Candid Scope
JF-Expert Member
- Nov 8, 2010
- 11,883
- 6,883
:A S 465:Harison Mwakiembe VS Omar Nundu:A S 465:
KAMPUNI iliyokuwa kiini cha mjadala na hatimaye kung'olewa kwa aliyekuwa Waziri wa Miundombinu, Omar Nundu, China Communications Construction Company (CCCC) Ltd, iliyokuwa ikipiganiwa na uongozi wa Mamlaka ya Bandari (TPA) uliosimamishwa pamoja na wabunge kupitia Kamati ya Bunge ya Miundombinu, inatuhumiwa na Benki ya Dunia kwa kughushi na kula rushwa, imefahamika. Kutokana na tuhuma hizo ambazo hata hivyo kampuni hiyo imekanusha kupitia gazeti la Guyana Times la nchini Guyana, nchi iliyoko Pwani ya Kusini ya Amerika, Benki ya Dunia imezuia kuipa mkopo na dhamana yoyote kampuni hiyo kutokana na kuhusishwa katika kashfa hizo za rushwa na kughushi.
Mbali na uamuzi huo wa Benki ya Dunia, Mamlaka ya Ununuzi wa Umma nchini (PPRA) imeizuia kampuni hiyo kwa miaka 10 kutopewa kazi nchini (blacklisted), huku Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema, akimtupia ‘mpira' Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, kuamua kuinyang'anya kazi kampuni hiyo au la, kwa kuzingatia kashfa za sasa. Kwa mujibu wa taarifa ya Benki ya Dunia inayopatikana katika tovuti ya taasisi hiyo kubwa ya kifedha duniani, ambayo imekuwa na sera ya kutoa mikopo na dhamana kwa kampuni kubwa za kimataifa ili kufanikisha shughuli zao katika nchi mbalimbali wanakoshinda zabuni za uwekezaji au ujenzi, China Communicatiosn Construction Company sasa haitapewa mkataba wowote na benki ya dunia.
"Orodha hii ni ya hivi karibuni, inahusu kampuni ambazo hazitapewa mkataba wa fedha na Benki ya Dunia kwa ajili ya shughuli zao. Amri hii ni utekelezaji wa sera ya Benki ya Dunia katika kupinga masuala ya rushwa na kughushi," inaeleza taarifa ya Benki ya Dunia iliyopo katika tovuti ya taasisi hiyo.
Katika tuhuma dhidi yake, CCCC inadaiwa kupata baadhi ya zabuni zake kwa njia ya rushwa na kughushi katika baadhi ya nchi, kwa namna mbalimbali ikiwamo kupitia kampuni zake tanzu. Kati ya nchi hizo ni pamoja na China, ambako hadi sasa kuna kesi kati ya kampuni tanzu ya CCCC na mamlaka ya nchini humo. Lakini katika utetezi wao kupitia taarifa iliyochapishwa katikaGuyana Times, CCCC wanakanusha wakisema katika miradi yao mingi wamekuwa wakiiendesha kwa ubia kati ya mamlaka za nchi husika na kampuni yao na kwa hiyo, katika utetezi wao huo licha ya kukanusha wameeleza kuwa sehemu ya maelezo yanapaswa kutolewa na wabia wao na kusisitiza kuwa, kila upande katika mkataba una haki sambamba na wajibu.
Moja ya kampuni tanzu ya CCCC, China Road and Bridge Corporation (CRBC) iliyochukuliwa mwaka 2005 na CCCC, inatuhumiwa kutoa mlungula ili kushinda zabuni ya ujenzi wa barabara na daraja nchini Philippine, mradi ambao ulikuwa ukifadhiliwa na Benki ya Dunia. Tuhuma dhidi ya CCCC zilianza kuiandama kampuni hiyo wiki kadhaa baada ya kutetewa na wabunge ipewe zabuni ya upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam.
Kutokana na Waziri wa Uchukuzi kwa wakati huo, Omar Nundu kuitilia shaka kampuni hiyo kiasi cha kuhoji ni kwa nini inatetewa kwa nguvu kubwa, waziri huyo aliingia katika mgawanyiko wa dhahiri na aliyekuwa Naibu Waziri wake, Dk. Athumani Mfutakamba. Katika mvutano wao, Waziri alifikia hatua ya kumtuhumu Naibu wake kugharimiwa safari kwenda nje ya nchi na kampuni aliyokuwa akiitetea ipewe jukumu la upanuzi wa bandari, lakini hatimaye Rais Kikwete aliwatupa wote nje ya Baraza la Mawaziri na kumteua Dk. Harrison Mwakyembe kuwa Waziri wa Uchukuzi, na Naibu wake Dk. Charles Tizeba.
Mbali na hali hiyo katika mvutano huo, Bandari pamoja na Bodi kwa kushirikiana na wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu inayoongozwa na Mbunge wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba, nao walikuwa wakiipigia debe CCCC, lakini baadhi ya wabunge wakiwamo wa kambi ya upinzani walitaka suala hilo likabiliwe kwa umakini mkubwa.
Tahadhari ya wabunge wa upinzani, hususan Zitto Kabwe na John Mnyika, ilikuwa kwamba Serikali isitoe kazi ya upanuzi wa bandari gati namba 13 na 14 hadi ijiridhishe kuhusu gharama halisi za upanuzi kwa kutafuta mkandarasi huru atakayefanya upembuzi yakinifu badala ya serikali kukariri gharama zilizotokana na upembuzi yakinifu wa CCCC ambaye ndiye mjenzi wa gati hiyo. Katika mvutano huo ulikuwa wa wazi kati ya bandari na bodi yake kwa kushirikisha wabunge kwa upande mmoja na waziri kwa upande mwingine.
Mamlaka za Tanzania
Wakati PPRA ikiwa tayari imeamua kuifungia kampuni hiyo kwa miaka 10 kutoshindania zabuni za umma nchini, Mwanasheria Mkuu (AG) Frederick Werema amekwishatoa ushauri wa kitaalamu kwa Waziri Mwakyembe kuhusu kampuni hiyo ambayo ilipiganiwa na wanasiasa na uongozi wa bandari. Katika ushauri wake, AG anasema kampuni hiyo tayari ilikuwa na mkataba na Mamlaka ya Bandari kuhusu upanuzi wa gati namba 13 na 14 kabla ya uamuzi wa Benki ya Dunia na kwamba kwa kuzingatia taarifa mpya za kashfa kwa kampuni hiyo, uamuzi wowote unaweza kuchukuliwa.
Chanzo chetu cha habari kimemweleza mwandishi wetu kwamba, sasa ni jukumu la wizara kuamua kuiacha kampuni iendelee na kazi ya upanuzi wa bandari au kuinyang'anya mkataba. Hata hivyo, uchunguzi zaidi unabainisha kuwa upanuzi wa bandari hiyo unaendeshwa kwa fedha za Benki ya Exim ya China, na kwamba hata kama kampuni hiyo itanyang'anywa kazi hiyo ni lazima kampuni nyingine ya China ipewe zabuni hiyo kwa sababu masharti ya mkopo ni kwamba kazi itolewa kwa kampuni ya China.
Mwandishi wetu aliwasiliana na Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, kujua uamuzi wa serikali baada ya Benki ya Dunia kuiwekea pingamizi kampuni hiyo ya China Communications and Constructions Ltd. Katika maelezo yake, Dk. Mwakyembe mbali na kuthibitisha kuwa PPRA wameiweka ‘kizuizini' kampuni hiyo kushindana katika zabuni za umma kwa miaka 10, lakini pia alithibitisha wizara yake kupokea ushauri wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. "Tumepokea ushauri wa AG (Mwanasheria Mkuu), kwa sasa tunalifanyia kazi suala hilo ili tuone namna bora ya kufanya uamuzi. Uamuzi unaweza kuwa ama kuendelea kuiacha kampuni hiyo ifanye kazi kwa sababu pengine iliingia mkataba kabla ya misukosuko hii ya sasa, au kuteua kampuni nyingine ya China ifanye kazi hiyo na kuachana na CCCC. Tutafanyia kazi suala hilo bila kuchelewa ndani ya mwezi huu, hatutaki upanuzi wa bandari kuchelewa," alisema Dk. Mwakyembe.