita (Geita Gold Mining Ltd – GGML) na Kampuni ya Resolute (Resolute Mining Tanzania Ltd).

Kwa pamoja, kampuni hizo zinadaiwa zaidi ya Dola za Marekani milioni 5.2 (zaidi Sh8.188 bilioni) kwa viwango vya sasa vya kubadilishia fedha ambavyo ni wastani wa Sh1,574.74 kwa Dola moja ya Marekani. Fedha hizo ni malimbikizo ya tozo na kodi mbalimbali ambazo zilipaswa kulipwa kwa Serikali Kuu na Serikali za Mitaa.

Kutokana na hali hiyo, Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini imeanza kuchukua hatua dhidi ya madeni hayo kwa kuzinyima kampuni husika vibali mbalimbali vya kutekeleza shughuli zao kama hatua ya kushinikiza malipo hayo.

Kwa upande wa Tanzanite One, Serikali imeripotiwa kukataa kuhuisha leseni yake ya uchimbaji ambayo uhai wake ulitarajiwa kumalizika Juni 30, mwaka huu wakati kwa upande wa GGML na Resolute zinakabiliwa na hatari ya kunyimwa leseni za kusafirisha madini kwenda nje ya nchi (Export Licenses).

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Steven Masele alithibitishia kampuni hizo kudaiwa na kwamba Serikali imeanza kuchukua hatua.

“Lazima tusimamie sheria na kwa kweli katika hili, Serikali haitanii hata kidogo. Kama kuna kampuni inadaiwa fedha zozote za umma lazima zilipwe na huo ndiyo wajibu wetu kwa niaba ya Watanzania,” alisema Maselle.

Tanzanite One
Kampuni ya Tanzanite One inayoendesha shughuli za uchimbaji wa madini ya vito katika eneo la Mererani mkoani Arusha, inadaiwa zaidi ya Dola za Marekani milioni mbili kutokana na kutolipa kodi mbalimbali kati ya mwaka 2004 – 2008.

Kutokana na hali hiyo, Serikali imezuia kutolewa kwa leseni mpya kwa Tanzanite One hadi itakapokuwa imelipa au imeanza kulipa deni hilo pamoja na kutekeleza matakwa mengine ya Sheria ya Madini ya 2010.

Masharti hayo ni pamoja na kurejesha asilimia 50 ya hisa zake serikalini kwa mujibu wa sheria hiyo ili zigawanywe kwa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro na kwa wananchi wazawa.

Chanzo chetu katika Wizara ya Nishati na Madini kilisema leseni ya uchimbaji ya kampuni hiyo ilitarajiwa kumalizika Juni 30, mwaka huu na kwamba hadi juzi, ilikuwa haijapewa leseni mpya na ilitakiwa kutimiza masharti iliyopewa kwanza.

Sharti jingine ambalo kampuni hiyo imepewa ni kuhakikisha kwamba inaweka mfumo salama wa utiririshaji maji kutoka kwenye migodi yake kuepusha kutiririka kwenye migodi ya wachimbaji wadogo hali ambayo imekuwa ikihatarisha maisha yao.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Tanzanite One, Ammy Mpungwe akizungumza kwa simu alisema: “Muda wa leseni yetu ya kuchimba siyo Juni 30, ila tuko kwenye process (mchakato) wa kupata leseni nyingine, hicho ndicho ninachojua.”

Alipoulizwa kuhusu madeni ambayo kampuni yake inadaiwa alisema kwa kifupi: “Hilo jambo silifahamu, labda mwulize aliyekwambia akupe ufafanuzi.”

Hata hivyo, habari zilizopatikana kutoka Wizara ya Nishati na Madini zinasema kutokana na kubanwa huko, kampuni hiyo imeanza kulipa madeni yake na imeomba ifanye hivyo kwa awamu.

GGML na Resolute

Inadaiwa kwamba Kampuni za GGML na Resolute, zilikataa kulipa malimbikizo ya nyuma ya Dola za Marekani 200,000 kila mwaka kwa mujibu wa mikataba ya kuchangia maendeleo (Mining Development Agreement).

GGML inatajwa kudaiwa kiasi cha Dola za Marekani 1,400,000 ambazo ni malimbikizo ya tozo za miaka saba, wakati Resolute ambayo inaendesha uchimbaji wa madini katika Mgodi wa Golden Pride, Nzega inatajwa kudaiwa kiasi cha Dola 1,800,000 ambazo ni malimbikizo ya miaka tisa.

Hatua ya Serikali kutaka kuzinyima kampuni hizo leseni kwa ajili ya kusafirisha madini kwenda nje inalenga kuzibana kulipa madeni hayo katika Halmashauri za Wilaya ya Geita kwa upande wa GGML na Nzega kwa Resolute.

Ofisa Mtendaji wa GGML, Gary Davies alisema hata kama kampuni yake ingekuwa inadaiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Geita, madeni hayo hayawezi kuwa na uhusiano na taratibu za kampuni yake kupewa au kutopewa leseni ya kusafirisha dhahabu kwenda nje ya nchi.

“Suala la kudaiwa Dola 1.4 milioni na Halmashauri ya Geita na kusimamishwa kwa leseni yetu ya kuuza dhahabu nje ni mambo mawili tofauti na wala hayana uhusiano wowote,” alisema Davies na kuongeza:

“Geita Gold Mining Limited si kwamba haiamini kuwa inadaiwa kiasi cha fedha na Halmashauri ya Geita kutokana na malipo ya kodi zake, lakini tayari tumeanza mazungumzo na Wizara (Nishati na Madini) ambayo tunaamini yatatuelekeza katika matokeo yenye tija kwa pande zote mbili.”

Alisema leseni ya GGML kwa ajili ya mauzo ya dhahabu nje ya nchi ilisimamishwa kutokana na kampuni yake kutokubali nyongeza ya malipo ya mrabaha wa asilimia nne badala ya tatu ambazo zimetajwa katika mkataba wa kisheria baina yake na Serikali ya Tanzania.

“Wawakilishi wa GGML Juni 5, mwaka huu walimtembelea Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na wakurugenzi wetu walimweleza utayari wa kampuni yetu kuwa na suluhisho la kudumu katika suala hilo baada ya kufanya majadiliano.”

Alisema GGML ni moja ya walipa kodi wa kubwa nchini na kwamba kwa mwaka huu pekee inakadiria kulipa kodi na mrabaha inayofikia Dola 180 milioni pamoja na kodi nyingine na kuchangia miradi ya kijamii.
Alisema kampuni yake inachangia dola milioni sita kwa ajili ya kutekeleza mradi wa maji na dola milioni tatu kwa ajili ya kutekeleza mradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Nyankumbu.

Hatua hizo za Serikali huenda zikakwamisha mpango wa Kampuni ya Resolute kuanza uchimbaji mpya wa dhahabu katika eneo la Nyakafuru, Bukombe, Shinyanga baada ya kufunga Mgodi wa Golden Pride mwishoni mwa mwaka huu baada ya dhahabu kuisha.

Mmoja wa maofisa wa Kampuni ya Resolute ambaye hakutaka jina lake liandikwe alitoa maelezo kwa maandishi akisema: “Yamekuwapo mawasiliano kwa miezi kadhaa kati ya Halmashauri ya Wilaya ya Nzega na Kampuni ya Resolute (Tanzania) Limited ambayo ndiyo mmiliki wa Mgodi wa Golden Pride... Kwa ufahamu wetu na kwa kumbukumbu tulizonazo, hakuna chochote ambacho kampuni inadaiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Nzega.”

Alisema kama ilivyo kwa kampuni zozote kubwa zinazochimba dhahabu na zenye mikataba na Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Nishati na Madini, Resolute imekuwa ikilipa Dola 200,000 kwa halmashauri hiyo bila kukosa kila mwaka tangu utaratibu huo ulipoanzishwa.

Alisema kampuni yake haina taarifa zozote kuhusu mpango au tishio la Serikali kusitisha utoaji vibali vya kusafirisha nje dhahabu wala habari kwamba itazuia uendelezaji wa mradi wa Nyakafuru iwapo deni hilo linalotajwa na halmashauri ya halitalipwa.

Hongera TRA na TMAA kwa kuwabana hawa wawekezaji kisawasawa. Wametugagadua kwa muda mrefu mno, sasa kupitia kwenu watalipa kodi kisawasawa. Hakuna kuwachekea. Hongera sana Mhe. Masele, wembe uleule.
 
Back
Top Bottom